Wakati wa Kuamua Kutembea kwa Jina la Mungu Gani
1. Je! hekalu hilo la pili katika Yerusalemu ndilo ambalo mataifa na makundi ya watu wangelijia kumwabudu Yehova milele, na kwa sababu gani?
HEKALU la pili lililojengwa Yerusalemu, siku za nabii Zekaria, lilikuwa mfano tu na, likiwa hivyo, lilikuwa na maana ya unabii. Halikuwa hekalu la milele ambalo kwalo mataifa yote na makundi ya watu walipaswa kuja kumwabudu Yehova Mungu milele. Kwa sababu ya uhakika huo, hekalu la kidunia la Yerusalemu liliharibiwa mwaka wa 70 C.E., wakati Yerusalemu ulipoharibiwa mara ya pili, wakati huu na majeshi ya Mamlaka ya Sita ya Ulimwengu, Milki ya Kirumi.
2. Ni nani aliyetoa unabii juu ya hili, na nyakati alizotaja zilikwisha lini?
2 Hii ilikuwa imekwisha semwa na Yesu Kristo miaka 37 mapema, mwaka wa 33 C.E., na alisema kwamba nyuma ya hapo Yerusalemu ungeendelea kukanyagwa mpaka yatimie “majira ya Mataifa” (“nyakati zilizowekwa za mataifa”). (Luka 21:20-24) Majira ya Mataifa hayo, saba kwa jumla, yalianza katika ukiwa wa kwanza wa Yerusalemu na nchi ya Yuda ulioletwa na Wababeli mwaka wa 607 B.C.E. Yerusalemu haukumpata tena mfalme wa ukoo wa kifalme wa Daudi juu ya kiti chake, na kwa kulingana Majira ya Mataifa hayo yaliendelea kwa miaka 1,844 nyuma ya uharibifu wa pili wa Yerusalemu wa kidunia. Hiyo maana yake ni kwamba Majira ya Mataifa hayo yalikwisha mwaka wa 1914 C.E.
3. Ni ulizo gani linalotokea juu ya ujenzi wa hekalu la tatu kwa Yehova Yerusalemu kwa kuwa Majira ya Mataifa yalikwisha mwaka wa 1914, na kuenea kwa ibada ya Yehova kunategemea hekalu kama hilo?
3 Hii haikumaanisha kwamba mwisho wa Majira ya Mataifa mwaka wa 1914 ulionyesha wakati wa kujenga upya hekalu la tatu kwa ibada ya Yehova Yerusalemu. Hapana, ingawa mwanzo wa Majira ya Mataifa, mwaka wa 607 B.C.E. katikati ya wakati wa joto na wa baridi, hekalu la Yehova liliachwa likiwa magofu na ukiwa bila waabudu katikati ya nchi yenye ukiwa bila mwanadamu na mnyama wa kufugwa. Haikutakiwa hekalu la kidunia la kuonekana lijengwe Yerusalemu kwa ibada ya Yehova, lichukue mahali pa msikiti wa Kiislamu, Kuba la Mwamba, ulioko hata sasa. Wala mwanzo wala kuenea kwa ibada ya Yehova nyakati za kisasa havikutegemea kusimamishwa kwa hekalu kama hilo huko, ili mataifa yalimiminikie huko. Sababu ya kutokuwa hivyo tutaiona karibuni.
4. Ni kwa kadiri gani ibada ya Yehova ilikuwa imefifia kufikia mwaka wa 1914 C.E., na nini ambacho hata Wanafunzi wa Biblia hawakufahamu juu ya jina lake?
4 Duniani ibada ya Yehova kama Mungu ilikuwa imefifia mwaka wa 1914 C.E. Ndiyo, hata kati ya wale waliodai kuwa Wakristo, si kutia ndani na Wayahudi wa asili, waliotahiriwa. Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, iliyotokea mwaka huo, iliifanya ibada ya Yehova ififie hata zaidi. Shirika la Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote, ambalo lililikataa fundisho la Utatu kwa sababu ya kutopatana kwalo na Maandiko, bado lilitatanishwa katika ufahamu kwa njia fulani kwa sababu ya matumizi ya tafsiri za Biblia zilizoamriwa kwa kawaida (kama Authorized au King James Version) zilizokuwa na jina la Yehova mara chache au ambazo hazikuwa nalo hata kidogo. Lakini, kupitia kwa safu za gazeti la The Watch Tower walitokeza makala zilizoitwa kwa kufaa kama vile “Kuwako kwa Milele kwa Yehova pamoja na Watu Wake” (10/1/14), “Yehova Mungu Wetu ni Mmoja” (8/15/15), “Yehova Anausafisha Ulimwengu” na “Tendo la Yehova—Tendo Lake la Ajabu” (1/1/16), na“Yehova Mwangalizi wa Wakati Asiyekosea” (3/15/19). Lakini, hao Wanafunzi wa Biblia hawakufahamu wakati huo kwamba wakati ulikuwa karibu wa Yehova Mungu kujifanyia mwenyewe jina.—Isa. 63:14.
