Mna Haja ya Uvumilivu
“Mna haja ya uvumilivu, ili, mkiisha kuyafanya mapenzi ya Mungu, mpate kupokea utimizo wa ahadi.”—Ebr. 10:36, NW.
1. (a) Kwa sababu gani ilitazamiwa kwamba miaka ambayo ingefuata wa 1914 ingekuwa yenye magumu? (b) Ni magumu gani yaliyotabiriwa kwa ukweli sana?
MIAKA iliyofuata kuinuka kwa taifa juu ya taifa na ufalme juu ya ufalme katika mwaka wa 1914 imekuwa yenye magumu kwa taifa la kibinadamu, lakini haikupaswa itazamiwe kwamba ingekuwa tofauti. Unabii wa Biblia juu ya nyakati hizi ambamo tunaishi ulionyesha kwamba kungekuwa na “njaa, na matetemeko ya nchi mahali mahali” na kwamba mambo haya yote yangekuwa “mwanzo wa utungu” tu. (Mt. 24:7, 8) Ufunuo 12:12 ulitabiri kwamba ungekuwa wakati wa “ole” katika dunia kwa kuwa Ibilisi anajua ana “wakati mchache” tu. Mtume Paulo, katika 2 Timotheo sura ya 3, alionyesha sababu gani hizi “siku za mwisho” zingekuwa “nyakati za hatari,” wakati ambapo watu wengi wasingekuwa na imani wala ukamilifu.
2. Wakristo wangepaswa wavumilie hali gani zenye kujaribu?
2 Tena, unabii wa Yesu katika Mathayo sura ya 24 ulitabiri namna Wakristo katika siku hizi wangechukiwa na mataifa yote, wengine hata wakisalitiwa na kuuawa. Ungekuwa wakati ambapo kungekuwa na manabii wa uongo katika dunia, ambapo uasi ungeongezeka, ambapo upendo wa watu ungepoa. Na nyuma ya kueleza hali hizi zote zinazokuja, Yesu alisema: “Lakini mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka.”—Mt. 24:13; Ufu. 12:17.
3. (a) Habari inayolingana katika Luka 21 inaonyesha nini kingetukia kwa Wakristo? (b) Kwa sababu gani, basi, uvumilivu ni wa maana sana?
3 Kwamba uvumilivu huo katika nyakati kama hizi ni wa lazima sana kwa watumishi wa Mungu inatiliwa mkazo vile vile katika habari inayolingana ya unabii wa Yesu, katika Luka sura ya 21, inayotoa habari juu ya taabu na mateso yanayokaribia kuwapata Wakristo waaminifu wakati huu. Hapo Yesu alisema hivi: “Kwa uvumilivu kwa upande wenu mtajipatia nafsi zenu.” Kuupata uzima wa milele, basi, kunatiwa ndani.—Luka 21:12-19, NW.
4. (a) Ijapokuwa magumu yote ya ‘wakati wa mwisho,’ inawapasa Wakristo wafanye kazi gani ya kipekee? (b) Ni nini kinachohakikisha inafanywa ulimwenguni kote?
4 Pamoja na uvumilivu huu na taabu kwa miaka ya magumu, Wakristo walikusudiwa wajitie katika kuzihubiri habari njema za Ufalme katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote mbele ya kuja kwa mwisho wa taratibu hii ya mambo, kulingana na unabii wa Biblia. 1973 Yearbook of Jehovah’s Witnesses kinaonyesha kwamba kuhubiri huko sasa kunafanywa katika nchi 208 ulimwenguni kote.—Mt. 24:14.
5. Mfano wa Yesu Kristo unatusaidiaje?
5 Ni nini kinachowasaidia Wakristo kuvumilia katika hizi “siku za mwisho”? Miaka mingi imepita tangu mwaka wa 1914, wakati ambapo vita ya kwanza ya ulimwengu ilipoanza, na katika kipindi hiki watumishi wa Mungu wamepatwa na majaribu mengi. Chini ya hali kama hizo za majaribu jambo moja lililowasaidia sana sana ni mfano wa Kristo wa uvumilivu akiwa katika taabu. Petro anaukazia fikira zetu: “Kwa sababu ndio mlioitiwa; maana Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia kielelezo, mfuate nyayo zake. Yeye hakutenda dhambi, wala hila haikuonekana kinywani mwake. Yeye alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa haki.” (1 Pet. 2:21-23) Tunakumbuka ambavyo Yesu Kristo alivyomtegemea Baba yake na kuendelea kusali kwake. Sisi vile vile inatupasa tumwombe Yehova msaada wa kuvumilia.—Mt. 26:39, 42, 44.
