Maoni ya Mkristo Ni Nini Juu ya Kucheza Dansi?
NI DANSI nyingi mpya zilizotokezwa na kizazi cha rock ‘n’ roll (mojawapo ya namna za dansi) katika miaka ya karibuni. Zinaelekea kuendelea kwa muda mfupi na karibuni nafasi zake zinachukuliwa na nyingine. Ingawa dansi za siku zilizopita zinapendelewa na wengine, wengine wanapenda namna ya kucheza polepole ambayo katika hiyo mwanamume na mwanamke wanacheza dansi pamoja, wameshikana. Kati ya vijana katika nchi fulani dansi za rock zisizo za kushikana zimezoewa sana, wanaocheza wakifanya hivyo bila kushikana lakini wakijipindua-pindua kwa njia mbalimbali. Kwa sababu ya taratibu hizo za dansi zinazopoteza leo, Mkristo anaweza kushangaa, Ni nini maoni yanayofaa ya kucheza dansi kulingana na Biblia?
Katika Israeli wa kale, dansi ilichezwa zaidi katika vikundi, zaidi na wanawake. Wanaume walipoingilia dansi, kwa wazi walikuwa katika vikundi tofauti. Hakuna mtajo wa moja kwa moja wa wanaume na wanawake wakichangamana katika dansi zao.
Katika Neno la Mungu hakuna katazo la wazi la kucheza dansi. Lawama ya kimungu ilipofanywa juu ya wacheza dansi, kama kwa habari ya Waisraeli walipocheza dansi mbele ya ndama ya dhahabu, ilikuwa ni ibada ya sanamu iliyoshirikiana na dansi iliyokuwa kosa, ingawa vile vile huenda kulikuwa na jambo la kutojizuia katika dansi hiyo. Ibada hiyo ya sanamu na dansi vilileta heshima mbaya kwa Yehova.—Kut. 32:1-35.
Kati ya mataifa ya kale ya kipagani, dansi za uzaaji zilikuwa za kawaida. Hizi zilikuwa dansi zilizokusudiwa kuchochea nyege za washiriki wote na watazamaji. Wakanaani walicheza dansi za duara kuzunguka sanamu zao na nguzo takatifu zao wakitukuza nguvu za uzaaji. Ibada ya Baali ilishirikiana na dansi za upotovu, zisizozuiwa.
Tukiendelea mbele, katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo tunaona dansi ikitajwa bila maana ya kutoipendelea. Yesu Kristo, kwa kweli, alisimulia mfano ambamo dansi ilitajwa kama sehemu ya wakati wa kufurahi. Mwana mpotevu aliporudi nyumbani, baba yake alifurahi na kuandaa sherehe. Dansi ilichezwa pamoja na karamu. (Luka 15:25) Ni wazi kwamba Mwana wa Mungu hakuonyesha kutopendelea dansi yenyewe; awa sivyo asingeitaja kama sehemu ya sherehe njema.
Lakini inampasa Mkristo aoneje dansi ya kisasa na namna zake mbalimbali? Mungu, katika Neno lake lililoandikwa, ameweka kanuni ambazo zinapaswa kumwongoza Mkristo katika njia zake zote. Kulingana na kanuni hizo, nia na kusudi la kucheza dansi zenyewe, kupinduka-pinduka kwa miili inayocheza dansi na maoni ambayo kupinduka-pinduka huko kunawaletea wanaoshiriki na watazamaji ni mambo ya maana kufikiria.
DANSI ISIYO YA KUSHIKANA
Karibu katika dansi zote za rock ‘n’ roll zinazochezwa na vijana, watu wale wawili hawashikani. Twist (dansi ya kuzungusha kiuno kwa nguvu) inaonwa na wengi kama ndiyo ilikuwa mwanzo wa namna hii ya kucheza dansi. Mtu wa kuhoji wa gazeti la Look aliripoti wakati fulani uliopita:
“Dansi za kizazi chetu kipya za kufurahisha katika karamu zote ni namna mbalimbali za twist. . . . Wachezaji hawashikani, hawazungumzi. . . . Kila mmoja anafanya fumbo lo lote jina la dansi linalotaka. . . . Wanaonekana kana kwamba miili yao inalia.
“‘Ni namna ya kawaida ya uzaaji, iliyokusudiwa kuzuia hali ya kuwa tasa ya maisha ya kisasa,’ anasema mwanafunzi wa udaktari, aliyeulizwa kueleza mtindo wa kucheza dansi wa kizazi chake. Lakini hii ni namna ya ajabu ya uzaaji pasipo mwungano wa kimwili. . . . Mwanafunzi wa ukunga . . . anasema, ‘Ni ya kuchochea nyege kwa njia fulani . . . miili yote hiyo ikitikisika, lakini bila kushikana wakati wo wote.’”
