“Mwenye Furaha Ni Yeye Anayesoma kwa Sauti Kuu”
“Mwenye furaha ni yeye anayesoma kwa sauti kuu na wale wanaosikia maneno ya unabii huu, na wanaoshika mambo yaliyoandikwa ndani yake; kwa maana wakati uliowekwa u karibu.”—Ufu. 1:3, NW.
1. Kwa sababu gani uwezo wa kusoma na kuandika ni zawadi ya ajabu kweli kweli ambayo Yehova amempa mwanadamu?
LO! NI zawadi ya ajabu kama nini ambayo Muumba, Yehova Mungu, amempa mwanadamu kwa kumpa uwezo wa kusoma na kuandika kusudi apate kufahamu na kuishika maana ya mambo yaliyo bora! Unaposoma habari hii, fikiria ni baraka kama nini kuweza kufahamu yanayomaanishwa na maneno yaliyomo katika ukurasa huu na zinazofuata. Na kusudi ukazie akilini mwako namna zawadi hii ilivyo ya ajabu, jaribu kusoma namna ya habari ii hii katika lugha nyingine, ambayo huifahamu wala kuizungumza. Je! isingekuwa kazi bure? Ndiyo, ni ajabu kama nini kuweza kusoma, kufahamu na kushika matumizi ya mambo yaliyoandikwa kwa ajili ya furaha ya wanadamu, zaidi kwa maana yanafungamana na kumjua na kumtumikia Muumba mwenyewe, Yehova Mungu!
2. Twawezaje kuutumia kwa faida zaidi uwezo wa kusoma, na, kwa habari hii, ni amri gani ya Yehova inayopatikana katika Kumbukumbu la Torati 31:9-12?
2 Ukiwa na uwezo wako wa kusoma, je! unasoma kwa sauti kuu kwa faida yako mwenyewe na ya wengine? Je! wewe ulijua kwamba ni amri ya Mungu ya kale katika Neno lake la Kweli, Biblia, kwamba watu wake wamepaswa wasome kwa sauti kuu? Katika Biblia yako katika Kumbu-kumbu la Torati 31:9-12 utayaona maneno haya yameandikwa: “Musa akaiandika torati hii, akawapa makuhani, wana wa Lawi, waliolichukua sanduku la agano la [Yehova], na wazee wote wa Israeli. Musa, akawaamuru, akasema, Mwisho wa kila mwaka wa saba, wakati wa maachilio, wakati ulioamriwa wa sikukuu ya vibanda, Israeli wote wafikapo ili kuonekana mbele za [Yehova], Mungu wako, mahali pale atakapopachagua, uisome torati hii mbele ya Israeli wote masikioni mwao. Wakusanye watu, wanaume na wanawake na watoto, na mgeni wako aliyemo malangoni mwako, wapate kusikia na kujifunza, na kumcha [Yehova], Mungu wenu, na kuangalia kutenda maneno yote ya torati hii.”
3. (a) Kwa sababu gani kusoma kwa waziwazi katika nyakati za kale zaidi kulikuwa kwa lazima? (b) Wafalme wa Israeli walipaswa wapate nakala ya torati kwa njia gani, na kwa sababu gani walipaswa waisome kwa kawaida?