6. (a) Kwa sababu gani inampasa mtu ajihadhari asije akaanguka? (b) Kwa sababu gani twaweza kumtegemea Yehova kwa msaada tunapokuwa katika jaribu?
6 Mbali na kuvumilia taabu, vile vile kuna haja ya kuyashinda majaribu. Maelezo ya juu ya Paulo ya mwenendo mbaya wa wanadamu katika “siku za mwisho” yalionyesha namna ambavyo uvutano wa kutenda mabaya ungekuwa wenye nguvu duniani. Kwa hiyo, inawapasa Wakristo waendelee kuwa waangalifu sana na kumtegemea Yehova sikuzote ili awasaidie wakati wa kujaribiwa. Katika 1 Wakorintho sura ya 10 Paulo alionyesha machache ya majaribu ambayo watumishi wa kale wa Yehova walipasishwa, kama vile ibada ya sanamu au uasherati, kisha akasema: “Kwa hiyo anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke. Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.”—1 Kor. 10:12, 13.
7. (a) Kuna vyanzo gani vya kutia moyo kwetu? (b) Ni uhakika gani unaweza kutoa kuonyesha kwamba wengine wanajiacha walegee kwa kiroho?
7 Yehova anatusaidia kuvumilia majaribu na kushinda taabu kwa kutupa uongozi wa kiroho na kututia moyo. Vile vile, Yehova amewapa watu wake ongezeko la ajabu ulimwenguni kote la mashahidi wenzetu, na hii inatutia moyo. Kwa kuwa tunapendana mtu na mwenzake, imetupasa sikuzote tuwe tukiwatia wengine moyo katika jamaa yetu na katika kundi. Ni wazi kwamba wengi wanatakiwa wasaidiwe kuujua uhitaji wao wa kiroho kwa kuwa, nyuma ya kufundishwa na kuanza kumtumikia Yehova, wengine wanajiacha walegee kwa kiroho; wanapoteza ubora wa haki ya Yehova na kuangukia hali ya kutotenda kwa habari ya mambo ya kiroho. (Mt. 5:3) Wale wanaokuwa wasiotenda hivyo imewapasa waamke na kuanza kutenda tena. Hii, basi, inatupa kazi nyingi sisi tulio na nguvu.a—Gal. 6:1.
8. Ni jambo zito namna gani kuwa asiyetenda, na hii inatokeza maulizo gani?
8 Inasikitisha kumwona mtu akianza kumtumikia Yehova kisha kupunguza mwendo, kwa sababu hii inaweza kumaanisha kukosa nafasi ya uzima wa milele kwa mtu huyo. (Ufu. 3:15, 16) Vivyo hivyo ndivyo ilivyo na hali ya wanaoshindwa na majaribu, kuvunja sheria za Mungu kwa uzito, na, kama matokeo, ikawa lazima waondolewe katika kundi. Inapokuwa lazima kutenga na ushirika, sikuzote kunafanywa kwa maana Neno la Mungu linaweka kanuni kwa washiriki wa kundi. (1 Kor. 5:9-13) Ulizo ni, Twawezaje kuyazuia mambo haya yasije yakatupata sisi wenyewe au wengine walio karibu nasi? Ni nini kinachoweza kufanywa kuuzidisha uvumilivu wetu?
KATIKA KARNE YA KWANZA C.E.
9. (a) Ni hali gani zilizofanya uvumilivu wa lazima sana kwa Wakristo Waebrania wa karne ya kwanza C.E.? (b) Ni nini kinachotusaidia kufahamu namna ya mikazo iliyowapata Wakristo Waebrania?
