Kushukuru Kipawa Kinachoitwa “Kazi”
“Lo lote mkono wako utakalolipata kujifanya, ulifanye kwa nguvu zako.”—Mhu. 9:10.
1. Watu wengine wanaonaje kazi, na kwa sababu gani? Kwa hiyo, ni maulizo gani yanaulizwa?
KATIKA wakati huu katika historia ambapo watu wanafanya kazi saa chache na kudai malipo zaidi kwa kazi zao, lingekuwa jambo la hekima kwa wote wanaotafuta furaha katika wanayofanya na vile vile kibali cha Mungu kuchunguza nia yao wenyewe kuelekea kazi. Uchungu mwingi ulimwenguni leo unaweza kuonekana kwa watu wasioridhishwa na kazi yao. Hesabu inayoongezeka ya wafanya kazi, zaidi kati ya vijana, inaelekea kuonyesha kazi kama laana, adhabu au ajali ya kutorokwa, ikiwezekana. Malalamiko yao ni kwamba kazi inamaliza nguvu na kumwacha mfanya kazi mchovu sana kadiri ya kutofurahia maisha. Wanabisha, ‘Sababu gani kufanya kazi ikiwa itaharibu furaha ya maisha?’ ‘Watu wengi kupita kadiri wanafanya kazi bila riziki,’ wanasema. Kuonyesha kutopendeza kwa kazi, wafanya kazi mara kwa mara wanaelekeza kwenye mateto mengi na migomo kati ya wafanya kazi wa viwanda, wa afisi na wa jamii ya watu, wanaoshughulikia, si mishahara peke yake, bali na saa na hali za kazi. Wengine wanaona kwamba maisha mazuri kabisa yangekuwa ulimwengu usio na kazi ya taabu. Wachache wanachukua kazi kama baraka au kama kipawa kutoka kwa Mungu. Je! nia yako ni nini kuelekea kazi? Je! unaiona kama baraka kutoka kwa Mungu au kama ubaya wa lazima tu? Je! inampasa mtu aioneje kazi yake?
2. (a) Katika Maandiko, kazi inaonwaje? (b) Biblia inasema nini juu ya wavivu? (c) Sababu gani haitupasi kuwa na ushirika na wavivu?
2 Maandiko Matakatifu yanapendekeza kazi. Yanatangaza kwamba mwanadamu anapaswa kula, kunywa na “kuona mema kwa kazi yake yote yenye bidii.” Ni mapenzi ya kimungu kwamba mwanadamu “afurahie kazi zake.” (Mhu. 5:18; 3:13, 22, NW) Hakuna po pote katika Biblia panapotia moyo ulegevu, uzembe na uvivu kama njia ya maisha. Tofauti na hivyo, mwanadamu anasihiwa ‘ajitahidi.’ Bidii ndilo jambo linalosifiwa. Mwanadamu anapaswa ‘kufanya kwa nguvu zake mikono yake itakayolipata kulifanya.’ (Luka 13:24; Mhu. 9:10; Ebr. 6:10, 11) Nafsi zenye uvivu zinaambiwa ‘zimwendee chungu, zitafakari njia zake zikapate hekima.’ (Mit. 6:6) Kupenda starehe kunashirikishwa na wapumbavu. Ni ‘starehe yao itakayowaangamiza.’ (Mit. 1:32, NW) Kuliko kuwa njia ya maisha nzuri kabisa, “mkono mlegevu” karibuni unajikuta umezungukwa na umaskini. Wale wanaopenda usingizi wao, kujikalia na kukunja mikono yao hawastahili furaha bali uharibifu. (Mit. 10:4; 18:9; 24:33, 34) Kwa hiyo, dini ya Biblia, haiwezi kuwa na ushirika wo wote na watu walegevu, wavivu. Watu wa Mungu wanaitwa, si kwa maisha yasiyo na utendaji, ya kivivu, bali kwa maisha yenye utendaji, ya kusisimua kwa kumwiga si mwingine ila Mungu wao Yehova. Ni maisha haya yenye utendaji, yenye matokeo ambayo ndicho kipawa kinacholeta furaha ya kweli.—Yohana 5:17.
