Mshuhudiaji Ndani Yetu
“Dhamiri yangu inashuhudia pamoja na mimi katika roho takatifu.”—Rum. 9:1, NW.
1, 2. (a) Kwa sababu gani imetupasa tupendezwe sana katika kujifunza juu ya mshuhudiaji ndani yetu? (b) Mshuhudiaji huyu ni nini, na anashirikiana na nini?
SISI sote tunaye mshuhudiaji ndani yetu. Anaweza kutusaidia sana katika kufanya maamuzi yanayopasa sana furaha yetu ya kisasa na ya wakati ujao. Kwa hakika, mshuhudiaji huyu anatoa ushahidi katika majaribu yanayotia uhai wetu wenyewe. Na maisha zetu na za wengine zinavutwa kwa lazima kwa namna tunavyoitikia sauti yake. Hii inafanya liwe jambo la hatari zaidi kwa kuwa anaweza kuwa shahidi aliyepotoka. Anaweza kutoa ushahidi wenye kupoteza au hata kushindwa kabisa kupaza sauti katika nyakati za hatari.
2 Mshuhudiaji huyu ni nini? Ni dhamiri yetu. (2 Kor. 1:12) Ni sauti ambayo waandikaji wa Biblia wanataja kama “nafsi ya siri,” “utu wa ndani,” “mtu wa siri wa moyoni.” (Zab. 51:6, NW; 2 Kor. 4:16; 1 Pet. 3:4, NW; linganisha Warumi 7:22.) Je! wewe umepata kutumia usemi kama huu, “Niliona moyoni mwangu ilifaa kufanya”? Au, “Mimi ningependa kufanya unalotaka lakini kitu fulani ndani yangu kinasema ‘Hapana’ “? Hii ni dhamiri inayosema, ufahamu wetu wa ndani au akili ya chema na kibaya.
3, 4. Dhamiri yetu “inashuhudia” namna gani? Na inaweza je kutuongoza kwa adili?
3 Ni “mshuhudiaji” namna gani? Kwa vile inashuhudia kwa kupinga au kwa kukubali mwenendo wetu kama ukipatana na kanuni za adili, ama kutushtaki ama kutuondoa katika shtaka. Inaweza kuwa jambo la adili lenye usalama kwa sababu inaweza kuumiza wakati inapolaumu, au kuleta furaha inapokubali.
4 Kwa mfano, Daudi alipokwisha kufanya tendo lisilo la heshima kwa Mfalme Sauli, habari inasema kwamba “moyo wake Daudi ukamchoma.” (1 Sam. 24:5; linganisha 2 Samweli 24:10.) Dhamiri yake ilimlaumu. Wakati tendo jingine baya sana lilipofuata, Daudi alipata maumivu makali ya dhamiri yenye hatia. Kama anavyosimulia mwenyewe: “Niliponyamaza mifupa yangu ilichakaa kwa kuugua kwangu mchana kutwa. Kwa maana mchana na usiku mkono [wa Mungu] ulinilemea. Jasho langu likakauka hata nikawa kama nchi kavu wakati wa kaskazi.” Lakini mwisho alipoungama kosa lake kwa Mungu na akapata msamaha Wake, Daudi aliona kutulizwa na furaha. Dhamiri yake ilitulizwa, ikafanywa safi tena.—Zab. 32:1-5; linganisha mistari ya 10, 11.
HEKIMA YA MUNGU INAONWA KATIKA DHAMIRI YA KIBINADAMU
5-8. (a) Kwa sababu gani haikuwa lazima Mungu awape wanadamu wa kwanza taratibu yenye sheria nyingi mno? (b) Hata wakati hali mpya zingetokea, wangewezaje kuamua mwendo ambao ungekuwa mzuri kuchukua? (c) Toa mifano juu ya namna uwezo wa dhamiri ungetenda ndani yao.
5 Katika mwanzo wa historia ya wanadamu, Yehova Mungu hakuwapa wanadamu wa kwanza kanuni nyingi mno za kuongoza kila jambo dogodogo na kila sehemu ya maisha. Maagizo yake ya jumla na amri moja ya kukataza aliyowapa yanaweza kusimuliwa kwa maneno machache katika Biblia. (Mwa. 1:28-30; 2:15-17) Sababu gani taratibu ya sheria nyingi mno haikuwa ya lazima?