9 Mfano wa kupendeza wa namna ya kuwasaidia wengine wavumilie ni juu ya Waebrania ambao walipata kuwa Wakristo nyuma ya Pentekoste katika mwaka wa 33 wa Wakati wa Kawaida. Walikwisha acha nyuma mazoea yaliyoendeshwa chini ya agano la torati, kutia na kutoa kwa dhabihu za wanyama, kukubali ukuhani na kulitegemeza hekalu. Walikwisha kuukubali mpango mpya wa Mungu ulio bora, ambao ulianzishwa kupitia kwa dhabihu ya ukombozi ya Kristo Yesu. Wakristo hawa waliishi katika “wakati wa mwisho” wa “taratibu ya mambo” ya Kiyahudi na walikuwa wamekwisha vumilia kupinga kukali na kwa ushupavu kutoka kwa Wayahudi wenzao katika Yerusalemu na Uyahudi. Paulo mwenyewe alikuwa amepatwa na mateso yale yale ya kishupavu ya Kiyahudi mbele ya kupelekwa Rumi akatoe ombi lake mbele ya Kaisari. (Matendo sura za 22 na 23) Ijapokuwa hali hizo zenye mikazo, Wakristo Waebrania walipaswa washike ukamilifu. Tena, karibu tu mbele yao ulikuwako utimizo wa unabii wa Yesu katika Luka 21:20-24, ambao sasa tunajua ulikuwa wakati wa taabu sana kwao. Majeshi ya Kirumi yangeletwa kwenye eneo kwa sababu ya uasi wa Wayahudi (66 C.E.), halafu majeshi hayo yangerudishwa kwa ghafula, kuiruhusu nafasi kwa wale waliotii unabii wa Kristo wa kukimbia. Kwa kweli lingekuwa jaribu kwa ye yote aliyeona ubora mkubwa wa mambo ya kimwili. Ili kuziacha nyumba na mali na kuukimbia Uyahudi, walipaswa wawe wenye imani ya kweli. Kwa kweli, basi, ulikuwako utimizo mdogo wa Mathayo sura ya 24 na Luka sura ya 21, ambazo zina utimizo mkubwa zaidi wakati wetu. Kwa sababu ya hali zilizoko katika siku zetu tunaweza kufahamu, kwa kadiri fulani, namna ya mikazo waliyokutana nayo Wakristo Waebrania kwa kipindi cha miaka mingi katika karne ya kwanza C.E.—Tazama Mnara wa Mlinzi, Mei 1, 1969.
10. (a) Paulo aliwaandikia nini Waebrania? (b) Paulo aliwatiaje moyo, na kutazama nyuma kwenye majaribu yaliyopita kunamsaidiaje mtu kupambana kijasiri na litakalofuata?
10 Ilipoonekana kwamba wengine walikuwa wameanza kupoa katika kujitoa kwao, mtume Paulo aliandika barua kuwatia moyo. (Ebr. 13:22) Kwa kuchunguza ambayo mtume Paulo alisema, twaweza kujifunza namna ya kujisaidia wenyewe na kuwatia wengine moyo vile vile wapate kuvumilia. Njia moja nzuri ya kumtia moyo mtu ni kumkumbusha huyo namna Yehova alivyomtegemeza alipopatwa na majaribu makubwa. Paulo alisema: “Lakini zikumbukeni siku za kwanza, ambazo, mlipokwisha kutiwa nuru, mlistahimili mashindano makubwa ya maumivu; pindi mlipotwezwa kwa mashutumu na dhiki, na pindi mliposhirikiana na wale waliotendewa hayo. Maana mliwaonea huruma wale waliokuwa katika vifungo, tena mkakubali kwa furaha kunyang’anywa mali zenu, mkijua kwamba nafsini mwenu mna mali iliyo njema zaidi, idumuyo. Basi msiutupe ujasiri wenu, kwa maana una thawabu kuu. Maana mnahitaji saburi, ili kwamba mkiisha kuyafanya mapenzi ya Mungu mpate ile ahadi.” (Ebr. 10:32-36) Ndiyo, walikuwa wamepitia katika majaribu makali na wakapoteza nyingine za mali zao, lakini walikuwa wangali hai, wenye mavazi, chakula na mambo mengine ya lazima. Kwa hiyo wangeweza kumshukuru Yehova na kuendelea kumtumikia. Zaidi ya yote, walikuwa na tumaini la kupata uzima wa milele kwa kuvumilia. Kwa sababu ya haya yote ingewapasa waone kwamba Yehova angeweza kuwasaidia wayashinde majaribu mengi wakati ujao, kwa hiyo sababu gani waogope litakalofuata? Kutiwa moyo huko kulikusudiwa kuwatia nguvu hao Wakristo Waebrania katika kuona ubora wa mambo ya Yehova na zawadi itakayopatikana kwa kushika ukamilifu.