5. Maandishi ya walio wengi wa waliodai kuwa Wakristo yalikuwa nini wakati wa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, na sababu gani hii inamkumbusha mtu juu ya Mika 3:9, 10 linavyosema?
5 Lakini, je! nini kingesemwa juu ya shirika kubwa zaidi la wale waliodai kuwa Wakristo, yaani, lile tengenezo la ulimwengu wote la kidini linaloitwa Kristendomu? Yalikuwa ni mauaji ya siri ndani ya mipaka yake yaliyochochea Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, iliyoanza Julai 28, 1914. Mwishoni mwa Majira ya Mataifa karibu na Oktoba 4, 1914, mataifa manane na milki za Kristendomu, pamoja na Japan, walikuwa wakipigana wao kwa wao. Na mwishoni mwa vita hiyo Novemba 11, 1918, yalikuwako mataifa 24 ya Kristendomu pamoja na nchi nne zisizo za Kikristo, waliokuwa wakipigana wao kwa wao. Tofauti na Shirika la Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote, makanisa na matengenezo ya kidini ya Kristendomu, vile vile Uyahudi na Uislamu, yalijitia katika vita hiyo. Washiriki wa makanisa hayo walioongoza umwagaji huu wa damu wa ulimwengu wote walikumbusha mojawapo la maelezo ya unabii wa Mika juu ya wakuu wa Yuda na Yerusalemu siku zake katika ‘kuijenga Sayuni kwa damu, na Yerusalemu kwa uovu.’—Mik. 3:9, 10.
6. Wakuu na viongozi wa kidini wa Kristendomu walilinganaje na maelezo yaliyotolewa na Mika, na ni mfano gani wa kutokeza ulikuwako juu ya Kristendomu ‘kulipotosha kila tendo adilifu’?
6 Wakati wa miaka hiyo minne na miezi mitatu na nusu ya vita kati ya bara zote, je! waamuzi katika Kristendomu walikuwa wakipotosha hukumu wapate rushwa, je! mapadre wa kidini walikuwa wakiifanya dini biashara kwa kutoa utumishi wao walipwe, je! manabii wa kidini walikuwa wakitoa unabii wao usiolingana na Maandiko kuwafurahisha watu wapate fedha? Ndiyo, sawasawa na watu kama hao walivyokuwa wakifanya kati ya watu wateule wa Yehova siku za Mika. Haki ya kweli ilichukiwa na ‘kila tendo adilifu lilipotoshwa.’ Hili lilitokeza wazi katika shughuli za Kristendomu kwa Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote, ambao walikataa kuchangamana na siasa na ambao hawakutaka sehemu yo yote katika vita juu ya maulizo ya kisiasa na ya kibiashara, vita ambayo haikuwa ya kitheokrasi. Mateso, marufuku yenye vizuizi na vifungo aliwaletea Wanafunzi wa Biblia hawa waaminifu, na wakati wa hari ya mapema ya mwaka wa 1918 alifanya rais wa Shirika la Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote na washiriki wengine saba na Watch Tower Society wafungwe katika Gereza la Serikali katika Atlanta, Georgia, U.S.A., wanyimwe dhamana na rufani.
7, 8. (a) Hivyo ibada ya Yehova ilikuwa ikibomolewa na tengenezo gani la kidini? (b) Makao ya kiroho ya waabudu Yehova yaliharibiwaje, kulingana na Mika 3:12?
