Toba ya Kweli—Twawezaje Kuifahamu
“TUKISEMA kwamba hatuna dhambi, twajidanganya wenyewe, wala kweli haimo mwetu.” Mtume Yohana alisema hayo kule nyuma katika karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida. Akiwaandikia Wakristo wenzake, alijitia ndani mwenyewe katika usemi “tukisema.”—1 Yohana 1:8.
Je! sisi tu Wakristo wa kweli? Basi mbele ya kubatizwa kama wanafunzi wa Mwana wa Mungu, ‘tulitubu na kugeuka’ kutoka katika mwendo mbaya tuliokuwa tukifuata. Hii ilituweka katika hali ya ‘kumwomba Mungu dhamiri njema,’ na kupatana na Yeye kupitia kwa dhabihu yenye fidia au “sadaka ya dhambi.” (Matendo 3:19, 26; 1 Pet. 3:21; 2 Kor. 5:19-21, NW, maelezo ya pembeni) Lakini takwa la toba halimalizikii hapo. Maneno ya Yohana yanaonyesha kwamba, tukiwa wasiokamilika na wenye dhambi kwa kurithi, bado tutafanya makosa. Mara nyingi haya yatakuwa madogo-madogo. Hata hivyo Mkristo anaweza kuangukia kosa kubwa. Iwe namna yo yote, anatakiwa kutubu na kutafuta msamaha wa Mungu.
KUTUBU KWA DHAMBI NZITO
Mkristo anaweza kujitumainia kupita kadiri, akishindwa kujua kwamba ‘anayejidhania kuwa amesimama anapaswa kuangalia asianguke.’ (1 Kor. 10:12) Au kwa sababu ya kutoshukuru kabisa mipango ya Mungu ya kuendelea kuwa wenye nguvu za kiroho na afya na ya kujikinga na mashambulio ya Shetani, huenda Mkristo akadhoofika na ikawa vyepesi kwake kujaribiwa. Huenda akafanya dhambi nzito. Halafu nini? Sasa inampasa afanye nini?
Anaweza kujifaidi kwa kufikiria alivyofanya Daudi. Katika Zaburi ya thelathini na mbili, labda iliyoandikwa nyuma ya dhambi nzito ya Daudi iliyowatia ndani Bathsheba na Uria, Daudi alisema: “Niliponyamaza mifupa yangu ilichakaa kwa kuugua kwangu mchana kutwa. Nalikujulisha dhambi yangu, wala sikuuficha upotovu wangu. Nalisema, Nitayakiri maasi yangu kwa [Yehova], nawe ukanisamehe upotovu wa dhambi yangu. Kwa hiyo kila mtu mtauwa akuombe wakati unapopatikana.” (Zab. 32:3, 5, 6) Kuahirisha kutafuta msamaha wa Yehova kunaendeleza tu taabu ya dhamiri iliyojeruhiwa. Kama Mithali 28:13 inavyoshauri: “Afichaye dhambi zake hatafanikiwa; bali yeye aziungamaye na kuziacha atapata rehema.” Ndiyo, kukamatana kwetu na Mungu ni kwa bei ya juu sana kutostahili kutojali kuomba msamaha wake na rehema. Inatupasa tuwe wepesi kufanya hivyo kupitia kwa Mwanawe kama ‘mwombezi wetu kwa Baba.’—1 Yohana 2:1.
Kuna zaidi, hata hivyo, ambayo mtu anayetubu anaweza kufanya. Mwendo wenye hekima sasa ungekuwa ni kuwaendea “wazee” kwa kiroho wa kundi. Sababu gani? Je! wana uwezo wa kutoa msamaha kutoka kwa Mungu wa dhambi iliyotendwa, au wanaweza kutenda kama wapatanishi kati ya aliyetenda dhambi na Mungu? Hapana. Mtu aliyekosewa anaweza kutoa msamaha. Jambo jingine: Ni Mungu peke yake anayeweza kutoa msamaha wa dhambi inayovunja sheria yake, na mpatanishi wetu mmoja ni Mwanawe.—1 Yohana 1:9; 2:1, 2; Ebr. 4:14-16.
Lakini je! Paulo hakusema juu ya ndugu wa Korintho kama ‘wakimsamehe’ mshiriki wa kundi aliyetenda kosa zito na akatubu? Ni kweli, lakini ‘msamaha’ wao kwa wazi haukuwa kusamehe kuvunja kwa sheria ya Mungu yenyewe. Pahali pake, ulikuwa msamaha wa taabu, suto na huzuni ambayo tendo lenyewe lililetea kundi. (Linganisha 2 Wakorintho 2:5-10; 7:11.) Kwa namna ile ile sisi wenyewe tunaweza ‘kuwasamehe watu waliyotukosea.’—Mt. 6:14, 15.
