Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w73 12/1 kur. 536-541
  • “Tufuate Mambo ya Amani”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Tufuate Mambo ya Amani”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUFAIDIKA NA AMANI AMBAYO YEHOVA ANALIPA TENGENEZO LAKE
  • NAFASI ZA KUPATANA SISI KWA SISI
  • AMANI NA YEHOVA NDILO KUSUDI LETU
  • KWA UNYENYEKEVU EPUKA KUHUKUMU MAKUSUDI YA WENGINE
  • FUATIA AMANI KWA KUENDELEZA MAONI YA YEHOVA JUU YA UZIMA
  • Jinsi Ambavyo Amani Yaweza Kupatikana Duniani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Jinsi Wewe Unaweza Kuona Amani ya Kimungu kwa Ukamili Zaidi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Acha “Amani Ya Mungu” Ilinde Moyo Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • ‘Tafuta Amani na Uifuatie’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
w73 12/1 kur. 536-541

“Tufuate Mambo ya Amani”

“Basi kama ni hivyo, na tufuate mambo ya amani na mambo yafaayo kwa kujengana.”​—Rum. 14:19.

1. (a) Karne ya ishirini imelazimishwa ikubali nini? (b) Lakini ni maulizo gani tunayolazimishwa kuyauliza?

UTAFUTAJI wa amani ndiyo shughuli kubwa ya kizazi chetu. Watu wengi wanasadiki ya kwamba ili jamii ya wanadamu wote ipate kuokoka ni lazima kuweko amani. Lakini je! mataifa na watu wote wanataka sana amani hata wana nia ya kupata hasara yake kubwa katika kutengeneza maisha zao, shabaha na kanuni? Ikiamuliwa kwa jitihada wanazofanya ili waipate, hawataki. Angalia ushuhuda:

2. (a) Ulimwengu unatafutaje amani, kwa matokeo gani? (b) Mwanasayansi Mfaransa anasema amani inapaswa iimarishweje?

2 Ulimwengu unatafuta amani kwa njia ya choyo, kwa njia ya usawa wa nguvu, mapatano na miungano ya mataifa yote. Unajaribu kutumia kwa werevu uwezo wa kibinadamu ili kuzuia vita. Kwa kweli, hali ya kujitayarisha silaha ndiyo namna ulimwengu unavyofahamu amani. Unatumaini kwamba woga utazuia ugomvi na jeuri. Amani hiyo ni ya juujuu tu, ya uongo. Haionyeshi utafutaji wa amani ya kweli hata kidogo. Kama Lecomte du Noüy mwanasayansi Mfaransa alivyosema: “Umefika wakati kwa mataifa, vile vile kwa kila mtu, kujua wanachotaka. Ikiwa nchi zilizostaarabika zinataka amani, inazipasa zifahamu kwamba ni lazima tatizo lifikiwe kwanza. Mjengo wa kale tulioachiwa na vizazi vya zamani unapasuka-pasuka kila upande. Hauwezi kutengenezwa kwa kutumia kitu kingine mahali pake, kwa njia za kushikamanisha na mapatano yenye kutiwa sahihi na Wakuu. Tena, kutengeneza hakutoshi. Ni lazima amani iimarishwe kwa kuwageuza wanadamu kwa ndani na si kwa kujenga nje.”

3. (a) Nabii Isaya anasema nini juu ya asili ya amani? (b) Kwa sababu gani mataifa hayawezi kujidai amani hiyo, lakini ni nani wanaoweza, na kwa sababu gani?