3 Bila shaka kusoma huku kwa waziwazi kulikofanywa na Walawi na wanaume wazee kulikuwa kwenye faida kwa wasikilizaji wote. Haikuwa kana kwamba kila mtu aliyekusanyika angeweza kujipatia habari mwenyewe kwa wepesi wakati wo wote alipotaka, kwa maana nakala za Neno la Mungu zilikuwa chache. Kwa hiyo kusoma kwa waziwazi kulikuwa kwa lazima kusudi mambo yaliyo bora yakaziwe katika akili za watu. Kwa kweli, Musa mwenyewe, chini ya uongozi wa Mungu, alikuwa amewaambia watu kwamba katika siku zijazo wakati ambapo wangeomba wapewe mfalme awatawale mfalme huyo angekuwa na daraka la kufanya nakala ya torati, iliyokuwa katika kabidhi ya makuhani, Walawi. Mfalme alipaswa, si kufanya nakala peke yake, lakini kuisoma siku zote za maisha yake vile vile, kusudi amche Yehova na kutenda maneno yote ya torati. Kuangalia huku kwa Neno la Mungu kungemsaidia mfalme aendelee kuwa na moyo mwema kwa ndugu zake. Kungemsaidia kuepuka kujikweza juu ya ndugu zake. Kungempa busara ili atembee katika njia ya Yehova, bila ya kugeuka kutoka kwa amri kwenda kulia ama kushoto. Na, kama matokeo, yeye mwenyewe angefaidika kwa maana angekuwa na kibali cha Yehova na kwa njia hiyo angerefusha siku zake za kukalia kiti cha enzi cha ufalme.—Kum. 17:18-20.
MATOKEO MAZURI YALIYOTEGEMEA KUSOMA
4. Yoshua alipokea onyo gani juu ya “kitabu hiki cha torati”?
4 Nyuma ya kifo cha Musa, mrithi wake Yoshua vile vile aliamriwa alitii onyo la Mungu lililoandikwa. Yanasema maandishi ya Biblia: “Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo; maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana.”—Yos. 1:8.
5. Yoshua alionyeshaje aliujua uhitaji wa kusoma na kuyatumia maneno yanayopatikana katika “kitabu hiki cha torati”?
5 Hapana shaka kwamba Yoshua aliiona hekima ya kushikamana na torati ya Mungu iliyoandikwa. Kwa habari ya matendo ya Yoshua si muda mrefu nyuma ya kuingia kwa taifa la Israeli katika nchi waliyoahidiwa na Mungu, maandiko matakatifu yanayo habari hii: “[Yoshua] akaandika huko juu ya mawe hayo nakala ya torati ya Musa, aliyoiandika mbele ya wana wa Israeli. Na Israeli wote, na wazee wao, na maakida yao, na makadhi yao, wakasimama upande huu wa sanduku na upande huu, mbele ya makuhani . . . Na baadaye alisoma maneno yote ya torati, baraka na laana, sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa katika kitabu cha torati. Hapakuwa na hata neno moja katika hayo aliyoamuru Musa, ambalo Yoshua hakulisoma mbele ya kusanyiko lote la Israeli, na mbele ya wanawake, na watoto, na wageni waliokaa nao.”—Yos. 8:32-35.
6. (a) Kitabu cha torati ya Mungu kilikuwaje ulinzi kwa Israeli? (b) Karibuni, ni kosa gani walilofanya watu, lakini Yehoshafati alichukua tendo gani kuiondoa hali?
6 Ndiyo, misemo ya Mungu ilikuwa kama ulinzi mzuri kwa Waisraeli wakati wa safari yao katika jangwa kwa miaka 40 na vile vile wakati wa kuishinda na kukaa katika nchi ya ahadi. (Mhu. 7:12) Kusoma kwa amri na maongozi ya Yehova kuliyafanya matakwa ya Yehova yaonekane wazi mbele yao. Lakini, wakati ulifika walipoacha kulishika takwa hili la maana, kuyafanya mapenzi ya Mungu kwa kusoma na kushikamana na amri zake. Wakati wa Mfalme Yehoshafati wengi katika nchi walikuwa wamegeuka kutoka katika ibada safi, wakiuacha utumishi wa Yehova kwa ajili ya ibada ya miungu ya kipagani na utumishi wa Mabaali. Lakini, kwa habari ya Yehoshafati, yeye alimpenda Yehova na akatembea katika amri zake, naye Yehova aliusimamisha imara ufalme wa Yuda mkononi mwake. (2 Nya. (Sik.) 17:4, 5) Mojawapo la matendo yenye maana zaidi ya utawala wa Yehoshafati lilitukia katika mwaka wa tatu. Mwandishi wa orodha ya tarehe Ezra analiandika kwa maneno haya: “Tena, katika mwaka wa tatu wa kutawala kwake [ Yehoshafati], akawatuma wakuu wake . . . ili kufundisha mijini mwa Yuda; na pamoja nao Walawi, . . . [na] makuhani. Wakafundisha katika Yuda, wenye kitabu cha torati ya [Yehova]; wakazunguka katika miji yote ya Yuda, wakafundisha kati ya watu.” (2 Nya. (Sik.) 17:7-9) Hii ilikuwa baraka kwao.