7 Bila shaka huko kulikuwa ni kubomoa ibada ya Yehova! Na nani? Na Babeli Mkuu wa kisasa, milki hii ya ulimwengu ya dini ya uongo ikitawaliwa na sehemu yake iliyo na wengi zaidi na yenye nguvu, yaani, Kristendomu. Ndiyo, Kristendomu, aliye na Biblia yote ambamo jina Yehova linapatikana, ndiye zaidi aliyetumikia kama wakili wa Babeli Mkuu kwa kuiharibu ibada ya Mungu Aliye Juu Zaidi Yehova. Kristendomu alikuwa akiiacha ibada yake Yeye ukiwa ndani yake mwenyewe. Alikuwa akiiharibu kati ya Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote, waliokuwa wakiifufua ibada ya Yehova kama Mungu na Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo. Kama matokeo, mwishoni mwa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu mwaka wa 1918 katikati ya wakati wa joto na baridi, si kwamba tu sehemu nyingi za ardhi ziliharibiwa na vita, lakini vile vile makao ya kidunia ya kiroho ya waabudu Yehova yaliharibiwa, yaani, kwa kadiri matumaini ya kurudishwa kwa kiroho na kukaliwa tena yalivyopaswa. Ililingana na aliyokuwa amesema Mika juu ya nchi yake mwenyewe kwa sababu ya ukatili wa Babeli:
8 “Sayuni utalimwa kama shamba lilimwavyo, na Yerusalemu utakuwa magofu; na mlima wa nyumba utakuwa kama mahali palipoinuka msituni.”—Mik. 3:12.
KURUDISHWA KWA KIMWUJIZA
9. (a) Sababu gani haikuwa lazima kwa makao ya kiroho ya waabudu Yehova kuachwa ukiwa kwa miaka 70? (b) Nyuma ya mwisho wa Majira ya Mataifa mwaka wa 1914, sehemu ya kati ya ibada ya Yehova inapaswa kuwa nini?
9 Haikuwa lazima, hata hivyo, kwa makao ya kiroho ya waabudu Yehova kuachwa katika hali hiyo ya kuharibika kwa miaka 70, kama vile nchi ya Yuda, iliyoachwa ukiwa bila mwanadamu au mnyama wa kufugwa kwa miaka 70 ya kwanza ya “majira ya Mataifa.” (Luka 21:20-24; 2 Nya. (Sik.) 36:20, 21) Hali iliyofunuliwa waziwazi ya mfano wa kufa ya mashahidi wa Yehova ilikwisha semwa mapema kuwa ya muda mfupi tu, kama siku tatu na nusu. (Ufu. 11:3-12) Majira ya Mataifa tayari yalikwisha, nyuma mwaka wa 1914, wakati ambao taifa liliinulia taifa upanga na wakaanza kujifunza vita kwa kadiri ya ulimwengu wote wengi wakikusanywa waingie vitani na mauaji mengi yakiwako. Mwishoni mwa Majira ya Mataifa hayo wakati tayari ulikwisha wa haki ya Yerusalemu kwa ufalme wa Kimasihi kukanyagwa na mataifa yasiyo ya Kiyahudi, na ufalme wa Kimasihi wa Yehova mikononi mwa mrithi wa haki wa Mfalme Daudi, Yesu Kristo, ulizaliwa mbinguni, katika “Yerusalemu wa mbinguni.” Kwa zaidi ya karne kumi na moja Yerusalemu wa kidunia alikuwa amekuwa sehemu ya kati ya ibada ya Yehova. “Yerusalemu wa mbinguni,” ufalme wake wa Kimasihi ukitawala, lazima sasa aendeleze ile ile ibada.
10, 11. (a) Kwa hiyo “Yerusalemu wa mbinguni” alitenda kwa kufaa kutimiza nini duniani? (b) Kulingana na Mika 4:1, hili lilipaswa kutukia lini, na kwa matokeo gani kwa watu?
10 Kulingana na hili, “Yerusalemu wa mbinguni,” sehemu ya kati ya kimbinguni ya ibada ya Yehova, alitenda sawa kutimiza kurudishwa kwa mapema kwa ibada ya Mungu wake duniani, na hivyo kwa kadiri isiyoonekana wakati wo wote mbeleni. Unabii wa mnenaji wa Yehova, Mika, ulikuwa umesema hili, na utimizo wa unabii mtukufu umekuwa wa ajabu. Akiendelea kutoa unabii juu ya kurudishwa, Mika aliongozwa na roho ya Mungu kusema: “Itakuwa katika siku za mwisho.” Hivyo ni kusema, nyuma ya uharibifu wa kutisha wa Sayuni na Yerusalemu na “mlima wa nyumba” ambao Mika alitoka tu kusema mapema katika mstari uliotangulia. (Mik. 3:12; 4:1) Ni nini kilipaswa kutukia? Geuzi la kustaajabisha! Sikiza:
11 “Lakini itakuwa katika siku za mwisho, ya kwamba mlima wa nyumba ya [Yehova] utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na watu wa mataifa watauendea makundi makundi.”—Mik. 4:1.