3 Walakini, amani kwa njia ya nguvu hiyo yenye kugeuza haitokani na maongozi ya kisiasa ya wanadamu, bali inatokana na haki ya Yehova Mungu. Ebu angalia ambavyo nabii wa Yehova Isaya alivyoandika juu ya amani hii karne saba mbele ya Wakati wetu wa Kawaida. Kwanza anasema kwamba amani ya kweli haiwezi kuja duniani mpaka “roho [ya Yehova imwagwe] juu yetu kutoka juu.” Ndipo Isaya anapoendelea kusema hivi: “Kazi ya haki itakuwa amani; na mazao ya haki yatakuwa ni utulivu na matumaini daima.” (Isa. 32:15-17) Ni mataifa gani yawezayo kudai kwamba, jambo ambalo walifikiria kwanza katika mazungumzo yao yote ya kisasa ya amani lilikuwa haki ya Mungu? Hawakukusudia hivyo hata kidogo. Kwa hiyo, hawajapata hata kidogo ile amani iliyosemwa na nabii wa Mungu. Lakini watu wa Mungu, mashahidi wake, wameonyesha kupendezwa kwa kweli na haki ya Mungu. Kwa maana Yehova ni Mungu wa amani; amani ni tunda la roho yake. (2 Kor. 13:11; Gal. 5:22) Basi mashahidi wake wamepata amani ya Mungu inayopita wazo lote, ambayo imeongoza mioyo na akili zao kwa njia ya Kristo Yesu. (Flp. 4:7) Wale wote wanaoipenda haki na wanataka kuishi milele yawapasa sasa waifikirie amani hii.

KUFAIDIKA NA AMANI AMBAYO YEHOVA ANALIPA TENGENEZO LAKE

4. Ni hali gani zilizomo katika tengenezo la Yehova, na hizi zilitabiriwaje?

4 Yehova amelipa tengenezo lake amani tele kwa sababu linapendezwa sana na haki. Amani hii inaonyeshwa na hali ya utulivu na upatano ulioko kati ya mashahidi wa Yehova. Wao hawana mashaka au kubishana juu ya namna Yehova anavyoliongoza tengenezo lake. Hali hii ya amani ilitabiriwa katika Isaya 60:17: “Tena nitawafanya wasimamizi wako wawe amani, na hao wakutozao fedha kuwa haki.” Bila haki ya Mungu, amani ya kweli au ya milele haiwezi kuwako.

5. Tengenezo la Yehova linaendelezaje umoja wake wenye amani?

5 Wakati Yehova anapotoa busara iliyo wazi juu ya fundisho au mwendo mpya wa kufuata, ndipo maagizo yanapotumwa kwa njia yenye utaratibu kwa matawi mbalimbali ya tengenezo. Ndipo tengenezo zima linapotenda kwa usawa katika mwendo mpya katika kupatana zaidi na mapenzi yaliyofunuliwa ya Yehova. Marekebisho yanatimizwa kwa amani, bila washiriki wake mbalimbali kushindana wao kwa wao. Kwa njia hiyo tengenezo linasonga mbele na linasimamia kazi ya Yehova ipate kufanywa.

6, 7. (a) Jambo gani laweza kufahamika juu ya amani iliyomo katika tengenezo la Yehova? (b) Kila mshiriki ana wajibu gani juu ya kuendeleza amani, kama inavyoshauriwa na Petro na Yohana?

6 Kutokana na Biblia na kutokana na ambayo kila mtu anaona, inafahamika kwamba amani ya tengenezo ya mashahidi wa Yehova si kitu cha kuwazia tu bali ni kweli, matokeo ya mapenzi ya kimungu, tunda la roho takatifu ya Mungu. Imetoka kwa Mungu, kuliko kufanyizwa kwa jitihada za wanadamu zisizo na msaada. Ijapokuwa hivyo, huenda mtu akauliza: Kila mtu aliye katika tengenezo anasaidiaje kusitawisha amani yake?

7 Amani ya kipekee haitokei mara hiyo ati kwa sababu mtu ameingia katika tengenezo la Yehova lenye amani. Inampasa kila mmoja atimize sehemu yake. Kama mtume Petro alivyotangaza: “Atakaye kupenda maisha, na kuona siku njema, auzuie ulimi wake usinene mabaya, na midomo yake isinene hila. Na aache mabaya, atende mema; atafute amani, aifuate sana.” (1 Pet. 3:10, 11) Kutokana na maneno ya Petro yaliyoongozwa na roho ya Mungu ni wazi kwamba, ili tujifurahishe amani ya tengenezo la Yehova, ni lazima amani ianzie kwa kila mtu. Haipaswi iwe sifa inayopatikana katika tengenezo tu. Vile vile mtume Yohana anakazia jambo hili, akisema: “Watoto wadogo, tusipende kwa neno, wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.” (1 Yohana 3:18) Maneno peke yake hayatatosha; kunahitajiwa matendo na kweli.

8. Ni maulizo gani yanayoweza kuulizwa ili kufunua kama tunaendeleza amani katika maisha yetu ya kila siku?

8 Je! tunafuatia mambo yanayoleta amani katika kushughulika kwetu na wengine katika kundi? Tunaweza kujua kwa kujiuliza wenyewe kama mwenendo wetu au namna tunavyoutumia ulimi wetu inafanyiza mashaka, ugomvi wo wote, au kama tuna kinyongo na mtu ye yote. Namna gani hali iliyo katika jamaa yetu? Je! kuna matata yo yote humo, kuzozana na kulaumiana ko kote? Je! kuna ukali humo? Bila shaka nyakati nyingine sisi sote tunakosea katika mambo hayo. Lakini kuazimia kwetu kumepaswa kuwe kwa amani, na, bila shaka, sisi sote twaweza kutengeneza mambo haya.

9. Ni mambo gani juu ya amani ambayo mtume Paulo na mwanafunzi Yakobo wanatukumbusha?

9 Kwa sababu tengenezo la Yehova lina amani, ni lazima kila mtu aliye ndani yake ajitahidi kusitawisha amani bila kukoma. Mtume Paulo alisema kama amri hivi: “Basi kama ni hivyo, na tufuate mambo ya amani na mambo yafaayo kwa kujengana.” (Rum. 14:19) Hatuwezi kudhania kwamba amani inaweza kutokea ivi hivi tu. Ni ushuhuda wa kuonyesha hekima ya kimungu ambayo watu wenye kumpenda sana Mungu wanatumia. Mwanafunzi Yakobo alieleza hili waziwazi, akisema: “Hekima itokayo juu, kwanza ni safi, tena ni ya amani . . . Na tunda la haki hupandwa katika amani na wale wafanyao amani.” (Yak. 3:17, 18) Tena hapa, fikira zinakazwa juu ya kila mtu kusitawisha amani.

NAFASI ZA KUPATANA SISI KWA SISI

10, 11. (a) Ni wakati gani uwezo wetu wa kuendelea kuwa wenye amani unapojaribiwa? (b) Mambo ya kawaida ya maisha yanatoaje nafasi za kuendeleza amani?

10 Amani ya kweli ni zaidi ya kuwa wenye urafiki wakati mambo yanapofanyika vizuri katika upande wetu au yanapofaa maoni yetu au yale tunayopendelea. Wakati wa hali hizo amani yetu haijaribiwi. Lakini tunafanyaje tunapokuwa chini ya mkazo wa namna fulani? Je? tunafuatia amani wakati huo? Je! tunahifadhi hali yetu ya amani tunapokuwa chini ya mkazo?

11 Shughuli za kawaida kati ya watu walio nje na walio ndani ya kundi zinatoa nafasi nyingi za kupatana sisi kwa sisi. Kwa kuwa sisi ni watu wasiokamilika, mara nyingine kukutana na watu wengine kunafanyiza mikazo ya kuvunja amani. Mambo hayo yanatujaribu ili tuonyeshe kama kweli tunaitafuta amani. Kwa mfano, mambo mengi sana leo yanawafanya watu wagombane, na kwa kawaida ni mambo madogo sana na yasiyo na maana. Unapojiona mwenyewe unaelekea kuwa katika jambo linaloelekea kuwa ugomvi, unafanya nini ili ulizuie? Tukituliza hasira zetu na kuendeleza amani kwa matokeo mazuri chini ya mikazo hii midogo ya kila siku, kweli tunaweka msingi wa kuendeleza amani chini ya mikazo mikubwa. Yesu Kristo alisema hivi: “Aliye mwaminifu katika lililo dogo sana, huwa mwaminifu katika lililo kubwa pia.” (Luka 16:10) Tukizoea kugombana juu ya mambo madogo, hatuwezi kushughulika na makubwa yanayotaka kuharibu amani.

12. Ni hali gani zinazoweza kuharibu amani?

12 Ni hali gani kati ya zile zinazoweza kuharibu amani katika jamaa zetu na katika kundi? Wakati Jumba la Ufalme lenu lilipokuwa likijengwa, labda kutofautiana juu ya mambo fulani ya ujenzi kulisababisha kusemwa kwa maneno makali makali. Mara nyingine watoto wanaudhika wakati wazazi wao kwa mzaha wanapofunua tabia zao mbele ya wengine, pasipo kujua wakiwafanya wajione wapumbavu. Mara nyingine wake nao wanafanya mzaha kwa kufunua makosa madogo-madogo ya siri ya waume zao mbele ya watu, kwa kutokufahamu wakiwafanya waone aibu. Jambo linaloleta matata sana ni wakati waume wanaposhindwa kuwaongoza watoto wao au wakati hawawasaidii wake zao wakati wa shida.

13. Inafaa tujiulize maulizo gani?

13 Je! wewe umo katika mojawapo ya hali hizi, au nyingine zinazofanana na hizo? Unafanya nini kwa ajili ya amani? Wakati amani inapohatirishwa, je! sikuzote unamlaumu mtu mwingine? Je! unamngojea mtu mwingine ndiye achukue hatua ya kwanza ya kurudisha na kufanya amani? Kushinda mikazo midogo ya kila siku kunaongeza maisha yenye amani na kazi yenye kufurahisha katika tengenezo la Yehova.

14, 15. (a) Jambo gani linalowezesha kufuatia kwa amani kuwe na matokeo mema? (b) Ni kanuni gani iliyowekwa na mtume Yohana inapasa shughuli yetu ya amani, na Yesu anakaziaje maana ya kupatana na ndugu?

14 Kumbuka, amani inatokana na hekima ya kimungu, maana yake ni kufuata kanuni za Mungu, kuzoea haki. Kwa wazi basi, kujaribu kuwa mtu mzuri katika wakati unaofaa, kwa namna ya kusuluhisha ili uepuke matatizo tu, sivyo amani ya Kikristo ilivyo. Sivyo, amani ambayo Yehova anatoa inaonyesha jambo ambalo ni zaidi ya hilo.

15 Kanuni hiyo inakaziwa kwa ajili yetu katika 1 Yohana 4:20, 21, inayosema hivi: “Mtu akisema, Nampenda Mungu, naye anamchukia ndugu yake, ni mwongo; kwa maana asiyempenda ndugu yake ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hakumwona. Na amri hii tumepewa na yeye, ya kwamba yeye ampendaye Mungu, ampende na ndugu yake.” Kanuni kubwa hapa ni hii: Ikiwa twataka tuwe na amani na Mungu, inatupasa tuwe na amani sisi kwa sisi. Yesu alisema jambo hili waziwazi katika Mahubiri yake juu ya Mlima, akisema: “Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako.” (Mt. 5:23, 24) Katika maneno mengine, kwamba kumwabudu kwetu Yehova kunakubalika ama hakukubaliki inategemea jambo lenyewe hili la kupatana na ndugu yetu.