6 Yehova Mungu aliviumba viumbe vyake vya kibinadamu vikiwa na akili na mioyo yenye akili ya adili. Kwa kushirikiana kwa akili na moyo uwezo wa dhamiri unatokea. Chanzo cha dhamiri ya mwanadamu kiko katika uhakika wa kwamba mwanadamu alifanywa katika ‘mfano na sura’ ya Mungu mwenyewe, kwa wazi, si katika maana ya kimwili, bali katika adili. (Mwa. 1:26, 27; linganisha 2 Wakorintho 3:18.) Hivyo, ndivyo uwezo wa dhamiri ulivyotiwa katika wanadamu tangu wakati wa kuumba na kuendelea.
7 Mahali pa kutoa sheria zenye kutoa maana na kueleza kila jambo dogodogo la chema na kibaya, Mungu aliweza kutia nguvu akili ya mwanadamu ya adili kwa kufunua utu Wake, njia na kanuni kwa mwanadamu. Kwa njia hiyo Mungu alitoa kanuni za kuongoza watoto wake wa kibinadamu. Wakati ambapo wangeendelea kupata ujuzi, ufahamu wake, dhamiri au akili yao ya adili ingewawezesha kutumia kanuni hizi kwa hali yo yote ambayo ingetukia.
8 Kwa mfano, haikuwa lazima kwa Mungu kumpa Adamu sheria maalum kumwambia asimpige mke wake au kumtupia mawe, au kukataza kuua wanyama na ndege kwa mchezo tu. Kwa sababu, kuzunguka wanadamu wawili wangeweza kuuona ushuhuda wa upendo wa Muumba wao, ukarimu wake, kufikiria na fadhili zake. Wangeweza kuuona katika miili ya ajabu, yenye nguvu ambayo aliwapa, uzuri na namna nyingi za mazingira yao, mambo ya kupendeza ambayo alikuwa ametoa kwa milango yao yote ya maarifa—kunusa, kuonja, kugusa, kuona na kusikia. (Zab. 139:14; 104:10-24; Mhu. 3:11) Namna hili linavyopaswa kuvuta kwa nguvu zaidi mioyo ya kibinadamu kwenye haki na wema kuliko sheria ya vivi hivi! Upendo wa Mungu kwao uliweka mfano kwa kutendeana kwa wanadamu wawili. Uliweka msingi kwa dhamiri yao kupaza sauti kupinga ukatili au kukosa kufikiria kwa namna yo yote.
DHAMBI INAINGIZA VITA VYA NDANI
9. Kutokutii kungekuwa na matokeo gani juu ya mwanadamu mkamilifu, na kwa sababu gani?
9 Kwa kuwa aliumbwa katika sura ya Mungu, kwa Adamu kuonyesha sifa za Baba yake, kuonyesha namna Muumba wake alivyo kwa mwenendo mzuri, lingekuwa jambo la kawaida, la asili kwa Adamu kufanya. Hata hivyo yeye alikuwa na uhuru wa kuchagua, kujifanyia mwenyewe uchaguzi. Ikiwa angepewa nafasi ya kuchagua kati ya kutenda kupatana na utu na njia za Mungu au kutenda kwa kukosana nazo, Adamu angeweza kuchukua mwendo mmojawapo wa hiyo. Lakini ila kwa kuchagua mwendo unaopatana ndipo mwanadamu angeweza kujiona ana haki juu ya jambo hili. Kuchukua mwendo ulio tofauti ingekuwa kutenda vingine, kutokeza usumbufu wa ndani katika mwanadamu.