7. Ni ugumu gani ulioendelea kusitawi kati ya watu wa Mungu, nalo itikio la Yosia lilikuwa nini alipoyasikia maneno kutoka kwa “kitabu hiki cha torati”?
7 Hata hivyo, inaelekea kuwa takwa hili la Mungu, kusoma neno lake na kuzitimiza amri zake, lilisahauliwa kwa wepesi na watu wa Mungu. Katikati ya wakati wa Yehoshafati (936-911 B.C.E.) na Yosia (659-629 B.C.E.) mfalme na watu walikosa kuzishika sheria na amri za Yehova mara nyingi. Kuzitii amri za Yehova kulionwa kwa upotovu sana hivyo kwamba wakati wa Yosia ulipofika, ambaye alianza kutawala akiwa kivulana tu, watu, kwa kadiri kubwa, walikuwa wamesahau nyingi za amri za Yehova. Kwa kweli, ni katika mwaka wa kumi na nane wa Yosia, alipoamuru kwamba hekalu la Yehova lirekebishwe hali yake ya kubomoka na kuachwa, kwamba kuhani mkuu katika hekalu akakiona “kitabu cha torati” katika nyumba ya Yehova. Mfalme Yosia alisomewa yaliyokuwamo katika kitabu hiki cha torati kilichopatikana karibuni. Mara tu alipoyasikia yaliyosomwa, Yosia aliyararua mavazi yake mara moja. Na kwa sababu gani? Ebu Yosia mwenyewe na ajibu: “Hasira ya [Yehova] ni kubwa aliyotukasirikia, kwa sababu baba zetu hawakuyaangalia maneno ya kitabu hiki, kufanya kama hayo yote tuliyoandikiwa.”—2 Fal. 22:3-13.
8. Halafu Yosia alichukua mwendo gani wa tendo, nao watu waliitikiaje?
8 Tendo alilozidi kufanya Yosia limeandikwa kwetu kwa maneno haya: “Mfalme akapanda kwenda nyumbani kwa [Yehova], na watu wote wa Yuda, nao wote waliokaa Yerusalemu, pamoja naye, na makuhani, na manabii, na watu wote, wadogo kwa wakubwa; akasoma masikioni mwao maneno yote ya kitabu cha agano kilichoonekana katika nyumba ya [Yehova].” Nyuma ya hapo mfalme na watu walifanya agano mbele za Yehova kutembea kulingana na yaliyoandikwa katika kitabu. Lo! kusoma huko kwa waziwazi kwa torati kuliwafaidi namna gani wale waliokusanyika huko!—2 Fal. 23:2, 3.
NAMNA KUSOMA KULIVYOFANYA MABAKI KUWA YENYE FURAHA
9. (a) Kwa sababu ya kuliacha Neno la Mungu, nini kilichotukia kwa taifa la Israeli? (b) Yehova aliwaonyeshaje watu wake rehema, na kusoma kwa waziwazi kulitumikaje tena kama kusudi lenye msaada? (c) Mbali na kusoma, ni hatua gani nyingine zilizochukuliwa kuwasaidia watu?