16. (a) Ni kwa sababu gani si vyepesi sikuzote kufuatia amani? (b) Yesu alijionyeshaje mwenyewe kuwa mfanya amani? Taja mifano.

16 Walakini, si vyepesi sikuzote kufuatia amani; kwa kweli, nyakati nyingine inaweza kuwa vigumu. Mara nyingi ni shauri la nani ambaye imempasa achukue hatua ya kwanza na namna ya kuichukua. Yesu alisema hivi: “Basi [wewe] ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku [wewe] ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako [wewe],” imekupasa wewe ndiwe uchukue hatua ya kwanza ya kupatana. Paulo anaeleza zaidi jambo hili, akisema: “Basi imetupasa sisi tulio na nguvu kuuchukua udhaifu wao wasio na nguvu, wala haitupasi kujipendeza wenyewe. Kila mtu miongoni mwetu na ampendeze jirani yake, apate wema, akajengwe. Kwa maana Kristo naye hakujipendeza mwenyewe.” (Rum. 15:1-3) Kwa hiyo, imempasa aliye na nguvu za kiroho ndiye awe wa kwanza kuchukua hatua ya kupatana. Wakati Petro alipojionyesha mwenyewe kuwa dhaifu na akamkana Kristo, ni nani aliyechukua hatua ya kwanza ya kufanya mapatano? Alikuwa Kristo, lo! namna alivyoichukua kwa upole vile vile! (Yohana 21:15-17) Wakati Tomaso alipokuwa na mashaka, Kristo hakujipendeza mwenyewe bali alimpendeza Tomaso kwa kumtokea na kuirudisha imani yake, iliyomrudisha Tomaso katika hali yenye amani na Kristo. (Yohana 20:24-29) Lo! mfano bora ambao Kristo alituwekea sote! Huu ulikuwa upendo kwa matendo.​—Luka 22:24-27.

17. Ni mara ngapi imempasa mtu aendelee kuitengeneza hali ya amani?

17 Ni mara ngapi imempasa mtu ajaribu kuimarisha hali ya amani pamoja na ndugu yake? Paulo anajibu hivi: “Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote.” (Rum. 12:18) Tena anasema: “Tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho.” (Gal. 6:9, 10) Walakini, ndugu yetu akikataa kukubali upendo na kujitahidi kwetu sana tufanye amani, hapo ni juu yake.

AMANI NA YEHOVA NDILO KUSUDI LETU

18. Ni nini ulio msingi wa kuweka juu yake hali zenye amani pamoja na wengine?

18 Tamaa yetu ya kuwa na amani na Yehova imepaswa iwe ndilo kusudi letu la kuanza kuimarisha amani kati ya sisi kwa sisi. Bila kuwa na msingi wenye amani na Yehova wa kuanzia, je! jitihada zetu zitatimiza nini? Hakuna. Hivyo tukiona kwamba tuna shida ya kupatana na wengine, tukiona kwamba sikuzote tuna mashauri na mtu huyu au mtu huyu, tukiona kwamba maisha yetu yanazuiwa na matata kidogo na vizuizi kwa sababu ya kutosema, basi ujamaa wetu na Yehova ndio wa kutafuta ili kupata mapatano. Huenda boriti yenye kuleta kosa ikawa katika jicho letu wenyewe, na kibanzi katika jicho la ndugu yetu.​—Mt. 7:1-5.

19. Imetupasa sote tukumbuke nini, na mtume anakaziaje jambo hili?

19 Sisi sote mmoja mmoja tunazo tabia zenye makosa. Lakini bila kujali tofauti na tabia zetu tumempenda Yehova na haki yake, na hilo ndilo jambo kubwa! Paulo aliandika hivi: “Mkichukuliana, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama [Yehova] alivyowasamehe ninyi, vivyo na ninyi. Na amani ya Kristo iamue mioyoni mwenu; ndiyo mliyoitiwa katika mwili mmoja.” (Kol. 3:13, 15) Hapa Paulo alikubali kwamba zingekuwako sababu za kulaumiana. Lakini kuliko wanadamu wote, sisi tumepatanishwa na Mungu. Yeye ametusamehe. Kwa kujiweka wakf na kubatizwa kwetu, tulipokea dhamiri njema na mwanzo wenye amani kutoka kwa Yehova. Ikiwa Mungu mwenye haki anaweza kuwa tayari hivyo kusamehe na kusahau, sababu gani sisi tusisameheane sisi kwa sisi?

20. Ni nini lililo jawabu la kuwa na hali zenye amani na ndugu zetu?

20 Jawabu ni amani na Yehova ambayo tunajifurahisha kupitia kwa Kristo, ikitupa uwezo juu ya maelekeo yetu ili na sisi vile vile tuweze kusamehe na kusahau. Ndipo hatuwi na kumbukumbu lenye uchungu katika moyo wetu linalotokeza uadui kwa ndugu ambaye tunafikiri alikosea. Ikiwa tunailinda amani yetu na Mungu iwe bila kuharibiwa, basi hatutajiachilia wenyewe tukasirike. Wala hatutalipa kwa mabaya wala kwa kimya kuweka kizuizi akilini mwetu kati yetu wenyewe na ndugu yetu.

KWA UNYENYEKEVU EPUKA KUHUKUMU MAKUSUDI YA WENGINE

21. Kwa sababu gani unyenyekevu ni wa maana sana wakati tunapofuatia mambo yaletayo amani?

21 Kwa kawaida ni katika mambo madogo kwamba matata yanatokea na kuwa makubwa. Kuonyesha mfano: Je! wewe umepata kudhani kwamba maoni yako juu ya kushughulika na jambo fulani ndiyo yaliyokuwa bora kuliko ya mwenzio na ukakasirika katika kujitahidi kwako kuthibitisha jambo? Kwa sababu gani ulishikilia sana maoni yako mwenyewe hata amani ikaanza kuhatirishwa? Biblia inasema kwamba haitupasi tujifikirie makuu zaidi kuliko inavyotupasa kufikiri, ‘bali kuwa na nia ya kiasi.’ (Rum. 12:3) Ikiwa sisi tunataka kazi ya Yehova ifanywe, basi kumbuka kwamba kwa kawaida kuna njia nyingi zinazokubalika kufanyia kazi inayopewa. Ili kazi ya kitheokrasi ifanywe inategemea zaidi roho yenye amani ya wale wanaofanya kazi kuliko kutegemea kufaa kwa mipango.

22. Huenda tukayahukumuje makusudi ya wengine, na kwa sababu gani hii ni hatari?

22 Huenda tukawa na maelekeo ya kuwa na mashaka kama makusudi ya watu ni mazuri kwa sababu tu hawaitikii katika njia tulivyofikiri imewapasa waitikie. Kwa mfano, labda mtu fulani hakutusalimu kwenye Jumba la Ufalme wakati tulipofikiri imempasa atusalimu. Sisi tukamsalimu, lakini hakuitikia. Je! tunaanza kulifikiria sana jambo hilo na kujiona kuumizwa kidogo na kuanza kuwa na maoni mengine, tukiwaza kwamba ana kinyongo na sisi au hatupendi? Je! sasa tunaacha kizuizi cha kutosema naye na uadui vianze kuendelea? Mtu asipoangalia makusudi yake, anakuwa na maelekeo ya kuhukumu, na bila kufahamu anatufanya tuutilie mashaka Ukristo wa ndugu yetu. Huko kungekuwa ni kuhukumu kusudi lake kama lenye kutiliwa mashaka. Ni kweli kwamba matendo ya ndugu yako ni yenye makosa, lakini je! wewe ungetaka makusudi yako yahukumiwe na matendo yako yenye makosa? Basi onyo li wazi: Kuliko kumlaumu ndugu yako, jaribu kumsamehe. Kwa njia hiyo unaepuka kusitawisha roho yenye kulaumu ndani yako mwenyewe.​—Mt. 7:1, 2.

FUATIA AMANI KWA KUENDELEZA MAONI YA YEHOVA JUU YA UZIMA

23. Kwa sababu gani ni jambo la maana kutii shauri lililo katika Waebrania 13:17 katika kufuatia amani?

23 Inatupasa tutii shauri lililo katika Waebrania 13:17 katika kufuatia amani na kuwatii na kuwanyenyekea wazee waliomo katika kundi. Huenda tumemjua mzee kwa miaka mingi, na huenda tumeyaona makosa yake yote na tabia-tabia alizo nazo. Lakini ijapokuwa makosa yake yote Yehova ameona inafaa amweke katika cheo. Sasa je! sisi tutashindana na hukumu ya Yehova? Je! tutaliharibu tengenezo lake kwa kuwa na roho yenye kulaumu? Si afadhali kujibidiisha na kushirikiana, na kufurahi kwa vile Yehova amefanya mpango huu.

24. Kwa sababu gani ni jambo la haraka kufanya sasa ambayo 2 Wakorintho 13:11 inayotuambia?

24 Ugomvi hautaruhusiwa uharibu amani katika taratibu mpya, na kwa sababu gani tuuache uiharibu sasa? Je! 2 Wakorintho 13:11, NW inasema nini? “Ndugu, endeleeni kufurahi [sasa], kutengenezwa upya [sasa], kufarijiwa [sasa], kufikiri kwa umoja [sasa], kuishi kwa amani [sasa]; na Mungu wa upendo na wa amani atakuwa pamoja na ninyi.” Kwa kufuata shauri hili jema sasa ibada yetu itakuwa safi na yenye kukubalika mbele za Mungu.

25. Ni maoni gani ya Yehova yatakayotusaidia tuwe na amani pamoja na ndugu zetu?

25 Ili kutusaidia tuendeleze maoni ya Yehova juu ya uzima, Waefeso 4:32 inasema hivi: “Tena iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkasameheane kama na Mungu katika Kristo alivyowasamehe ninyi.” Unawezaje kuwa na kinyongo juu ya ndugu ambaye Yehova ameonyesha upendo? Katika matata fulani, kumbuka kuna pande mbili na makosa yako yanasaidia kuleta matata. Ili kamba ipate kukazika ni lazima kuivuta pande zote mbili. Ndugu yako anataka uzima kama wewe unavyotaka. Unahitaji msaada wake kama yeye anavyotaka msaada wako.

26. Ni mambo gani ambayo imetupasa tuyakumbuke na kuyatumia ili tuwe na amani pamoja na Mungu wetu na sisi kwa sisi?

26 Yakumbuke mambo makubwa wakati yanapotokea matata juu ya mambo madogo. Jiulize mwenyewe hivi, ‘Ni kwa sababu gani sisi tu wahudumu wa Yehova? Tunaongozwa wapi? Ni nini kusudi letu katika maisha?’ Sikuzote yaweke mambo haya ya maana sana mbele yako. Ujue kwamba Yehova awapenda watu wake; wote ni wenye bei kwake. Ifanye njia ya ndugu yako iwe nyepesi, kama vile wewe ungemtaka yeye aifanye njia yako iwe nyepesi. Ili upate zawadi ya uzima wa milele ni lazima uwe na amani na Chanzo cha uzima, Yehova. Lakini utapata amani hiyo ikiwa una amani na ndugu yako tu. Basi, katika mambo yote ifuatie amani, kwa utukufu wa Yehova na furaha yako ya milele.

[Picha katika ukurasa wa 539]

Unapojiona mwenyewe unaelekea kuwa katika jambo linaloelekea kuwa ugomvi, je! unachochea hasira? Au unafuatia amani kwa kuzuia hasira zako?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki