Je! Ushirika wa Kanisa Unatosha
‘JE! MIMI nitakuwa kati ya wale watakaokombolewa kuingia katika taratibu mpya ya Mungu?’ Kila mtu anayeamini ahadi ya Mungu anapaswa ajiulize ulizo hilo. Wengi vile vile wanataka kujua, ‘Je! ushirika wangu wa kanisa utanihakikishia kibali cha Mungu?’
Maulizo haya kwa kweli yanastahili kufikiriwa kwa uzito, zaidi kwa sababu ya ukweli wa kwamba kuna makanisa mengi, yenye mafundisho na mazoea yanayotofautiana.
Namna gani, basi, juu ya wale ambao ni washiriki waliobatizwa wa mashahidi wa Yehova? Hawa vile vile wanaweza kuuliza, ‘Je! ushirika wangu, kutia ndani na kushiriki kwangu katika mikutano ya mafunzo ya mashahidi wa Yehova na katika kuhubiri nyumba kwa nyumba, vinanihakikishia ukombozi taratibu hii ya mambo inapoharibiwa?’
Ili kujibu lo lote la maulizo haya inakupasa ufikirie, Je! Mungu anataka nini kutoka kwangu? Yeye anasema: “Mimi [Yehova], Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu [au, “Mungu anayetaka ibada ya pekee”].” (Kum. 5:9; linganisha New World Translation.) Kwa hiyo, anataka kutoka kwako wewe kama mtu mmoja ibada ya pekee. Ni lazima umtumikie wewe mwenyewe, kwa moyo, pamoja na ujuzi wa kweli wa yanayompendeza.—1 Nya. 28:9; Mt. 22:37.
UJUZI WA NENO LA MUNGU NI WA MAANA
Ujuzi huu unaweza kupatikana katika Neno la Mungu la kweli Biblia tu. Mtu anayedai kumtumikia Mungu huenda akawa ni mwenye bidii, mwenye unyofu wa moyo. Huenda akaona kwamba viongozi wake wa kanisa vile vile ni wanyofu. Lakini mambo hayo tu hayatahakikisha kibali cha Mungu.
Biblia inatupa mfano wa ajabu wa jambo hili. Inatia mkazo kwamba, hata ingawa ni mnyofu, mtu au hata tengenezo zima linaweza kukosa ibada ya pekee kwa Mungu. Mtume Paulo alisema juu ya watu wa nchi yake Wayahudi, ambao alipenda: “Ndugu zangu, nitakayo sana moyoni mwangu, na dua yangu nimwombayo Mungu, ni kwa ajili yao, ili waokolewe. Kwa maana nawashuhudia kwamba wana juhudi kwa ajili ya Mungu, lakini si katika maarifa. Kwa maana, wakiwa hawaijui haki ya Mungu, na wakitaka kuithibitisha haki yao wenyewe, hawakujitia chini ya haki ya Mungu.”—Rum. 10:1-3.
Kujua anayotaka Mungu si vigumu, ukisoma kwa unyofu na kukubali vile Biblia inasema, ukifanya hivyo bila maoni mabaya yasiyo na msingi ya mambo uliyokuwa ukiamini au mafundisho ya kwanza. Kwa mfano: Mbele tu ya kusema juu ya takwa lake la ibada ya pekee, Mungu alisema:
“Usijifanyie sanamu ya kuchonga, mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, au kilicho chini duniani, au kilicho majini chini ya nchi. Usivisujudie wala kuvitumikia.” (Kum. 5:8, 9) Angalia kwamba Mungu anasema “usijifanyie” wala “usivisujudie.” Nyumaye, Mungu alitangaza: “Mimi ni [Yehova]; ndilo jina langu; na utukufu wangu sitampa mwingine, wala sitawapa sanamu sifa zangu.”—Isa. 42:8.
Ikiwa, basi, umekuwa ukitumia sanamu katika ibada, ziwe ni za Kristo, malaika au watakatifu, utajua, hata watu wasemeje, ya kwamba hukuwa ukimpa Mungu ibada ya pekee.
Kwa hiyo bila shaka unaweza kufahamu kwamba kanisa linalokufundisha kutumia sanamu katika ibada, ingawa inaonwa kana kwamba si ibada ya vitu hivyo, haliwezi kukulinda kwa kuwa mshiriki wake. Kitu cho chote kisichomtukuza Mungu kinapungukiwa na ibada ya pekee kwake. Na tengenezo lo lote linalofundisha mafundisho yasiyomtukuza Mungu, au yanayopinga Neno lake, haliwaletei washiriki wake baraka za Mungu. Kuliko hivyo, kwa ushirika, au kwa kulitegemeza tengenezo hilo, utapatwa na uharibifu wakati Mungu atakapoyaondoa mambo yote yasiyomtukuza duniani.—2 The. 1:7-9.