11. Ni nini kinachoonyesha kwamba wengine kati ya Waebrania walikuwa wameacha kuwa macho kwa kiroho, na kwa sababu gani ni hatari kuwa katika hali hiyo?
11 Paulo aliwaandikia waziwazi sana Wakristo hawa. Walikwisha ‘kuwa wavivu wa kusikia.’ (Ebr. 5:11) Hii haikumaanisha kwamba masikio yao yaliacha kusikia, bali, kusikia kwao kwa kiroho na kuwa macho kwa mambo ya kiroho kulidhoofika. Walikuwa wameonyesha ubaridi fulani kwa Neno la Yehova na makusudi yake, wakiwa hawajali haja zao za kiroho. Pengine hawakuona hatari ya hali yao. Alipaswa mtu fulani awaamshe. Kwa hiyo Paulo alieleza haja yao ya wakati huo kama “ikitaka mtu fulani awafundishe tangu mwanzo mambo ya msingi ya matangazo matakatifu ya Mungu.
12. (a) Ni njia gani bora ya kumsaidia mtu ambaye amekuwa mvivu katika kusikia kwa kiroho? (b) Paulo alisema nini kuwatia moyo wasiridhishwe na kweli ya msingi, bali wapone?
12 Huo ndio utaratibu wenyewe wa kuwasaidia wanaokuwa wasiotenda na kulala kwa njia ya kiroho, yaani, kuwafundisha kweli mara nyingine. Wakiwa wavivu katika kusikia kwao kwa mambo ya kiroho wanashindwa kukitwaa chakula kigumu cha Neno la Mungu. Kwa kiroho wanakuwa vitoto, wakinywa maziwa peke yake, bila kuzifahamu kweli zenye nguvu za Neno la Mungu. (Ebr. 5:13) Kitoto kinahitaji mtu wa kukitunza, kwa kuwa hakiwezi kujitunza chenyewe. Hakiwezi kufanya maamuzi juu ya wema na ubaya. Bila shaka Wakristo hawastahili kuwa hivyo, kwa maana kufanya uamuzi usiofaa kunaweza kumaanisha kupoteza kibali cha Yehova na uzima wenyewe. Ikiwa watavumilia inawapasa wale chakula kigumu, kuutumia uwezo wao wa akili na Maandiko, na kuwa na msingi wa kuamua kinachofaa na kisichofaa. Kwa habari ya Waebrania, Paulo aliwavuta wauzidishe ujuzi wao wa kweli na kusonga mbele hata kukomaa. (Ebr. 6:1, 2) Wakristo hao hawakuwekwa na Paulo katika kundi moja na wale walioanguka wasiweze kupona, bali, yeye alisema: “Katika habari zenu tumesadiki mambo yaliyo mazuri zaidi, na yaliyo na wokovu. Maana Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu, na hata hivi sasa mngali mkiwahudumia. Nasi twataka sana kila mmoja wenu aidhihirishe bidii ile ile, kwa utimilifu wa matumaini hata mwisho; ili msiwe wavivu, bali mkawe wafuasi wa hao wazirithio ahadi kwa imani na uvumilivu.” (Ebr. 6:9-12) Maneno hayo ya Paulo ni ya kutia moyo sana kwetu vile vile.
KUJENGA KUONA UBORA
13. Katika sura ya kwanza ya barua yake kwa Waebrania, Paulo alianzaje kujenga kuona ubora wa ambayo Yehova alikuwa amefanya?