9 Inasikitisha kufikiri kwamba nyuma ya kufanya agano hili la kutembea kulingana na yaliyoandikwa katika kitabu, watu wa Mungu walimsahau Mungu wao na Neno lake na kulisoma kwa uongozi nao wakajitoa kwa mapenzi ya mataifa yaliyokuwa karibu yao. Kutojali kwao kulikozidi kuliongoza kwenye anguko lao kama taifa katika mwaka wa 607 B.C.E. Lakini Yehova, kwa kuwa mwenye rehema, aliyasikia maombi yao, na katika wakati wake, akaruhusu mabaki yao warudi kutoka uhamishoni kwenda kwenye Yerusalemu wao mpendwa na Yuda wakajitie katika ibada safi. Hata hivyo, maoni ya Yehova ya umuhimu wa Neno lake lililoandikwa hayakupunguzwa na wakati. Ezra, mwandishi wa Mungu, anawaita tena wakiwa katika hali yao ya kurudishwa kusudi wayakumbuke mambo yaliyoandikwa. Twaambiwa hivi na Gavana Nehemia: “Na watu wote wakakusanyika kama mtu mmoja katika uwanja uliokuwa mbele ya lango la maji; wakamwambia Ezra, mwandishi, akilete kitabu cha torati ya Musa, [Yehova] aliyowaamuru Israeli. Naye Ezra, kuhani, akaileta torati mbele ya kusanyiko, la wanaume na wanawake, na wote walioweza kusikia na kufahamu, siku ya kwanza ya mwezi wa saba. Akasoma humo mbele ya uwanja uliokuwa ukikabili lango la maji, tangu mapambazuko hata adhuhuri, mbele ya hao wanaume na wanawake, na wale walioweza kufahamu; na masikio ya watu wote yakakisikiliza kitabu cha torati.” (Neh. 8:1-3) Wale waliokuwako na Ezra, Walawi, walikuwa wakiwaeleza watu torati, hali watu wamesimama. “Nao wakasoma katika kitabu, katika torati ya Mungu, kwa sauti ya kusikilika; wakaeleza maana yake, hata wakayafahamu yaliyosomwa.” Matokeo? Kulikuwa na “kufanya furaha nyingi, kwa sababu walikuwa wameyafahamu maneno yale waliyohubiriwa.”—Neh. 8:6-8, 12.
BWANA YESU ALISOMA WAZIWAZI
10. Yesu alilionaje Neno lililoandikwa la Mungu na kusomwa kwake waziwazi?
10 Mwelezaji mkuu kupita wote wa Neno la Mungu lililoandikwa, Bwana Yesu Kristo, ni mfano mzuri sana wa mtu anayependezwa katika kufanya mapenzi na kazi ya Muumba wake na Baba, Yehova Mungu. Katika nyakati tatu mbalimbali alijaribiwa na Shetani Ibilisi, adui ya Mungu na mwanadamu vile vile, naye akakataa kuishuku hali yake na Yehova, akimkemea Shetani mara tatu kwa kulitumia Neno la Mungu mwenyewe, akisema, “Imeandikwa.” (Mt. 4:1-11) Katika ziara yake ya kwanza kwenye sinagogi katika Nazareti kama Masihi, alipewa kitabu cha kukunja cha nabii Isaya na, akipafungua ambapo kazi yake katika maisha ilionyeshwa, alilisomea waziwazi kundi lililokusanyika. Matokeo yakawa kwamba watu waliyastaajabia maneno ya kupendeza yaliyotoka kinywani mwake.—Luka 4:16-22.
11. Mtume Paulo alitiaje moyo kusoma kwa maneno ya kweli?
11 Vivyo hivyo wanafunzi wa Yesu walilisoma na wakajifunza Neno la Mungu lililoandikwa. Mtume Paulo aliwaandikia Wakolosai na akawatia moyo kwa maneno haya: “Waraka huu ukiisha kusomwa kwenu, fanyeni kwamba usomwe katika kanisa la Walaodikia pia; na ule wa Laodikia usomwe na ninyi.” (Kol. 4:16) Kwa kundi katika Thesalonike, Paulo aliandika: “Nawaapisha kwa Bwana, ndugu wote wasomewe waraka huu.” (1 The. 5:27) Kwa kijana Timotheo, Paulo alitoa onyo hili la upole: “Hata nitakapokuja, ufanye bidii katika kusoma na kuonya na kufundisha.”—1 Tim. 4:13.
