Watoto Wafufuliwa Kwa Wafu
Makala hii imekusudiwa hasa kwa wazazi waisome pamoja na watoto wao
JE! SI ajabu kujua kwamba fulani anakupenda? Ni jambo zuri kuwa na watu ambao wanakuangalia kweli. Lakini wajua kwamba kuna mtu fulani anayekupenda zaidi kuliko ye yote duniani? Huyo ni Yehova.
Yehova anatupenda sisi kwa kadiri gani? Je! yeye anatufikiria wakati tupo hapa tu, kisha anatusahau wakati hatupo? Au je! kweli anatukumbuka sisi? Biblia inasema wala ‘mauti wala uzima, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, hayataweza kututenga na upendo wa Mungu.’—Rum. 8:38, 39.
Hivyo Mungu hasahau. Yeye anakumbuka watu wanaomtumikia, naye anakumbuka watoto wao vile vile. Hata ikiwa wanakufa, yeye atawarudisha tena kwenye uzima.
Wakati Mwana wa Mungu Yesu alipokuwapo duniani, alionyesha kwamba Yehova anawaangalia watoto wadogo. Yesu angepata nafasi kuzungumza na watoto juu ya Mungu. Hata alitumia nguvu ya Mungu kuwarudisha watoto kutoka kwa wafu! Ungependa kusikia namna Yesu alivyofanya hili kwa jamaa moja?
Kulikuwako mtu mmoja jina lake Yairo. Yeye na mkewe na binti yao mwenye umri wa miaka kumi na miwili waliishi kama mwendo mfupi kutoka Bahari ya Galilaya. Baba na mama walimpenda binti yao sana. Alikuwa ndiye mtoto wao pekee.
Basi unaweza kuwazia namna walivyohuzunika wakati binti yao mdogo alipokuwa mgonjwa sana. Walifanya kila kitu kadiri walivyoweza apate kupona, lakini akazidiwa. Yairo angeweza kuona kwamba bintiye atakufa. Na hapakuwa na neno ambalo yeye au madaktari wangeweza kufanya wamsaidie.
Labda Yesu angeweza kusaidia. Yairo alikuwa amesikia juu ya mtu huyu wa ajabu na namna yeye angeweza kuponya watu. Basi Yairo alitoka kwenda kumtafuta. Akamwona Yesu pwani ya Bahari ya Galilaya akifundisha watu wengi.
Yairo alipita kati ya watu wengi akaanguka miguuni mwa Yesu. Akamwambia: ‘Binti yangu mdogo ni mgonjwa sana. Tafadhali njoo umsaidie. Nakuomba uje.’
Mara hiyo Yesu alikwenda na Yairo. Watu wengi waliokuwa wamekuja kumwona Mwalimu Mkuu walifuata vile vile. Lakini walipotembea mwendo kidogo, watu fulani walitoka katika nyumba ya Yairo, na kumwambia: “Binti yako amekwisha kufa; kwani kuzidi kumsumbua mwalimu?”
Yesu aliwasikia watu wakisema hivi. Akajua namna Yairo alivyokuwa mwenye huzuni kwa kupoteza mtoto wake wa pekee. Basi akamwambia: ‘Usiogope. Mwamini Mungu tu. Binti yako atapona.’
Basi wakaendelea na safari mpaka wakaja nyumbani kwa Yairo. Hapa rafiki za jamaa walikuwa wakilia. Walihuzunika sana kwa sababu rafiki yao mdogo alikuwa amekufa. Lakini Yesu akawaambia: ‘Acheni kulia. Kijana hakufa, bali amelala tu.’
Yesu aliposema hivi, watu walianza kumcheka. Maana walijua msichana alikuwa amekufa. Lakini Yesu alisema mwanamke kijana alikuwa akilala tu ili kufundisha watu hao somo tu. Alitaka wajue kwamba kwa nguvu za Mungu yeye angeweza kurudisha wafu kwenye uzima kwa vyepesi kama vile angeweza kumwamsha mtu kutoka katika usingizi.
Kwa sasa Yesu akawa ameamuru kila mtu aondoke chumbani isipokuwa watatu wa mitume wake na baba na mama ya mwanamke kijana. Akaingia mahali kijana alipokuwa. Akamshika mkono, akasema: ‘Msichana, inuka!’ Na mara hiyo akasimama akaanza kutembea! Baba na mama walijaa furaha wee.—Marko 5:21-24, 35-43; Luka 8:40-42, 49-56.
Je! umekuwa na rafiki aliyekufa? Ungependa ikiwa mtu huyo angeweza kurudi kwenye uzima hata ungeweza kujifurahisha tena urafiki wake? Unafikiri hili laweza kutukia?
Kwa kuwa Yesu aliweza kumrudisha binti yule kwenye uzima, yeye anaweza kufanya yale yale kwa wengine, sivyo? Lakini je! kweli yeye atafanya? Ndiyo, kwa sababu Yesu mwenyewe alisema: “Saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka.” Na wakati huo unakuja upesi, chini ya utawala wa ufalme wa Mungu.—Yohana 5:28, 29.
Ebu fikiri namna itakavyokuwa ajabu kukaribisha watu kurudi kwenye uzima! Wengine kati yao watakuwa watu tuliowajua. Nasi tutajua ni akina nani wakati wanarudi kutoka kwa wafu, kama vile Yairo alivyomjua bintiye wakati Yesu alipomfufua. Wengine watakuwa watu waliokufa maelfu ya miaka iliyopita. Lakini kwa sababu tu waliishi zamani, Mungu hatawasahau.
Je! si ajabu kujua kwamba Yehova Mungu na Mwana wake Yesu wanatupenda hivyo sana? Wao wanataka tuishi, si miaka michache tu, bali milele!