MWENENDO WA MTU MWENYEWE NI WA MAANA
Tena, huenda ikawa wewe ni mwanafunzi mwenye bidii wa Biblia. Huenda ikawa unajua kanuni inazofundisha, zaidi kanuni zake za adili. Uwe unashirikiana na wengine wanaojidai kuwa Wakristo au sivyo—kwa kweli, hata ikiwa unashirikiana na wale unaojua wanamtolea Mungu ibada ya pekee—ulizo la maana ni, Je! wewe unaishi kulingana na kanuni hizi za haki?
Mtume Petro anaelekeza kwenye daraka la kila mtu anayedai kuwa Mkristo anaposema: “Ikiwa mnamwita Baba, yeye ahukumuye kila mtu pasipo upendeleo, kwa kadiri ya kazi yake, enendeni kwa hofu katika wakati wenu wa kukaa hapa kama wageni [kama vile kuishi katika ulimwengu huu lakini bila kuwa sehemu yake].” Nyumaye anaonya: “Wakati umefika wa hukumu kuanza katika nyumba ya Mungu; na ikianza kwetu sisi, mwisho wao wasioitii injili ya Mungu utakuwaje? Na mwenye haki akiokoka kwa shida, yule asiyemcha Mungu na mwenye dhambi ataonekana wapi?”—1 Pet. 1:17; 4:17, 18.
Kwa hiyo, mtu hawezi kutegemea ushirika wake wa kanisa au uanachama wake. Wala hawezi kuwa salama kwa kuacha tu kanisa linaloendeleza mafundisho ya uongo au kuruhusu mazoea yanayotofautiana na Biblia. Ni lazima vile vile afanye tendo la waziwazi kwa upande wake ili kujifunza mapenzi ya Mungu, kisha kuyafanya. Hii maana yake ni kwamba inampasa ashirikiane na kuwa mfanya kazi mwenzi wa wale wanaomtolea Mungu ibada ya pekee na safi kwa bidii.
Hata nyuma ya hapo, ni lazima ajiangalie. Nyuma ya kutaja mifano ya wale ambao, ingawa walishirikiana na watu wa Mungu waliokubalika wakati wa kale, walishindwa kwa kufanya mabaya katika maisha yao wenyewe, mtume Paulo aliwaandikia Wakristo katika Korintho: “Kwa hiyo anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.” (1 Kor. 10:6-12) Inataka kukesha wakati wote na kujichunguza nafsi ili kuendelea kumtumikia Mungu. Hakuna mtu au tengenezo lo lote linaloweza kumwokoa mtu ye yote, kwa kuwa “kila mtu miongoni mwetu atatoa habari zake mwenyewe mbele za Mungu.”—Rum. 14:12; linganisha Waebrania 4:12, 13.
Hata mtu aliyekubalika sana kama mtume Paulo alisema juu yake mwenyewe: “Mimi napiga mbio vivyo hivyo, si kama asitaye; napigana ngumi vivyo hivyo, si kama apigaye hewa; bali nautesa mwili wangu na kuutumikisha; isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine, mwenyewe niwe mtu wa kukataliwa.”—1 Kor. 9:26, 27.
Kwa kumalizia, basi, juu ya ulizo, Je! ushirika wa kanisa unatosha? tunajibu waziwazi Hapana! Mtu anayetaka kumtumikia Mungu ni lazima aachane na taratibu yake ya kidini ikiwa haifuati Neno la Mungu. Hatua yake inayofuata itakuwa ni kushirikiana na wale wanaomtumikia Mungu katika ibada safi. Kisha, kwa kumtolea Yehova Mungu ibada ya pekee, ni lazima aishi katika njia ambayo maisha yake ‘yatayapamba mafundisho ya Mwokozi wetu Mungu katika mambo yote.’ (Tito 2:10) Mtu anayefanya hivyo anaweza kuwa na uhakika katika ahadi ya Mungu:
“[Yehova] yu karibu na wote wamwitao,
Wote wamwitao kwa uaminifu.
Atawafanyia wamchao matakwa yao,
Naye atakisikia kilio chao na kuwaokoa.”—Zab. 145:18, 19.