13 Tunapochunguza barua hii iliyoandikwa na mtume Paulo, tunaona haja ya Wakristo kujenga kuona ubora wa mambo ya kiroho katika akili za Wakristo wengine. Pale pale mwanzoni mwa barua yake, katika sura za kwanza na pili, mtume alitaja namna Yehova alivyozungumza kale kwa watumishi wake kupitia kwa manabii (waliopokea habari kutoka kwa malaika mara nyingi). (Linganisha Wagalatia 3:19.) Waebrania walifahamiana sana na historia na walijua namna Yehova alivyokuwa amewatumia malaika katika kushughulika na babu zao. Hiyo ilikuwa ajabu. Kama mmoja wetu angezungumziwa yeye mwenyewe na malaika wa Yehova asingelisahau jambo hili kwa muda wa maisha yake yote. Lakini katika karne ya kwanza jambo fulani la pekee lilikuwa limefanywa kwa Wakristo. Jambo fulani kubwa zaidi lilikuwa limetukia. Mungu alikuwa amesema kwa kumtumia Mwanawe, aliyekuwa na cheo kikubwa zaidi kuliko kile cha malaika. “Je! yuko malaika [Mungu] aliyemwambia wakati wo wote, Uketi mkono wangu wa kuume hata nitakapoweka adui zako chini ya nyayo zako?”—Ebr. 1:13.
14. Kwa sababu gani ni lazima kuyaangalia zaidi kuliko kawaida mambo tuliyoyasikia?
14 Kwa kuona ubora wa kweli hizi kuu Mkristo mwenye busara anaona namna ilivyo bora kuyasikiliza anayosema huyu Mwana wa Mungu. Kwa hiyo Paulo anaendelea kuandika: “Ndiyo sababu ni lazima kwetu tuyaangalie zaidi kuliko kawaida mambo yaliyosikiwa na sisi, tusije tukapeperushwa kamwe. Kwa kuwa ikiwa neno lililosemwa kupitia kwa malaika lilikuwa imara, na kila kosa na tendo la kutokutii lilipata adhabu kulingana na haki; tutaokokaje ikiwa tumeudharau wokovu mkuu namna hiyo kwa kuwa ulianza kusemwa kupitia kwa Bwana wetu na ukahakikishwa kwetu kupitia kwa waliomsikia yeye?” (Ebr. 2:1-3, NW) Kwa hiyo, tusipokuwa na nia ya kuyaangalia zaidi kuliko kawaida yaliyosikiwa nasi, bila shaka tutarudi nyuma polepole na kuupoteza uzima wa milele.
15. (a) Tunawezaje kutumia mashua kufananisha kurudi nyuma? (b) Eleza namna Mkristo anavyoweza kurudi nyuma kutoka kwa Mungu na kundi la Kikristo.
15 Inapendeza sana kuona kwamba Paulo alitumia usemi huu “tusije tukapeperushwa kamwe.” Pengine umemwona mtu fulani katika mashua ndogo akifanya haraka kuondoka anapofika pwani, bila kuifunga mashua. Ikiwa mtu anatazama ataona kwamba mwendo wa mashua kutoka pwani mara ya kwanza ni wa taratibu, ikitegemea mikondo na upepo. Lakini kwa kadiri wakati unavyopita, ndivyo mashua inavyochukuliwa mbali zaidi na zaidi katikati ya ziwa. Kwa upande mwingine, ikiwa mtu hakuwa akitazama wakati wote, huenda akagutuka muda kidogo nyumaye kuiona mashua imekwisha fika katikati ya ziwa. Kwa hiyo mwendo wa kurudi nyuma kwa kawaida ni wa taratibu, na hili ndilo linaloweza kutukia kwa Wakristo wanapoacha ‘kuyaangalia zaidi kuliko kawaida mambo yaliyosikiwa,’ wanapokuwa ‘wavivu katika kusikia kwao.’ Kwa kadiri ambavyo kuacha kuona ubora wa mambo ya kiroho kunavyokua, ndivyo mtu polepole anavyokuza tabia mbaya, labda kushindwa kujifunza, kisha kukosa mikutano ya Kikristo. Kuwa asiye wa kawaida katika kuwaambia wengine habari njema si jambo linalotukia kama mashua yenye mwendo wa kasi sana inayotaka kuvuka ziwa, bali ni mwendo wa taratibu, kama vile mtumbwi, inchi kwa inchi, unavyosogea ukiiacha nanga salama. Kwa kweli ni ambavyo mtume Paulo anavyokuita, ‘kuudharau wokovu.’
