Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w26 Aprili kur. 20-25
  • Jifunze Kutoka kwa “Mungu wa Faraja Yote”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jifunze Kutoka kwa “Mungu wa Faraja Yote”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2026
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UFAFANUZI WA FARAJA KATIKA BIBLIA
  • JINSI YA KUWAFARIJI WENGINE
  • UNAPOHITAJI FARAJA
  • Mpango wa Kuwafariji Wale Walio Betheli
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2023
  • Kamwe Hatuko Peke Yetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • ‘Wafariji Wote Wanaoomboleza’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Faraja kwa Watu Waliotendewa Vibaya Kingono
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2026
w26 Aprili kur. 20-25

JUNI 22-28, 2026

WIMBO 90 Tianeni Moyo

Jifunze Kutoka kwa “Mungu wa Faraja Yote”

‘Tuwafariji wengine kwa faraja ambayo tunapokea kutoka kwa Mungu.’—2 KOR. 1:4.

JAMBO KUU

Jinsi ya kuwafariji wengine kwa kuiga mfano wa Yehova na wale wanaomwiga.

1. Kwa nini tunapaswa kuwafariji wengine?

SOTE ‘tumehuzunishwa kwa majaribu mbalimbali,’ hivyo pindi fulani tunahitaji kufarijiwa na kutiwa moyo. (1 Pet. 1:6) Kwa kuwa tunathamini tunapofarijiwa na wengine, tunapaswa kuwa wepesi wa kuwafariji wale wanaoteseka. (Mt. 7:12) Yehova, “Mungu wa faraja yote,” anatuonyesha jinsi ya “kuwafariji wengine walio katika majaribu ya namna yoyote.” Tunaweza kuiga kielelezo chake kwa “kufarijiana.” (2 Kor. 1:​3, 4; 1 The. 4:18) Tunafanya hivyo, si kwa sababu tunalazimika, bali kwa sababu tunawapenda ndugu na dada zetu. Katika makala hii, tutachunguza (1) maana ya faraja kama inavyofafanuliwa katika Biblia, (2) jinsi tunavyoweza kuwafariji wengine, na (3) mambo tunayoweza kufanya tunapohitaji faraja.

UFAFANUZI WA FARAJA KATIKA BIBLIA

2. Katika Biblia, neno linalotafsiriwa “faraja” linaweza kuwa na maana gani nyingi?

2 Katika Biblia, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “faraja” linaweza kuwa na maana nyingi ikitegemea muktadha. Linaweza kumaanisha “kutia moyo,” “kuhimiza,” au “kuchochea,” (Rom. 12:8; tazama habari za utafiti, ““encourages.” nwtsty.) Kihalisi neno hilo linamaanisha “kumwita mtu aje upande wako.” Hivyo, tunaweza kumwazia rafiki akija kwa haraka kumsaidia rafiki yake anayeteseka, kwa kumpatia utegemezo au msaada wowote anaohitaji. Haidhuru aina ya msaada unaotolewa na rafiki huyo, faraja ya kweli huwa na matokeo yaleyale—yule anayeteseka anajengwa na kuimarishwa.

3. Barnaba aliweka kielelezo gani cha kuwafariji wengine? (Tazama pia picha.)

3 Fikiria mfano huu wa Biblia. Mkristo anayeitwa Yosefu alionyesha uwezo mkubwa wa kuwatia moyo na kuwafariji wengine hivi kwamba mitume wakamwita Barnaba, jina linalomaanisha “Mwana wa Faraja.” (Mdo. 4:36) Jina hilo lilimfaa sana hivi kwamba Biblia haimrejelei tena kwa jina lake, Yosefu. Katika pindi mbalimbali, Barnaba aliishi kulingana na jina lake kwa kuwasaidia waabudu wenzake walipohitaji msaada. Kwa mfano, mwanafunzi Sauli aliyegeuzwa imani karibuni alipofika Yerusalemu, alitaka kukutana na wanafunzi wa Yesu. Hata hivyo, walimwogopa kwa sababu ya sifa yake ya kuwa mtesaji. Lakini Barnaba hakuogopa kumwonyesha fadhili Sauli, na akamtambulisha kwa mitume.—Mdo. 9:​26-28.

Kwa fadhili, Barnaba anamleta Sauli ili akutane na baadhi ya mitume katika mojawapo ya nyumba zao. Mitume wanamtazama Sauli kwa wasiwasi anapowakaribia.

