Kwa Sababu Gani Iliandikwa Vile?
“Unifahamishe nami nitaishika sheria yako, naam, nitaitii kwa moyo wangu wote.”—Zab. 119:34.
1. Je! uhitaji wa kutiwa moyo ni ugumu wa kawaida, na mara nyingi kutiwa moyo huko kwaweza kupatikana wapi?
JE! WEWE hukuona kwamba mara nyingi unapohitaji kutiwa moyo, kweli kutoka kwa ghala ya Mungu, Biblia Takatifu, zimekupa nguvu za kushindana na majaribu na magumu ya kipekee? Inaelekea kuwa sote tumepatwa na jambo hili katika maisha zetu kama Wakristo.
2. Ni kuvunjika moyo gani walikoshindana nako mashahidi wengi wa Yehova kwa miaka mingi, nao wamewezaje kusimama imara walipokutana nako?
2 Kwa mfano, wengi leo wamepitia katika vipindi vya kuvunjika moyo wakati ambapo wapinzani wamezungumza kwa kuwadharau watu wa Mungu na hata kukimbilia jeuri kwa sababu ya kuwa kwao mashahidi wa Kikristo wa Yehova ambao wameitegemeza kweli. Wengi ambao wamekuwa wakishirikiana na Ukristo wa kweli kwa miaka 50 au 60 wanayakumbuka vizuri maneno ya uadui na matendo ya majirani na wengine mnamo Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, na nyuma ya hapo, kwa mashahidi wa Yehova. Ni mara ngapi wengi waliitwa wafuasi wa Russell na “Millennial Dawners”! Wengine walipigwa, wakapakwa lami na kufunikwa kwa manyoya, wakafungwa, wakatukanwa, wakapigwa mijeledi na kutemewa mate. Wakipitia katika yote, mashahidi wa Yehova wa Kikristo wameendelea kuifanya kazi iliyoamriwa na Mungu wao, Yehova. Wamewezaje kufanya hivyo? Sababu moja ni ufahamu, kutiwa moyo na nguvu walizozipata kutoka kwa Neno la Mungu na kutoka kwa vitabu vinavyochapwa na “mtumwa mwaminifu mwenye akili” katika siku hizi za uovu.
3. Imeyapasa maoni yetu yawe nini tunapoisoma Biblia?
3 Na, kwa kweli, hilo ndilo kusudi la Neno la Mungu, kuwajenga watumishi wa Yehova. Kwa sababu hiyo mtu anapovisoma vitabu mbalimbali vya Biblia imempasa akumbuke habari ya msingi ya kitabu na mwandikaji wake. Ingekuwa vizuri msomaji wa Maandiko Matakatifu ajiulize mwenyewe, ‘Kwa sababu gani iliandikwa vile?’
4. Ni kwenye kitabu gani cha Biblia tutakachokazia fikira sasa?
4 Ebu na tuchukue kitabu kimoja cha Biblia na tutumie wakati fulani tukizionyesha sababu za kuandikwa kwacho hivyo kikiwa na maneno yanayotumiwa. Mazungumzo yetu yataelekeza kwenye barua ya mtume Paulo kwa Wakristo katika Yerusalemu; kwa kawaida inaitwa barua kwa Waebrania, katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. (Ebr. 13:22) Kwa kuziangalia hali zilizokuwako miaka elfu moja na mia tisa iliyopita wakati ambapo Paulo aliiandika barua yake, tutasaidiwa kufahamu na kuona ubora wa sababu gani aliandika aliyoyaandika kusudi awatie nguvu watu wa Mungu na kuwafariji.
MAONI YA KARNE YA KWANZA JUU YA UKRISTO
5. Ni hali gani ya kidini iliyoko Yerusalemu karibu na mwaka wa 61 C.E.?
5 Ebu na turudie nyuma kwenye karibu mwaka wa 61 C.E., na kwenye mji wa Yerusalemu. Miaka karibu 28 imepita tangu kifo cha Yesu juu ya mti wa mateso nje tu ya kuta za Yerusalemu. Yerusalemu ni mji mtakatifu kwa Wayahudi. Kwa kadiri ionekanavyo, Yerusalemu ulikuwa salama katika siku za Yesu wa Nazareti aliyedharauliwa. Dai ni kwamba dini ya Wayahudi ni dini ya zamani za kale, ikirudia nyuma mpaka kwa babu yao Ibrahimu. Viongozi wa kiroho wa Wayahudi, waalimu wa dini, wanaheshimiwa sana na watu. Wanapewa fahari na kustahiwa. Wamekikalia kiti cha Musa nao ndio wenye mahali pa fahari kwenye vyakula vya jioni na viti vya mbele katika masinagogi, na wanazipokea salamu masokoni na kuitwa “Rabi” na watu. Wao ni sehemu ya tengenezo lenye mamlaka la siku hizo.—Mt. 23:6, 7.
