Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w73 12/1 kur. 542-549
  • Kusafisha Kundi la Mungu Katika Wakati wa Hukumu Yake

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kusafisha Kundi la Mungu Katika Wakati wa Hukumu Yake
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUSHUGHULIKA NA SWALI LA KUZOEA DAWA ZENYE KULEVYA
  • MAONI YALIYOPATANA JUU YA MAZOEA YA TUMBAKO
  • LAZIMA YA KUAMUA KABISA SASA
  • WAKATI WA HUKUMU ZA KIMUNGU
  • Je, Biblia Inaweza Kukusaidia Kushinda Uraibu wa Dawa za Kulevya?
    Habari Zaidi
  • Watetea Tumbaku Waanzisha Puto la Hewa-Joto
    Amkeni!—1995
  • Mungu atahisije nikitumia tumbaku?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Kuongozwa na Dhamiri Katika Kufanya Mema kwa Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
w73 12/1 kur. 542-549

Kusafisha Kundi la Mungu Katika Wakati wa Hukumu Yake

“Hamjui kwamba chachu kidogo hulichachusha donge zima?”​—1 Kor. 5:6.

1. Kwa sababu gani Wakristo wanapendezwa sana na usafi?

USAFI wote wa namna mbili, wa kimwili na wa adili, una faida kwa mwili wa kibinadamu. Kuwa na usafi huu kunasaidia kuleta maisha yenye afya. Kama mwili wa kibinadamu ndivyo na kundi la wanafunzi wa kweli wa Kristo Yesu ambalo ni kama mwili, linalopatikana katika sehemu zote za dunia leo. Yehova Mungu anataka usafi huo wenye afya katika kundi hilo la watumishi wake​—kwa ajili ya heshima ya jina lake mwenyewe na kwa ajili ya faida ya milele ya wote wanaompenda.​—2 Kor. 6:17; Isa. 52:11; Mal. 3:2, 3.

2, 3. Kupatana na shauri la kimtume, basi ni wajibu gani ambao inawapasa wachungaji au waangalizi wa Kikristo waangalie kuufanya?

2 Akiwaandikia Wakristo wenzake miaka 1900 iliyopita, mtume Paulo alisihi hivi: “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao; mkiangalia sana . . . shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo. Asiwepo mwasherati wala [ye yote asiyeona faida ya mambo matakatifu], kama Esau, aliyeuuza urithi wake wa mzaliwa wa kwanza kwa ajili ya chakula kimoja.”​—Ebr. 12:14-16.

3 Basi, wanapofuatia amani pamoja na watu wote, inawapasa wachungaji wa kundi la Mungu walilinde lisiingiliwe pole-pole na mambo yasiyotakiwa. Inawapasa wafahamu sana kwamba “chachu kidogo hulichachusha donge zima.”​—1 Kor. 5:6; Matendo 20:28.

KUSHUGHULIKA NA SWALI LA KUZOEA DAWA ZENYE KULEVYA

4, 5. (a) Ni ulizo gani ambalo limetokea karibuni hivi ili lifikiriwe kwa sala? (b) Katika kuwalinganisha watu walio katika mipango hiyo ya dawa zenye kulevya na wale walio katika namna nyingine za matabibu, ni tofauti gani kubwa zilizoko?

4 Leo, mazoea ya dawa zenye kulevya yamekuwa kama ugonjwa wenye kuambukia katika nchi nyingi. Kwa hakika mazoea hayo hayaruhusiwi katika kundi safi la Mungu.a Lakini namna gani wale watu ambao huenda wako katika mpango fulani unaoongozwa na serikali ambao kwa huo wanapewa kadiri ndogo za dawa (kama ile inayojulikana kama methadone) mahali pa kupewa dawa yenye hatari zaidi, kama heroin? Huenda watu walio katika mipango hiyo ya serikali wakasema kwamba hawafanyi jambo ambalo ni ‘haramu’; kwamba hawapotewi akili kama wakati wanapotumia dawa zenye kulevya; kwamba wanaweza kutenda kama ‘jamii ya wachunguzi.’ Namna gani ikiwa wanataka wawe washiriki waliokubaliwa na waliobatizwa wa kundi la ulimwenguni pote la mashahidi wa Yehova? Je! wakubaliwe kwa ubatizo?