10. Habari katika Mwanzo 3:6-11 inaonyesha namna gani kwamba Adamu alikuwa na mshuhudiaji ndani yake?
10 Maandishi ya historia yanashuhudia hili. Wakati Adamu na mke wake walipovunja amri moja ya kukataza ambayo Mungu aliwapa, walipata matata ya ndani. Walianza kujiona wenye hatia, mashaka, haya na kukosa usalama. Wakati Muumba wake aliposema naye, Adamu alikubali kwamba alijaribu kujificha, kwa sababu ya woga. Ilikuwa kana kwamba kitu fulani cha kuchunguzia uongo kilichotiwa ndani kilikuwa kikifanya kazi ndani yake, ili kutoa sababu ya haki kwa Mungu kuuliza hivi mara hiyo: “Je! umekula wewe matunda ya mti niliyokuagiza usiyale?” Kwa kweli, mshuhudiaji ndani ya mwanadamu alikuwa akishuhudia neno ilo hilo.—Mwa. 3:6-11.
11, 12. Ni nguvu gani nyingine ambayo sasa ikawa sehemu ya ubinadamu, na ina matokeo gani juu ya adili na dhamiri ya mwanadamu?
11 Kutoka hapo na kuendelea mwanadamu amekuwa na nguvu mbili zenye kupingana ndani yake mwenyewe. Ijapokuwa aliumbwa katika mfano wa Mungu, sasa akawa mwenye dhambi, asiyekamilika. Dhambi iliharibu wonyesho wa wanadamu wa “sura” ya Muumba wao, ilifanyiza kosa lililorithiwa na watoto wote wa Adamu, bila hata wa kuweza kujiokoa wenyewe nayo kwa jitihada zao wenyewe. Maelekeo ya kutenda mabaya sasa yakawa sehemu ya ubinadamu. Lakini je! ilifutilia mbali au kuondoa ile akili ya ndani ya chema na kibaya inayoitwa dhamiri? Hapana, hii iliendelea vile vile kama sehemu ya ubinadamu. Hivyo—zaidi wakati wanapopatwa na maulizo yanayopasa mema na mabaya na maamuzi—wanadamu wanapatwa na vita vya ndani kwa sababu ya nguvu hizi zenye kupingana ndani yao.
12 Lakini dhambi ikiwa inatenda ndani yao, je! dhamiri ya kibinadamu ingeweza bado kutenda kwa kufaa bila taratibu yenye sheria nyingi za kuiongoza? Ndiyo, kama maandishi ya historia yanavyoonyesha.
DHAMIRI INAENDELEA KUTENDA BILA TARATIBU YA SHERIA
13, 14. Hata dhambi ikiwapo, jambo gani linaonyesha kwamba dhamiri ya kibinadamu ingeweza kutenda sawasawa bila taratibu ya sheria?
13 Mpaka Gharika ilipokwisha ndio wakati tunapoona sheria iliyosemwa juu ya uuaji. (Mwa. 9:5, 6) Hivyo, basi, je! watu waliokuwa mbele ya wakati huo walijiona huru kuua bila kujiona kuwa na hatia? Hata kidogo.
14 Katika Edeni, mauti ya wanadamu ilifunuliwa na Mungu kuwa ndiyo adhabu ya wenye kuvunja mapenzi yake. (Mwa. 2:16, 17) Basi, kwa akili, mauti inatokea kama adhabu ya dhambi, na Mungu, kama Mpaji wa Uzima anayejulikana, ndiye mwenye kuonyesha wale wanaostahili mauti. Basi, jambo gani lilitukia wakati Kaini aliporuhusu dhambi imwongoze katika kumwua ndugu yake katika hasira kali? Hakuna sheria iliyosemwa iliyolaumu uuaji; hata hivyo dhamiri ya Kaini ilishuhudia kwa kumpinga, kama inavyoonwa kwa kuepa kwake wakati alipokuwa akiulizwa na Mungu. (Mwa. 4:3-9) Mwisho, kwa wazi dhamiri ya Lameki mzao wa Kaini ilimwondolea hatia ya kumwua kijana aliyemwumiza. Lameki alijitetea, kwa wazi akijidai kutoweza kuuawa na mlipiza kisasi ye yote wa mauti ya mtu huyo. Kwa sababu gani? Kwa sababu alijua juu ya ahadi ya Mungu ya kumchukulia hatua mtu ye yote anayejaribu kulipiza kisasi katika shauri la Kaini na akajiona kwamba shauri lake lilikuwa la haki zaidi kuliko la Kaini. (Mwa. 4:17, 18, 23, 24) Hivyo, wanadamu hawakuwa bila kanuni na masharti ya kuziongoza dhamiri zao.
15. Dhamiri za watu zingewezaje kushuhudia juu ya kuasi ukichwa, juu ya uvivu, ufisadi na makosa yanayofanana, kwa historia peke yake ya Mwanzo 1:26 mpaka 4:16 kama msingi?
15 Watu waliijua kanuni ya ukichwa, kwa maana Mungu alikuwa amejulisha ukichwa wake katika Edeni na alikuwa amemweka mwanamume kuwa kichwa cha mwanamke. Bila sheria zinazolaumu uvivu, walijua kwamba imempasa mwanamume afanye kazi katika kuangalia mipango ya Mungu ya kidunia. Hii, vile vile, ilifunuliwa katika Edeni. Wakati agano la Torati pamoja na Israeli halijalaumu waziwazi tendo la kulalana wanaume kwa wanaume na wanawake kwa wanawake, uzinzi na kulala wanawake kwa nguvu, walijua kwamba ngono zilipaswa zifanywe kati ya mwanamume na mwanamke na kwamba ngono hizo hazikupaswa ziwe za muda (kama katika uasherati au uzinzi) bali zenye kuendelea, katika kifungo cha jamaa na wale walioungana ‘wakimwacha baba na mama’ ili waingie katika kifungo hicho chenye kuendelea, kama “mwili mmoja.” (Mwa. 2:24; angalia tena mwendo wa Yusufu; Mwa. 39:7-9) Bila sheria zo zote juu ya kukosa au kuiba, waliweza kufahamu kanuni ya haki za uenyeji, kulingana na amri ya Mungu juu ya miti katika Edeni. Bila sheria juu ya kudanganya, kupunja, kuchongea, shtaka la uongo, waliweza kuona matokeo mabaya yaliyotokana na uongo wa kwanza.—Mwa. 1:26–4:16.
16. Je! hali tofauti au mpya zingegeuza hili?
16 Basi, hata ikiwa taratibu ya sheria haikupewa ikiwa na amri na kanuni zilizo waziwazi, watu walikuwa na kanuni na masharti ya kuwaongoza na kuzitayarisha dhamiri zao kutenda kama washuhudiaji wa kweli. Huenda hali zilikuwa tofauti kwa mtu huyu na mtu huyu, labda hali mbalimbali zilitokea, hata hivyo waliweza kutumia kanuni hizo ili wafikie maamuzi ya kweli, kufanya maamuzi ya hekima. Katika karne zilizofuata, na hata wakati agano la Torati halijapewa kwa Israeli, kushughulika kwa Mungu na wanadamu na maneno yake yalitoa ufunuo zaidi kwa wale ambao bado walikuwa wakijitahidi kuonyesha sura yake.
17. Onyesha namna Yesu na mitume wake walivyoonyesha ubora wa kanuni na masharti haya kama uongozi wa haki.
17 Katika karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida, Yesu na mitume wake walitumia kanuni hizo na masharti hayo ya kwanza katika kutegemeza maoni ya haki yanayopaswa kuchukuliwa juu ya mambo kama talaka, mateso na uchongezi, unyenyekevu wa mke kwa mume, kuua mtu.—Mt. 19:3-9; Yohana 8:43-47; 1 Tim. 2:11-14; 1 Yohana 3:11, 12.
18. (a) Ni watu wa namna gani wanaofanya sheria maalum, za waziwazi zihitajiwe kama ogofyo? (b) Tofautisha hawa na mtu anayeipenda haki kweli kweli.