Ingawa dansi ya rock inatofautiana sana, kupinduka-pinduka katika namna zake nyingine kunafanana na kule kwa dansi za uzaaji, na matokeo yanaweza kuwa yale yale. Kwa kadiri ya kwamba dansi yo yote ya kisasa ni mwigo wa ishara za kuamsha nyege za dansi fulani ya kipagani, kanuni za Maandiko zingeikataza kwa Wakristo, kwa kuwa Neno la Mungu linaonya kujihadhari na “aibu” na ‘mambo yasiyopendeza.’ (Efe. 5:4) Wanawake wa Kikristo wanaonywa na Neno la Mungu kuvaa kwa njia ya kadiri na kuonyesha ‘mwenendo safi,’ kanuni ambazo vile vile zinatumika kwa mwenendo wa wanaume. (1 Pet. 3:1, 2; Tito 2:4, 5; 1 Tim. 2:9) Lakini nyingi za dansi zisizo za kushikana si za kadiri au safi.
Ni jambo la maana kukumbuka kwamba nyege za watu haziamshwi wakati tu kuna kugusana kwa miili. Kutazama tu kupinduka-pinduka kwa wachezaji vile vile kunaweza kuchochea nyege. Zaidi, mwanamume anavutwa sana kwa habari ya nyege na anayoona. Hiyo ndiyo sababu karibu vitabu vyote na picha za umalaya vinauzwa kwa wanaume. Hivyo, kijana wa kike huenda akakosa kujua kwamba kucheza dansi bila kushikana kunaweza kumchochea kijana wa kiume sana, na hali inaweza kuwa hivyo.
Kunapokuwa na dansi ya rock ya kasi, fikira zikivutwa kuelekea sehemu ya mwili palipo na viungo vya uzazi, kijana wa kike huenda akadhani haidhuru. Na hali anajitia katika taabu. Huenda akafikiri hakuna linalotukia, lakini nyege za kijana wa kiume huenda zikawa zimechochewa, na anaweza kumtaka kijana huyo wa kike afanye ngono naye.
Kwa hivyo, kijana wa kike anapaswa kufikiria ni namna gani ya mvuto kijana wa kiume anaweza kuona kwake. Je! anavutwa kwake kwa sababu ya nyege tu anazopata kwa sababu yake? Lakini anaweza kupata raha hii kutoka kwa wanawake wengine wengi wanaovaa mavazi ya kubana, wanaozungusha viuno vyao, na kufanya ishara nyingi za kuchochea nyege. Kwa hiyo kijana wa kike anapaswa kujiuliza mwenyewe: Je! nataka kumvuta mwanamume kwa sababu hiyo tu? Au namtaka mwanamume anayenipenda kwa sababu ya nilivyo? kwa mazungumzo yangu? kwa mambo ninayoona ni ya maana katika maisha? Je! ninapendezwa na namna ya mwanamume anayefurahia kufanya mambo kwa ajili yangu, au anayenipenda kwa sababu ya anayoweza kupata kutoka kwangu tu?
Wakristo wengine huenda wakapata furaha katika dansi; lakini dansi yo yote inapotia ndani tabia isiyo ya kadiri au kuchochea nyege (kwa njia ya kupindua-pindua matiti na viuno), basi kwa hekima wanaiepuka, pahali pa kuona kwamba wanapaswa kufuata wingi wa watu. (Rum. 12:2) Wengine huenda wakakucheka kwa sababu hufuatani na wingi wa watu, lakini jambo la maana ni kwamba una dhamiri njema kwa Mungu.—1 Pet. 4:3, 4.
MATOKEO YA MUZIKI
Jambo jingine la kufikiria ni matokeo ya muziki fulani wa rock. Juu ya muziki wa rock, gazeti la High Fidelity lilisema:
“Si ajabu kwamba wazazi wanakasirishwa na rock—mambo yanayowapasa wanaume na wanawake ni msingi wa siri ya rock, . . . Waimbaji wanasihi ‘Na tushinde pamoja usiku,’ na msimamizi wao kwa dharau anasema, ‘Muziki unaojulikana sana ni juu ya mambo ya wanaume na wanawake, na inawapasa mwavute kwa huo.’ Jambo ambalo linaleta ulizo lenye kusumbua, je! ni kadiri gani ya haya inaendekeza kuamsha tamaa za kimwili kwa vijana?”
Wacheza dansi wa muziki kama huo huenda wakasema kwamba hawasikilizi maneno ya wimbo; ‘wanacheza tu.’ Lakini ikiwa maneno yenyewe si ya adabu nzuri au ni ya ufisadi, au yanayoelekea hayo, mawazo haya bado yanatiwa ndani ya akili changa. Kwa kweli, wacheza dansi mara nyingi wanaweza kurudia mistari wanayodai kutosikiliza. Lakini si maneno peke yake ya muziki huo wa rock ambayo pengine yanapita mipaka ya adabu nzuri; ni matokeo ya muziki.
Majuzi mchunguzi wa United States President’s Commission on Pornography alifanya uchunguzi wa kinachoamsha nyege za vijana wachanga wa kike. Katika uchunguzi wake, msemaji, Bi. Patricia Schiller, aliona kwamba vijana wachanga wa kike wanachochewa nyege mara nyingi na muziki unaojulikana na rock ‘n’ roll, zaidi wanapokuwa na vijana wa kiume. Alisema: “Muziki, kwa kucheza ili kuamsha upendo na upendano wa kijana wa kike, mara kwa mara unakuwa kama kichocheo cha upendo na kwa sababu hiyo ukiamsha nyege katika kijana wa kike. . . . Muziki huo unaleta maoni haya.”—Denver Post, July 23, 1971.
Kwa hiyo Wakristo vijana ni lazima wawe waangalifu juu ya namna ya muziki ambao wanachezea. Kwa kuwa wanawake, zaidi ya wanaume, wanavutwa na wanayosikia, hili ni shauri la maana zaidi kwao. Muziki wa rock unaoamsha nyege na kuchochea kutojizuia kwa upotovu ni jambo ambalo linapaswa kuepukwa kwa hekima ikiwa wanatamani ukubali wa Mungu.
DANSI NYINGINE
Namna gani, basi, juu ya dansi za desturi, zinazochezwa polepole zaidi, ambamo wale watu wawili wanashikana? Hapa mkazo mara nyingi ni juu ya uzuri wa kutazama. Mara nyingi watu waliooa wanafurahia namna hii ya kucheza dansi. Mume na mke wanaoshirikiana pamoja katika dansi zinazofanywa katika majumba makubwa kwa muda wa miaka mingi wanaweza kupata burudisho jingi na furaha kwa kutumia ujuzi wao katika dansi ya namna hiyo, hali wakati huo wakiwa na ushirika wenye furaha pamoja.
Lakini kwa kuwa watu ambao hawajaoa au kuolewa huenda vile vile wakatiwa ndani katika namna hii ya dansi ya kukaribiana, ulizo linakuja juu ya kadiri ambavyo wanapaswa kujihadhari. Akionyesha sababu gani hiki ni chanzo kinachowezekana cha hatari ya adili, Dr. Fritz Wittels, M.D., anaeleza katika kitabu chake Sex Habits of American Women:
“Kusudi la dansi inayofanyiwa katika majumba makubwa . . . ni kuwapa watu wawili mwanamume na mwanamke nafasi ya kuwa na kukaa kwa muda pamoja karibu-karibu zaidi kuliko vile desturi zetu zingeruhusu. . . . Muziki wa dansi uliofupishwa haukufaa kwa kuendeleza ubikira.”
‘Lakini hiyo haielekei kupita kadiri?’ wengine wanaweza kushangaa. Kwa kupendeza, New York Times Magazine la Juni 18, 1972, lilitaja, kwa habari ya dansi ya kushikana inayochezwa polepole katika vyuo, kwamba vijana wa kiume wanaiona kama “udhuru wa haki wa kuzungusha mikono yao kwa kijana wa kike na kumshika karibu-karibu.” Je! furaha inatiwa ndani ya mitindo mizuri ya kuchezesha miguu na namna nyingine za kucheza za dansi? Makala iliendelea: “Dansi za polepole ni za kukumbatiana kwa muda, kugusa mgongo, kupapasa matako.”
Kwamba furaha ya mwili inatiwa ndani katika dansi nyingi inaonyeshwa wazi na uhakika wa kwamba kijana wa kiume, mwenye tamaa kubwa ya kucheza dansi mbele ya kuoa, mara nyingi anaona kwamba nyuma ya ndoa kupendezwa kwake katika dansi kunapungua. Mkewe sasa huenda akambembeleza washirikiane katika dansi anayofurahia sana.
Kijana wa kiume huenda akafurahia kucheza dansi, hali huenda asijue kabisa sababu yake. Hii ni kwa sababu nguvu za asili katika mwili wake mwenyewe zinajitokeza wakati huo, na kijana huyo wa kiume anajua zinamletea maoni ya raha ya kuridhisha. Lakini yungali hajafikia upeo wake kwa kuwa hajaoa. Kwa hiyo kijana wa kiume huenda akafanya hivyo bila nia mbaya. Lakini ikiwa kwa kweli anafahamu mambo haya na kujaribu kuishi kulingana na kanuni za kimungu, atajaribu kufanya kama Biblia isemavyo: “Basi, vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya.”—Kol. 3:5.
Kwa hiyo, ikiwa unashiriki katika dansi zinazochezwa katika majumba makubwa, fahamu kabisa uwezekano wa kwamba mwenzi wako anaweza kuchochewa vibaya hata ingawa huenda ukaona kwamba hamkaribiani sana kadiri ya wewe kuamsha raha ya mwili kutokana na dansi yenyewe. Watu wengine waliooa au kuolewa wameamua kucheza dansi na wenzi wao tu, hivyo kuepuka matata yo yote.
Kila mmoja, basi, anapaswa kuchunguza nia yake mwenyewe kwa habari ya kucheza dansi. Wengine kwa kweli wanaweza kuifurahia dansi yenyewe na huenda ikawa hawana nia isiyofaa. Si dansi zote zinazochezewa katika majumba makubwa zinatia ndani kumshika mwenzi karibu-karibu hivyo kwamba miili inagusana. Dansi nyingi zinaweza kuchezwa ama kwa njia inayofaa ama kwa isiyofaa, ikitegemea watu wanaocheza.
KUEPUKA SABABU ZA KUKWAZA
Hata ingawa huenda Mkristo akaona anaweza kushiriki katika dansi kwa dhamiri njema mbele za Mungu kwa sababu ya kutokuwa na nia mbaya, kuna jambo zaidi la kufikiria. Inampasa afikirie matokeo juu ya watazamaji. Je! mtazamaji inaelekea ataona kwamba Mkristo anajitia katika tabia isiyo ya adabu? Mtazamaji anajua linaloweza kutukia katika akili yake mwenyewe anapoona dansi ya kuamsha mwili, na anadhani kwamba mawazo kama hayo yanaendelea katika akili za wanaocheza dansi. Kusema kwa mtu, “Akili yangu na dhamiri ni safi,” hakutoshi, kwa kuwa Maandiko yanakazia maana ya kuepuka “kuwa sababu za kukwaza.”—1 Kor. 10:32, NW.
Hakuna Mkristo anayetaka kuwaondoa watu kutoka kwa kweli ya Mungu kwa sababu ya mwenendo wake, hata ambapo mwenendo wenyewe huenda usiwe mbaya. Lakini hali zinaweza kufanya mwenendo huo mbaya. Linaloweza kukubalika katika sehemu moja linaweza kukuvunjia heshima mahali pengine. Ikiwa watu wanaona dansi fulani kama uhakika wa kutojizuia, wanawachukua wote wanaoshiriki namna ile ile. Kwa hiyo kila Mkristo atafanya vizuri kutii shauri la mtume Paulo: “Tusiwe kwazo la namna yo yote katika jambo lo lote, utumishi wetu usilaumiwe.”—2 Kor. 6:3.
Vile vile, Mkristo aliyekomaa atachukua maoni ya Maandiko Matakatifu kwa habari ya dansi yo yote mpya inayoweza kutokea. Je! dansi hiyo inaufaa mwenendo mtakatifu? Neno la Mungu linasema: “Iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote” Biblia inapinga ‘tamaa za viungo vya mwili.’ Inawauliza Wakristo waonyeshe kiasi. Na wanaambiwa wafikirie na kuzoea ‘mambo yo yote yaliyo “safi.”—1 Pet. 1:15; Yak. 4:1; Efe. 5:4; Flp. 4:8; 1 Tim. 2:9.
Kwa hiyo kijana, au Mkristo mzee, katika kufikiria maoni ya Mkristo juu ya kucheza dansi, anaweza kujiuliza mwenyewe: ‘Je! dansi ninayofikiria inalingana namna gani na matakwa ya Maandiko?’ Kanuni za adili za hii taratibu mbovu ya mambo zinapoendelea kuharibika, halitakuwa jambo la kushangaza kwamba unaona nyingi za dansi za leo zikiwa zisizofaa kwa watu watakatifu wa Mungu. Kwa hivyo, Wakristo wote, wawe ni wazee au vijana, wanapaswa kukumbuka aliyoonya mtume Paulo: “Mlapo, au mnywapo, au mtendapo neno lo lote, fanyeni yote kwa utukufu wa Mungu.”—1 Kor. 10:31.