5 Maulizo haya yametokea ili yafikiriwe kwa sala. Kulingana na maoni ya Biblia inaonekana kwamba hao walio katika mipango hiyo hawastahili kulingana na Maandiko, kwa kuwa huenda wakaonwa kwa kufaa kuwa bado wanazoea dawa zenye kulevya. Kwa kweli, kuna matumizi yanayofaa ya dawa zenye kulevya katika kutibu magonjwa ya viungo vya mwili. Lakini, kwa mfano, mtu anayetumia dawa methadone si sawa na mtu mwenye ugonjwa wa sukari aliye na ugonjwa wa viungo vya mwili, anayetaka dawa ya kuyeyusha sukari mwingi mno mwilini, au mwenye ugonjwa uliosedeka sana wa yabisi kavu au mtu aliye na donda baya anayepokea dawa ili kupunguza maumivu. Wenye ugonjwa wa sukari, ugonjwa wa yabisi kavu au wenye ugonjwa wa donda baya hawatumii dawa hizi ili wasipatwe na mabaya, hata yenye uchungu sana yanayotokana na kuacha mazoea ya dawa zenye hatari; wala hawaitumii dawa hii kuwa kama kitu cha kuwasaidia wapate usawa wa akilini na wa moyoni. Na, ijapokuwa huenda madaktari wakaagiza mtu apewe dawa za kutuliza ili apate kutulizwa au usingizi wakati wa shida, au kumtayarisha mgonjwa apate kupasuliwa kwa kumpa dawa za kuondoa maumivu, huku si sawa na kujifanya mtumwa wa kuzoea dawa zenye kulevya.

6, 7. Ijapokuwa labda ni ya halali, ni udhaifu gani mkubwa wa mipango hii, na hii inatokeza maulizo gani?

6 Uhalali wa kutumia dawa, kama methadone, katika mpango fulani wa serikali silo jambo lenye kuamua. Katika nchi nyingine huenda wenye kuzoea dawa zenye kulevya wakanunua heroin kwa halali kupitia kwa nyumba za serikali za dawa. Huku hakulifanyi liwe jambo linalofaa kulingana na Maandiko.

7 Kwa kawaida mipango hiyo ina kusudi la kutumia dawa moja mahali pa dawa nyingine, inayoonwa kuwa haidhuru sana kuliko dawa kama heroin tu. Hata hivyo sasa tunasoma katika magazeti juu ya dawa methadone kuwa ikiuzwa kama dawa nyingine zenye kulevya ambazo ni ‘haramu’ katika njia kuu za mji kwa wenye kuzoea dawa zenye kulevya. Watu wanaoendelea na mipango hii wanatafuta kuepuka au kuahirisha wasishughulike na magumu yao na kuyashinda, kuliko kupatwa na maumivu makali ya kuacha mazoea ya dawa zenye kulevya na kuishi bila kuzitumia. Jambo hili latokeza maulizo haya: Je! ubatizo wao ungekuwa wenye maana gani? Ungeonyesha nini?

8. Linganisha kutotaka kwa wenye kuzoea dawa waache mazoea hayo na matakwa ya Maandiko kwa wanafunzi wa Mwana wa Mungu.

8 Kristo Yesu alisema kwamba ye yote anayetaka kuwa mwanafunzi wake imempasa ‘auchukue mti wake wa mateso’ amfuate, akiwa tayari kupoteza hata uhai wake kwa ajili ya Kristo. (Luka 9:23, 24, NW; Yohana 12:25) Imempasa mtu afanye uamuzi huo wa moyo wote mbele ya kubatizwa. Ikiwa mtu yu tayari kuuchukua ‘mti wa mateso’ na ambaye angekuwa tayari kumfuata Yesu hata atundikwe mtini, je! hapo anaweza kusema kwamba hataki kuvumilia maumivu ya kuacha mazoea ya dawa zenye kulevya? (Linganisha Warumi 6:6; Wagalatia 5:25; Wakolosai 3:5.) Kwa kweli, maumivu yanayoletwa na kuacha mazoea ya dawa ni matokeo ya kawaida ya mazoea mabaya, ‘kuvuna ambacho kimepandwa.’​—Gal. 6:7.

9. (a) Ni maulizo gani yanayoulizwa kwa kufaa juu ya watu walio katika mipango hiyo ya dawa zenye kulevya wanaotaka kubatizwa? (b) Ni mfano gani ambao Mwana wa Mungu alituwekea katika jambo hili?