16. (a) Ni kweli gani za maana imetupasa tuone ubora. wazo, kama zinavyotajwa katika Waebrania 2:10, 14, 18? (b) Imetupasa tufanye nini uvumilivu wetu unapojaribiwa?
16 Adui yetu, yeye anayeleta taabu na kupoteza wokovu, ni Shetani Ibilisi. Kwa kuja kwa Kristo Yesu njia ya kumharibu Ibilisi ilipatikana. Kristo akawa Wakili Mkuu wa wokovu na akapatwa na kifo ili aufanye mpango huu. (Ebr. 2:10, 14) Bila shaka mpango huu mzuri mno wa wokovu umepaswa utazamwe kwa shukrani nyingi na Mkristo. Paulo alitilia mkazo kwa ndugu zake Waebrania wenye kutaabika kwamba Kristo Yesu anafahamu hali yetu; yeye vile vile alitaabika kama mwanadamu wakati mmoja. Paulo alikuwa mwenye kutia moyo sana katika kuonyesha uhakika huu: “Kwa kuwa mwenyewe aliteswa alipojaribiwa, aweza kuwasaidia wao wanaojaribiwa.” (Ebr. 2:18; 4:15, 16) Ah, ndiyo, Wakristo wanajua yuko Kristo anayeishi katika mbingu aliye tayari kuja kuwasaidia wanapojaribiwa! Kwa hiyo uombe msaada huu wa kimungu wakati mwingine uvumilivu wako na ukamilifu vitakapokuwa vikijaribiwa sana.
[Maelezo ya Chini]
a Kwamba kuna hatari kubwa ya kushindwa kuvumilia kama Mkristo inaonyeshwa na mambo ya hakika. Mnamo mwaka wa utumishi wa 1970, tukichukua nchi moja tu kama mfano wa ugumu huu, United States ilionyesha jumla ya watu 13,732 waliokuwa wasiotenda kwa habari ya kuhubiri kwa waziwazi kwa habari njema, hili likipaswa kuangaliwa kwa kiroho na waangalizi wa makundi wa huko. Walikuwako watu wengine 4,332 waliotengwa na ushirika kwa kuvunja kwa uzito sheria za haki za Mungu. Kwamba wengine wanaotengwa na ushirika wanatubu na mwishowe kurudishwa tena katika makundi inaonyeshwa wazi katika jumla ya watu 1,642 waliokuwa wameondolewa miaka iliyotangulia na waliorudishwa mnamo mwaka wa utumishi wa 1970. Kwa jumla, katika United States katika mwaka wa 1970, watu 13,469 walianzishwa tena katika utendaji. Ijapokuwa tarakimu hizi ni ndogo zikilinganishwa na kilele cha United States cha watangazaji wa Ufalme 388,920, zinapaswa zimwamshe kila mmoja ayaangalie mambo ya kiroho na kuendelea kuwa mwenye nguvu kwa kiroho.—1 Tim. 4:16.
[Grafu katika ukurasa wa 319]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
ONGEZEKO KATIKA WATANGAZAJI WA UFALME TANGU MWAKA WA 1920
Yehova amewapa watu wake ongezeko kubwa ulimwenguni kote la Mashahidi wenzao. Hii inatutia sisi moyo na kutusaidia tuvumilie
1920 8,402
1940 74,804
1960 851,378
1972 1,596,442
[Picture katika ukurasa wa 322]
Nyakati zilizopita Mungu alisema kwa wanadamu kupitia kwa malaika, kama vile kwa habari ya Manoa na mkewe. Lakini katika karne ya kwanza Mungu alimtuma Mwana wake mzaliwa pekee aje kusema kwa wanadamu. Tunaweza kuyasoma maneno ya Mwana katika Biblia.