Kujitayarisha kwa Taratibu Mpya ya Mungu
KAMA ukihamia nchi ya ugenini, kuwa mkazi wa milele huko, kwa kawaida mageuzi mengi yanatakiwa. Ili uendelee vizuri sana, ni lazima ujifunze lugha ya huko. Ni lazima ujue mambo fulani juu ya sheria, desturi na mazoea ya watu wa huko. Kuna namna za usemi mbalimbali na tabia ambazo huenda zinakubalika kabisa katika nchi yako mwenyewe, lakini ambazo ni lazima uachane nazo kwa sababu zitawakosea watu wa nchi uliyoingia karibuni. Inachukua muda fulani kuondoa namna zako za kuwaza na njia za maisha mbele ya kufaa kabisa na kuendelea bila haya au ugumu.
Namna gani, basi, ikiwa ungehamishwa kuingia katika jamii tofauti, taratibu mpya, ambamo haki yote imo, na kutendeana mema na majirani, ndiyo, hata ukarimu wa kweli na upendo bila ubaguzi wa kabila au taifa—mahali ambapo ungeweza kumtumaini mwenzako? Ungesema kwamba hilo ni geuzi linalotofautiana na jamii inayokuzunguka sasa, geuzi hata kubwa zaidi kuliko kuhamia nchi nyingine?
KANUNI ZA JUU ZAIDI ZA KUWAZA NI ZA LAZIMA
Uhamisho huu ndio Mungu anaahidi. Na bila shaka ina maana ya mageuzi mengi makubwa ya kanuni na mazoea ya jamii iliyopo. Je! wale wanaoishi hata katika mataifa ya “Kikristo” watapaswa kufanya geuzi hilo? Taifa la Israeli, ingawa lilidai kumtumikia Mungu, lilikuwa likiishi kwa namna ambayo watu walio katika nchi zinazoitwa za “Kikristo” wanaishi leo. Yaani, walikuwa na ‘mfano wa utauwa, lakini wakakana nguvu zake’ kwa kutokuziruhusu kanuni zilizo juu za sheria za Mungu ziongoze maisha yao. (2 Tim. 3:5) Walitupilia mbali amri za Mungu na kuishi walivyotaka, jambo hili likiwaongoza kwenye mazoea machafu. Kwa hiyo Yehova aliwaambia: “Maana mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu; . . . Kwa maana kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.”—Isa. 55:8, 9.
Je! geuzi katika taratibu mpya lingetaka geuzi katika kuwaza kwako, namna zako za usemi na unayofanya? Bila shaka. Namna inavyoweza kuwa tofauti kushirikiana na watu unaoweza kutumaini katika shughuli, ambao mwenendo wao kukuelekea ungekuwa wa mema, ambao namna zao za usemi zingekuwa safi na za kujenga. Bila shaka geuzi lingetakiwa ikiwa mtu angetaka kuwa sehemu ya jamii fulani iliyo na kanuni kama hizo za juu.
Lakini maulizo yanajitokeza, Kama tunataka kujitayarisha sasa kuishi katika taratibu mpya, je! tunawezaje kufanya hivyo, kati ya mazoea mabaya yanayoendelea? Na je! mtu anaweza kuendelea vyema katika taratibu iliyopo ya mambo ikiwa anazoea uaminifu na maisha safi? Je! itawezekana airuzuku jamaa yake? Je! ataokoka katika ulimwengu huu bila kufuatana nao katika mazoea yake mapotovu?
Jibu ni, Ndiyo. Namna gani? Basi, ni lazima tumkubali Muumba kwa sababu ya ahadi yake. Kutokana na Neno lake la kweli Biblia tunaweza kupata kanuni za haki, zile ambazo Muumba mwenyewe anaweka, na ambazo kwa kweli zinafanya kazi kwa faida ya wale wanaozifuata. Kwa hiyo ni shauri letu tuzoee kanuni hizi katika maisha yetu na kumtumainia yeye aone kwamba tumefanikiwa, kama inavyomlazimu kufanya kulingana na ahadi yake. Lakini ebu na tuone ambayo Mungu anataka na kuahidi.
GEUZI KATIKA “LUGHA”
Kulingana na Biblia, ili kufanya geuzi linalotakiwa imetupasa tujifunze “lugha” mpya. Mungu aliposema juu ya kuwarudisha Waisraeli kutoka uhamishoni wa Kibabeli, alisema: “Maana hapo ndipo nitakapowarudishia mataifa lugha iliyo safi, wapate kuliitia jina la [Yehova], wamtumikie kwa nia moja.” (Sef. 3:9) Hili halikuwa geuzi katika lugha yenyewe ya Waisraeli, bali geuzi katika kile walichosema, njia yao ya kusema, lugha ya ukweli mtupu, usafi wa lugha iliyomletea Mungu sifa na umoja wa ibada, pamoja na amani.
Sasa Mungu anatenda kama alivyotenda huko nyuma, ‘kuwakusanya mataifa, kuzileta pamoja falme, ili azimwagie ghadhabu yake, hasira yake yote inayowaka.’ Kwa hiyo, vile vile, sasa anawapa watu wenye mioyo inayotaka haki wa nchi zote, wawe wanasema lugha ipi, ‘lugha safi’ ya kweli.—Sef. 3:8.
Sasa, geuzi hili la lugha lina maana ya geuzi katika maisha yetu yote. Tunaamriwa:
“Lakini uasherati usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wo wote wala kutamani, kama iwastahilivyo watakatifu; wala aibu wala maneno ya upuzi wala ubishi; hayo hayapendezi; bali afadhali kushukuru.”—Efe. 5:3, 4.
Geuzi tunalofanya linaelezwa vyema na mtume Paulo:
“Basi, vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, mawazo mabaya, na kutamani, ndiyo ibada ya sanamu: kwa ajili ya mambo hayo huja ghadhabu ya Mungu. Katika hayo ninyi nanyi mlitembea zamani, mlipoishi katika hayo. Lakini sasa yawekeni mbali nanyi haya yote, hasira, na ghadhabu, na uovu, na matukano, na matusi vinywani mwenu. Msiambiane uongo, kwa kuwa mmevua kabisa utu wa kale, pamoja na matendo yake; mkivaa utu mpya, unaofanywa upya upate ufahamu sawasawa na mfano wake yeye aliyeuumba.”—Kol. 3:5-10.
Ili kusema lugha hii mpya, basi, inatakiwa tuondoshe namna za usemi za zamani, tabia mbaya na njia za maisha, na pahali pake kuweka ‘matunda ya roho’ ili kwamba tustahili ukombozi na kuingia katika taratibu mpya ya Mungu. (Gal. 5:22, 23) Haya ndiyo “yaliyo mema” yanayosemwa na mtume ambayo yanataka ujuzi wa kweli na ufahamu wote. (Flp. 1:9, 10) Wote ni lazima ‘wasiifuatishe mitindo ya taratibu hii ya mambo, bali wageuzwe kwa kufanya upya akili zao, wapate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.’—Rum. 12:2.
USIOGOPE KUFANYA GEUZI
Geuzi hili katika maisha linaweza kufanywa, hata katika ulimwengu mpotovu. Mungu anasema kwamba atakuwa pamoja na wale wanaofuata kanuni zake za haki na uaminifu. Hakuna sababu ya kuogopa kwamba kufanya hivyo kutatuletea hali mbaya za uchumi jamaa zetu zisipate chakula cha kutosha. “Kwa kuwa yeye mwenyewe amesema, Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa.”—Ebr. 13:5, 6.
Tunaweza kuwa huru na woga unaozunguka ulimwengu, kwa kuwa tunajua kwamba “Mungu akiwapo upande wetu, ni nani aliye juu yetu?” Musa, aliyepata ulinzi wa Mungu katika taabu nyingi, kwa kweli angeweza kusema: “Kwa kuwa [ulisema] Wewe [Yehova] ndiwe kimbilio langu; umemfanya Aliye juu kuwa makao yako. Mabaya hayatakupata wewe.”—Rum. 8:31; Zab. 91:9, 10.
Kuna sababu nyingine ya sisi kuishi kulingana na kanuni za Mungu hata sasa, tukiwa na tumaini la kuishi katika taratibu mpya ya mambo yenye haki kabisa. Sababu hiyo ni kwamba Mungu ana tengenezo duniani, lililofanyizwa ili kuwasaidia wale wanaotaka kumtumikia sasa. Mashahidi wa Yehova wamezikubali kanuni za Neno la Mungu. Wanazitumia katika maisha yao. Wanafahamu kwamba kwa kuzaliwa wao ni wenye dhambi, kama wanadamu wote walivyo, lakini kwa kuzungumza “lugha mpya” wanageuza utu wao na wanatumikia kama mtu mmoja, “kwa nia moja.”—Efe. 4:20-24; Flp. 1:27, 28.
Kulingana na ahadi yake Mungu amekisaidia kikundi hiki cha watu, wenye kazi mbalimbali, wa mataifa yote na makabila yote. Kama mwili wa watu milioni moja na nusu, wote wakishirikiana kwa umoja, wanaweza kushuhudia ukweli wa maneno ya Mfalme Daudi: “Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, lakini sijamwona mwenye haki ameachwa, wala mzao wake akiomba chakula.” (Zab. 37:25) Vile vile, mashahidi wa Yehova ni wenye furaha. Furaha yao imevuta fikira za wengine ambao wameungana nao katika kazi yao. Taratibu za Kristendomu za kidini zinapopungua, Mashahidi, ambao kwa unyofu wanazoea Ukristo wa kweli, wanaongezeka katika hesabu yao, kwa umoja na kwa amani. Wanajihakikisha wenyewe kuwa watu wanaojitayarisha kwa maisha katika taratibu mpya ya Mungu.