Barnaba aliishi kulingana na maana ya jina lake (Tazama fungu la 3)


JINSI YA KUWAFARIJI WENGINE

4. Taja mojawapo ya njia bora ya kutoa faraja. (Waroma 1:​11, 12)

4 Watembelee ikiwa inawezekana. Yehova anatumia watumishi wake kuwafariji wengine. Kwa mfano, nabii Eliya alipokuwa ameshuka moyo, Yehova alimtuma malaika amtie moyo. (1 Fal. 19:​4-7) Mtume Paulo pia alitambua umuhimu wa kuwatembelea ana kwa ana ndugu zake ili kuwatia moyo. (Soma Waroma 1:​11, 12.) Unapomtembelea mtu ili kumfariji, tumia wakati wa kutosha pamoja naye. (1 Kor. 16:7) Hata hivyo, ikiwa huwezi kumtembelea mtu mwenye uhitaji, usipuuze umuhimu wa kupiga simu, kuandika barua, kadi, au ujumbe mfupi wa simu ili kumwimarisha. Je, utamruhusu Yehova akutumie kuwapatia faraja wengine?

5. Tunaweza kutarajia kukabili changamoto gani?

5 Kadiri siku za mwisho zinavyokuwa hatari zaidi, tunaweza kutazamia changamoto zaidi tunapojitahidi kuwafariji ndugu na dada zetu ana kwa ana. Paulo alipokuwa amefungwa gerezani jijini Roma, Onesiforo, aliyekuwa katika jiji la Efeso alimtafuta ingawa angeweza kufungwa au hata kuuawa. (2 Tim. 1:​16-18) Mashahidi nchini Urusi wameonyesha pia roho hiyo wakati ndugu na dada zao wanapoteswa kwa sababu ya imani yao. Mashahidi wanapopelekwa mahakamani, ndugu na dada wanaenda mahakamani ili kuwatia moyo, ingawa kufanya hivyo kunaweza kuhatarisha uhuru wao. Kwa nini usijitayarishe ili ufuate mfano wao wenye ujasiri kwa kujifunza jinsi watu wa Mungu katika nyakati za kale na nyakati zetu walivyotegemezana na kupata shangwe licha ya mateso?

6. Tunawezaje kumwiga Yehova tunapowafariji wengine? (Tazama pia picha.)

6 Wasikilize. Nabii Eliya alipohisi kwamba uhai wake uko hatarini, alimmiminia Yehova moyo wake. Mungu wetu mwenye upendo alimsikiliza Eliya alipomweleza kuhusu mahangaiko yake hata ingawa tayari alijua jambo lililokuwa likimsumbua. Yehova hata alimsikiliza kwa subira Eliya alipokuwa akirudia kusema mambo yaleyale! (1 Fal. 19:​9, 10, 14) Pia, Yehova alimruhusu nabii Habakuki aeleze mahangaiko na wasiwasi wake kwa njia ambayo huenda ingeonekana anatilia shaka mamlaka ya Mungu. (Hab. 1:​2, 3) Leo, Yehova anasikiliza kwa makini sala zetu ingawa tayari anajua mambo tunayohitaji. Tunaweza kumwiga Yehova kwa kuwasikiliza kwa makini na heshima ndugu na dada zetu wanapozungumza. Uwe “mwepesi wa kusikia” wanapozungumza, na epuka kuwakatisha au kukasirika, hata ikiwa wanaonekana kwamba wanazungumza kwa ukali au ikiwa wanarudia kusema maneno yaleyale.—Yak. 1:19; Mhu. 7:9.

Dada akimsikiliza kwa subira dada anayetaabika anapomweleza mahangaiko yake huku usiku ukizidi kusonga.

Mwige Yehova kwa kuwasikiliza kwa makini ndugu na dada zako wanapozungumza (Tazama fungu la 6)


7. Tunawezaje kutambua mahitaji ya mtu anayetaabika?

7 Jitahidi kutambua mahitaji ya mtu. Hatuwezi kusoma mioyo kama Yehova anavyofanya, hivyo tunaweza tu kutambua faraja ambayo mtu anahitaji ikiwa tutamsikiliza kwa makini. Usifikiri kwamba unajua jambo ambalo mtu anahitaji kwa sababu unajua jambo ambalo wewe ungehitaji ikiwa ungekuwa katika hali kama yake. Sisi sote tuko tofauti. Hivyo, tumia wakati wa kutosha, sikiliza kwa makini, na kwa busara, uliza maswali ambayo yatakusaidia kuelewa hisia zake.—Met. 20:5.

8. Yesu aliwafariji jinsi gani Martha na Maria baada ya kifo cha Lazaro? (Tazama pia picha.)

8 Fikiria jinsi ambavyo Yesu alimfariji Martha na Maria baada ya kifo cha Lazaro, ndugu yao. Wanawake hao wawili walikuwa na huzuni ileile ya kumpoteza ndugu yao; hata hivyo, Yesu aliwafariji kwa njia tofauti. Baada ya Martha kuzungumza naye, Yesu alimweleza kweli kuhusu ufufuo na kumsaidia aimarishe imani yake katika uandalizi huo wenye upendo. Lakini Maria alipokuja kwake huku akilia, inaonekana Yesu hakuzungumzia ufufuo. Badala yake, alilia pamoja na Maria na akaomba aonyeshwe mahali ambapo alikuwa amelazwa. (Yoh. 11:​20-35) Tunajifunza nini? Tunapowafariji wale wanaoteseka, ni lazima tujitahidi kutambua mahitaji yao, badala ya kujaribu kumfariji kila mtu kwa njia ileile.

Mkusanyo wa picha: Mzee akiwatembelea nyumbani ndugu wawili waliofiwa na wake zao. 1. Mzee huyo anamshika begani ndugu anapolia. 2. Mzee anamsomea andiko ndugu mwenye umri mkubwa wanapotazama picha pamoja.

Unapowafariji wengine, jitahidi kutambua mahitaji yao (Tazama fungu la 8)a


9. Tunawezaje kutumia Biblia kuwafariji wengine? (Waroma 15:​4, 5)

9 Tumia Biblia. Unaposhiriki na mtu mwingine “faraja kutoka kwa Maandiko,” unaweza kumsaidia apate tumaini. (Soma Waroma 15:​4, 5.) Kisha, tumaini hilo humpatia faraja zaidi na kumtia moyo. (Isa. 40:31) Unawezaje kupata andiko la Biblia litakalomtia moyo? Baadhi ya watu hutunza orodha ya maandiko wanayoweza kuyatumia inapohitajika, kama vile yale yaliyo chini ya kichwa “Faraja” katika kitabu, Maandiko kwa Ajili ya Maisha ya Mkristo. Mwombe Yehova akusaidie kutumia Neno lake kwa njia bora ili uweze kuwatia moyo wengine. Roho yake inaweza kukusaidia kukumbuka maandiko yanayofariji unapoyahitaji.—Yoh. 14:26.

10. Kwa nini ni lazima tuzungumze kwa fadhili tunapojitahidi kumtia moyo mtu?

10 Zungumza kwa fadhili. Neno la lugha ya awali linalotafsiriwa “faraja” linaweza pia kumaanisha “himiza,” au “chochea.” Pindi fulani, huenda ukahitaji kumhimiza, au kumchochea mtu unayemfariji ili arekebishe njia yake ya kufikiri. Ikiwa utahitaji kufanya hivyo, tafakari kwa makini kabla ya kuzungumza ili maneno yako yaponye badala ya kuumiza. (Met. 12:18) Yehova alituwekea kielelezo kikamilifu alipozungumza na Eliya, aliyekuwa na maoni yasiyo sahihi kuhusu thamani ya kazi yake na kiwango cha uasi-imani katika taifa la Israeli. Kwa fadhili, Yehova alimsaidia Eliya arekebishe njia yake ya kufikiri bila kumweleza moja kwa moja makosa yake. (1 Fal. 19:​15-18) Ukionyesha fadhili na kutafakari kwa makini kabla ya kuzungumza, unaweza kufanya vivyo hivyo. Unapotoa hotuba au kutoa maelezo katika mikutano ya Kikristo, sikuzote zungumza kwa fadhili na kwa njia inayofaa unapojitahidi kuwatia moyo na kuwaimarisha ndugu na dada zako.

11. Wale wanaotaabika mara nyingi wanahitaji nini? (1 Yoh. 3:18)

11 Toa msaada hususa. Mara nyingi, wale wanaotaabika wanahitaji mengi zaidi ya maneno ya faraja. (Soma 1 Yohana 3:18.) Barnaba aliweka mfano mzuri alipouza shamba na kutoa mchango wa pesa alizopata ili kuwategemeza ndugu na dada waliotoka kubatizwa ambao walikuwa na uhitaji. (Mdo. 4:​36, 37) Leo, Wakristo wenzetu wengi wanafuata mfano wake mzuri kwa kutoa msaada hususa ili kuwasaidia wenye uhitaji. Gabriela, kutoka nchini Poland, alivunjika moyo sana baada ya mafuriko kuharibu sana nyumba yake. Anaeleza hivi: “Nilikuwa na wasiwasi na niliogopa sana, na hata pia wazazi wangu walioishi pamoja nami walihisi hivyo. Nilijiuliza ikiwa nitaweza kukabiliana na hali hiyo. Lakini akina ndugu kutoka makutaniko ya karibu walifika na kufanya kazi kubwa ya kurekebisha nyumba yetu ndani ya siku moja. Jambo hilo liliimarisha imani yangu kwamba Yehova anawatumia watu wake kuwafariji wale wanaoteseka.”

12. Unawezaje kuwasaidia Wakristo wenzako unapovumilia majaribu kwa uaminifu?

12 Vumilia majaribu yako. Paulo aliwaambia Wathesalonike kwamba alipata faraja na nguvu mpya aliposikia kuhusu jinsi wanavyovumilia kwa uaminifu. Alijua kwamba kazi aliyofanya miongoni mwao haikuwa ya bure. (1 The. 3:​5-8) Naye Paulo alitumaini kwamba atawafariji ndugu zake—hata wale ambao hawakuwa wamekutana naye—kupitia jinsi alivyopambana kwa ajili yao. (Kol. 2:​1, 2) Vivyo hivyo, kadiri Wakristo wenzetu wanavyoona jinsi Yehova anavyotusaidia kuvumilia majaribu yetu kwa mafanikio, ndivyo wanavyotiwa moyo zaidi.

13. Ni lazima tuendelee kufanya nini tunapowafariji wengine?

13 Uwe mwenye subira. Huenda ndugu na dada waliovunjika moyo wasiitikie mara moja jitihada zetu za kuwafariji. Hata hivyo, Maandiko yanatuhimiza hivi: “Endeleeni kutiana moyo.” Maneno “endeleeni kutiana moyo” yanafafanua kitendo kinachoendelea. (1 The. 5:11) Uwe mwenye subira unapoendelea kuwafariji wale wanaohitaji msaada wako. (1 The. 5:14) Bila shaka, pindi fulani, kila mmoja wetu atahitaji kufarijiwa. Tunaweza kufanya nini tukiwa katika hali hiyo?

UNAPOHITAJI FARAJA

14-15. Tunapaswa kufanya nini tunapokuwa na mahangaiko au wasiwasi?

14 Sali kwa Yehova. Mwombe akufariji unapokuwa na mahangaiko au wasiwasi. (Zab. 94:19) Sali kwake ukitaja mambo kihususa, huku ukimmwagia moyo wako. (Zab. 62:8) Ni kweli kwamba Yehova tayari anajua jinsi unavyohisi hata kabla ya kusali. Lakini kumweleza mawazo yako ya ndani kabisa kupitia sala ya kutoka moyoni kunaonyesha imani yako. Na Yehova hashindwi kamwe kujibu kwa njia yake mwenyewe sala zinazotolewa kwa imani. (Marko 11:24) Andiko la Wafilipi 4:​6, 7 linatuhimiza hivi: “Mjulisheni Mungu maombi yenu; na amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili.”

15 Waombe wengine msaada. Mweleze rafiki mkomavu hisia zako, au zungumza na mzee wa kutaniko unayemwamini. Ndugu na dada zako wanaweza kuwa chanzo cha faraja, lakini usipowaeleza hali yako huenda wasijue jinsi unavyohisi au kile unachohitaji. (Met. 14:10) Unaweza kuwaomba wakusikilize au washiriki nawe andiko au makala ambayo imewafariji wao.

16. Ni jambo gani linaloweza kutokea wengine wanapojaribu kukutia moyo, lakini unapaswa kukumbuka nini?

16 Uwe mwenye subira na mwenye kusamehe. Huenda ndugu na dada zako wakakukosea wanapojitahidi kukutia moyo. Kwa mfano, huenda wakasema au kutenda jambo ambalo likakufanya ujihisi vibaya zaidi, badala ya kutiwa moyo. Hilo likitokea, waonyesha subira. (1 Kor. 13:​4, 7) Na kumbuka maneno yanayopatikana katika andiko la Yakobo 3:​2, linalosema hivi: “Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyo ni mtu mkamilifu.” Kazia fikira nia nzuri ya ndugu na dada zako. Kumbuka kwamba “roho inataka lakini mwili ni dhaifu.”—Mt. 26:41.

17. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

17 Sote tunahitaji faraja na kitia moyo, na uhitaji huo utaendelea kuongezeka kadiri siku za mwisho zinavyozidi kuwa hatari zaidi na kadiri maadui wa Mungu wanavyozidi kutupinga vikali zaidi. Acheni tuazimie kujitahidi kuendelea kufarijiana.

UNGEJIBUJE?

  • Kama inavyofafanuliwa katika Biblia, neno “faraja” linamaanisha nini?

  • Tunawezaje kuwafariji wengine?

  • Tunaweza kufanya nini tunapohitaji faraja?

WIMBO 130 Uwe Mwenye Kusamehe

a MAELEZO YA PICHA: Mzee anamsikiliza kwa hisia-mwenzi ndugu ambaye amefiwa na mke wake karibuni. Baadaye, mzee huyo anamtembelea ndugu aliyefiwa na mke wake muda fulani uliopita, na wanazungumzia mambo mazuri wanayokumbuka kumhusu dada huyo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki