Je! Matakwa ya Maskini Yatatoshelezwa Wakati Mmoja?
UMASKINI si jambo jipya katika ulimwengu. ” Karibu miaka 3,500 iliyopita Waisraeli waliambiwa: “Maskini hawatakoma katika nchi.” (Kum. 15:11) Karne nyingi nyumaye, alipokuwa akikubali tendo la ukarimu, Yesu Kristo aliukubali uhakika ule ule mgumu, akisema: “Sikuzote mnao maskini pamoja nanyi; lakini mimi hamnami sikuzote.”—Mt. 26:11.
Inasikitisha kwamba katika hii taratibu ya mambo isiyokamilika mamilioni ya wanaume, wanawake na watoto wanaendelea kuishi katika umaskini. Pengine wewe mwenyewe u kati ya mamilioni hayo.
Je! wewe waona kwamba kupata kazi ya sikuzote ni vigumu? Je! wasikitikia namna utakavyopata chakula cha kutosha kwa jamaa yako? Je! unasumbuka kwamba kukosekana kwa mambo ya lazima ya maisha kunakunyima wewe na jamaa yako afya njema? Je! unaona kwamba umetegwa katika hali yako ya makao na huna njia ya kuondoka katika mazingira yenye kuhuzunisha? Je! wakati mmoja umejiuliza mwenyewe, Sababu gani mambo yawe namna hiyo? Je! matakwa ya maskini yatatoshelezwa wakati mmoja?
Hata ikiwa wewe hujitii kati ya maskini wa wakaaji wa dunia, bila shaka unawajua maskini. Hata mataifa yaliyositawi yana umaskini. Senator Hubert H. Humphrey alisema juu ya United States ya Amerika, katika kitabu chake War on Poverty, kwamba ‘mmoja kati ya kila Waamerika watano anaishi katika umaskini, aibu, taabu, na hali mbaya.’ Je! wewe unawaonea hawa huruma?
Duniani kote watu wengi walio maskini wanayo matumaini kwamba serikali za kibinadamu zitawasaidia kwa njia fulani. Lakini wanakubali upesi kwamba wamekata tamaa mara nyingi sana.
Angalia, kwa mfano, lililotukia katika Colombia, Amerika ya Kusini. Huko nyuma katika mwaka wa 1962 wakati ambapo marehemu Guillermo Leon Valencia alipopigania urais, mara nyingi aliutaja mstari mmoja wa mashairi ya babaye: “Kikombe kilichojaa kwa kila mtu.” Aliahidi kwamba yake ingekuwa “serikali ya maskini.” Lakini je! ndivyo ilivyokuwa? Alipopandisha gharama ya matumizi ya fedha aliwaumiza wale wale aliojidai kupendelea. Tangu mwishoni mwa mwaka wa 1962 mpaka mwanzoni mwa mwaka wa 1964 gharama ya kuishi ilipanda kwa 50 kwa mia! Karibuni serikali ya Valencia ikaanza kuitwa na mpita barabarani “serikali ya matajiri walio maskini.”
Kwa sababu ya kukata tamaa mara kwa mara, watu wengi wanaugeukia Ukomunisti na maongozi ya Marx wakitumainia kwamba hali yao yaweza kutengenezwa. Lakini, kama vile nchi zinazoongozwa na namna nyingine za serikali ya kibinadamu, nchi za Ukomunisti hazikuweza kutoa ufumbuzi wa magumu makubwa mengi ya maisha. Si kweli kwamba zimepatwa na hali zilizochafuka za kisiasa, mafarakano ya kitaifa na kuvunjika kwa jamaa na adili, kutia na ugumu wa unywaji wa vileo? Vile vile, raia zao wamepoteza uhuru mwingi sana.
Kweli isiyoweza kukanushwa ni kwamba hakuna serikali ya kibinadamu iliyoweza kuwapa wakaaji waliohuzunika wa dunia kitulizo cha kutosha. Je! maana yake ni kwamba jamii ya maskini haina tumaini? kwamba umaskini hautakwisha wakati wo wote? Hata kidogo. Kunaye Mmoja aliye juu zaidi kuliko mwanadamu anayetaka na anayeweza kuuondoa umaskini. Huyu Ndiye Muumba wa mwanadamu. Yehova Mungu. Juu yake, Biblia inasema: “Waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.”—Zab. 145:16.