18 Yote haya yanatusaidia tufahamu kufaa kwa usemi wa mtume Paulo kwamba “sheria haimhusu mtu wa haki, bali waasi, na wasio wataratibu, na makafiri, na wenye dhambi, na wanajisi, na wasiomcha Mungu, na [wauaji wa baba na wauaji wa] mama zao, na wauaji, na wazinifu, na wafiraji, na waibao watu, na waongo, nao waapao kwa uongo; na likiwapo neno lo lote linginelo lisilopatana na mafundisho yenye uzima.” (1 Tim. 1:9, 10) Mtu aliye na upendo wa kweli kwa haki katika moyo wake hana haja ya sheria za waziwazi zenye kulaumu mambo hayo ili kumfanya aepukane nayo. Ikiwa kweli yeye anajitahidi kuonyesha “sura” ya Mungu na ‘kutembea na Yeye’ atayakana mazoea yote hayo. Kwa upande mwingine, ikiwa mtu ye yote hana tamaa hiyo ya haki, huenda sheria za waziwazi zenye adhabu kwa mvunjaji zikawa kama ogofyo—lakini hazitaweza kuzuia kabisa hata kidogo asifanye kosa. Historia ya kibinadamu inatoa ushahidi mwingi juu ya hili.
AGANO LA TORATI NA DHAMIRI YA KIKRISTO
19. Agano la Torati lililopewa kwa Israeli lilitumikia makusudi gani mengi?
19 Mwisho Yehova Mungu alitoa taratibu kamili ya sheria na maagizo kwa taifa la Israeli. Ijapokuwa hii ilitumika kama ogofyo kwa kutenda mabaya na vile vile kutoa busara bora ya kanuni za Mungu na sifa, Yehova alikuwa na kusudi kubwa zaidi, lenye mfiko wa mbali sana katika kutoa taratibu hii ya sheria. Mungu aliitoa kwa Israeli “ili kufunua makosa,” ili wao, wajapokuwa watu wake wateule, wasiweze kujidai haki juu ya msingi wa wema na kazi zao wenyewe. Kutoweza kushika sheria hiyo kwa ukamilifu kulifunua sana hali yao yenye dhambi na kwa nguvu kukaonyesha uhitaji wao wa mpango wa ukombozi ambao Mungu angefanya kupitia kwa Kristo Yesu. Wakati uo huo, agano la Torati lilikuwa na ‘vivuli’ au mifano ndani yake ya makusudi ya Mungu ya wakati ujao na njia ya kuyatimiza haya.—Gal. 3:19, NW; Rum. 3:19, 20, 24.
20. (a) Agano jipya linatofautiana namna gani na agano la Torati? (b) Sababu gani kutokuwapo kwa taratibu yenye sheria nyingi mno hakuruhusu kanuni za chini zaidi kati ya Wakristo?
20 Walakini, hata wakati Torati hiyo ilipokuwa ingali ikitumika, Yehova alitabiri juu ya kufanya kwake agano jipya pamoja na watu ambao wangewekewa sheria yake “ndani yao,” si kupitia kwa taratibu fulani ya sheria iliyochorwa au kuchapwa, bali ‘iliyoandikwa katika mioyo yao.’ (Yer. 31:33) Agano hilo jipya lilifanywa na Israeli wa kiroho, kundi la Kikristo. Hawakuwa chini ya Torati iliyopewa kwa Israeli. (Gal. 4:4, 5; Ebr. 8:7-13) Je! kutokuwapo huku kwa taratibu hiyo ya sheria nyingi mno kunaruhusu kanuni ya chini zaidi ya adili kati ya Wakristo? Sivyo, Ukristo unataka kanuni ambazo ni za juu hata zaidi, kama mafundisho ya Yesu mwenyewe yalivyoonyesha. (Mt. 5:21, 22, 27, 28, 31-48) Na kwa wazi unataka mazoezi makubwa zaidi ya dhamiri. Kama Wakristo tunajaribiwa juu ya kama ‘tumeandikwa njia za Mungu katika mioyo yetu’ au sivyo. Kutokuwekwa kwetu chini ya taratibu ya sheria nyingi mno kunatujaribu juu ya mambo ambayo kweli yamo katika mioyo yetu.
21. Kama Wakristo, ni ujuzi gani ambao umepaswa uwe msingi kwa ushahidi ambao dhamiri yetu inatupa sisi? Je! ni lazima maandiko yawe kwa namna ya amri, katazo au sheria ya waziwazi ili kufanyiza matokeo mazuri juu ya dhamiri yetu?
21 Bila shaka, kama Wakristo tunayo Maandiko ya Kiebrania na ya Kigiriki yanayotupa sisi busara bora juu ya utu wa Mungu, njia na kanuni, makusudi na mapenzi yake. Ndani yao tuna maandishi ya maneno na matendo ya Mwana wa Mungu aliyekuja duniani ‘akamfunua’ au akamweleza Baba yake kwa wanadamu, ili tuweze ‘kumjua Baba’ kabisa kupitia kwa yeye. (Yohana 1:18; Mt. 11:27) Hivyo, basi, hata ijapokuwa huenda sheria na amri za waziwazi zinazopewa kwetu kama Wakristo zikawa chache zikilinganishwa na agano la Torati na mamia yake ya amri na sheria, sisi tunavyo vifaa bora vya kutusaidia kujua namna ya kutenda katika ‘sura na mfano wa Mungu.’ Kwa kweli, sisi tuna daraka kwa YOTE tunayojua juu ya Mungu, na ujuzi huo WOTE unafaa kuwa na matokeo yake katika dhamiri yetu, kwamba inasemwa kama amri, sheria au katazo kwa Wakristo au sivyo.
JE! KANUNI ZIWE MAHALI PA KILA DHAMIRI?
22. Wengine wangependa baraza inayoongoza ya kundi la Kikristo ifanye nini, na kwa sababu gani hili halipatani?
22 Lakini watu wengi hawaridhiki na hili. Wangali wanataka kufanyiwa kanuni za waziwazi, mipaka ya kufika, kuliko yaliyoandikwa katika Neno la Mungu. Basi, je! baraza inayoongoza ya kundi la Kikristo leo ichukue daraka la kutoa taratibu yenye kanuni nyingi mno ili kueleza kila hali inayowazika? Hapana, kwa maana huku kungekuwa kufuata maoni yenye makosa, maoni yanayofanana na yale yaliyokuwamo kati ya Wayahudi wakati wa huduma ya Yesu ya kidunia, yajapokuwa hayana mwanzo wala mwisho wakati huo.
23, 24. Nani vile vile waliopendezwa sana na kanuni za waziwazi? Toa mfano.
23 Walikuwa Mafarisayo na viongozi wengine wa kidini waliozoea maoni hayo. Waliweka taratibu ya nyongeza yenye mapokeo na kanuni juu ya agano la Torati, wakijaribu kueleza kila sehemu dogodogo ya matumizi ya agano la Torati. Kila katazo lililokuwa katika Torati liligawanywa katika njia hiyo katika makatazo mengi mno madogo zaidi.
24 Kwa mfano, sheria ya sabato ilikataza kufanya kazi siku ya saba. Lakini mna nini katika “kazi”? Viongozi hawa wa kidini walijaribu kufafanua mno yaliyokuwamo katika “kazi” hiyo. Kuvunja masuke ya ngano ya kula (kama mitume walivyofanya siku ya sabato) kuliamriwa kuwa namna ya kuvuna, kwa hiyo ni “kazi” iliyokatazwa kufanywa siku ya sabato. (Marko 2:23, 24) Mapokeo fulani yaliamuru kwamba hata kukamata kiroboto katika siku ya sabato lilikuwa kosa kwa sababu ilikuwa namna ya uwindaji. Kanuni zilikuwa nyingi mno. Kanuni moja ilisema kwamba ‘ikiwa mtu alipasua mavazi au akachoma vitu kwa moto akiwa na kusudi la kuviharibu, hakuwa na hatia ya kuvunja sabato. Lakini ikiwa yeye aliviharibu kwa kusudi la kufanya matengenezo mwishowe (kama vile kubomoa nyumba ili kuijenga upya) alipaswa apate adhabu.’—The Jewish Encyclopedia, 1909, Vol. X, ukur. 599; linganisha Mathayo 15:4-6; 23:16-19.
25. (a) Lilikuwa jambo gani lenye hatari juu ya kuweka taratibu hiyo yenye sheria nyingi na ngumu? (b) Yesu alisema nini juu ya mwendo huu?
25 Yalikuwa matokeo gani yenye hatari, yenye kuharibu ya kujaribu kufafanua mno matumizi ya kila sheria? Cyclopædia M’Clintock na Strong inakubali hatari kubwa iliyotolewa na mwendo huu wa viongozi wa kidini, ikisema kwamba “walitafuta kushika sana sheria, na kutokujali sana uamuzi na dhamiri ya watu.” (Vol. IX, ukur. 191) Kwa kweli, jambo ambalo viongozi wa kidini walifanya lilikuwa ni kuwatwika watu wote wengine dhamiri yao wenyewe, mambo madogomadogo ya uangalifu sana na ambayo mtu bi nafsi anapendelea na maamuzi yao wenyewe yasiyo na sababu nzuri. Yesu alifananisha kuongeza huku kwa mapokeo kwenye sheria ya Musa na “mizigo mizito” mabegani mwa watu na akaonya kwamba kuweka huku kwa mapokeo ya wanadamu juu ya Maandiko kulitokeza kulifanya Neno la Mungu lisiwe na maana. (Mt. 15:1-9; 23:1-4) Yesu aliwaambia viongozi wa kidini waliolaumu wanafunzi wake kwa kuvunja masuke ya ngano siku ya sabato, akisema: “Kama mngalijua maana yake maneno haya, Nataka rehema, wala si sadaka, msingaliwalaumu wasio na hatia.”—Mt. 12:1-7.
26. Ni mfano gani unaoonyesha namna kanuni zenye mapokeo zilivyowazuia Wayahudi kutumia dhamiri zao sawasawa? Na ilikuwa na matokeo gani juu ya mioyo yao?
26 Wakati mwingine, katika sinagogi, Yesu aliacha dhamiri zao ziamue juu ya kutumia sheria ya Mungu. Agano la Torati halikusema juu ya jitihada zinazofanywa ili kuwaangalia wagonjwa siku ya sabato, lakini mapokeo ya Kiyahudi yaliruhusu kufanya hivi wakati uhai wa mtu ungekuwa hatarini tu. Akikutana na mtu aliyekuwa na mkono wenye kupooza na akiulizwa na viongozi wa kidini kama ilikuwa ‘halali kuponya siku ya sabato’ au haikuwa halali, Yesu aliuliza hivi, ‘Ni mtu gani kati yenu ninyi mwenye kondoo mmoja ambaye asingemwinua kutoka katika shimo ikiwa angetumbukia humo siku ya sabato?’ Kwa kweli, namna mtu alivyo bora zaidi sana kuliko kondoo! Je! ni halali kufanya tendo jema, tendo bora, siku ya sabato?! Lakini walikataa kutumia dhamiri zao; wakanyamaza. Ndipo Yesu alipokasirika sana, “akiona huzuni kwa ajili ya ugumu wa mioyo yao,” naye akaendelea kumponya mtu yule.—Mt. 12:9-13; Marko 3:1-5.
27. (a) Kwa sababu gani ni kosa kutaka mtu mwingine kutufanyia maamuzi ya kipekee katika mambo ya adili? (b) Ni maulizo gani yanayotokea sasa, yatakayojibiwa katika makala ifuatayo?
27 Basi, kutaka mtu fulani, mzee au baraza ya wazee katika kundi, au baraza inayoongoza ya kundi la Kikristo itunge taratibu ya sheria kuliko zile zilizomo katika Biblia, kunaonyesha maoni yenye makosa. Katika mambo ambayo Neno la Mungu linatutaka tutumie uwezo wa dhamiri—wa uamuzi, akili, busara na hekima—haitupasi tumwekee mwingine daraka kwa kumtaka atunge ‘kanuni.’ Tunaweza kwa hekima kutafuta shauri na uongozi—hata hivyo linalosemwa haliwezi kupita hilo wala haitupasi kutaka iwe hivyo. Lakini tunawezaje kuwa na uhakikisho kwamba “mshuhudiaji” huyu ndani yetu anatoa ushahidi wa kweli? Tunawezaje kuifanya sauti yake kuwa yenye nguvu na waziwazi? Soma makala ifuatayo kwa majibu ya maulizo haya.
[Picha katika ukurasa wa 124]
DHAMIRI inatokana na ushirikiano wa akili na moyo ukiwa na uwezo wa adili