9 Basi, ‘kutubu na kugeuka’ kwa mtu na kuiacha njia yake ya zamani ya maisha kumekamilikaje? (Mt. 3:8; Matendo 26:20, NW) Ikiwa anaendelea kuwa mtumwa wa mazoea ya dawa zenye kulevya, yeye anawezaje kweli kujitoa kwa Mungu kama mtumwa wake kwa moyo wote, nafsi yote, akili na nguvu zote? (Marko 12:29, 30) Je! mtu aliye katika mpango huo ana imani kweli katika Neno la Mungu, kama linavyosema katika Wafilipi 4:6, 7, ambapo tunapata ahadi ya kwamba amani ya Mungu ‘itahifadhi mioyo yetu na nia zetu’ tukimwomba katika imani? Je! mtu huyo ataitumainia nguvu ya roho ya Mungu au ataitilia nguvu hiyo mashaka na mahali pake ategemee dawa fulani zenye kulevya zihifadhi moyo wake na nia yake ili asipoteze kujiweza mwenyewe? Ni wapi anapoonyesha “kujiweza” ambalo ni tunda la roho ya Mungu? (Gal. 5:22, 23, NW) Wakati wa kupigiliwa kwake misumari, Yesu alikataa kunywa “mvinyo iliyotiwa manemane,” kwa wazi alikataa kwa sababu aliazimia awe macho wakati alipotimiza ukamilifu wake katika mauti. (Marko 15:23) Katika njia hiyo alituwekea mfano wa kuitegemea nguvu ya Mungu itusaidie katika majaribu hayo yenye maana sana.

10, 11. Kwa sababu gani ni jambo linalofaa kutazamia wale wanaotaka kubatizwa kwanza washinde mazoea yao yo yote ya dawa zenye kulevya, na ni kwa sababu gani isingekuwa fadhili kuwakubalia wabatizwe wakati hawajafanya hivyo?

10 Hatukani kwamba si vigumu sana kushinda mazoea ya kutumia dawa zenye hatari, au kwamba wachache sana hawakuweza kufanya hivyo. Walakini, uhakika wa kwamba watu wachache wamefanya hivyo unaonyesha kwamba inawezekana. Uhakika wa kwamba watu wa ulimwengu wameweza kufanya hivyo unatoa sababu yenye nguvu kwa kusadiki kwamba wale wanaotaka kuwa wanafunzi wa kweli wa Mwana wa Mungu wanaweza kufanya hivyo vile vile. Kuliko kuacha utumwa wa kutumia dawa moja na kuwa katika utumwa wa kutumia dawa nyingine, kama methadone, imewapasa washindane na ugumu huu na kuutumainia msaada wa Mungu ili waushinde utumwa huo.

11 Kuwakubali watu wabatizwe mbele ya kufanya hivi kungekuwa kuwaachilia wasishindane na ugumu huu. Kwa kweli lisingekuwa jambo la msaada kwao, kwa maana mwishowe inawapasa washindane na ugumu huu na kusimama imara. Huenda upesi ukafika wakati mipango hiyo ya serikali itakapokuwa haipatikani kwao. Ikiwa watu wenye kuzoea dawa zenye kulevya wanakubaliwa sasa kama washiriki wa kundi, je! haielekei wakati fulani unaokuja watakuwa chanzo cha hatari sana au suto kubwa? Hata mbele ya wakati huo, je! haielekei kwamba kukubaliwa kwao kabisa katika kundi kutadhoofisha nguvu ya ndugu zetu wengine wa Kikristo wasiweze kupinga matumizi ya dawa zenye kulevya? Hatuwezi tukampendelea mtu mmoja na kuachilia mbali faida ya kundi zima.​—Gal. 5:9; 6:10.

MAONI YALIYOPATANA JUU YA MAZOEA YA TUMBAKO

12-14. Je! mazoea ya tumbako yanaweza kulinganishwa na mazoea mengine ya dawa zenye kulevya, na hili linatokeza ulizo gani?

12 Walakini, jambo hili latokeza ulizo juu ya upatano wa kuwakubalia watu ambao bado wanatumia tumbako wabatizwe. Wao vile vile ni watumwa wa kitu chenye kudhuru, kwamba ni kwa kuvuta, kutafuna ama kwa kunusa kama ugolo. Ebu angalia ambavyo ripoti katika Science World la Aprili 9, 1973, inavyosema:

13 “Dawa . . . inayofanyiza mazoea ni nicotine (sumu iliyomo katika tumbako). . . . Kwa muda wa dakika moja mbili hivi mtu akiisha kuvuta sigara, sumu yake inakuwamo ubongoni. Lakini akiisha kuvuta mara ya mwisho kwa dakika 20 kufika 30, karibu sumu yote imetoka katika ubongo ikaenda kwenye viungo vingine. . . . Karibu huu ndio wakati mvutaji anapohitaji sigara nyingine. . . . Sumu inapokuwa haipo, mwili unaitamani sana. Unaitamani sana hata mara nyingine mwili unakuwa mnyonge kwa sababu ya kuikosa. Dalili za kuacha kutumia sigara​—kujiona mnyonge​—kunaanza. . . . Nyingine za dalili hizi ni hali ya kusinzia, maumivu ya kichwa, machafuko ya tumboni, kutoka jasho, na kupiga kwa moyo kusiko kwa kawaida.”