KUSOMA AMBAKO KUNALETA FURAHA LEO
12, 13. Kwa kuwa “wakati uliowekwa u karibu,” katika Ufunuo 1:3, tunaombwa kufanya nini, na kwa faida gani?
12 Tukiwa na msingi huu juu ya hekima ya kusoma, kujifunza, na kulitumia Neno la Mungu wetu na Muumba kwa ufahamu, twaweza kushukuru zaidi kwa amri ya Ufunuo 1:3. Kwa kweli, ni ujumbe wa siku yetu. Chini ya uongozi wa roho ya Mungu mtume Yohana anaandika: “Mwenye furaha ni yeye anayesoma kwa sauti kuu na wale wanaosikia maneno ya unabii huu, na wanaoshika mambo yaliyoandikwa ndani yake; kwa maana wakati uliowekwa u karibu.”—Ufu. 1:3, NW.
13 Ili tuwe kati ya hawa wenye furaha, imetupasa tusome kwa sauti kuu na kuyasikia maneno ya unabii wa Mungu katika Ufunuo, na katika barua zote zilizoongozwa na roho ya Mungu 66 za Neno la Mungu, na lazima tutende kupatana na tunayoyasoma. Mtunga Zaburi anasema, kwa habari ya mtu mwenye furaha kweli kweli, kwamba “sheria ya [Yehova] ndiyo impendezayo, na sheria yake huitafakari mchana na usiku.” Matokeo? “Kila alitendalo litafanikiwa.” Lakini, “sivyo walivyo wasio haki”!—Zab. 1:1-4.
14. Ni kwa njia gani tengenezo la Yehova lionekanalo linavyojaribu kutusaidia katika kuyajua vema yaliyomo katika Neno la Mungu?
14 Vijana na wazee, wanaume na wanawake kati ya watu wa Mungu wanaitwa walisikilize na kujifunza kutoka kwa Neno la Mungu. Kwa sababu hii tengenezo la Yehova lionekanalo linachapa Biblia na vile vile magazeti, vijitabu, vitabu na vikaratasi vinavyokazia fikira zetu kwenye Biblia. Linadhaminia mikutano ya kawaida ya watu wa Mungu kila juma kwa saa tano za kujifunza. Hii ni pamoja na kusoma Biblia, maagizo katika Neno la Mungu kutoka katika jukwaa ya watu wote, kushiriki katika mazungumzo yaliyokusudiwa yatufundishe mambo ambayo Mungu angependa tufanye, na msaada wa kujifunza namna ya kuwasaidia wengine wajiunge nasi katika ibada safi.
15. Zaidi ya kusoma kwa waziwazi na kujifunza, tunatiwa moyo tufanye nini?
15 Kama vile katika siku za Israeli wa kale walipokuwako Walawi, makuhani na wanaume wazee walioongoza katika kusoma na kulitumia na kulifundisha Neno la Mungu, leo Yehova analo kundi la Kikristo lenye “wanaume wazee” wa kutusaidia katika kusoma na kulifahamu Neno la Mungu. Kuna baraza inayoongoza, na wako “wanaume wazee” katika makundi ya mahali. Wanakabidhiwa daraka la kusoma, kufundisha, kuonya, na kulitumia Neno la Mungu kwa halali. Kwa kweli, kati ya sifa za mzee au “mwanamume mzee,” mtume Paulo aliandika kwamba lazima awe “anayestahili kufundisha,” awe “mwalimu mzuri.” (1 Tim. 3:2; New English Bible) Zaidi ya hayo, tengenezo la Yehova lionekanalo linamtia kila mmoja wetu moyo ajifunze kwa faragha, asome kwa faragha, na kufanya hivyo kama jamaa na pamoja na marafiki.
16. (a) Taja mitego fulani iliyowafanya Israeli waache kufanya mapenzi ya Mungu. (b) Wakristo wanashindanaje na vizuizi vya namna ile ile?
16 Ili kuiepuka mitego ambamo Israeli waliangukia kuadibishwa kunahitajiwa hata zaidi leo kuliko kulivyohitajiwa katika siku ambazo taifa la Israeli lilikuwa watu waliokubaliwa wa Mungu. Kama vile wao walivyoacha kumtumikia Yehova, wakaacha kujifunza Neno lake na kulisikiliza likisomwa, kwa sababu ya mikazo kutoka kwa mataifa na watu waliokuwa karibu yao, ndivyo nasi tulivyo na hali kama hizo mbele yetu. Israeli walikuwa wamezungukwa na ibada ya kidini ya uongo pande zote, ibada ya Baali, ibada ya ndama, ibada ya sanamu. Tunakutana na ibada ya uongo leo duniani kote na katika njia zile zile. Kunayo mafundisho ya uongo ya kushindana nayo. Kunao utukuzo wa taifa au wa vyama. Kunayo filosofia yenye aibu ya kwamba anasa ndilo jambo zuri zaidi katika maisha. Ni vyepesi kuacha kujifunza Neno na amri za Mungu na kuacha kuyaongoza maisha yetu kwa sheria zake. Imetupasa tuzidi kujikumbusha wenyewe uhitaji wa kujifunza Neno la Mungu, tukishikamana kwa uaminifu na amri zake na kutafuta kumpendeza Muumba wetu, Yehova.
ISAIDIE JAMAA YAKO IWE YENYE FURAHA
17. Nini kinachoweza kusaidia kusoma Biblia kuwe kwenye maana zaidi kwa wale wanaofanya hivyo?
17 Katika jamaa linaweza kuwa jambo lenye msaada zaidi kusoma kwa sauti kuu na kufikiria maana ya Neno la Mungu. Kumbuka, katika siku za Ezra na Nehemia kulikuwako kusoma kwa sauti kuu kutoka kwa torati ya Mungu. Kulikuwako vile vile kutia ndani maana na ufahamu katika kusoma. Hii ni sehemu ya maana ya kusoma Neno la Mungu: kuiona maana kisha kufahamu ujumbe wake kama unavyotupasa sisi wenyewe.—Neh. 8:8.
18, 19. Eleza maana ya maneno ya Waebrania 2:1-4.
18 Kwa kuonyesha faida ya kusoma kwa sauti kuu labda katika kikundi cha jamaa au kati ya marafiki, kisha kuyafikiria yaliyosomwa, kuyafahamu, angalia Waebrania 2:1-4. Hapo twasoma: “Kwa hiyo imetupasa kuyaangalia zaidi [kuliko kawaida] hayo yaliyosikiwa tusije tukayakosa. Kwa maana, ikiwa lile neno lililonenwa na malaika lilikuwa imara, na kila kosa na uasi ulipata ujira wa haki, sisi je! tutapataje kupona, tusipojali wokovu mkuu namna hii? ambao kwanza ulinenwa na Bwana, kisha ukathibitika kwetu na wale waliosikia; Mungu naye akishuhudu pamoja nao kwa ishara na ajabu na nguvu za namna nyingi, na kwa magawanyo ya [roho takatifu], kama alivyopenda mwenyewe.” Ili tupate maana ya mistari hii, ebu na tuirudie habari hii. Kunayo mambo mengi tuwezayo kufahamu kwa njia hii.
19 Maneno yanayotangulia ya sura ya pili yanasema “kwa hiyo.” Hii inafungamanisha habari na sura ya kwanza ya Waebrania. Wakristo Waebrania walipaswa “kuyaangalia zaidi [kuliko kawaida] hayo yaliyosikiwa.” Kwa sababu gani? Kwa sababu yalisemwa na Mwana wa Mungu, yeye aliye mkuu kupita manabii wengine wote na hata mkuu kuwapita malaika. Kisha angalia kilichotukia kwa Waisraeli kwa sababu ya kutolijali ‘lile neno kama lilivyopelekwa kupitia kwa malaika,’ agano la Torati. Waliadhibiwa kwa sababu ya uasi wao wa makusudi kwa neno hilo, wakipata “ujira wa haki.” Kwa kuwa ndivyo ilivyo, je! twaweza kutazamia kupata mengine kuliko hayo kama tukikataa kuliangalia Neno la Mungu zaidi kuliko kawaida? Mstari wa nne unatusaidia kujua anayelitegemeza neno la Bwana Yesu. Na huyo ndiye nani? Muumba mwenyewe, Yehova Mungu, ambaye, kwa roho yake takatifu, alitoa ushuhuda juu ya maneno na kazi za Yesu. Ishara, mifano na kazi zenye nguvu zilizowezeshwa na Mungu zilionyesha ukweli na ruhusa ya kimungu ya kazi ya Yesu. Kwa mfano, angalia miujiza ambayo Yesu na mitume wake walifanya, kuwaponya viziwi, vipofu na vilema, kutoa mashetani, na hata kuwafufua wafu. Katika njia hizi tunao uhakika wa uhitaji wa “kuyaangalia zaidi [kuliko kawaida] hayo yaliyosikiwa.”
20. (a) Nini shauri la 2 Timotheo 2:15? (b) Basi imetupasa tuepuke nini? (c) Tuna usaidizi gani leo katika ‘kulitumia kwa halali neno la kweli’?
20 Kwa kusoma katika njia hii, tukiufuata mfano wa Ezra, makuhani na Walawi wa Israeli wa kale, na vile vile Yesu na mitume wake, twaweza kuuona msaada mkubwa sana tunaoweza kuupata katika kuona maana na ufahamu wa Neno la Mungu. Bila shaka, kuna jambo moja lililo la lazima kwetu kufanya, kama Paulo alivyomwonya Timotheo kwa upole: “Jitahidi kujionyesha kuwa umekubaliwa na Mungu, mtenda kazi asiye na sababu ya kutahayari, ukitumia kwa halali neno la kweli.” (2 Tim. 2:15) Imetupasa kuwa macho sikuzote ili tuwe na ufahamu unaofaa wa Neno la Mungu. Imetupasa tuepuke kuyapotosha Maandiko, kwa maana hii ingetuongoza kwenye maamuzi mabaya na inaweza kuwakwaza wengine. (2 Pet. 3:16) Vile vile imetupasa “kuepuka maneno yasiyo na maana yanayokichafua kilicho kitakatifu; kwa maana yataendelea kuwa yasiyo ya kimungu zaidi na zaidi.” (2 Tim. 2:16, NW) Hii maana yake ni kuwa wenye kuchagua habari za kusoma. Maandiko yanatuambia kwamba “hakuna mwisho wo wote wa kutunga vitabu vingi; na kusoma sana huuchosha mwili.” (Mhu. 12:12) Yehova kupitia kwa Mwanawe na utendaji wa roho takatifu amewamiminia watumishi wake waaminifu duniani baraka nyingi sana naye amezifungua akili na mioyo ya jamii yake ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” waifahamu maana iliyo ya kweli ya Neno lake. Nayo, jamii hiyo ya mtumwa mwaminifu inazipitisha kweli bora kwa watu kila mahali watakaojipatia hazina za kweli. Basi, tamaa yetu imepaswa kwa kweli iwe kulitumia Neno la Mungu kwa halali. Katika makala inayofuata, ebu na tuchunguze namna hii inavyoweza kufanywa kwa faida yetu tunapolisoma na kujifunza Neno la Mungu.
[Picha katika ukurasa wa 440]
Katika sinagogi katika Nazareti Bwana Yesu alisoma kwa sauti kuu kutoka kwa kitabu cha kukunja cha Isaya