Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Je! Mungu aliachilia kulewa kwa Lutu na kuzaa wana na binti zake mwenyewe?—U.S.A.
Jibu la ulizo hili ni lazima liamuliwe kulingana na hali zilizozunguka kisa hiki na kulingana na maandiko mengine.
Lutu na binti zake wawili ndio waliokuwa watu wa pekee kuokoka uharibifu wa Sodoma na Gomora. Nyuma ya uharibifu huu walianza kukaa katika mji wa Soari. Lakini, kwa sababu fulani Lutu aliogopa kuendelea kukaa huko na, pamoja na binti zake, akakaa pangoni. (Mwa. 19:30) Nyuma ya hapo mzaliwa wa kwanza akamwambia dada yake mdogo: “Baba yetu ni mzee, wala hakuna mtu mume katika nchi atuingilie kama ilivyo desturi ya dunia yote. Haya, na tumnyweshe baba yetu mvinyo, tukalale naye, ili tumhifadhie baba yetu uzao.”—Mwa. 19:31, 32.
Uhakika wa kwamba walijaribu kumlewesha baba yao unashauri kwamba walijua hangekubali hata kidogo kufanya ngono nao akiwa katika hali yake ya kawaida. Lakini chini ya hali hizo, waliona kwamba hiyo ndiyo ilikuwa njia ya pekee ya kuzuia kutoweka kwa jamaa ya Lutu. Walikuwa wageni katika nchi na hapakuwa na mtu ye yote wa ukoo wao ambaye wangeweza kuolewa naye na hivyo wahifadhi ukoo wa jamaa. Inapaswa ikumbukwe vile vile kwamba binti za Lutu walikuwa wameishi kati ya wakazi wenye adili mbaya wa Sodoma. Kwa sababu ya kweli hizi, haingalikuwa vigumu kwao kutetea mwendo wao wa tendo katika akili zao wenyewe. Sababu gani, basi, habari hii inapatikana katika Maandiko?
Maelezo hayo hayakuwekwa katika Biblia kuchochea mawazo yenye tamaa. Yako pale kwa kusudi, yakifunua kukamatana kwa Wamoabu na Waamoni kwa wazao wa Ibrahimu waliokuja kujulikana kama Waisraeli. Lutu akiwa mpwa wa Ibrahimu, Waisraeli walikuwa na ujamaa na Wamoabu na Waamoni, waliotoka kwa wana wawili ambao Lutu alizaa na binti zake. (Mwa. 11:27) Nyumaye ujamaa huu wa kimwili ulikuja kuongoza matendo ya Waisraeli katika shughuli na Wamoabu na Waamoni. Kwa mfano, walipokuwa wakichukua nchi iliyo mashariki ya Mto Yordani, Waisraeli, chini ya maagizo ya kimungu, walikuwa waangalifu wasije wakaruka mpaka na kuingia katika nchi za Waamoni na Wamoabu.—Kum. 2:9, 18, 19, 37.
Je! kuna msomaji ye yote wa Biblia mnyofu atakayeachwa na shaka juu ya mwisho utakaofikiwa kutokana na habari hii ya Lutu na binti zake? Je! anafanywa kuona kwamba mwenendo kama huo, labda, unakubaliwa na Mungu?
Ni kweli kwamba katika Mwanzo sura ya 19 mambo ya hakika ya historia yametolewa bila maelezo yo yote juu ya ukubali wa Mungu au kutokukubali kutenda mara mbili kwa Lutu zinaa ya maharimu akiwa katika hali ya kupotewa na akili. Lakini katika sehemu za nyumaye za maandishi ya Biblia, katazo la Mungu kwa ulevi linatajwa waziwazi tena na tena. (Mit. 20:1; 23:20, 21, 29-35; 1 Kor. 6:9, 10) Vivyo hivyo, katika Torati yake kwa Waisraeli, Mungu nyumaye alieleza waziwazi katazo lake la zinaa, akisema: “Mtu ye yote aliye wa kwenu asimkaribie mwenziwe aliye wa jamaa yake ya karibu ili kumfunua utupu; . . . Utupu wa baba yako, wala utupu wa mama yako, usifunue.” (Law. 18:6, 7) Adhabu ya kuvunja sheria juu ya zinaa ilikuwa kifo. (Law. 18:29) Ingawa Lutu na binti zake hawakuwa chini ya Torati, walikuwa, hata hivyo, wanajua kutofaa kwa kufanya ngono na baba yao wenyewe, kama inavyoonyeshwa na uhakika wa kwamba kwanza walimlevya.
Sababu gani, basi, Lutu anaitwa “mwenye haki,” katika 2 Petro 2:8? Si kwa sababu Mungu alikubali kulewa kwake, wala si kwa sababu Mungu alikubali zinaa. Mungu hakukubali mwenendo kama huo. Lakini inapaswa iangaliwe kwamba hakuna lo lote katika maandishi la kuonyesha kwamba Lutu alikuwa mlevi wa kuzoea, wala hakuzoea kuingia katika matendo ya zinaa. Sifa yake ilikuwa ile ya “mwenye haki,” na sifa hii alikuwa nayo kwa Mungu, anayechunguza moyo. Lutu alisikitikia ‘matendo yasiyo na sheria’ ya watu wa Sodoma. Na, kwa wazi, ili Mchunguzi wa mioyo amwone kama mwenye haki, ni lazima Lutu awe alisikitikia mwenendo mbaya ambao katika huo yeye mwenyewe aliingia.
Kuwekwa kwa habari juu ya Lutu na binti zake katika maandishi ya Maandiko kunapaswa kweli kutusaidie kufahamu kwamba Biblia ni kitabu cha kweli. Hata wakati watu waliojulikana kama watumishi wa Mungu walipoingia katika matendo yasiyofaa, Biblia haifichi. Lakini, nyakati zote mambo hayo yanasimuliwa, si kufurahisha au kuchochea tamaa ya kuingia katika mwenendo wa ufisadi, bali kutoa msingi wa kufahamu matukio mengine.