12. Ni nini uliokuwa utimizo mdogo wa unabii huo na ni nini linalolingana na hilo nyakati za kisasa?
12 Kadiri ndogo ya utimizo wa unabii huo ilianza mwaka wa 537 B.C.E. walipofunguliwa mabaki waaminifu wa Kiyahudi kutoka Babeli, kwa kupewa maagizo ya kifalme kurudi Yerusalemu na kuijenga upya nyumba ya Yehova ya ibada juu ya kilele cha mlima wa mji. Kwa kuwa Majira ya Mataifa yalimalizika mwaka wa 1914 C.E., tunaishi katika “wakati wa mwisho” wa Mataifa, ambao kutawala kwao zaidi dunia kumekaidiwa na ufalme wa Kimasihi wa Yehova Mungu uliozaliwa karibuni mbinguni. (Dan. 12:4; Mt. 24:3-14) Kwa wakati wake barabara, mwaka wa kwanza nyuma ya vita, yaani, mwaka wa 1919, kufunguliwa kwa kimungu kwa waabudu Yehova waliookoka kwa uaminifu maono ya kuhuzunisha ya Vita ya Kwanza ya Ulimwengu kulitukia, kufunguliwa huku kukijulikana sana kwa kufunguliwa kwa baraza inayoongoza ya Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote katika Gereza la Serikali, ambao walijua wazi kwamba ufalme uliosimamishwa wa Yehova lazima utangazwe kwa mataifa yote katika dunia yote inayokaliwa, kwa ushuhuda.
13. Ni kwa kadiri gani mabaki ya kisasa wamekweza cheo cha ibada ya Yehova?
13 Kama mabaki hayo yaliyorudishwa ya Kiyahudi waliojitia katika kujenga upya nyumba ya Yehova juu ya kilele cha mlima wa Yerusalemu, ndivyo mabaki ya kisasa ya waabudu Yehova yalivyojitia katika kuendeleza ibada Yake safi, wakiiinua juu ya mambo mengine yote wapendayo ya maisha ya kidunia. Ibada hii inayostahili ya Mungu aliye wa pekee wa kweli lazima liwe jambo la kukwezwa zaidi katika maisha zao. Hakuna ibada nyingine yo yote, hata iwe inakwezwaje na wanadamu, inayopaswa kuruhusiwa kuwa juu zaidi ya ibada ya Mungu Aliye Juu Zaidi, Yehova. Cheo chake lazima kiwekwe imara juu ya namna zote za ibada ya kibinadamu, bila kujali zinavyotukuzwa na wanadamu na mashetani.
14. (a) Sababu gani Yehova hakuyaamuru mabaki ya Israeli wa kiroho kulijenga upya hekalu Yerusalemu? (b) Ni hekalu gani wanalopaswa kushukuru, na sababu gani?
14 Kwa hiyo mabaki haya yenye uaminifu wa Waisraeli wa kiroho hawakujitia katika ujenzi wa hekalu la kuonekana katika Yerusalemu wa kidunia. Hekalu ambalo Yehova alikuwa ametangaza liharibiwe na Warumi mwaka wa 70 C.E. hakuwaamuru mabaki wa Waisraeli wa kiroho walijenge upya huko. Yeye hataki hekalu kama hilo la kujengwa na mwanadamu katika palipokuwa mahali patakatifu wakati mmoja, kwa kuwa ametuambia waziwazi kwamba haishi katika mahekalu yaliyojengwa kwa mikono ya kibinadamu. Yeye analo hekalu lake la kweli, la kiroho ambamo yeye mwenyewe anaishi. Ni katika hekalu ndani ya chumba cha Patakatifu Sana ambamo Kuhani Mkuu wake Yesu Kristo aliingia katika masika ya mwaka wa 33 C.E., akiwa na ustahili wa bei kubwa ya dhabihu yake kamilifu ya kibinadamu kwa ajili ya wanadamu wote wenye dhambi, wanaokufa. (Ebr. 9:24-26; Matendo 7:24) Ni hekalu hili la kiroho tunalopaswa kushukuru, na kwa hiyo tumpe Mungu Aliye Juu Zaidi adhama yake ya kweli na utakatifu na utukufu. Ni kwenye hekalu hili tunapopaswa kukaribia kwa roho ya unyofu ya ibada, na hili twaweza kufanya po pote duniani, kwa kuwa ndivyo alivyosema Yesu Kristo mwenyewe, Kuhani Mkuu wa Yehova. (Yohana 4:21-24) Yerusalemu wa kidunia hana maana tena!