14 Hata serikali za kilimwengu zimeona lazima zitoe maonyo makali juu ya hatari ya matumizi ya tumbako. Basi, je! watu ambao hawajaacha mazoea yao ya kutumia tumbako wanastahili kubatizwa?

15. Hata ingawa tumbako haitajwi katika Biblia, kanuni za Biblia zinatoaje jibu kwa ulizo hili?

15 Ushuhuda wa Maandiko unasaidia kuamua kwamba hawastahili. Kama ambavyo imeelezwa katika matoleo mengine ya gazeti hili, neno la Kigiriki phar·ma·kiʹa. lililotumiwa na waandikaji wa Biblia na likatafsiriwa “uchawi” lina maana ya msingi ya “matumizi ya dawa.” (Gal. 5:20; Ufu. 9:21) Neno hili likaja kuwa na maana ya mazoea ya uchawi kwa sababu ya ukamatano ulio kati ya matumizi ya dawa na uchawi. Hapo mwanzoni tumbako ilitumiwa vile vile katika njia hii na Wahindi wa Kiamerika. Kwa hiyo, tumbako inaweza kupangwa kwa kufaa katika jamii ya dawa zenye kulevya na zenye kuleta mazoea mabaya kama zile zilizotoa asili ya neno la Kigiriki phar·ma·kiʹa. Ile sumu iliyomo katika tumbako haina matokeo yale yale ya akilini na ya moyoni yanayofanyizwa na dawa zenye hatari zaidi kama heroin au zile dawa zenye kurusha akili kama LSD; hata hivyo mazoea ya tumbako kweli yanaharibu akili na yanaleta utumwa wenye nguvu. Mwishoni mwa Vita ya Ulimwengu ya Pili, mara nyingine sigara zilikuwa bora kuliko fedha katika Ulaya. Kulingana na ripoti, malaya walijiuza wenyewe ili wapate sigara chache, na watu wa kawaida walijinyima hata chakula makusudi wapate tumbako.

16. (a) Ziko sababu gani zenye nguvu kwa kuacha mazoea hayo mabaya? (b) Je! Mwanzo 1:29 unatoa sababu yo yote ya kuwaruhusu watumiaji wa tumbako?

16 Matokeo yenye kudhuru ya tumbako katika mwili yanajulikana sana na vile vile matokeo yake yenye kuchafua ni wazi. Bila shaka haionyeshi heshima kwa Muumba kwa kutupa uhai ikiwa tunaitumia ovyo na kuichafua miili yetu kwa mazoea ya kutumia tumbako. Madaktari wanaonya kwamba wanawake walio na mimba na wanaotumia tumbako wanaelekea zaidi sana kuharibikiwa mimba kuliko wengine, na hili, vile vile, lingeonyesha kutojali sana utakatifu wa uhai. Wavutaji wa tumbako hawawezi kujitetea wenyewe kulingana na Maandiko kwa kubisha kwamba Mungu aliumba tumbako na kwamba ni sehemu ya “mche” au mimea ambayo Mungu aliwapa wanadamu kiwe “chakula.” (Mwa. 1:29) Watumiaji wa tumbako hawaitumii kama “chakula” kwa kula majani yake kama mboga au kuipika kama vile “sukumawiki.” Hata, bali wanayatengeneza majani haya ndipo wakayatumia yakiwa makavu kwa kuvuta, kutafuna (bila kumeza maji yake), au kunusa kama ugolo ili wapate raha ya kimwili, na yote haya kwa kuharibu sana mwili na akili.

17-19. (a) Ni maulizo gani yenye kuchunguza ambayo imewapasa watu wenye mazoea ya kutumia tumbako wayafikirie ikiwa wanataka wabatizwe? (b) Mambo aya haya yangetumika kwa watu gani wengine wenye mazoea mabaya

17 Maulizo kama yale yaliyotolewa juu ya watu walio katika mipango ya serikali ya dawa yanaweza kuulizwa kwa njia iyo hiyo juu ya watu wanaozoea kutumia tumbako na ambao wanajitoa wenyewe ili wabatizwe. Je! kweli ‘wametubu na kugeuka,’ au wangali wana mazoea ambayo wao wenyewe wanajua kuwa ni tofauti na kanuni za Maandiko? (Rum. 6:19; 1 The. 4:7; 5:22) Katika 2 Wakorintho 7:1 mtume anasema hivi: “Basi, wapenzi wangu, kwa kuwa tuna ahadi hizo, na tujitakase nafsi zetu na uchafu wote wa mwili na roho, huku tukitimiza utakatifu katika kumcha Mungu.” Je! watumiaji wa tumbako wamelifikiria sana hili? Bila shaka wote watakubali kwamba watu watakaokuwa wakiishi katika taratibu mpya ya Mungu hawatakuwa na mazoea ya kutumia tumbako na kuhitaji vitasa vya kutemea mate na vitasa vya majivu ya tumbako na kuichafua hewa kwa moshi wa tumbako ili wengine wavute.

18 Hivyo, basi, je! haiwapasi wale ambao sasa wanazoea kutumia tumbako waache kuitumia kama ushuhuda wa kuonyesha kwamba wana imani na taratibu hiyo mpya iliyo safi na kwamba wanaipenda haki itakayopatikana humo? Ikiwa wanataka waonekane na Mungu kuwa ‘hawana mawaa wala aibu’ wakati wa kutekeleza kwake hukumu, je! si afadhali wasimame imara sasa kuliko kutumaini kwamba labda kuokoka kwao “dhiki kubwa” kungeleta mageuzi na kuwaondolea mazoea yao ya tumbako? (2 Pet. 3:11-14) Wakati “dhiki kubwa” inayokaribia itakapofanya tumbako ya biashara isipatikane, isingekuwa vyepesi zaidi wakati huo kuacha mazoea ya tumbako kwa sababu ya kulazimishwa na hali kuliko kufanya hivyo sasa kwa kutaka kumpendeza Mungu.

19 Linalosemwa juu ya tumbako lingetumika kwa nguvu ile ile juu ya matumizi ya mazao yenye kufanyiza mazoea yenye kudhuru katika mahali fulani, kama tambuu na majani ya mmea unaoitwa coca (mimea hii ina cocaine, sumu inayopumbaza akili).b

LAZIMA YA KUAMUA KABISA SASA

20, 21. Kwa sababu ya mambo haya, ni maoni gani yenye mkataa yanayochukuliwa sasa na mashahidi wa Yehova, na kwa sababu gani haya ni kwa faida hata ya wenye kuzoea dawa?

20 Kwa miaka mingi vitabu vya mashahidi wa Yehova vimeonya juu ya vitu hivyo vyenye kufanyiza mazoea mabaya kama tumbako. Watu wanaoshirikiana na makundi ya mashahidi wa Yehova wanajua sana ubaya wa mazoea haya. Basi, imewapasa wanaopendezwa hivi karibuni wasimame imara na wasiahirishe mambo kwa kuomba wabatizwe na kukubaliwa katika kundi, au washiriki katika kutoa habari jukwaani katika Majumba ya Ufalme yao, na huku wangali wana mazoea ya tumbako au mengine yenye kudhuru.c Kwa kuwa taratibu mpya inakaribia sana sasa, inapatana sana na Neno la Mungu kutoa maoni yetu kwamba wale wasiotaka kuyaacha mazoea yo yote haya yenye kudhuru hawastahili tuwabatize na kuwakubali kama washiriki waliokubaliwa wa kundi la Kikristo la Yehova.

21 Kwa hakika, kuwakubali watu hao katika kundi kungeweza kuwa kwa hatari kwao, kuzituliza dhamiri zao. Kukataa kuwakubali kunaweza kuwa baraka, kuwasaidie waone lazima sana ya kuamua kabisa na kujitayarisha wenyewe kwa maisha katika taratibu mpya ya Mungu. Kwa kushughulika na magumu haya mtu anapata ushindi wa haki unaoleta nguvu za kweli na kuutumainia uwezo na nia ya Mungu ya kusaidia.

22-24. (a) Ikiwa mtu alibatizwa akiwa bado ana mazoea hayo ya kutumia dawa, sasa imempasa afanye nini, na kwa sababu gani ni jambo linalofaa kumtazamia kufanya hivi? (b) Imeyapasa makundi yachukue mwendo gani juu ya watu waliobatizwa wasiotaka kuacha mazoea hayo ya dawa?

22 Basi, namna gani wale watu ambao zamani walibatizwa wakiwa bado wanatumia vitu vyenye mazoea mabaya kama tumbako, dawa nyingine zenye kulevya, au wale wanaopata matibabu fulani kama vile “mpango wa methadone” na wanaoendelea na mazoea hayo? Sasa wanaweza kupewa muda unaofaa, kama miezi sita, ili katika muda huo waache mazoea hayo mabaya. Kwa kufanya hivyo, wataonyesha kwamba wanatamani kwa unyofu wa moyo waendelee kuwa katika tengenezo safi la Yehova la watumishi walio wakf.

23 Bila shaka ikiwa mtu anaweza kupata maumivu makubwa yanayotokana na kuacha mazoea ya kutumia dawa zenye hatari zaidi ili awe mwanafunzi wa kweli wa Mwana wa Mungu, basi wazoevu wa tumbako au vitu kama hivyo hawana sababu nzuri ya kukataa kupata maumivu madogo zaidi yanayotokana na kuacha mazoea yao. Kukataa kufanya hivyo bila shaka kungemwekea mfano mbaya sana yule mtu anayejitahidi ashinde mazoea ya kutumia dawa zenye hatari zaidi na aliye na tatizo gumu zaidi sana.

24 Namna gani ikiwa watu waliokwisha kubatizwa hawataki kuacha mazoea yao ya kutumia dawa zenye kudhuru na zenye kutumikisha? Basi, kama Esau, wanaonyesha kwamba ‘hawaoni faida ya mambo matakatifu,’ wakipendelea zaidi mazoea hayo kuliko pendeleo la kuwa upande wa watu safi wa Yehova. Kwa hiyo wamepaswa waondolewe katika kundi kwa sababu ya mwenendo huo usiowafaa Wakristo.​—1 Kor. 5:7; Ebr. 12:15, 16, NW.

25. Je’ wale washiriki wa kundi wanaoacha sasa mazoea yenye kudhuru ni lazima wabatizwe upya?

25 Je! ingewalazimu wale wanaoacha mazoea yao ya kutumia tumbako au dawa nyingine zenye kudhuru wabatizwe upya? Hapana, hii haionekani kuwa ni lazima. Maarifa yanaleta daraka na yanaielimisha dhamiri. (1 Tim. 1:13) Kundi liliwafahamisha kwamba mazoea yao ‘hayakuwazuia,’ nao walibatizwa kulingana na ufahamu huo. (Matendo 8:36) Kwa kweli, mtu akiona kwamba alibatizwa akiwa na ‘dhamiri mbaya’ kwa sababu ya mazoea hayo, labda anaweza kuamua abatizwe upya. Huo ungekuwa uamuzi wake mwenyewe.

WAKATI WA HUKUMU ZA KIMUNGU

26. Jambo gani likumbukwe juu ya maamuzi ambayo yamefikiwa?

26 Labda kwa wengine maamuzi haya juu ya mambo ya kiroho na ya adili ya mashahidi wa Yehova wa Kikristo yataonekana kuwa makali sana. Lakini hii haionyeshi kwamba tunajaribu kutenda kwa namna ya kuhukumu. Kwa kweli ukali unatoka kwa Mungu, anayejisemea mwenyewe katika Neno lake lililoandikwa. Kwa sababu ya wakati ambao katika huo kizazi hiki cha wanadamu kinaishi, ndio wakati ambao imewapasa wale wanaotaka kumpendeza Mungu na kuingia katika taratibu yake mpya yenye haki inayokaribia waangalie sana usafi wa mwenendo.

27-29. (a) Kwa sababu gani mtume Petro, kama mshiriki wa Baraza Inayoongoza katika karne ya kwanza, aliona lazima ya kuwaandikia ndugu zake, na juu ya habari gani? (b) Ni ulizo gani zito lililoulizwa juu ya mtu ambaye angekubaliwa wakati wa hukumu ya Mungu?

27 Karne kumi na tisa zilizopita mtume Petro alikuwa mshiriki wa Baraza Inayoongoza ya kundi la Kikristo la karne ya kwanza C.E. Akiwa hivyo, aliyaandikia makundi ya watu wa Mungu barua za mashauri na maagizo. Petro alifahamu kwamba wakati huo kundi la Kikristo lilikuwa likiishi katika kipindi cha mwisho cha taratibu ya mambo ya Kiyahudi iliyokuwa juu ya Yerusalemu na hekalu lake. Yesu Kristo Bwana wake, alikuwa ametabiri kwamba mwisho huo ungetukia wakati wa muda wa kizazi hicho. (Mt. 23:36; 24:34) Ulikuwa wakati wenye hatari sana, zaidi kwa Wayahudi waliogeuka kuwa Wakristo, na vile vile kwa sababu kuteswa kwa Wakristo na Milki ya Kirumi kulikuwa karibu kutukie. Basi Petro aliona lazima ya kuwaandikia Wakristo wenzake.

28 Barua yake ya kwanza iliandikwa yapata mwaka wa 62-64 C.E., punde kidogo mbele ya kuasi kwa Wayahudi juu ya Milki ya Kirumi katika mwaka wa 66 C.E., kukifuatana na mwisho wa Yerusalemu wa Kiyahudi na hekalu lake katika mwaka wa 70 C.E. Petro alijua kwamba kufa kwake kulikuwa kunakaribia, naye aliona lazima awaonye Wakristo wenzake juu ya kuandamana na walimwengu wasio Wakristo “katika ufisadi [wao] ule ule usio na kiasi.” Ili akazie haraka ya kuepuka mwendo huo wenye kuharibu hata kwa kupata mateso, Petro alionyesha kumalizika kwa wakati kwa kuandika hivi: “Lakini mwisho wa mambo yote umekaribia; basi, iweni na akili [si kurushwa na dawa zenye kulevya ili kuepuka matukio], mkeshe katika sala.” (1 Pet. 4:4-7) Shauri hili lilifanywa kuwa zito zaidi, kwa sababu hukumu ya kimungu ilikuwa imekwisha kuanza juu ya kundi la Kikristo. Ni akina nani ambao wangeonekana kuwa wenye kukubalika chini ya uchunguzi wa kimungu? Si wazembe, si wale waliozifuata njia za ulimwengu za ufisadi, si wale waliojiingiza kwa makusudi katika mambo yasiyo ya Kikristo yaliyoupatia mwili wenye dhambi raha. (Mit. 1:32, 33) Mtume Petro aliandika hivi:

29 “Ikiwa [yeye anateswa] kwa sababu ni Mkristo asione haya, bali amtukuze Mungu katika jina hilo. Kwa maana wakati umefika wa hukumu kuanza katika nyumba ya Mungu; na ikianza kwetu sisi [nyumba ya Mungu], mwisho wao wasioitii injili ya Mungu utakuwaje? Na mwenye haki akiokoka kwa shida, yule asiyemcha Mungu na mwenye dhambi [aliye ndani ya kundi la Kikristo] ataonekana wapi? Basi wao wateswao kwa mapenzi ya Mungu na wamwekee amana [nafsi] zao, katika kutenda mema, kama kwa Muumba mwaminifu.”​—1 Pet. 4:16-19.

30. Kwa sababu gani ni jambo lenye hatari sana kwa Mkristo aliyebatizwa kuchukua mfano wa “asiyemcha Mungu” na wale ‘wanaofanya dhambi’ kwa kadiri yo yote, zaidi katika wakati huu?

30 Mfuasi mwaminifu wa Yesu Kristo ‘anaokoka kwa shida’ hata anapoendelea kuwa “mwenye haki” ndani ya kundi la Kikristo. Ikiwa Mkristo aliyebatizwa angefuata mfano wa mtu “asiyemcha Mungu” na “mwenye dhambi” kwa kadiri yo yote, wokovu wake ungefanywa kuwa wa shida zaidi. Au je! yeye angeonekana kustahili wokovu kwa vyo vyote? Hili ni jambo ambalo inawapasa Wakristo wakumbuke leo. Bila shaka kwa habari ya kizazi chetu inaweza kusemwa kwa kweli hivi: “Mwisho wa mambo yote umekaribia.” Hukumu za Mungu juu ya “nyumba” yake mwenyewe ya waabudu zinaendelea sasa. Hii ilitajwa katika unabii wa Malaki, sura ya tatu, unaotuambia juu ya kuja kwa Yehova kwenye hekalu lake la kiroho, akiandamana na Yesu Kristo kama “mjumbe wa agano.” Ni juu ya nani Hakimu wa kimungu, Yehova, atatoa ushuhuda kama juu ya wavunjaji wa sheria na wenye dhambi? Katika Malaki 3:5 anatuambia hivi:

31-33. (a) Malaki 3:5 anasemaje juu ya hatari ya wale ambao sasa ni watumwa wa dawa zenye mazoea mabaya? (b) Ni ushuhuda gani mwingine unaoonyesha ukamatano ulio kati ya mambo ya mizimu au uchawi na matumizi ya dawa zenye kulevya?

31 “Nami nitawakaribieni ili kuhukumu; nami nitakuwa shahidi mwepesi juu ya wachawi [phar·ma·kousʹ​—kulingana na Septuagint ya Kigiriki], na juu ya wazinzi, na juu yao waapao kwa uongo; na juu yao wamwoneao mwenye kuajiriwa, kwa ajili ya mshahara wake, wamwoneao mjane na yatima, na kumpotosha mgeni asipate haki yake, wala hawaniogopi mimi, asema [Yehova] wa majeshi.”

32 Fahamu kwamba wale wa kwanza ambao Yehova anawataja kuwa ndio shahidi wake mwepesi ataanzia kufikia kwa habari ya ubaya wao ni “wachawi.” Septuagint Version ya Kigiriki, kama ilivyotafsiriwa na Wayahudi wa Alexandria mbele ya Kristo, ilitafsiri “wachawi” kwa neno la Kigiriki phar·ma·kousʹ. Hili ndilo neno lile lile linalotumiwa katika Ufunuo 21:8, ambapo watafsiri wengine wanalitafsiri kama “wachawi,” lakini New World Translation inalitafsiri kama “wale wanaozoea mambo ya mizimu.” Kwa kweli wachawi wa kale walizoea mambo ya mizimu. Neno la Kigiriki linalotumiwa kwao linamaanisha “watumiaji wa dawa,” si wauzaji wa dawa (druggists au pharmacists). Wachawi wa kale walikuwa ndio watumiaji wa dawa zenye kulevya wakati huo.

33 Septuagint Version ya Kigiriki ya wakati uliotangulia Ukristo inatumia neno la Kigiriki pharʹma·kon linalokamatana na hilo (maana yake ya kweli ni “dawa zenye kulevya,” lakini linatafsiriwa kama “uchawi”) mara zisizopungua tano. Malkia Yezebeli mwabudu sanamu wa Israeli wa kale alizoea phar’ma.kon hiyo au “uchawi.” (2 Fal. 9:22, LXX) Aliuawa na Mfalme Yehu aliyekuwa akitenda kama mfishaji wa Yehova. Wale waliosaidia “wachawi” au wenye kuzoea mambo ya mizimu vile vile walishiriki mazoea ya mizimu na walilaumiwa.

34-36. (a) Kwa sababu gani ni jambo linalofaa kwamba mazoea hayo yahukumiwe sasa? (b) Basi ni daraka gani lililo juu ya wale wanaotumikia kama wachungaji kati ya kundi la Mungu?

34 Basi, si ajabu sana kwamba katika siku hizi ambazo mazoea mabaya ya kutumia dawa zenye kulevya na matumizi ya tumbako yameenea mahali pote na kuongezeka, imewapasa wale wenye kuzoea vitu hivi wahukumiwe. Yehova Mungu, Hakimu Mkuu kuliko wote, yu katika hekalu lake la kiroho na zaidi anawachunguza wale wanaojidai kumwabudu yeye katika mahali hapo patakatifu. Yeye ameahidi kuwa shahidi mwepesi juu ya wachawi au wenye kuzoea mambo ya mizimu, ambayo tangu nyakati za kale yalikamatana na dawa zenye kulevya, zenye kuleta mazoea mabaya na kutumikisha.

35 Je! sisi tunataka Yehova Mungu awe shahidi mwepesi juu yetu kama wazoevu wa dawa zenye kulevya au dawa nyingine zenye mazoea yenye kudhuru, vitu vinavyotuweka katika hali ya kupagawa na mashetani? Hukumu ya Yehova juu ya wazoevu hao wakati wa “dhiki kubwa” inayokuja itakuwa na maana ya uharibifu wao. (Ufu. 21:8) Bila shaka, Yehova Mungu hawataki watu hao wenye kuzoea dawa wawemo kati ya kundi la mashahidi wake wa Kikristo sasa katika huu “mwisho wa taratibu ya mambo.” Juu ya “Yerusalemu mpya,” Ufunuo 22:15 unasema hivi: “Huko nje wako mbwa, na wachawi [watumiaji wa dawa, tafsiri ya Kingdom Interlinear], na wazinzi, na wauaji, na hao waabuduo sanamu, na kila mtu apendaye uongo na kuufanya.”

36 Kwa hiyo, maagizo haya yanatolewa kwa kujiona kuwa na daraka kubwa kwa Yehova Mungu. Kwa hiyo ni wajibu wa wazee, kama waangalizi wa kundi la Mungu, kuhakikisha kwamba watu hao wasiotakiwa hawakubaliwi kama washiriki waliobatizwa wa makundi ya mashahidi wa Yehova wa Kikristo.

​—Kutoka The Watchtower, June 1, 1973.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa mazungumzo kamili juu ya mafundisho ya Biblia juu ya jambo hili, tazama Mnara wa Mlinzi wa Septemba 15, 1973

b Kwa habari zaidi juu ya dawa hizo, tazama Mnara wa Mlinzi wa Aprili 1, 1973, kur. 156-159.

c Tazama Organization for Kingdom-preaching and Disciple-making, ukur. 98, fu. 5.

[Picture katika ukurasa wa 544]

Kwa watu wengi katika ulimwengu, kuvuta tumbako ndiyo raha yao. Lakini je! ni njia ya Kikristo?

[Picha katika ukurasa wa 546]

Ikiwa mtu anataka awe shahidi wa Yehova aliye wakf na kubatizwa, ni lazima aepuke matumizi ya tumbako

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki