“Mkafanye Wanafunzi, Kuwabatiza”
“Mamlaka yote nimepewa mimi mbinguni na duniani. Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi. Na, tazama! mimi niko pamoja na ninyi siku zote mpaka mwisho wa taratibu ya mambo.”—Mt. 28:18-20, NW.
1. Nani walioisikia amri ya Yesu ‘kufanya wanafunzi kuwabatiza?
YESU KRISTO aliyasema maneno hayo juu ya mlima katika Galilaya kufuata kifo chake na ufufuo. Yalisikiwa na wanafunzi wake, akiwamo Mathayo, aliyeyaandika kwa faida yetu. Haijulikani ni wangapi wa wanafunzi wa Yesu waliomsikia akitoa amri hii. Mitume kumi na mmoja waaminifu walikuwapo, lakini huenda walikuwako wengine wengi. (Mt. 28:16) Wanafunzi wengi wa Biblia wanaamini kwamba wale mia tano wanaotajwa na mtume Paulo kama wakimwona Yesu kwa kipekee wakati fulani nyuma ya ufufuo wake walipaswa kuwa katika Galilaya kwa maana huko ndiko Yesu alikokuwa na wanafunzi wengi. (1 Kor. 15:6) Wengine wanadhani kwamba maneno ya Yesu katika Mathayo 28:10, “Enendeni, mkawaambie ndugu zangu waende Galilaya, ndiko watakakoniona,” yalisemwa kwa zaidi ya wale mitume kumi na mmoja waaminifu. Lakini, kwa habari hiyo hatuna hakika.
2. Kwa sababu gani amri ya Yesu ilikuja katika wakati unaofaa, nayo iliwafungulia wanafunzi wake nini?
2 Hata hivyo, ni hakika kwamba Yesu Kristo alifufuliwa na kulikuwako mashahidi wa kuhakikisha kwamba aliwaamuru wafuasi wake waende na kufanya wanafunzi, wakiwabatiza. Maneno haya ya Yesu yalikuja katika wakati wenye kufaa sana, wakati ambapo wanafunzi wake walikuwa wakihitaji uongozi juu ya walilopaswa kufanya. Amri ya Yesu iliwafungulia mbele yao kazi kubwa ya kuelimisha na ya mpanuo ambayo ingefanywa katika mataifa yote. Lo! walisisimuka kama nini kwa kupata amri hiyo iliyoambatana na uhakika wa kwamba Yesu Kristo mwenyewe angewategemeza katika utendaji huu mkubwa wa ulimwenguni pote!
3. (a) Kwa sababu gani isingewezekana uwepo ufahamu wenye makosa juu ya lililopaswa kufanywa? (b) Nini mwanafunzi?
3 Je! ingewezekana uwepo ufahamu wenye makosa juu ya kazi ambayo Kristo Yesu alisema ingefanywa na wafuasi wake wa kweli mpaka mwisho wa taratibu ya mambo? Haiwezekani. Kwa maana watu waliomsikia akisema walikuwa wanafunzi wake. Wao walijua kwamba mwanafunzi ni mtu anayejifunza au anayefunzwa. Kwa hiyo lazima wafundishe wengine wawe wafuasi wa Kristo kama vile wao walivyokuwa.
4. Ukitaja Yohana 1:35-42, onyesha namna Andrea na Simoni walivyokuwa wanafunzi wa Yesu.
4 Wanafunzi wa kwanza wa Yesu walifundishwa na Yohana Mbatizaji, aliyewatayarisha kuwa wanafunzi wa Yesu. Andrea alikuwa mmoja wa wale wanafunzi wa Yohana Mbatizaji aliyejulishwa kufundisha kwa Yesu na Yohana mwenyewe. Nyuma ya Andrea kutumia wakati fulani akimsikiliza Yesu, alilieneza neno kwa nduguye, Simoni, ambaye vile vile akawa mwanafunzi na mtume wa Yesu Kristo.—Yohana 1:35-42.
5. Kulingana na Yohana 1:43-51, Filipo na Nathanaeli walipataje kuwa wanafunzi?
5 Filipo alikuwa mwingine ambaye, mapema katika huduma ya Yesu, alijifunza namna ya kuwa mfuasi wa Yesu Kristo. Mara tu Filipo alipokuwa mwanafunzi alionyesha roho inayofaa ya kutaka kuwaambia wengine habari njema, na kwa hiyo akafanya Nathanaeli apendezwe kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo.—Yohana 1:43-51.
6. (a) Yesu, mapema katika huduma yake, alionyeshaje kwamba alikusudia wanafunzi wake wafanye watu wengine kuwa wanafunzi? (b) Walikuwa wanatayarishwaje kufanya kazi hiyo?
6 Hakuna shaka kwamba Yesu alikusudia tangu mwanzo wa huduma yake ya kidunia kazi ya kufanya wanafunzi iendelezwe na wafuasi wake. Hiyo ndiyo iliyokuwa maana ya maneno yake kwa Andrea na Petro waliokuwa wakivua samaki katika Bahari ya Galilaya: “Nifuateni, nami nitawafanya kuwa wavuvi wa watu.” (Mt. 4:19) Yakobo na Yohana ni wavuvi wengine wa samaki walioziacha mashua zao wamfuate Yesu na wao wenyewe wakasikia kufundisha kwake na kuhubiri, vile vile wakiiona miujiza aliyoifanya. (Mt. 4:21-23) Kwa hiyo kwa ushirika wao na Yesu walijifunza namna ambavyo wanafunzi wanafanywa. Wa kwanza walimwona Yesu akikaribisha wengine wawe wafuasi wake, kama, kwa mfano, Mathayo, aliyeacha kutoza kodi ili awe mfuasi, nao walifaidika kutokana na njia za kufundisha alizotumia Yesu.—Mt. 9:9.
7. (a) Yesu aliona ni wapi palipofaa kufundishia vikundi vya watu? (b) Ni mengine gani ya mambo aliyoyafundisha Yesu kama yalivyoandikwa katika Mathayo sura ya 5? katika Mathayo 6? katika Mathayo 7?
7 Kuambia watu waliokusanyika pamoja juu ya makusudi ya Mungu ni hatua ya kuelekea kufanya wanafunzi iliyotumiwa na Yesu. Habari za Injili zinataja nyakati nyingi wakati Yesu aliposema kwa vikundi au makundi. Yeye alihubiri katika miji na vijiji, katika masinagogi, po pote watu walipopatikana. (Mt. 9:35) Alizungumza katika pwani. (Mt. 13:1) Mathayo mwenyewe alivutwa sana na mahubiri aliyoyatoa Yesu katika upande ya kilima karibu na Kapernaumu, mji ambamo Mathayo alikuwa alipokaribishwa awe mfuasi wa Yesu. Mahubiri haya yameandikwa katika Mathayo 5:3 mpaka 7:27 nayo ni mfano wa kutokeza wa kufundisha kwa Yesu watu washike amri. Zile heri tisa zinaonyesha mambo ambayo imewapasa wanafunzi watafute, ambayo imewapasa kujua na ambayo imewapasa kufanya. Yesu alitia ndani habari kama uzinzi, talaka, kupenda adui za mtu, namna ya kusali, namna ya kuyaona mambo ya kiroho yakilinganishwa na mambo ya kimwili, namna ya kushughulika na wengine, maana ya kuifuata njia nyembamba ielekezayo kwenye uzima, sababu gani lazima watokeze tunda jema na maana ya kujenga juu ya msingi imara, wa kiroho kwa kufanya alivyosema Yesu. Lo! kilikuwa kipindi cha maagizo kama nini na lo! ni mfano kama nini wa namna ambavyo kazi ya kufanya wanafunzi inaweza kufanywa kwa kusema na makundi ya watu kama vile katika hotuba ya watu wote!
8. (a) Yesu aliyafundishia wapi yaliyoandikwa katika Luka 4:16-21, na je! mara nyingi alifundishia mahali kama hapo? (b) Kulingana na Yohana sura ya 5, ni mengine gani kati ya mambo aliyoyafundisha Yesu wakati wa sikukuu? (c) Taja mambo fulani aliyoyasema Yesu katika hekalu, kama yalivyoandikwa katika Mathayo sura ya 22.
8 Masinagogi ni mahali ambapo watu kwa kawaida walikusanyika kusudi wasikilize, kwa hiyo Yesu alihubiri na akafundisha katika masinagogi. (Mt. 9:35; 13:54; Luka 4:16-21, 44;6:6) Vile vile aliyatumia kwa faida makusanyiko makubwa zaidi ya watu wa Mungu wa agano katika nyakati za sikukuu kwa kuhubiri na kufundisha. (Yohana 5:1, 19; 7:14; 10:22-30) Ilikuwa kawaida ya makundi kukusanyika katika hekalu katika Yerusalemu, naye Yesu hakuipoteza nafasi ya kufundisha humo. (Mt. 21:23–23:39) Hivyo alijulikana mahali pote kama Bwana au Mwalimu.
KUFANYA WANAFUNZI KATIKA NYUMBA
9. Kwa sababu gani ilifaa Yesu azungumze na watu katika nyumba zao?
9 Bwana mkuu alijua namna ya kusema na watu katika nyumba zao na kwa njia hiyo aliwapa wengi nafasi ya kuwa wanafunzi wake. Je! kunapo mahali bora ambapo mtu aweza kujifunza kutoka kwa mwalimu anayetembelea? Pana nafasi kubwa ya faragha na mtu anaweza kusema mambo bila ya kusumbuliwa kutoka nje. Wanafunzi wa Yesu waliona namna Yesu alivyotumia nyakati kwa faida akiingia katika nyumba za watu na humo kuwafundisha.
10. (a) Ni kazi gani ya kufundisha aliyoifanya Yesu katika nyumba moja katika Bethania? (b) Yesu alifundishaje uhitaji wa imani kwa habari ya kifo cha Lazaro?
10 Katika Bethania, Martha alimkaribisha Yesu nyumbani, jambo lililofanya ifae kwa Martha, Mariamu na Lazaro wajifunze kutoka kwa Yesu. Yesu alifanya wafahamu kwamba mambo ya kiroho ni ya maana zaidi kuliko yale ya kimwili, akisema kwamba “Mariamu amelichagua fungu lililo jema” kwa kulisikiliza neno lake. Wakawa waamini, waliojawa na imani. Nyumaye, wakati wa kifo cha Lazaro, Martha alikubali waziwazi, “Naam, Bwana, mimi nimesadiki ya kwamba wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu, yule ajaye ulimwenguni.” Imani hiyo inayo thawabu yake, naye Yesu alifanya mwujiza mkubwa huko wa kumfufua Lazaro kutoka kwa wafu. Kwa kuona hili wanafunzi walipata mwonjo wa ufufuo ambao ungetukia wakati ujao. Lo! ni onyesho lenye kuimarisha imani kama nini kwa wanafunzi wote huko kujionea wenyewe!—Luka 10:38-42; Yohana 11:19-27.
11. Kwa sababu gani Yesu alikwenda nyumbani kwake Zakayo, na ni mengine gani kati ya mambo aliyoyafundisha humo?
11 Mtu mwingine aliyepokea maagizo ya Yesu nyumbani kwake ni Zakayo wa Yeriko. Kwa kufundisha huko Yesu alisitawisha imani ambayo ingeongoza watu wa nyumba hiyo kwenye wokovu, kwa maana alisema: “Leo wokovu umefika nyumbani humu . . . Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea.” Sehemu ya kilichotukia na aliyofundisha humo juu ya ufalme wa Mungu imeandikwa katika Luka 19:1-27.
12. Kulingana na Marko 7:17-23, Yesu alieleza nini kwa wanafunzi wake kwa faragha katika nyumba?
12 Mara nyingi wanafunzi wenyewe waliuliza maulizo nao wakapokea habari zenye maana walipokuwa nyumbani. Mifano ya hii inapatikana katika Mathayo 17:25-27, ambapo wanafunzi walijua kwa sababu gani zimepaswa kodi zilipwe. Vile vile katika Marko 7:17-23, ambapo waliomba maelezo juu ya mfano aliokuwa ametumia Yesu, na katika Marko 10:10-12, ambapo walijifunza mengi zaidi juu ya ndoa na talaka.
13. Yesu aliwaamuruje wanafunzi wake wakaseme na watu katika nyumba zao?
13 Yesu alipowatuma wanafunzi wake wakauhubiri ujumbe wa Ufalme katika miji na vijiji, aliwaambia wakajitafutie wenyewe mahali pa kulala katika nyumba za mahali walikokwenda. Walipokuwa nyumbani wanafunzi walisema na watu, kwa maana Yesu alisema: “Mtu asipowakaribisha wala kuyasikiliza maneno yenu, mtokapo katika nyumba ile, au mji ule, kung’uteni mavumbi ya miguuni mwenu.” Walipaswa wakae mahali ambapo watu wangeyasikiliza maneno yao juu ya Ufalme tu. Kwa wazi wenye nyumba wengine walisikiliza na wakawa wanafunzi na wengine waliikataa nafasi ya kujifunza. (Mt. 10:7-14; Luka 10:1-7) Kwa hiyo kwa mfano wa Yesu na vile vile waliyoyaona wenyewe wanafunzi walijifunza namna ambavyo wengine wangeweza kufanywa wanafunzi kwa faragha katika nyumba zao.
KUFUNDISHA KWA KUSEMA MBELE YA WAKUU
14. Toa mifano ya aliyoyasema Yesu mbele ya wakuu.
14 Wanafunzi wa Yesu walikuwa mashahidi wa mambo mengi yaliyosemwa kwa waandishi, Mafarisayo, makuhani na watawala. Kwa mfano, maneno ya Yesu kwa wengine wa watu wale waliotoka Yerusalemu, kama yalivyoandikwa katika Mathayo 15:3-11, yalitofautisha amri za Mungu na mapokeo ya wanadamu; wanafunzi walijifunza amri za Mungu zimepaswa zionwe kwa muhimu gani. Luka 15:1-10 anaonyesha Yesu akisema kwa mifano kwa Mafarisayo na waandishi juu ya kondoo aliyepotea na shilingi iliyopotea, lakini kwa faida ya wafuasi wake mwenyewe. Wanafunzi walijifunza Yesu alipokuwa akisema na Masadukayo juu ya ufufuo. (Luka 20:27-40) Yohana 18:19-37 anasema juu ya namna Yesu alivyosema kwa wakuu wa makuhani na gavana, ambayo kutokana nayo walijifunza si namna ya kusema na wakuu tu lakini vile vile namna matendo yao yalivyotiwa ndani na uhakika wa kwamba Ufalme si sehemu ya ulimwengu huu. Na kunayo mifano mingine zaidi katika maandishi ya Injili. Wafuasi wake vile vile walikusudiwa waseme mbele ya wakuu.—Mt. 10:17, 18.
MIKUTANO YA KUFUNDISHA WANAFUNZI AMRI ZAKE
15. Simulia wakati fulani Yesu alipofanya mkutano na kuwafundisha wanafunzi wake.
15 Mitume walioshirikiana sana na Yesu waliweza kujifunza kutoka kwake katika nyakati nyingi alipowakusanya pamoja mahali fulani. Kipindi cha maagizo kilichoandikwa katika Mathayo sura ya 10 kinaweza kuitwa mkutano wa utumishi ambapo Yesu aliusimamia. Mathayo 13:36 anatuambia juu ya mkutano wa kuelezea mifano fulani. Marko 9:1-13 anatoa mfano wa kikundi kidogo kilichokusanyika kwa ajili ya maagizo ya pekee juu ya wakati ujao, Petro, Yakobo na Yohana walipokuwa wakiona njozi ya kugeuka sura na nyumaye wakapata maneno fulani yenye kueleza juu ya Eliya. Mkutano ulifanywa juu ya Mlima wa Mizeituni, ambapo Yesu alijibu ulizo lao juu ya ‘ishara ya kuwako kwake na ya mwisho wa taratibu ya mambo.’ Leo, wafuasi wa Yesu wanafaidika kutokana na habari ile ile wanaposhiriki katika kuitimiza amri yake kuzihubiri habari njema za Ufalme katika dunia yote inayokaliwa na wanadamu.—Mt. 24:3-14, NW.
16. Yesu alipowafundisha wanafunzi wake kukishika chakula cha jioni wakiadhimisha kifo chake, ni mengine gani ya mambo aliyowafundisha katika mkutano huo, kama yalivyoandikwa katika Yohana sura za 13 mpaka 17?
16 Katika chumba cha orofani katika Yerusalemu ulikuwako mkutano wenye kutia imani nguvu Yesu alipozungumza na mitume wake waaminifu waliokuwa wamekusanyika kwa ajili ya siku ya Kupitwa ya mwisho yenye maana. Alianza mwadhimisho wa chakula cha jioni, kukumbuka kifo chake. Wakati huo Yesu alitoa amri mpya inayojulisha walio Wakristo wa kweli, yaani, kwamba wawe na upendo kati yao wenyewe. (Yohana 13:34, 35) Hii ilifuatwa na ambayo Yohana anaandika katika sura za 14 mpaka 17 za habari yake ya Injili, akionyesha mambo machache juu ya namna wale wampendao Kristo wanavyozishika amri zake, namna ambavyo wangeweza kuzaa matunda mengi kama matawi ya mzabibu, kwamba wao si sehemu ya ulimwengu na wangechukiwa na kuteswa kama alivyofanyiwa Yesu, kwamba roho takatifu ingekuja kama msaidizi, na mengine mengi. Si kwamba tu wakati huo sala ya Yesu ilikuwa yenye kutia nguvu moyoni, lakini ilikuwa yenye kufundisha sana vile vile. Iliwaonyesha kwamba wangekuwako wengine (wanafunzi wapya) ambao wangetia imani katika Yesu kwa sababu ya maneno yaliyosemwa na wanafunzi waaminifu, na kwamba imewapasa wote wawe wameungana pamoja. (Yohana 17:20, 21) Hivyo Yesu aliwaonyesha nyingine za amri zake alizojua nyumaye zilipaswa zifundishwe watu wa mataifa yote katika kazi kubwa ya kufanya wanafunzi.
WALIJUA LA KUFANYA
17. (a) Ni mfano gani alioutoa Yesu kwa kazi ya kufanya wanafunzi? (b) Toa mfano kutoka Matendo ya Mitume kuonyesha namna wanafunzi walivyotumia njia za kufanya kazi zinazofanana na zile za Yesu.
17 Yesu alitumia namna zote za mahali na njia kutimiza kazi ya kufanya wanafunzi, akizikumbuka desturi za watu na mahali ambapo wangekuwa wamekusanyika pamoja na kusikia mambo. Po pote alipopata nafasi, waziwazi ama faraghani, Yesu alizungumza kweli kwa watu na kuiacha nuru iangaze, kwa matokeo ya kwamba wengine wakawa wanafunzi. Maandishi marefu ya kazi ya kufanya wanafunzi iliyofanywa na Yesu na namna alivyowafundisha wanafunzi wake kuzishika amri zake yanatuhakikishia kwamba mitume walifahamu alichomaanisha Yesu alipowaambia ‘wakafanye wanafunzi.’ Aliwawezesha kuuiga mfano wake kwa kuongoza katika kazi: “Ikawa Yesu alipokwisha kuwaagiza wanafunzi wake kumi na wawili, alitoka huko kwenda kufundisha na kuhubiri katika miji yao.” (Mt. 10:5–11:1) Matendo ya Mitume kina habari ya kutokeza ya utendaji wa kufanya wanafunzi wa wengi wa wafuasi wa Yesu.Wao walizieneza habari njema kwa njia zote zilizofaa katika Milki ya Kirumi yo Matendo 1:8; 16:30-34.
18. Kwa maana wale waliokuwa katika kazi ya kufanya wanafunzi katika karne ya kwanza walitumia njia zilizofaa siku zao, ni njia gani nyingine zinazofaa ziwezazo kutumiwa kufanya wanafunzi katika karne hii?
18 Sasa katika nyakati za kisasa lazima kazi ya namna ile ile ifanywe nasi vile vile twajua namna ya kuifanya. Tunazo habari za huduma ya Yesu na namna wanafunzi walivyotimiza kazi ya kufanya wanafunzi kwa matokeo mazuri katika karne ya kwanza ya wakati wetu. Leo nasi vile vile tu wenye busara na tumetumia uwezekano wote wenye matokeo kwa kuzieneza habari njema kusudi tufanye wanafunzi, kutia na misaada ya kisasa kama vile vitabu, vifaa vya kukuzia sauti vinavyotumia umeme kwa ajili ya mikutano mikubwa, kutangaza kwa radio, simu, picha, kurekodi, na mingine kama hiyo. Lakini, mojawapo ya njia zetu zenye matokeo zaidi ya kufanya wanafunzi ni kwa kwenda nyumba kwa nyumba, kutafuta watu wanaopendezwa na kupanga kujifunza Biblia pamoja nao kwa faragha katika nyumba zao wenyewe. Zaidi ya hayo, watu wanasemwa nao wanaposafiri, katika mahali pa kazi, wakati wa chakula cha mchana, katika bustani, katika njia kuu, shuleni, au po pote zinapopatikana nafasi. Wakiwa na njia nyingi sana mbalimbali zilizo wazi kushiriki katika kuutoa ushuhuda, Wakristo wote wanaweza kupata njia ya kushiriki. Nyakati nyingine kazi ya kufanya wanafunzi ni jitihada yenye ushirikiano ya zaidi ya mtu mmoja, kama vile ilivyokuwa katika karne ya kwanza wakati Paulo alipoeleza kwamba yeye ‘alipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu.’—1 Kor. 3:6.
19. Ni ushuhuda gani kwamba Yehova Mungu ameyabariki matumizi ya njia hizi nyingi za kufanya wanafunzi?
19 Baraka ya Yehova Mungu ikiwa juu ya utendaji huu wa kufanya wanafunzi, kazi sasa imeenea kwenye nchi 208 ulimwenguni kote, kwa watu wa mataifa yote, nayo hesabu ya wale wanaoshiriki katika kazi imeongezeka kuwa zaidi ya mashahidi wa Kikristo wa Yehova 1,650,000.—Mt. 24:14.
[Picha katika ukurasa wa 491]
Yesu aliwaambia wengine juu ya Mungu katika nyumba za faragha na mahali pa watu wote, kama wakati Yesu alipokutana na mwanamke kisimani katika Samaria