MUNGU NA MWANAWE NI WAFANYA KAZI
3. Nini kinaweza kusemwa juu ya Mungu kama mfanya kazi na matokeo ya kazi zake kwa wanadamu?
3 Fungua macho yako na utazame karibu nawe. Unataka kutazama mara moja tu ukumbuke kwamba unazungukwa na kazi zisizoweza kuhesabika, uzuri wake usio na kifani na za maana kutazama. Kazi hizi zinatiwa ndani katika usemi ‘matendo makuu ya Mungu.’ (Zab. 145:4, 5; 148:3-10) Kuna mbingu juu ‘zikihubiri utukufu wa Mungu’; na “anga laitangaza kazi ya mikono yake.” Dunia, pamoja na wanyama wake wa namna mbalimbali, samaki na mimea, inafanya sifa itolewe. Mtunga Zaburi mwenye kushukuru alitangaza: “Ee [Yehova], jinsi yalivyo mengi matendo yako! Kwa hekima umevifanya vyote pia. Dunia imejaa mali zako.” (Zab. 19:1-4; 104:24) Ulimwengu wote unajaa kazi za Mungu. Hesabu zake ni nyingi sana, zikifanya sifa ibubujike. Uzuri wake ni wa ajabu mno. Ubora wake na hekima vinachochea sifa na shukrani. Matokeo yake yananyenyekeza. Alisema mtunga Zaburi: “Nikiziangalia mbingu zako, kazi ya vidole vyako, mwezi na nyota ulizoziratibisha; mtu ni kitu gani hata umkumbuke, na binadamu hata umwangalie?” (Zab. 8:3, 4; 92:5; 150:2) Uumbaji huu wote unapata uangalizi na utunzaji wa Mungu kwa kawaida.
4. Ni nani aliyekuwa uumbaji wa kwanza wa Mungu, na kuna uhakika gani wa yeye kuwa mfanya kazi?
4 Kazi zote za Mungu hazina kifani, ni za uaminifu na kweli. Zote zimefanyizwa kwa hekima. Katika kitabu cha Biblia cha Mithali, hekima ikisemwa kama mtu inaonyeshwa kama ikiwa kando ya Yehova Mungu katika kazi ya uumbaji kama “stadi wa kazi.” (Mit. 8:12, 22-31) Chini ya uongozi wa roho ya Mungu mtume Yohana alimfunua huyo Stadi wa Kazi kuwa “Neno,” uumbaji wa kwanza wa Mungu, Mwana mzaliwa wake wa pekee ambaye nyumaye katika dunia akawa Yesu Kristo. Alisema Yohana: “Huyo mwanzo alikuwako kwa Mungu. Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika.” (Yohana 1:1-3; Kol. 1:17) Huyu Mwana wa Mungu mwenye hekima alijionyesha kuwa stadi wa kazi duniani. Hakuna mwanadamu mmoja mbele au nyuma ya wakati wake amefanya mengi kama yeye, au akawa na jitihada kama hiyo katika historia ya mwanadamu. Methusela, aliyeishi miaka 969, hakuacha kazi hata moja inayostahili kukumbukwa. Maisha yake marefu huenda yakaonwa kama yalipotezwa bure. Kwa upande mwingine, nyuma ya kukumbusha habari za Injili za kazi za kidunia za Yesu, Yohana anaandika: “Kuna na mambo mengine mengi aliyoyafanya Yesu; ambayo yakiandikwa moja moja, nadhani hata ulimwengu usingetosha kwa vile vitabu vitakavyoandikwa.” (Yohana 21:25) Ni maisha ya nani yaliyokuwa ya furaha zaidi—ya Yesu au ya Methusela? Na hali Yesu aliishi maisha mafupi tu ya miaka thelathini na mitatu na nusu. Kwa wazi alikuwa mfanya kazi mwenye bidii!
5. Yesu alifuata tabia za kazi za nani? Hakikisha.
5 Wanadamu walipojaribu kumzuia asifanye kazi za fadhili siku ya Sabato, Yesu alijibu kwa kutaja utendaji wa Yehova siku zote za juma usiokwisha, akisema: “Baba yangu anatenda kazi hata sasa, nami ninatenda kazi.” (Yohana 5:17) Sababu gani kazi njema zisifanywe siku ya Sabato? Je! jua la Mungu linaacha kuangaza ati kwa sababu ni Sabato? Je! mito inaacha kutiririka? Je! majani yanaacha kukua? Je! matunda hayaivi na ndege kuimba? Je! Mungu si mwenye shughuli akitunza uumbaji wake? Sababu gani, basi, Mtiwa Mafuta wake akatae kufanya kazi za upendo ati kwa sababu ni Sabato? Yesu katika tabia zake za kazi alimwiga Baba yake wa kimbinguni. “Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka,” alisema, “nikaimalize kazi yake.” (Yohana 4:34) Je! katika tabia zako za kazi unafuata mfano wa nani? Je! nia yako ni nini kuelekea kazi?
MWANADAMU MFANYA KAZI
6. Kuna uhakika gani kwamba mwanadamu aliumbwa kufanya kazi, na sababu gani kazi inaweza kusemwa kama “kipawa cha Mungu”?
6 Mwanadamu alifanywa na Mungu awe mfanya kazi. Si kwamba tu Biblia inasema hivyo, bali lile lile umbo la mwanadamu, umbo lake lenye maungo, umbo la mikono yake na miguu, vinaonyesha kwamba kazi fulani ni za maana kwa afya yake. Ukuzi wote unategemea utendaji. Hakuna maendeleo ya kimwili au ya akili pasipo bidii, na bidii maana yake ni kazi. Kazi inatoa maana na kusudi kwa maisha. Kazi anazofanya mtu ndizo kipimo cha mtu mwenyewe. Kazi inayoongeza nguvu za mtu na kumpa uradhi na kujisemea ni ulinzi wa ufisadi na tamaa za mwili. Kwa kawaida watu wanaofanya kazi kwa bidii ndio wenye furaha zaidi. Lakini, wale wasiofanya kazi kwa sababu ya kuipenda bali kwa sababu ya fedha au kwa sababu nyingine ya kichoyo inaelekea hawatapata furaha nyingi katika maisha. Kazi ngumu inamfanya mtu aone njaa, kwa hiyo anakula na kufurahia chakula zaidi. Inamfanya aone kiu, kwa hiyo anakunywa. Inamfanya mchovu, ikiufanya usingizi wake mtamu. “Kila mtu apate kula na kunywa, na kujiburudisha [nafsi] yake kwa mema katika kazi yake yote. Hayo nayo naliona ya kwamba hutoka mkononi mwa Mungu.” (Mhu. 3:13; 2:24) Je! wewe unaiona kazi yako kama baraka kutoka kwa Mungu wa kweli? Hili ni la maana ikiwa utapata furaha ya milele na uradhi kutoka kwa kazi yako.
7. (a) Maisha katika ukamilifu yangekuwa na maana ya kutofanya kazi kwa mwanadamu? (b) Ni uhakika gani unaipa kazi maana?
7 Mwanadamu wa kwanza Adamu alizungukwa na ukamilifu, lakini hata chini ya hali hizi za paradiso ilimpasa awe mfanya kazi. Haikumpasa ajikalie na kujinyosha kivivu. Adamu aliamriwa na Mungu ailime bustani ya Edeni na kuitunza. (Mwa. 2:15) Hii ilimaanisha kazi. Ilitaka akili, kuwaza na busara. Kama mtunzaji wa Edeni, Adamu aliweza kujiona kama mfanya kazi mwenzi wa Mungu, akitimiza mapenzi ya Muumba na kusudi duniani. Kazi yake ilikuwa kufanya dunia yote bustani ya paradiso na kuijaza na taifa kamilifu la wanadamu. (Mwa. 1:28) Huu haukuwa mgawo mdogo; ulitaka ushujaa na bidii kuutimiza. Lakini ni kazi hii iliyoyafanya maisha yake ya maana. Ujuzi wa kuwa mfanya kazi pamoja na Mungu ndilo jambo liletalo uradhi na furaha. Po pote ujuzi huu unapokosekana, hata leo, kazi inakuwa haina maana. Karibuni inakuwa ya kuchosha, isiyofurahisha, mzigo, bila lengo la milele au kusudi.
8. Adamu alichagua kufuata nini, nao wanadamu wamechagua nini tangu wakati huo, na kwa matokeo gani?
8 Lakini, Adamu alichagua kufuata mwendo uliotofautiana na mapenzi ya Mungu. Alijaribu kuridhisha tamaa zake mwenyewe, mwendo ambao ukawa wa msiba kwake mwenyewe na kwa taifa lote la kibinadamu lililofuata nyuma yake. (Rum. 5:12) Umati ulio mkubwa wa wanadamu tangu wakati wa Adamu umefuata mfano wake usiofaa. Wanajitia katika shughuli ambazo zinaelekea kuwa za kichoyo kabisa. Mungu hayumo katika mawazo yao yote. (Zab. 10:4; 14:1) Zaidi sana kazi yao haikamatani na mapenzi ya Mungu juu ya wanadamu wala hawawezi kujiona kama wafanya kazi pamoja na Mungu. Kazi yao haina maana ya kujenga. Hivyo wanaachwa bila kitu na kutoridhishwa na wanachofanya. (Mhu. 2:22, 23) Kama wanadamu wamekuwa wakitaka kufanya kusudi la Mungu la kugeuza dunia hii kuwa bustani ya Paradiso, ebu fikiria namna dunia ingekuwa mahali pa kupendeza nyuma ya maelfu haya ya miaka! Na, vile vile, ni machozi kadiri gani, umwagaji wa damu kadiri gani, ni msiba kadiri gani na taabu visingaliwapata wanadamu katika kila sehemu ya dunia!
KAITWA KUFANYA KAZI YA PEKEE
9, 10. Sababu gani Nuhu alipewa mgawo wa pekee wa kazi, na ulitia nini ndani?
9 Tangu kuumbwa kwa Adamu mpaka Nuhu alipokuwa mwenye miaka 600, kipindi cha miaka 1,656, shughuli za wanadamu zilielekea kuwa za kimwili na za kichoyo kabisa, zikiwa na matokeo mabaya. Maandishi ya Biblia yanasema: “Dunia ikaharibika mbele za Mungu, dunia ikajaa dhuluma. Mungu akaiona dunia, na tazama, imeharibika; maana kila mwenye mwili amejiharibia njia yake duniani.” (Mwa. 6:11, 12) Tangazo hili linatukumbusha kwa njia fulani juu ya hali ya mambo duniani leo. Yesu Kristo, katika unabii wake juu ya mwisho wa taratibu hii ya mambo, alitangaza kwamba ingekuwa hivyo, akisema: “Kama vile ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu.” (Mt. 24:37-39) Katika nyakati hizo za hatari duniani, Mungu anawaita wanadamu wamfanyie kazi ya pekee. Nuhu alikuwa mtu aliyepata mgawo kama huo.
10 Mtu huyu wa Mungu, Nuhu, aliamriwa kujenga safina kujihifadhi mwenyewe na jamaa yake na wanyama. Hii ilitaka nguvu zaidi na juhudi, kwa kuwa ilikuwa na maana ya kukusanya mbao na vifaa vingine. Vivyo hivyo kupanga wingi wa wanyama ambao nyumaye waliingia katika safina kulitaka mpango na utaratibu. Kazi hii ilitia ndani na ujuzi wa kutengeneza vitu, ujuzi wa tabia za wanyama, chakula, ujenzi, useremala, kuzuia uvujaji wa maji. Mgawo wa Nuhu vile vile ulitia ndani na kuhubiri na kuzoea haki. Na huyu mfanya kazi Nuhu alikuwa na miaka zaidi ya 500 alipoanza kujenga safina.—Mwa. 6:9-22; 7:6; 2 Pet. 2:5.