Sababu gani, basi, tuwaendee wazee hawa? Ili kutafuta msaada wao kama wachungaji waliowekwa. Kufanya makosa ni uhakika wa ugonjwa wa kiroho. Akionyesha linalotakiwa, mwanafunzi Yakobo anasema: “Ungameni dhambi zenu ninyi kwa ninyi, na kuombeana, mpate kuponywa. Kuomba kwake mwenye haki kwafaa sana, akiomba kwa bidii.”—Yak. 5:16.
Ndiyo, kusudi la kuwaendea ndugu hawa wazee ni kupata msaada ili “kuponywa,” kupata tena afya ya kiroho na nguvu. Kutoa msaada huo ni sehemu ya kazi yao kama wachungaji. (Linganisha Ezekieli 34:4, 16; Waebrania 12:12, 13.) Bado kuna sababu nyingine, hata hivyo.
Ndugu hawa wanapendezwa na kulinda afya ya kiroho ya kundi kwa jumla, wakililinda lisije likaambukizwa. Vile vile wanapendezwa sana sana kulisaidia kundi kuendelea kila mara kuwa na hali njema mbele za Mungu na mbele ya watu wote, bila kuwa suto kwa jina la Yehova kwa njia yo yote. Kwa haki tunajaribu kushirikiana na watu kama hao na kuwasaidia katika daraka lao.
Pahali pa mtu kujulisha kosa lake kwa wazee wanaofanya halmashauri ya hukumu ya kundi kwa kutumia njia nyingine, na kwa sababu hiyo kuwalazimu kuuliza juu ya mkosaji kama ametubu kwa unyofu wa moyo na kuacha mwendo mbaya au hapana, mtu kama huyo anaonyesha roho nzuri kwa kuwapa kwa hiari habari hiyo yeye mwenyewe. “Maana wao wanakesha kwa ajili ya roho zenu, kama watu watakaotoa hesabu” kwa Mungu. Kwa matumaini yote, basi, tunaweza kuonyesha unyenyekevu kwa watu kama hao.—Ebr. 13:17; Matendo 20:28-30, 35; 1 The. 5:12-15, 23.
Wazee hawa, kwa wazi, wanataka sana kujua kama kweli kuna toba ya unyofu wa moyo kwa upande wa mkosaji na kama sasa ameifanyia miguu yake njia za kunyoka, kwa faida yake mwenyewe na kwa faida ya wengine wote katika kundi. Uhakika tu wa toba ya kweli ndio unaoweza kuwahakikishia kwamba Mungu amemsamehe mkosaji, ‘hakumhesabia dhambi yake.’ (Rum. 4:8) Kama isingalikuwa hivyo, huenda wakajikuta imewalazimu kumfukuza au kumtenga na ushirika mtu kama huyo kama hatari kwa afya ya kiroho ya kundi na hali yake njema mbele za Mungu.
Ndiyo, kinachoamua kama kundi litamtenga mtu na ushirika ama sivyo—si uzito wa dhambi yenyewe, wala kadiri ya kuenea kwa habari mbaya—bali ni toba ya unyofu wa moyo ya mtu au kukosa kuwa nayo. Ikiwa kweli ametubu, kundi halitamtupa mtu huyo nje ili tu liridhishe maoni ya mtu fulani au watu wote kwa jumla. Ni kweli, nyakati ambazo kosa zito limefanywa wanaweza kuona inafaa kumkaripia mkosaji kwa ukali na mbele ya watu wote, na bila shaka hangepewa daraka katika kundi kwa muda mrefu, labda kwa miaka mingi. Lakini hawangemwacha mtu ye yote anayetubu kwa unyofu wa moyo, kama vile Mungu hakumwacha Daudi alipotubu kwa unyenyekevu dhambi yake nzito. Wanamwiga Mungu katika upendo wake mwaminifu, fadhili yake yenye upendo.—2 Sam. 22:50, 51; 1 Fal. 8:22-26; Zab. 51:17.
Je! hawa wazee walio katika halmashauri ya hukumu wanawezaje kuridhika kwamba anayefanya kosa zito ametubu kwa kweli? Kwa habari hii, je! sisi wenyewe twawezaje kuwa na uhakika wa kwamba toba yetu ni ya kweli, kwamba ni ya namna inayompendeza Mungu?
HUZUNI YA KILIMWENGU AU HUZUNI YA KIMUNGU?
Kwa wazi masikitiko yanapaswa kuwako, toba na majuto kwa upande wa Mkristo ye yote anayetenda dhambi. Na hali maoni haya yenyewe siyo kipimo cha uhakika wa toba. Ulizo ni: Sababu gani mkosaji ana masikitiko hayo, toba na majuto? Ni jambo gani linalosababisha maoni haya?
Mtume anaonyesha maana ya kuangalia jambo hili anapoandika: “Maana huzuni iliyo kwa jinsi ya Mungu hufanya toba liletalo wokovu lisilo na majuto; bali huzuni ya dunia hufanya mauti.” (2 Kor. 7:10) Kwa hiyo ni habari ya uzima au kifo kwa nia yetu kuwa inayofaa. Huzuni ya kilimwengu haitokani na imani na upendo wa Mungu na haki. Inaletwa na majuto kwa sababu ya kushindwa, kutofanikiwa, hasara ya kimwili au ya kupoteza ushirika, tumaini la kupata adhabu au aibu. Huzuni ya kilimwengu inaombolezea matokeo yasiyopendeza yanayoletwa na kosa. Lakini haiombolezei jambo lenyewe lisilo la haki, au suto linaloletea Mungu.—Linganisha Yeremia 6:13-15, 22-26.
Kaini alionyesha huzuni ya namna hiyo. Mungu alipotangaza hukumu yake, Kaini alihuzunika kabisa—kwa ajili yake mwenyewe kwa sababu ya siku za usoni zenye huzuni alizofikiria. Lakini hakuonyesha majuto yo yote kwa sababu ya kumwua ndugu yake.—Mwa. 4:5-14.
Esau kwa kutoshukuru aliuza haki yake ya uzaliwa kwa ndugu yake Yakobo. Nyumaye, alipofahamu kwamba Yakobo amepokea baraka ya kinabii ya baba yake Isaka kama mzaliwa wa kwanza, Esau alilia “kilio kikubwa cha uchungu sana.” Kwa machozi alitafuta toba—si yake mwenyewe bali ya baba yake, akitaka kumsadikisha Isaka ‘atubu’ au ‘ageuze nia yake’ juu ya utoaji wake wa baraka. Esau hakujutia nia yake ya mambo ya kimwili iliyomfanya ‘aidharau haki yake ya uzaliwa.’ Alijutia hasara ya faida ambazo sasa angepoteza. Mungu alisema: “Nimempenda Yakobo, bali Esau nimemchukia.”—Mwa. 25:29-34; 27:34; Ebr. 12:16, 17; Rum. 9:13.
Kwamba hakuna wakati wo wote Mungu atapendezwa na mwenendo wa ‘kuvua na kuvaa’ kwa habari hii inaonyeshwa wazi na unabii wa Hosea. Kwa habari ya Israeli anasema, ‘Wanapokuwa katika taabu yao wanamtafuta Mungu.’ Lakini maneno ya kutubu waliyosema hayakukaa sana. “Fadhili zenu ni kama wingu la asubuhi na kama umande utowekao mapema.”—Hos. 5:15; 6:1-4.
Halafu Hosea 7:14-16 anaeleza wazi jambo kubwa linalokosekana katika maneno mengi ya kutubu hata leo, akisema: “Hawakunililia kwa moyo, lakini wanalalamika vitandani mwao; hujikutanisha ili kupata nafaka na divai . . . Wao hurudi, [si kwa cho chote kilicho juu zaidi]. . . ” ‘Kulalamika’ kwao kwa kitulizo wakati wa taabu kulikuwa na sababu ya kichoyo na, kama walipewa kitulizo, hawakutumia nafasi hiyo kusitawisha na kuimarisha kukamatana kwao na Mungu kwa kushikilia zaidi sana kanuni zake za juu. (Yak. 4:3) Hosea anasema walikuwa kama “upinde usiotumainika,” usiopiga shabaha wakati wo wote. (Hos. 7:16; Zab. 78:57) Toba yao haikutoka kweli katika moyo.—Yoeli 2:12, 13.
JAMBO LINALOSUKUMA TOBA YA KWELI
Huzuni inayofuatana na toba ya kweli ina nia tofauti sana kuliko huzuni ya kilimwengu. Kuna tamaa ya moyoni ya kurudi katika kibali cha Mungu, inayosukumwa na upendo kwake unaokuja kwa kumjua na sifa zake bora na makusudi ya haki. Shukrani kwa wema wake na ukubwa vinawafanya wakosaji wanaotubu kweli kujuta kabisa kwa sababu ya kuleta suto kwa jina lake. Upendo kwa jirani vile vile unawafanya wasikitikie ubaya waliowatendea wengine, mfano mbaya uliowekwa, dhara lililoletwa, labda namna walivyochafua sifa nzuri ya watu wa Mungu kati ya wale wa nje, na kwa sababu hiyo kuwazuia watu kutolikubali kundi la kweli la Mungu. Mambo haya, wala si aibu ya kujulikana au maelekeo ya adhabu, yanawafanya wajisikie ‘kuvunjika moyo’ na ‘kupondeka roho.’—Zab. 34:18.
Lakini toba (me·taʹnoi·a katika Kigiriki) vile vile inatia ndani ‘geuzi la akili’ au ‘geuzi la nia.’ Ili iwe ya kweli, ni lazima itie ndani kukataa kabisa kwa mwendo mbaya kama jambo la kukirihi, jambo la kuchukiwa. (Zab. 97:10; Rum. 12:9) Hii inafuatana na upendo wa haki unaomfanya Mkristo anayetubu aamue kabisa kushikilia mwendo wa haki tangu wakati huo na kuendelea mbele. Bila vyote hivi chuki ya mabaya na upendo wa haki hakungekuwa na nguvu zo zote katika toba yetu, hakungekuwa na kushika kwa ambayo mtume Paulo aliita “matendo yanayopatana na kutubu.” (Matendo 26:20) Kisa cha Mfalme Rehoboamu kinaonyesha jambo hili. Nyuma ya kwanza kujinyenyekeza kwa hasira ya Mungu, aligeuka tena na kuanza kufanya mabaya. Sababu gani? Kwa sababu “hakuukaza moyo wake amtafute [Yehova].”—2 Nya. 12:12-14.
Kundi la Korintho lilionyesha hii “huzuni iliyo kwa jinsi ya Mungu.” Walipokaripiwa na Paulo kwa sababu ya kumwacha mzoea maovu katikati yao, waliitikia na wakasawazisha mambo. Walionyesha huzuni yao wazi kwa sababu ya kosa lao si kwa woga tu bali vile vile kwa “bidii kama nini . . . naam, na kujitetea, naam, na kukasirika [kwa sababu ya suto ambalo mwendo wa mtenda maovu ulikuwa umeleta], . . . naam, na shauku, naam, na kujitahidi, naam, na [kuliondoa kosa]!” (2 Kor. 7:11) Kwa hiyo, wazee leo wanaweza kutazamia sifa za namna ile ile kwa wale wanaoonyesha toba mbele yao kwa sababu ya kosa.
KUTOKAMILIKA HAKUPASWI KUZUIE FURAHA
Dhambi, kwa kweli, zinaweza kutofautiana kwa uzito. Labda pahali pa dhambi kubwa kama uasherati, uzinzi au wivi, tunafahamu tumekuwa wenye hatia ya kuwa na “macho ya kiburi” au ya ‘kupendelea,’ mambo ambayo yanamchukiza Mungu sana. (Mit. 6:16, 17; Yak. 2:9) Na unapokuja wakati wa kutumia ulimi, “twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi,” tukisema mambo ambayo nyumaye tunajua si ya hekima, si ya fadhili, si ya upendo, si ya Kikristo. (Yak. 3:2, 8-13) Je! tunapendezwa kuona kwamba kukamatana kwetu na Mungu hakupatwi na madhara? Basi inatupasa ‘tutubu na kugeuka,’ tukitafuta msamaha.
Lakini kwa sababu kutokamilika kwetu kunaonekana kwa njia hii au ile kila siku, je! hii ina maana ya kwamba tunapaswa kuwa katika hali ya maombolezo kila mara, tukijuta wakati wote? Kwa vyo vyote hapana.
Anapopanga matunda ya roho takatifu ya Mungu, mtume anafuatisha “furaha” mara tu nyuma ya “upendo.” (Gal. 5:22) Mtunga Zaburi anasema: “[Yehova], kama Wewe ungehesabu maovu, Ee [Yehova], nani angesimama?” (Zab. 130:3) Tunaweza kuwa wenye furaha, tukikumbuka pahali pake kwamba “[Yehova] amejaa huruma na neema, haoni hasira upesi, ni mwingi wa fadhili. . . . Kwa maana Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” (Zab. 103:8-14) Ingawa kwa haki makosa yetu yanaleta majuto, haitupasi tujipe masumbufu kwa sababu ya kila kosa dogo au neno la kipumbavu.
Hata hivyo, ufahamu wetu wa makosa haya unapaswa uwe na matokeo ya unyenyekevu juu yetu, ukitusaidia tuwe wenye adabu na huruma kuwaelekea wengine. Halafu, tunapomwomba Mungu msamaha kwa sababu ya makosa yetu ya kila siku atapendezwa na sala yetu. Tukitembea kwa uaminifu katika njia zake na kwa kawaida kutafuta kibali chake katika sala, tunaweza kuwa wenye furaha kabisa, kuwa wenye matumaini ya kukamatana kwema naye.—Flp. 4:4-7.