Je! Wewe Unapata Furaha Unayotaka?
NI MAMBO gani yanayowafanya watu wasiwe wenye furaha? Jambo la kawaida sana ni kutoweza kufikia miradi fulani. Mara nyingi kuna maoni ya kushindwa, matokeo yake yakiwa ni kuvunjika moyo. Labda umepata kuona hivyo. Huenda utakubali kwamba, ili kuwa mwenye furaha kabisa, ni lazima uwe na kusudi katika maisha.
Lakini, maoni matupu ya kusudi lako hayataleta ufanisi. Wala haliwezi kufanikiwa likifanywa kwa njia ovyo ovyo. Unataka busara, yaani, uongozi kutoka kwa chanzo cha kutegemewa. Kila mahali karibu nasi tunaona matokeo ya kufuata hekima ya kibinadamu: mchafuko, kukata tamaa na jeuri isiyozuilika. Kwa kweli, uongozi wa kimungu ndilo jawabu la pekee. Soma namna hali yenyewe inavyoelezwa kwa usahihi katika Biblia katika Mithali sura ya 29, mstari wa 18.
Biblia inatuambia kwamba maneno yake ni maneno ya Mungu, na kusema: “Maagizo ya [Yehova] ni ya adili, huufurahisha moyo. Amri ya [Yehova] ni safi, huyatia macho nuru.” (Zab. 19:8) Lakini, watu wengine wanakuwa na maoni yasiyo na msingi juu ya Biblia kwa sababu ya unafiki wa kidini. Lakini wanafiki hawafuati Biblia. Ukifuata kanuni za Biblia, utaona kwamba zinafaa. Kwa kuwa zinapozoewa zinasaidia.
KUKOSA FURAHA KWA SABABU YA KUTOJALI KANUNI ZA BIBLIA
Katika ulimwengu ambao umekosa furaha sana, inaelekea unajua wengine wa rafiki zako ambao maisha yao ya jamaa si ya furaha. Bila shaka umeona kwamba choyo, kutopatana na kutojali ndizo zimekuwa sababu. Unaona katika jamaa kama hizo watoto wasiozuiwa, waliovunjika moyo, walioudhika ambao hawakupata upendo na uongozi wanaoutaka sana.
Leo maelekeo ni kufanya jamaa kuwa jambo lisilo la maana. Lakini katika mambo uliyoona mwenyewe, je! jamaa hazina furaha zaidi ambapo pana umoja wa jamaa, ambapo wazazi ni rafiki za kweli kwa watoto wao na wanawaongoza kuelekea njia inayofaa? Je! ni nani aliyeweka mpango huu mwema wa jamaa kama msingi wa jamii? Muumba wa mwanadamu, Mungu. Na sheria iko wapi kweli kwamba jamaa iendelee kuwa yenye nguvu? Katika Biblia.—Mwa. 10:31, 32; Kum. 6:6, 7; Efe. 3:14, 15.
Watoto wengi, waliochukizwa na kutojali kwa wazazi, wamegeukia matumizi ya dawa za kulevya na jeuri. Lakini kama wazazi wangefuata kanuni za Biblia juu ya ndoa na upendo wa wazazi, inawezekana wangeepuka misiba hiyo. Je! unafikiri inaelekea kwamba watoto wangefuata njia waliyofuata kama wazazi wangejua na kuchukua kwa uzito shauri la Biblia: “Nanyi, akina baba, msiwachokoze watoto wenu; bali waleeni katika adabu na maonyo ya [Yehova]”?—Efe. 6:4.
Tena, Biblia inasema: “Maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo.” (Luka 12:15) Leo tunaona maisha ya jamaa yakiachwa ivi hivi kwa sababu wote mume na mke wanafanya kazi, au waume wana kazi mbili. Wanachagua kuachilia ushirika wa jamaa na hali njema ya kiroho kwa sababu ya nafasi bora zaidi za maisha, mara nyingi kuwapa watoto wao zaidi ya vitu ambavyo wao walikuwa navyo.
Lakini je! mkazo huo wa fikira juu ya faida za kimwili unaleta matokeo yenye furaha? Hapana, unaelekea kuleta ufukara wa kiroho. Nyakati nyingi watoto, ingawa wanapewa masomo ya vyuo vikuu, wanaona maisha zao ni ovyo ovyo na zisizo na maana na hawaridhiki kabisa. Namna maonyo ya Biblia yangalizifaidi jamaa hizi!
NJIA YA KUFANIKIWA YA MAISHA
Ukiichukua Biblia namna inavyosema, utaona kwamba inatoa njia inayofaa ya pekee, ya busara katika njia zote za maisha. Kwa kuwa Biblia inatuambia namna sisi sote tunapaswa kuishi na kufanya kama wanadamu. Mmoja wa waandikaji wake anasema: “Yeye amekuonyesha yaliyo mema; na [Yehova] anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!” Ni jambo gani lingekuwa la busara kupita hilo? Je! kila mtu haimpasi kufanya hivyo? Na kama wakifanya hivyo, dunia haitakuwa mahali pa furaha zaidi kuishi?—Mik. 6:8.
Kama ungeulizwa ulizo, ‘Je! unajua kama unaishi kulingana na kanuni za haki, au sivyo?’ ungejibu kwa unyofu wa moyo Ndiyo? Kama sivyo, utafurahia kuchunguza Biblia na kuvumbua kanuni zake safi, za kufaidi. Ndipo unaweza kupata uradhi wa kweli na furaha unapoanza kuchunguza njia zako mwenyewe na kuona kwamba unapatana zaidi na zaidi na kanuni za Mungu. Inachukua wakati na jitihada, lakini utaona maisha yako yakiwa yenye furaha zaidi kila siku.
Katika kufanya uchunguzi kama huo wa Biblia huwezi kutegemea mambo ambayo kwa unyofu wa moyo umefuata wakati uliopita kwa desturi, mapokeo ya kidini au washauri stadi wakikusaidia. Ama sivyo, sababu gani hali ni mbaya namna hiyo leo, na sababu gani Biblia inasema: “Msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu”?—Rum. 12:2.
Mwana wa Mungu mwenyewe alijua, na alisema: “Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.” (Mt. 4:4) Mashahidi wa Yehova wameona kwamba, kwa kadiri walivyoishi kulingana na kanuni za Biblia, wamepata furaha, uhuru kutokana na kuvunjika moyo, kurudishwa kwa heshima ya kibinadamu na maoni ya utimizo—kusudi la kweli katika maisha. Wanaona kwamba maisha yao yanapatana zaidi na kusudi la Mungu ambalo Mungu alikuwa nalo alipowaumba mwanamume na mwanamke.
Hawawezi kujiwekea habari njema hizi wao wenyewe. Wana furaha kwa sababu ya waliyoona na wanajua kwamba wengine vile vile wanatafuta furaha. Mungu hapendelei. Anatoa furaha ile ile kwa ye yote anayechunguza kwa unyofu wa moyo Neno lake la kweli, Biblia.—Matendo 10:34, 35.