15, 16. (a) Mwaka wa 1925, mabaki walianza kufahamu nini juu ya jina la Mungu, na sababu gani wakajipa jina jipya mwaka wa 1931? (b) Hii ilikuwaje kwa utimizo wa Zekaria 10:9-12?
15 Kadiri miaka iliyofuata vita ilivyosonga mbele, hesabu ya Waisraeli wa kiroho waliojitoa katika kazi hii ya ujenzi wa mfano wa hekalu iliongezeka. Walikuwa Wakristo, wafuasi wa nyayo za Yesu Kristo, lakini safu ya washiriki wa makanisa wa Kristendomu vile vile ilidai kuongezeka. Kwa hiyo ni kwa jina la nani mabaki haya yenye kujenga hekalu ya Waisraeli wa kiroho walichagua kutembea? Ulikuwa uamuzi wa maana kwao kufanya. Tangu mwaka wa 1925 na kuendelea walianza kufahamu kwamba wakati ulikwisha fika wa Mungu Aliye Juu Zaidi kujifanyia mwenyewa jina. Walijitahidi wasilisingizie jina hilo pamoja na Wakristo wa kujidai wa Kristendomu. Kwa hiyo, nyuma ya miaka sita ya kujitahidi sana kufanya jina la kimungu lijulikane ulimwenguni kote, walikubali kwa moyo kujipa jina lenye msingi wa Maandiko, mashahidi wa Yehova, wakati wa hari ya mwaka wa 1931. Hili limetukia kwa utimizo wa unabii uliosemwa na Zekaria siku za kujenga upya hekalu katika Yerusalemu karne ya sita B.C.E.:
16 “Nao watanikumbuka katika nchi zilizo mbali; nao watakaa pamoja na watoto wao; tena watarudi. . . . Nami nitawatia nguvu katika [Yehova]; nao watatembea huko na huko katika jina lake, asema [Yehova].”—Zek. 10:9-12.
17, 18. (a) Tangu wakati huo, watu wa mataifa wamejuaje juu ya Yehova Mungu na hekalu lake la kweli la ibada? (b) Mika 4:2 palisemaje juu ya makundi ya watu ambao wangemiminika kwenye hekalu?
17 Kwa hiyo, tangu wakati wa uamuzi huo wa kihistoria mwaka wa 1931 C.E., mabaki haya yenye kujenga hekalu ya Waisraeli wa kiroho wamekwenda katika Mataifa yote wakizihubiri habari njema za ufalme wa Kimasihi wa Mungu kwa jina la Yehova, kama mashahidi wake wa Kikristo. (Isa. 43:10-12; 44:8) Kama matokeo ya hili yasiyoepukika, je! watu makundi makundi wa mataifa wamekuja kujifunza juu ya Yehova kama Mungu na juu ya hekalu lake la kiroho palipo pa kutolea ibada safi? Habari zinazomiminika kutoka sehemu zote za dunia zinajibu kwa uhakika Ndiyo! Angalia anavyosema nabii Mika juu ya watu hawa makundi makundi wanaolimiminikia hekalu la Yehova:
18 “Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa [Yehova], na nyumbani kwa Mungu wa Yakobo; naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake; kwa maana katika Sayuni itatoka sheria, na neno la [Yehova] litatoka Yerusalemu.”—Mik. 4:2.
19. (a) “Sheria” na ‘neno la Yehova’ vimetokaje katika Yerusalemu wa kimbinguni kwa makundi ya watu na mataifa? (b) Kusema kwao, “Tutakwenda katika mapito yake,” kunamaanisha nini kwa upande wao?
19 Kwa kazi za kuhubiri na kufundisha za mabaki yenye kujenga hekalu ya Waisraeli wa kiroho duniani kote ujuzi wa “sheria” na ‘neno la Yehova’ vimetoka Sayuni wa kimbinguni na Yerusalemu wa kimbinguni, makao ya ufalme wa kimbinguni uliozaliwa karibuni wa Masihi. Ripoti zinajazana mwaka kwa mwaka kuonyesha kwamba watu mmoja mmoja wa mataifa yote wanamiminika kwenye ‘nyumba ya Yehova’ iliyokwezwa kumwabudu Yeye katika hekalu lake la kiroho. Maana yake nini kwa watafutaji wa Yehova hawa kusema: “Naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake”? Maana yake ni kwamba watu hawa waliofundishwa wa mataifa yote wanajiweka wakf wenyewe kwa Yehova Mungu, kuyafanya mapenzi yake. Wanamchagua Mungu wao.
20. Zekaria 2:10, 11 alisema nini kuonyesha jambo hili hili mbeleni?
20 Jambo ili hili vile vile lilisemwa mapema na nabii Zekaria, alipokuwa akitoa unabii siku za kujengwa upya kwa hekalu la Yehova Yerusalemu. Akisema kwa wajenzi wa hekalu, alitamka: “Imba, ufurahi, Ee binti Sayuni; maana, tazama, ninakuja, nami nitakaa kati yako, asema [Yehova]. Na mataifa mengi watajiunga na [Yehova] katika siku ile, nao watakuwa watu wangu.”—Zek. 2:10, 11.
21, 22. Makundi haya ya watu wa “mataifa mengi” wanafanyaje tofauti ya waliyofanya Waisraeli 24,000 katika nyanda za Moabu, kulingana na Hesabu 25:3-5 na Hosea 9:10?
21 Watu hawa wa “mataifa mengi” wanafanya tofauti ya waliyofanya Waisraeli 24,000 katika nyanda za Moabu muda kidogo tu mbele ya taifa la Israeli kuvuka Mto Yordani na kuingia katika Nchi ya Ahadi. Hawa 24,000 walimwacha Yehova; kama ilivyoandikwa katika Hesabu 25:3-5: “Ikawa Israeli kujiungamanisha na Baal-peori; hasira za [Yehova] zikawaka juu ya Israeli. . . . Basi Musa akawaambia waamuzi wa Israeli, Waueni kila mtu watu wake waliojiungamanisha na Baal-peori.”
22 Juu ya Waisraeli hao makafiri unabii wa Hosea 9:10 unasema: “Walikwenda Baal-Peori, wakajiweka wakfu kwa kitu cha aibu, wakawa chukizo kama kitu kile walichokipenda.” Tofauti kabisa na hilo, leo, “binti Sayuni” anapoimba kwa furaha kwa kuwa Yehova amefanya makao yake ndani yake kama “mji wa Mungu aliye hai,” mamia ya maelfu ya watu wa “mataifa mengi” wanakuja ‘kujiunga,’ kujiweka wakf wenyewe, kwa Yehova na kuwa watu wake.—Ebr. 12:22.
AMANI YA MATAIFA YOTE KATI YA WAABUDU YEHOVA
23. Ni usikivu gani Mika 4:3. 4 anaosema wanapata kutoka kwa Yehova, na wanatendeanaje mmoja na mwenzake?
23 Kwa kuwa watu hawa waliojiweka wakf wa mataifa yote wanaikubali sheria inayotoka Sayuni wa kimbinguni na neno la Yehova linalotoka Yerusalemu wa kimbinguni, ni usikivu gani wanaopata kwake Yeye na wanatendeanaje mmoja na mwenzake? Unabii wa Mika unaendelea kutufahamisha, ukisema: “Naye atafanya hukumu kati ya watu wa kabila nyingi, naye atawakemea mataifa wenye nguvu walio mbali; nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe. Bali wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu; kwa kuwa kinywa cha [Yehova] wa majeshi kimesema hivi.”— Mik. 4:3, 4.
24. (a) Je! Umoja wa Mataifa ulitimiza unabii wa Mika 4:3, 4? (b) Sababu gani “mkutano mkubwa” uliomiminika kwenye nyua za hekalu tangu mwaka wa 1935 hauabudu Umoja wa Mataifa kama mungu?
24 Tengenezo lililoundwa na wanadamu la ulimwengu kwa amani ya mataifa yote na usalama, yaani, Umoja wa Mataifa, halikutimiza unabii huu. Tengenezo hilo la kisiasa lingali lina Mkutano wa Mpunguzo wa Zana za Vita ukitenda kwa kawaida katikati ya ulimwengu wenye zana zenye nguvu zaidi kuliko wakati mwingine wo wote katika historia. Lakini sivyo kwa “mkutano mkubwa” kutoka kwa “mataifa mengi” wanaomiminika kwenye nyua za kidunia za hekalu la kiroho la Yehova kumwabudu Yeye kwa umoja. Hawa wanajua kutokana na unabii wa Biblia kwamba Umoja wa Mataifa utashindwa na kwamba ni kosa kuufanya mungu. (Ufu. 13:14, 15; 7:9-17) Wanajua kwamba utashindwa sawasawa na ulivyoshindwa Ushirika wa Mataifa uliotangulia. Zaidi tangu masika ya mwaka wa 1935 C.E., au miaka minne mbele ya Vita ya Pili ya Ulimwengu kutokea, watafutaji hawa wa Mungu aliye mmoja na wa kweli walianza kumiminika ndani ya nyua zake za hekalu. Je! walitimiza unabii wa Mika?
25. (a) Kwa usemi wa mfano, waabudu Yehova wamefuaje panga zao kuwa majembe na mikuki yao kuwa miundu? (b) Kwa hiyo, penye Har–Magedoni, watashikamana na kanuni gani ya kimungu katika mwenendo wao kwa mataifa?
25 Je! kwa usemi wa mfano, “mkutano mkubwa” huu wa waabudu wa mataifa yote katika hekalu la Yehova, walifua panga zao zikawa majembe na mikuki yao ikawa miundu? Kuna uhakika wa historia iliyoandikwa kuhakikisha kwamba walifanya hivyo na wanafanya hivyo hata siku ya leo. Mwezi wa Novemba mwaka wa 1939, katikati ya Vita ya Pili ya Ulimwengu iliyokuwa ikiendelea vikali kwa miezi miwili, walitegemeza kutoshiriki kwao katika siasa za kitaifa kwa kutangaza kihodari kutokuwamo kwao kwa Kikristo juu ya mapigano yote ya kilimwengu ya kutumia silaha. Hata siku ya leo, ijapokuwa mateso ya kupita kadiri juu ya ulizo hili, wameshikilia kabisa kutokuwamo kwao kulikotangazwa. (Angalia makala “Neutrality” katika toleo la Novemba 1, 1939, la The Watchtower.) Hata mahali pa Har–Magedoni patakapofikiwa na mataifa yenye silaha na Yehova Mungu kuleta “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwa mataifa wakinzani, waabudu hawa wasio na silaha wa Yehova Mungu hawatayainulia mataifa hayo hata mkono usio na silaha. Watashikamana na kanuni ya kimungu: “Vita si yenu bali ni ya Mungu.”—2 Nya. (Sik.) 20:15; Ufu. 16:14, 16.
26. (a) Ni hali gani ya mambo tunayoona katika makao ya kiroho ya waabudu Yehova duniani? (b) Hali yao ya makao itakuwaje duniani nyuma ya Har–Magedoni?
26 Ni nini, basi, tunaloona leo kwa habari ya makao ya kiroho ya waabudu Yehova duniani? Hili: Ijapokuwa jamaa yao ni ya mataifa yote na makabila, kuna amani ya kimungu kati yao. Hawakimbilii vita kali kumaliza kutopatana kwao. Wanaweka amani yao kwanza na Yehova Mungu na kisha amani yao na mwanadamu. Wakiwa wameazima lugha ya kinabii ya mfano wa amani na usalama, wameketi bila woga katika bustani yao, kila mmoja chini ya mzabibu wake na mtini wake, wakifurahia ufanisi wa kiroho, wenye kutoa uzima ambao Mungu wanayeabudu kwa umoja anawamiminia. Kwa ujirani wa kidugu, kama ulivyoonyeshwa katika unabii wa Zekaria (3:10), ‘wanamwalika kila mtu jirani yake chini ya mzabibu, na chini ya mtini.’ Huu kwa kweli ni mwonjo wa mbele wa maana sana wa amani, usalama na ufanisi nyuma ya Mungu Mwenyezi kuwaharibu adui zake waliosalia penye Har–Magedoni na kisha kuirudisha paradiso duniani. Waabudu Yehova wataketi kweli chini ya mizabibu na mitini karibu na maskani yao yenye furaha.
WAKATI WA MBELE YA HAR-MAGEDONI KWA UAMUZI
27, 28. (a) Kufurahia kwetu maono hayo ya wakati ujao kunategemea chaguo gani sasa, na kuna namna gani mbalimbali za chaguo leo? (b) Ni kukadiri gani kwa cheo Biblia inafanya kwa miungu kama hiyo ya kilimwengu?