11. Sababu gani twaweza kusema kwamba kazi ya Nuhu ilimaanisha wokovu wake na si onyesho tu la imani yake?
11 Nyuma ya kuangalia mambo yote ya maana zaidi, Nuhu aliingia safinani katika mwaka wa 2370 B.C.E., pamoja na jamii iliyopangwa akiwa ndiye kichwa chake. Katika mwaka wa miezi na siku kumi aliokuwa safinani alifanya kazi. Bila shaka aliongoza mazungumzo ya ibada, aliongoza katika sala za shukrani, aliwalisha wanyama, kuondoa taka na kuhesabu wakati. Hii ilikuwa kazi yenye maana. Ilimaanisha wokovu wake. Mwanafunzi Yakobo alisema: “Mwaona kwamba mwanadamu huhesabiwa kuwa ana haki kwa matendo yake; si kwa imani peke yake.” (Yak. 2:24) Kazi ya Nuhu ilishuhudia imani yake. Je! kazi zako zinashuhudia nini? Mfano wa Nuhu unatuhakikishia kwamba Mungu Ndiye anayeamua kazi zinazofaa na kazi zisizofaa. Mungu anatoa onyo sasa kwamba yeye “ataleta hukumuni kila kazi, pamoja na kila neno la siri, likiwa jema au likiwa baya.” (Mhu. 12:13, 14) Nuhu hakushindwa na mwito wa wakati wake. Je! ndivyo inavyoweza kusemwa juu yako? Je! unaitikia kazi, kazi ya Mungu?
TAIFA LINALOFANYA KAZI PAMOJA NA MUNGU
12. Je! Israeli lilikuwa taifa la wafanya kazi pamoja na Mungu namna gani?
12 Katika kusudi la Mungu la kutoa taifa, wanaume kama Ibrahimu, Isaka na Yakobo, na wengine, walipokea migawo ya pekee ya kazi kutoka kwa Yehova. Sura ya kumi na moja ya Waebrania ina kazi zao za imani. Mwishowe, katika Mlima Sinai katika mwaka wa 1513 B.C.E., Yehova aliongoza taifa la Israeli kwa kusudi lake la pekee, akisema: “Sasa basi ikiwa mtaitii sauti yangu kweli kweli, na kulishika agano langu, hapo ndipo mtakapokuwa tunu kwangu kuliko makabila yote ya watu; maana dunia yote pia ni mali yangu, nanyi mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani, na taifa takatifu.” Kwa maneno hayo watu wakajibu kwa umoja: “Hayo yote aliyoyasema [Yehova] tutayatenda.” (Kut. 19:5, 6, 8) Kusudi la hilo agano la Torati, alisema mtume Paulo, lilikuwa ni kuwaelekeza Wayahudi kwa Kristo, “ili tuhesabiwe haki kwa imani.”—Gal. 3:23-25.
13. (a) Ni nini kinaweza kusemwa juu ya kazi za makuhani na namna walivyotofautiana katika migawo yao? (b) Ni uhakika gani tunasaidiwa kuona juu ya kazi tunayofanya?
13 Katika taifa la Israeli peke yake, makabila mbalimbali yalikuwa na kazi za pekee. Kwa mfano, kazi za kikuhani zilikuwa za washiriki wa kiume wa jamaa ya Haruni tu, wengine wote waliobaki wa kabila la Lawi wakitenda kama wasaidizi. (Hes. 3:3, 6-10) Kujenga, kubomoa na kubeba hema zilikuwa kazi za Walawi wa sio wa kikuhani. Kazi yao iliongozwa sana chini ya Mfalme Daudi, aliyeamuru wasimamizi, maafisa, waamuzi, mabawabu na waweka hazina. Nyumaye, nyuma ya ujenzi wa hekalu la Sulemani, umati mkubwa uliwasaidia makuhani katika vitalu (viwanja) na vyumba vya kulia vilivyokamatana na sadaka, dhabihu, kazi ya kutakasa, kupima, na kazi mbalimbali za ulinzi. Nyingi ya kazi hii ilikuwa ngumu na ya kuchosha. Wakati mmoja hesabu ya makuhani ilifika 1,760, wote “watu wenye ustadi waliofaa sana kwa kazi ya huduma ya nyumba ya Mungu.” (1 Nya. 9:10-13) Hawa walikuwa makuhani wa uwezo wa namna mbalimbali. Hatuwezi, hata hivyo, kuwaza kwamba makuhani hawa wote walistahili sana au kupewa kipawa walipozaliwa, kwamba ilikuwa vyepesi kwao tu kuwa stadi kwa lo lote walilogawiwa. Hapana, lakini kwa bidii ya kujifunza kazi zao na kwa uangalifu wao imara wa kazi waizogawiwa, wote karibuni walipata sifa ya kuwa watu wenye uwezo kwa kazi ya Yehova. Hii inakazia ukweli wa kwamba watu wanaweza kujitahidia vitu ambavyo ama wanapenda ama hawapendi. Mtu akijitahidi, hakuna kazi ambayo haina maana lakini kwamba anaweza kuikuza; hapana kazi yenye kuchosha au isiyofurahisha lakini kwamba anaweza kufanya iwe ya kupendeza kidogo; hakuna kazi isiyopendeza lakini kwamba mtu anaweza kufanya iwe ya kupendeza kwa kuwaza kwake, ikiwa tu anajitahidi mwenyewe.
14. Makuhani walijionaje, na nia gani inayoelezwa na mtume Paulo huenda ikatusaidia katika kazi yetu?
14 Katika kazi yao makuhani wa Yehova walijiona wenyewe kama wafanya kazi pamoja na Mungu, jambo ambalo liliwafanya waone migawo yao kama pendeleo na si kama kazi ya kawaida tu. Ijapokuwa wepesi wa migawo yao, waliweza kuendelea kuwa na roho nzuri kama ile iliyosihiwa na mtume Paulo, aliyesema: “Mlapo, au mnywapo, au mtendapo neno lo lote, fanyeni yote kwa utukufu wa Mungu.” Na tena anasema: “Lo lote mfanyalo, lifanyeni kwa moyo, kama kwa [Yehova], wala si kwa wanadamu.” (1 Kor. 10:31; Kol. 3:23) Lakini hata wakati watu wanajiona kama wafanya kazi pamoja na Mungu, bado ni lazima wajitahidi. Ni jitihada hii ya mtu mwenyewe kama mfanya kazi mwenzi wa Mungu ambayo mwishowe inaleta matokeo bora na furaha ya kweli. Je! hii ndiyo nia yako kuelekea kazi?
15. Waebrania waliichukuaje kazi, na bidii na ufundi vilionwaje?
15 Waebrania wa kale, kama makuhani wao, hawakutia shaka juu ya maana ya kazi wakati wo wote. Ilichukuliwa kama ya kuheshimiwa sana, kazi takatifu, kipawa kutoka kwa Mungu. Mapokeo ya Kiyahudi yanafundisha: “Yeye ambaye hamfundishi mwanawe ufundi anamlea kuwa mnyang’anyi.” “Kazi inapaswa ipendwe sana, kwa kuwa inamfurahisha mfanya kazi, na kumtegemeza.” Biblia inasifu bidii na kazi yenye ufundi, ikisema: “Je! wamwona mtu mwenye bidii katika kazi zake? Huyo atasimama mbele ya wafalme; hatasimama mbele ya watu wasio na cheo.” (Mit. 22:29) Bidii ilikuwa sawasawa na utajiri. (Mit. 10:4; 12:27) Mtume wa Kikristo vile vile alitangaza: “Ikiwa mtu hataki kufanya kazi, basi, asile chakula.”—2 The. 3:10.
16. Kazi kwa upande wa wanawake wa Kiebrania ilionwaje, na Mithali zinasema nini juu yake?
16 Hata kati ya wanawake wa Kiebrania, bidii ilisifiwa. Mwanamke ambaye alifanya kazi kwa mikono yake kwa kupenda alisifiwa sana kama “mke mwema.” “Hufanya kazi yake ya mikono kwa moyo.”— Mit. 31:10, 13, 31.
17. Sababu gani Wayahudi walipendwa kama watumwa?
17 Wakiwa na heshima kuu kama hiyo kwa kazi, si vigumu kuona sababu Waebrania kama taifa walifanikiwa. Vile vile, si vigumu kuona sababu mataifa yenye kushinda yalipenda wawe watumwa. Nebukadreza, kama vile mfalme wa Tiro, bila shaka alipata kati ya maelfu aliyokuwa amechukua utumwani mafundi wa namna zote wa Kiyahudi: wafua madini, maseremala na waashi, wahunzi wa meli, wastadi wa kusokota na kufuma sufu (manyoya ya wanyama) na kitani, washoni viatu, washonaji wa nguo na wapaka rangi.—2 Nya. 2:13, 14.
MAANA YA KAZI NA PUMZIKO
18, 19. Tunaweza kusema nini juu ya pumziko, na sababu gani kusudi la usiku halipaswi kuwekwa kando?
18 Maisha yana miendo ya kupendeza. Kuna wakati wa kazi na wakati wa pumziko. Sheria za Mungu za Sabato kwa Israefi zilisema kwamba kila saa moja kati ya saba isiwe ya kazi. Hii ilikuwa ya kupumzisha mwili na kusitawisha akili, inayoelekea kumtia mtu nguvu na kumtegemeza. Katika siku ya Sabato mwanadamu alipaswa apumzike na kuabudu. Mwili ulitaka kupumzika, hali akili na moyo vilipata nguvu kutoka kwa ibada, kutokana na kujilisha mawazo ya Mungu. (Mt. 4:4) Kwa kuwa mwanadamu ni lazima amwabudu Mungu ili aishi, ni jambo la busara kwamba ibada isivutwe na mambo mengine yo yote. Ingawa kazi ni ya maana, ni lazima kuwe vile vile na wakati wa kutulia ili kufikiri juu ya bidii ya mtu na kutoka kwa kufikiri huko maana ya maisha na kazi bora. Hii haishauri kwamba wafanya kazi wawe wakiota saa za mchana. Hapana, lakini kwamba wakati fulani uchukuliwe nyuma ya siku kwisha ili kuwaza umetulia. Usiku ni wakati mzuri kwa kusudi hilo.
19 Kusudi la usiku halipaswi kudharauliwa au kusukumwa kando, hata hivyo. Kwa wengi wakati huo ndio wa kusikiliza muziki wa namna ya kisasa kama rock, ndio wakati wa kunywa pombe katika vilabu vya usiku na kucheza dansi, vyote ambavyo vinamchosha mwanamume au mwanamke zaidi kuliko kazi yote ya siku. Lakini Mungu alitoa usiku kwa namna ya pumziko ambalo kwa kweli linatengeneza mwili na akili. Pumziko la kutosha kama vile kazi ya kutosha linaleta afya njema na furaha.
20. Sababu gani wanadamu wanapaswa kujiuliza juu ya kazi wanayofanya sasa, na sababu gani hakuna sababu ya kukata tamaa?
20 Hakuna jambo linaloamua faida ya mtu kama kazi anayofanya kila siku. Mungu alimpa mwanadamu mikono na misuli ya kutenda. Ni matendo yake, basi, yanayoamua faida yake. Kwa kweli, Mungu atawahukumu wanadamu kulingana na matendo yao. (Ufu. 20:12) Hiyo ndiyo sababu ni vizuri tujiulize wenyewe: Tumezitumiaje maisha zetu? Ni kazi zipi tumefanya au tunazoweza kuonyesha kuhakikisha faida yetu? Ikiwa una jambo dogo au ikiwa huna lo lote la kuonyesha kwa wakati ambao umekuwako duniani, usikate tamaa. Habari njema ni kwamba si kuchelewa mno kugeuka. Bado kuna wakati kwako kufanya kazi ya maana kwa utukufu wa Mungu na ambayo kutoka kwake unaweza kupata uradhi wa milele. Katika nyakati hizi ngumu za hatari Mungu anayo kazi ambayo unaweza kufanya na kuwa mfanya kazi mwenzake. Juu ya kazi hiyo na namna unavyoweza kushiriki ndani yake kwa furaha yako ya milele, tunaiachia makala ifuatayo ieleze.
[Picha katika ukurasa wa 82]
Nyuma ya kuingia katika safina aliyojenga kwa amri ya Mungu, Nuhu aliwatunza wanyama na kufanya kazi nyingine. Je! wewe unaitikiaje kazi ya Mungu?