6. (a) Wakristo katika mji huo walionwaje na viongozi wa kidini wa Kiyahudi? (b) Mtume Paulo alikuwa na maono gani alipokuwa katika mji miaka michache iliyotangulia? (c) Uhitaji mkubwa ulikuwa nini kwa kikundi kidogo cha Wakristo katika Yerusalemu?
6 Vile vile katika mji wa Yerusalemu wako watu wachache kwa kulinganisha wa dhehebu linalochukiwa linaloitwa Wakristo au “Njia hii.” (Matendo 9:2; 19:9; 22:4) Wanadhihakiwa na viongozi wa kidini wa Kiyahudi na wafuasi wao. Wanateswa na kushutumiwa. Isitoshe, wao ni wazao wa Kiyahudi kwa asili na kwa hiyo wanachukiwa zaidi kwa sababu waliiacha dini ya Wayahudi kusudi wawe wafuasi wa Yesu, yeye “aitwaye” Kristo. Kwa hiyo Wakristo wanachukiwa sana hivyo kwamba mtume Paulo alipokuwa amekuwa katika mji huo miaka fulani mapema kuonekana kwake tu katika hekalu kulikuwa kumezusha ghasia, Wayahudi wenye kufuata dini wakipiga kelele sana: “Mwondoe huyu katika nchi, kwa maana haifai aishi.” (Matendo 22:22) Zaidi ya Wayahudi 40 walijifunga kwa kiapo wasile wala kunywa mpaka wamemwangamiza Paulo. (Matendo 23:12-15) Katika hali hii ya ushupavu wa kidini na chuki kwa Wakristo lilipaswa kundi liishi, lihubiri na kujiweka imara katika imani. Lo! namna walivyohitaji kutiwa moyo na ujuzi mwema na ufahamu wa Kristo na namna yeye alivyoitimiza sheria ya Musa kusudi wasije wakaangukia nyuma kwenye dini ya Wayahudi na kuishika sheria ya Musa! Bila shaka Paulo alijua walichohitaji. Yeye mwenyewe aliyajua majaribu yaliyokuwa yakiwapata.
7. Taja sababu nyingine ambazo huenda viongozi wa Kiyahudi na wafuasi wao walitumia juu ya Wakristo.
7 Yafikirie kwa muda mabishano na kupinga ambako wale Wakristo wa kwanza wa Kiyahudi walipaswa washindane nayo. Kwanza, viongozi wa kidini wa Kiyahudi na wafuasi wao wasingewaruhusu Wakristo hao waliochukiwa wafikiri walikuwa wenye kibali cha Mungu hata kidogo. Je! si Wayahudi waliokuwa na ushuhuda wa kweli wa baraka ya Mungu? Je! haikuwa kweli kwamba Mungu alishughulika na Wayahudi kupitia kwa malaika? Bila shaka, kwa maana kitabu cha Musa kinasema: “Malaika wa [Yehova] akamtokea [Musa], katika mwali wa moto uliotoka katikati ya kijiti.” Nyumaye Yehova alisema: “Tazama, mimi namtuma malaika aende mbele yako, ili akulinde njiani na kukupeleka mpaka mahali pale nilipokutengezea.” (Kut. 3:2; 23:20) Ati! huenda Wayahudi wakawa walijisifu kwamba Musa hata alisema na Mungu kinywa kwa kinywa. Zaidi ya hayo, litazame hekalu lenye fahari, likiwa na vyumba vya Patakatifu na Patakatifu Zaidi Sana. Utazame uzuri wake wa ajabu, nguvu zake, msingi wake imara! Hayo ndiyo waliyokuwa nayo Wayahudi! Na jambo jingine: ebu ufikirie ukuhani wa Kiyahudi! Kumbe! ulirudia nyuma mpaka kwa Haruni na wanawe, washiriki wa kabila ya Lawi. Kuhani mkuu alikuwa mzao wa ukoo huu wa pekee. Wayahudi walikuwa na agano la Torati, alilopewa Musa na Mungu mwenyewe. Ufalme wa kimungu ulikuwa wa Wayahudi; nao Yerusalemu, lo! Yerusalemu ndio uliokuwa na kiti cha enzi palipopaswa kuendeshewa utawala wa Mungu.
8, 9. (a) Huenda viongozi wa Kiyahudi walimshutumu mwanzilishi wa Ukristo na wafuasi wake kwa njia gani? (b) Labda waliwatofautisha Wakristo wenyewe na sehemu zao za kukutania za vivi hivi na nini?
8 Sasa watazame Wakristo katika Yerusalemu. Wao walikuwa na nini? Kulingana na maoni ya viongozi wa Kiyahudi, Wakristo hawakuwa na cho chote kwa kulinganisha. Kiongozi wao Yesu alikuwa amekufa, naye alikuwa amekufa kama mhalifu wa kawaida. Yeye alikuwa nani? Hakuwa maarufu kulingana na viongozi wa Kiyahudi. Yeye alikuwa mwana wa seremala wa vivi hivi tu, na zaidi ya hayo alikuwa mtoka Nazareti. Kwa habari ya elimu, hakuwa na masomo ya kawaida katika shule za ualimu na za kidini. Lo! namna asivyokuwa mwenye ujuzi na elimu kulingana na maoni ya Wayahudi akilinganishwa na yale ambayo waalimu wao na wakufunzi walikuwa wameyajua na kufundishwa! Na zaidi ya hayo, kati ya wafuasi wake ni watu wachache sana waliokuwa wenye elimu. Wavuvi wa samaki, watoza kodi, na hata watu wa Mataifa ndio waliokuwa wengi wa wafuasi wake, na watu hao wa Mataifa bila shaka hawakuwa wa uzao wa asili wa Ibrahimu machoni pa viongozi wa Kiyahudi. Ingewezekanaje Wakristo hao wadhani kwamba walikuwa na kibali cha Mungu na kwamba Mungu alikuwa akishughulika nao? Wayahudi walijiona ndio waliokuwa watu waliochaguliwa na Mungu, kwa maana wao ndio waliokuwa uzao wa Ibrahimu. Tena, Wakristo walikutana katika vyumba vya juu au sehemu za vivi hivi, hali Wayahudi walikuwa wana hekalu lao zuri la kukusanyikia.
9 Bila shaka, sababu kama hizi, na nyingine nyingi, zilitumiwa juu ya Wakristo wa Kiyahudi. Walihitaji kutiwa moyo na ufahamu wa hali hiyo namna gani! Kama tu mtu fulani angeujua uhitaji wao na kuwafariji na kuwasaidia!
SABABU NYINGINE ZAMPENDELEA KRISTO KULIKO MUSA
10. Nani aliyeyajua magumu haya yaliyowapata Wakristo, na kwa hiyo nani aliyeongozwa na roho ya Mungu awaandikie kusudi awajenge?
10 Bila shaka, Yehova Mungu mbinguni aliijua hali yao. Kwa uongozi wa roho yake alifanya mtume Paulo apendezwe na hali walizoshindana nazo. Na kwa hiyo Paulo aliwaandikia waaminifu hao katika Yerusalemu, nacho kitabu cha Waebrania kinalo jibu lake kwa mashtaka mengi ambayo bila shaka yalifanywa juu ya Ukristo wa karne ya kwanza na adui zake.
11, 12. (a) Sasa Paulo alitoa sababu ya namna gani, na kwa sababu gani hii ilifaa? (b) Paulo alionyeshaje ukuu wa Yesu akilinganishwa na malaika? (c) Na Musa?
11 Akiyachukua madai yale yale ya Wayahudi, Paulo anaonyesha ukuu wa taratibu ya Kikristo na ukuhani wake unapolinganishwa na dini ya Wayahudi. Bila shaka, wengi wa Wakristo hao katika Yerusalemu walikuwa na asili ya Kiyahudi. Walifahamiana sana na torati ya Musa na sababu za viongozi wa Kiyahudi. Kwa hiyo ilimlazimu Paulo kuwaonyesha sababu nyingine, kweli ya mambo na kuufunua uongo wa mashtaka yaliyofanywa juu yao na viongozi wa kidini wa Kiyahudi. Kwa mfano, ni kweli kwamba sheria ya Musa ilipelekwa kupitia kwa malaika. Lakini je! malaika wanalinganaje na Bwana Yesu? Hivi ndivyo Paulo alivyoandika katika Waebrania 1:4-6: “[Yesu] amefanyika bora kupita malaika, kwa kadiri jina alilolirithi lilivyo tukufu kuliko lao. Kwa maana alimwambia malaika yupi wakati wo wote, Ndiwe mwanangu, mimi leo nimekuzaa? Na tena, Mimi nitakuwa kwake baba, na yeye atakuwa kwangu mwana? Hata tena, amletapo mzaliwa wa kwanza ulimwenguni, asema, Na wamsujudu malaika wote wa Mungu.” Kwa kweli, basi, Paulo anaonyesha, malaika ni watumishi, lakini Yesu ndiye Mwana wa Mungu.
12 Lakini namna gani juu ya uhakika wa kwamba Mungu alizungumza kinywa kwa kinywa na Musa? Haliwezi kuwapo shaka kwamba hili lilikuwa jambo kubwa. Lakini, juu ya Yesu Kristo, Paulo anaandika: “Kwa maana huyo [yaani, Yesu] amehesabiwa kuwa amestahili utukufu zaidi kuliko Musa, kama vile yeye aitengenezaye nyumba alivyo na heshima zaidi ya hiyo nyumba. . . . Na Musa kweli alikuwa mwaminifu katika nyumba yote ya Mungu kama mtumishi . . . bali Kristo, kama mwana, juu ya nyumba ya Mungu.” Kwa kweli, hapa, Paulo alikuwa anasema, ‘Akina ndugu, nani mkubwa zaidi katika nyumba—mtumishi, kama vile Musa alivyokuwa, ama Mwana wa Mwenye nyumba, kama vile Yesu Kristo alivyo?’ Namna lilivyokuwa jambo la kutia moyo kwa Wakristo wa Kiyahudi waliokuwa wakiishi huko Yerusalemu kuupata ufahamu huu wa mambo!—Ebr. 3:3-6.
UKUU WA KRISTO KAMA KUHANI MKUU
13. (a) Nini kingeweza kuwa bora kupita hekalu linaloonekana katika Yerusalemu, naye Kristo Yesu alikuwa wapi? (b) Paulo aliuonyeshaje ukuu wa ukuhani wa Kristo ukilinganishwa na ule wa Haruni?
13 Sasa Paulo anaendelea na sababu nyingine, ile ya hekalu zuri lenye kuonekana katika Yerusalemu. Na, kwa kweli, lilikuwa zuri na la gharama kubwa. Lakini je! hekalu linaloonekana lingekuwa na maana gani likilinganishwa na kuwa pale pale mbele za Mungu? Mfalme Sulemani ndiye aliyelijenga hekalu zuri la kwanza juu ya Mlima wa Moria katika Yerusalemu nyuma katika karne ya kumi na moja mbele ya Wakati wetu wa Kawaida, na penye wakf wake yeye alisema kwamba Yehova kwa kweli asingekaa ndani ya jumba hilo lililojengwa na mwanadamu. Bali, alisema kwamba mbingu ya mbingu isingeweza kumchukua ndani Mungu Mwenye Nguvu Zote Yehova, acha hekalu alilokuwa amelijenga! (1 Fal. 8:27) Kwa hiyo, kuwa mbele za Yehova kwenyewe katika mbingu kungekuwa jambo kubwa sana sana kuliko kutumikia katika hekalu lo lote la kidunia. Kwa hiyo Paulo anaandika juu ya Kristo Yesu kwamba ‘aliingia katika mbingu’ kuja mbele za Baba yake, Yehova. (Ebr. 4:14) Na juu ya ukuhani wa Kiharuni, ambao katika siku hizo ulikuwa ukitumika katika hekalu la Yerusalemu, Paulo anaulinganisha na ukuhani wa Kristo na kuuonyesha huu wa pili kama mkuu zaidi, kwa maana ni wa mfano wa Melkizedeki. Maneno ya Paulo katika Waebrania 5:5, 6 yalikuwa: “Kristo naye hakujitukuza nafsi yake kufanywa kuhani mkuu, lakini yeye aliyemwambia, Ndiwe mwanangu, mimi leo nimekuzaa. . . . Ndiwe kuhani milele kwa mfano wa Melkizedeki.” Ndiyo, kuhani milele, nalo lilikuwa jambo lililotegemea, si urithi wo wote wa mwili wenye dhambi, lakini kiapo kutoka kwa Mungu. Maneno ya Paulo juu ya jambo hili yameandikwa katika Waebrania 7:19-22: “Kwa maana ile sheria haikukamilisha neno; na pamoja na hayo kuliingizwa matumaini yaliyo mazuri zaidi, ambayo kwa hayo twamkaribia Mungu. Na kwa kuwa haikuwa pasipo kiapo, . . . kwa kadiri hii Yesu amekuwa mdhamini wa agano lililo bora zaidi.” Na juu ya kuendelea bila lazima ya mrithi, halafu Paulo anasema: “Zaidi ya hayo, iliwapasa wengi wawe makuhani kwa kufuatana [chini ya Sheria ya Kiyahudi] kwa sababu ya kuzuiliwa na kifo wasiendelee kuwa hivyo, lakini yeye [Yesu] kwa sababu ya kuendelea kuwa hai milele anao ukuhani wake pasipo warithi wo wote. Kwa hivyo anaweza vile vile kuwaokoa kabisa wale wanaomkaribia Mungu kupitia kwake, kwa maana yeye yu hai sikuzote kuwatetea.”—Ebr. 7:23-25, NW.
14. Onyesha namna ukuu wa dhabihu ya Kristo ulivyowatia moyo Wakristo walioisoma barua yake.
14 Bila shaka hizi zilikuwa sababu zenye nguvu kutoka kwa mtume wao mpendwa Paulo za kuitia nguvu hali ya Wakristo na kuwasaidia waendelee kuwa imara katika imani. Lakini hayo si yote. Paulo anaendelea kuuonyesha ukuu wa Yesu kama kuhani mkuu katika hekalu la Yehova la kimbinguni. Anaonyesha hali yenyewe kabisa kwa kuwapa Wakristo sababu zaidi. Anailinganisha dhabihu ya Bwana Yesu na zile dhabihu zilizotolewa na ukuhani wa Kiharuni walizojivunia sana viongozi wa Kiyahudi. Katika mistari ya 26 mpaka 28 ya sura ya saba Paulo anaandika: “Maana ilitupasa sisi tuwe na kuhani mkuu wa namna hii aliye mtakatifu, asiyekuwa na uovu, asiyekuwa na waa lo lote, aliyetengwa na wakosaji, aliyekuwa juu kuliko mbingu; ambaye hana haja kila siku, mfano wa wale makuhani wakuu wengine, kwanza kutoa dhabihu kwa ajili ya dhambi zake mwenyewe, kisha kwa ajili ya dhambi za hao watu; maana yeye alifanya hivi mara moja [kwa ajili ya wakati wote], alipojitoa nafsi yake. Maana torati yawaweka wanadamu walio na unyonge kuwa makuhani wakuu; bali hilo neno la kiapo kilichokuja baada ya torati limemweka Mwana, aliyekamilika hata milele.” Fikiria namna maneno hayo yalivyowatia moyo walio waaminifu katika Yerusalemu. Ndiyo, Kristo kuhani mkuu aliyeutoa uhai wake mwenyewe mkamilifu kwa ajili ya wanadamu sasa ni kuhani milele bila ya mrithi kwa kiapo alichoapa Mungu.
AGANO JIPYA LAFANYA LA KALE KUWA KUUKUU
15. Nini maana ya sababu ya Paulo katika Waebrania 8:7-13 juu ya agano bora, na ni uamuzi gani wa busara juu ya agano la kale?
15 Paulo anaendelea na sababu nyingine itakayowafaidi Wakristo vile vile, na hiyo ni juu ya agano la Torati lililopatanishwa na Musa likilinganishwa na agano lililo bora lililopatanishwa na Kristo kati ya Mungu na waaminifu wake juu ya dunia hii. Iangalie sababu ya Paulo katika Waebrania 8:7-13: “Maana kama lile [agano] la kwanza lingalikuwa halina upungufu, nafasi isingalitafutwa kwa lile la pili.” Je! agano la kwanza lilikuwa lisilo na upungufu? Hapana, kwa maana ni Yehova mwenyewe aliyesema: “Nami nitawatimizia nyumba ya Israeli na nyumba ya Yuda agano jipya; halitakuwa kama agano lile nililoagana na baba zao, katika siku ile nilipowashika mikono yao niwatoe katika nchi ya Misri. Kwa sababu hawakudumu katika agano langu.” “Maana hili ndilo agano nitakaloagana na nyumba ya Israeli baada ya siku zile,” asema Yehova. “Nitawapa sheria zangu katika nia zao, na katika mioyo yao nitaziandika; nami nitakuwa Mungu kwao, nao watakuwa watu wangu.” “Kwa kule kusema, Agano jipya,” Paulo anatoa sababu, Mungu “amelifanya lile la kwanza kuwa kuukuu. Lakini kitu kianzacho kuwa kikuukuu na kuchakaa ki karibu na kutoweka.”—Linganisha Yeremia 31:31-33.
16. Nani waliohitaji kutiwa moyo? Nani waliopaswa kuvunjwa moyo? Kwa sababu gani?
16 Fikiria namna maneno haya yalivyokuwa yenye kutia moyo: “Lakini kitu kianzacho kuwa kikuukuu na kuchakaa ki karibu na kutoweka.” Nani sasa ambao wangeweza kufurahi wala si kuhuzunika na kuomboleza? Kumbe! ni Wakristo, kwa kuwa walikuwa wakishikilia agano lililokuwa likichukua mahali pa lile lililo kuukuu, agano la Torati. Wenye huzuni na wenye kuomboleza wangekuwa wale wenye kujisifu wa kidini waliokuwa wakishindana na Ukristo. Kile ambacho walikuwa wanategemea hakikuwa tena njia ya Mungu ya kushughulika na watu wake. Mwanawe, Bwana Yesu Kristo, aliyefufuliwa kwenye utukufu wa kimbinguni, alikuwa amepatanisha agano jipya lililo bora lenye msingi wa ahadi bora na zenye kuendelea zaidi, na lililopatanishwa na dhabihu bora zaidi, damu yake mwenyewe iliyomwagwa.
UFALME WASIMAMISHWA JUU YA MLIMA WA SAYUNI WA KIMBINGUNI
17. (a) Tofauti na Musa kuukaribia Mlima wa Sinai kwa ajili ya agano la Torati, wale Wakristo walikuwa wanakaribia nini? (b) Yerusalemu wa kimbinguni unalinganaje na Yerusalemu wa kidunia?
17 Lakini namna gani juu ya dai lo lote kwamba haki ya Ufalme ilikuwa ya Wayahudi na kwamba Yerusalemu ulikuwa mji wa Mungu ambapo utawala wa kimungu ungeendeshewa? Paulo alishughulikaje na sababu hii katika barua yake kwa Waebrania? Kwa njia ya kupendeza sana, yeye anaianza sababu yake, inayopatikana katika sura ya kumi na mbili, mistari ya 18-27, hivi: “Maana hamkufikilia mlima uwezao kuguswa, uliowaka moto, wala wingu jeusi, na giza, na tufani.” Ni kweli, Wakristo hawakuwa wameukaribia Mlima Sinai wa kale, mahali ambapo agano la Torati kwa ajili ya taifa la Israeli lilitolewa. Wao hawakuwa wamekaribia kitu fulani ambacho wangeweza kugusa na ambacho kutoka kwacho wangeweza kuuona mwali wa moto ukipanda juu. Sivyo, lakini kuanzia katika mstari wa 22, maneno ya Paulo ni haya: “Ninyi mmeufikilia mlima Sayuni, na mji wa Mungu aliye hai, Yerusalemu wa mbinguni, na majeshi ya malaika elfu nyingi, mkutano mkuu na kanisa la wazaliwa wa kwanza walioandikwa mbinguni, na Mungu mwamuzi wa watu wote, . . . na Yesu mjumbe wa agano jipya.” Ndiyo, hicho ndicho walichokuwa wamekaribia, kiti cha enzi cha mamlaka na serikali kilicho kweli kweli, si cha kidunia, bali Yerusalemu wa kimbinguni, pamoja na Mungu, maelfu ya malaika, kundi la mzaliwa wa kwanza na Yesu mpatanishi wa agano jipya. Kwa kulinganisha, Yerusalemu wa kidunia, vile vile Mlima wa Sinai, na vile vile hekalu na ukuhani wa Wayahudi, vilififia.
18. (a) Yerusalemu wa kimbinguni utaendelea kuwako kwa muda mrefu namna gani? (b) Nini tayari kilichokuwa kimetukia kwa Yerusalemu wa kidunia ambacho kingetukia kwa mara ya pili?
18 Na je! Mlima wa Sayuni na Yerusalemu wa kimbinguni ni wenye nguvu, wenye kuendelea na wenye imara kadiri gani? Hatuachwi katika shaka, kwa maana Paulo anaongezea: “Basi kwa kuwa tunapokea ufalme usioweza kutetemeshwa, na tuwe na neema, ambayo kwa hiyo tumtolee Mungu ibada ya kumpendeza, pamoja na unyenyekevu na kicho.” (Ebr. 12:28) Ufalme huo usingetikiswa kama vile Yerusalemu wa kidunia ulivyotikiswa sana kwa miaka 70, tangu mwaka wa 607 mpaka 537 B.C.E., nao ungetikiswa tena na majeshi ya Kirumi wakati ujao usio mbali mno.
19, 20. Sasa Wakristo hao wa Kiyahudi walipaswa wafanye nini, na Paulo alikuwa amevuta nini katika sababu zake?
19 Lo! maneno ya Paulo yalikuwa yenye kufariji na kutia nguvu kama nini kwa Wakristo hao wa kwanza wa Kiyahudi! Karne kumi na tisa nyumaye, maneno hayo yangali hai na ni yenye maana kwetu sisi Wakristo katika kame hii ya 20.
20 Kwa hiyo, wakati ambapo wapinzani wa Kiyahudi walipokuwa wakitegemea mambo ya kale, utajiri wa kimwili, uwezo, fahari ya matendo ya ibada, sherehe na hekima ya ulimwengu huu, Wakristo walipaswa wasitawi katika imani, katika tumaini lililohakikishwa la mambo yanayotazamiwa, katika onyesho la mambo ya hakika, ijapokuwa hayaonekani. Barua hiyo ilikuwa yenye kutia moyo kama nini kwa waaminifu wa Mungu karibu na mwaka wa 61 C.E.! Kwa kweli, “Njia hii” ya kwenye uzima pamoja na baraka za milele iliwekwa mbele yao waziwazi. Naye Paulo aliiandika barua yake kwa njia ambayo ingeyavuta mawazo yao na busara kama Wayahudi waliozaliwa hivyo kwa asili na kufanya wajengwe katika imani. Maneno ya Paulo katika kitabu cha Waebrania vile vile ni yenye kufariji kwa Wakristo wa kisasa.
21. Kama ilivyoonyeshwa katika masomo yetu, sisi sote twawezaje kuongeza ufahamu wetu wa Neno la Mungu, kwa sababu gani?
21 Ili tufaidike kabisa kutokana na Maandiko, imetupasa tufahamu sababu gani yameandikwa kama yalivyoandikwa. Kwa msaada wa vitabu kama Aid to Bible Understanding, na vile vile “All Scripture Is Inspired of God and Beneficial” na vitabu vingine vingi, kwa kweli tunakuwa na ghala ya ujuzi wa kutusaidia kujua namna gani na sababu gani kila kitabu cha Biblia kimeandikwa vile. Tukiwa na maoni hayo yaliyopanuliwa bila shaka tunaweza tukawa tayari kwa kila kazi njema ambayo huenda Mungu akatupa tuifanye. Kama vile tulivyokitumia kitabu cha Biblia cha Waebrania twaweza kufanya namna ile ile na vitabu vile vingine 65 vinavyofanyiza Neno la Mungu, Biblia Takatifu. Namna yanavyofaa maneno yanayopatikana katika sura ya kumalizia ya barua kwa Waebrania kwa Wakristo wote leo: “Mungu wa amani . . . awafanye ninyi kuwa wakamilifu katika kila tendo jema, mpate kuyafanya mapenzi yake; naye akifanya ndani yetu lipendezalo mbele zake.”—Ebr. 13:20, 21.
—Kutoka The Watchtower, April 1, 1973.