27 Tumaini la kuvutia zaidi hilo! Lakini kufurahia kwa mtu maono hayo ya Paradiso kunategemea kumchagua Mungu anayefaa sasa. Duniani kote watu wanaabudu vitu mbalimbali kama miungu. Mmoja wa miungu inayopendwa na wengi katika kila nchi ni utukuzo wa taifa. Kwa watu wengi wazo fulani la kisiasa ni mungu. Chama cha kisiasa kinachoitwa Taifa ni kama mungu vile vile kwa wengi. Tabia ya kutaka vita ina waabudu wake katika kizazi hiki cha uvumbuzi wa anga za juu. Sayansi inayofundisha kutokuwako kwa viumbe vya kiroho ina wafuasi wake. Namna gani juu ya sanamu za michezoni, sanamu za sinemani, sanamu za muzikini? Hizi zinao waabudu wake kati ya “wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu.” (2 Tim. 3:4) Pasipo kujua, watu wengi wanayaabudu mashetani, kwa maana mtume Paulo alisema: “Vitu vile wavitoavyo sadaka wavitoa kwa mashetani, wala si kwa Mungu.” (1 Kor. 10:20) Na miungu hii yote inaongozwa na aliyeitwa na Paulo “mungu wa dunia hii,” yaani, Shetani Ibilisi.—2 Kor. 4:4.
28 Kwa kweli mtunga Zaburi aliyeongozwa na roho ya Mungu alishusha cheo cha miungu ya mataifa kwa kusema: “Miungu yote ya watu si kitu.” (Zab. 96:5) Miungu hii itakuwa ya faida gani kwa wanadamu Yehova Mungu atakapoiondoa wakati wa Har–Magedoni na wakati wa kumfunga na kumtupa shimoni Shetani Ibilisi na mashetani wake?—Ufu. 16:16; 20:1-3.
29. (a) Sababu gani sasa hakuna nafasi ya kutokuwamo kwa habari ya miungu? (b) Kulingana na Mika 4:5, ni uamuzi gani wa hakika waliofanya wale wanaojitia katika ujenzi wa ibada ya kweli?
29 Tunaukaribia sana wakati huo, wakati wa Mungu. Hali ya kutokuwamo kuielekea miungu haiwezekani tena. Hali ya ulimwengu inayokua sasa inatulazimisha kufanya uamuzi wa mwisho. Tutamchagua nani—Mungu wa kweli au miungu ambayo si kitu ambayo kwayo watu wa mataifa wamejiweka wakf? Kumbuka, unabii wa Mika 4:1-4 unaendelea kutimizwa leo. Kwa hivyo, inatupasa kuyafikiria maneno ya Mika yanayofuata mara tu nyuma ya unabii huo. Maneno ya Mika yanataka tuidharau miungu yote ya uongo ya ulimwengu huu uliohukumiwa. Anasema Mika: “Mataifa yote, kwa upande wao, watatembea kila moja katika jina la mungu wake; lakini sisi, kwa upande wetu, tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu kwa wakati usiojulikana, hata milele.” (Mik. 4:5, NW) Huu ndio uamuzi usiogeuka ambao mabaki wote wa Waisraeli wa kiroho wanaojitia katika kuijenga ibada iliyo safi katika hekalu la kiroho la Yehova Mungu wamefanya. Huo ndio uamuzi wanaofanya wale wa “mkutano mkubwa” wa mataifa yote wanaomiminika kwenye nyua za kidunia za hekalu la kiroho la Yehova. Je! ndio uamuzi wa kila mmoja wetu?
30. (a) Yesu mwenyewe alionyeshaje kwamba huu ndio uamuzi unaofaa kufanywa? (b) Ni mungu gani tunayeweza kuabudu “kwa wakati usiojulikana, hata milele,” na hii itamaanisha nini kwetu?
30 Ndio uamuzi tu unaofaa. Unakubaliana na Mungu aliye mmoja ambaye Yesu Kristo mwenyewe anachukua mahali pa kwanza kumwabudu yeye kwa ibada ya pekee. Hakuna anayeweza kuwa Mkristo wa kweli isipokuwa anauiga mfano mkamilifu wa Kristo. (Zab. 69:9; Yohana 2:13-17; 20:17; Ufu. 3:12) Miungu yote ya uongo itatoweka, na waabudu wake pamoja nayo. Yehova peke yake ndiye Mungu wa kweli, asiyeweza kutoweka, asiyekufa, anayeishi “milele na milele.” Chaguo hili la ibada linamaanisha ushuhuda wa milele kwake Yeye na baraka zisizokoma na furaha kwetu sisi katika taratibu mpya yake yenye amani.—1 Tim. 1:17; Zab. 90:2.
—Kutoka The Watchtower, Dec. 15, 1972.