Fadhili Ina Nguvu
JE! SI ni furaha kuwa karibu na watu ambao ni wenye fadhili na wenye huruma? Ndiyo, fadhili ina matokeo mema juu ya wengine. Mashahidi wa Kikristo wa Yehova wameona kwamba kufuata kwao kwa onyo la Biblia la kuwa wenye fadhili kwa watu wote kumewasaidia wengi kupata ujuzi mwema wa kweli.—Rum. 12:20; Kol. 3:12.
Hayo ndiyo mambo aliyoyaona Shahidi mmoja mchanga katika Hong Kong. Kijana huyu wa kike alifurahia kucheza mpira pamoja na wenzi wake wa darasa shuleni, lakini akamwona mmojawao ambaye hakuweza kushiriki katika michezo kwa sababu ya kizuizi fulani cha kimwili. Kwa kumwonea rafiki yake huruma, yule Shahidi mchanga akaleta kitabu ambacho yule kijana wa kike mwenzake mwenye kizuizi angeweza kusoma wakati wa michezo. Kitabu chenyewe kilikuwa ni msaada wa kuelewa Biblia kinachoitwa “Kweli Iongozayo kwenye Uzima wa Milele.” Onyesho hilo lenye fadhili na la uangalifu lilimpendeza yule kijana wa kike mwenye kizuizi. Alisoma kwa kupendezwa ahadi za Mungu juu ya taratibu mpya, ambayo ndani yake vizuizi vya kimwili vitakuwa ni mambo ya zamani. Kijana huyu wa kike sasa anafurahia kuhudhuria mikutano ya mashahidi wa Yehova.
Akiwa katika likizo katika Ufaransa, Shahidi wa kutoka Ubelgiji aliona fadhili ikileta matokeo yasiyotazamiwa. Akiwa katika kambi, alimwona kijana wa kike wa Kiislamu akishindwa kuchota maji kutoka kwenye bomba. Kuliko kumsaidia, kikundi cha watu katika roshani (veranda iliyo juu gorofani) ya jumba la dansi kilikuwa kikimfanyia mzaha. Yule Shahidi alimkaribia, akimwonyesha namna ya kutumia bomba. Mwenendo wake ulimvuta yule kijana wa kike sana hata akasimama karibu na hema yake kumshukuru, akiongeza: “Wewe u tofauti sana na wengine. Sababu gani?” Shahidi na mkewe wakaeleza kwamba, kama Wakristo, upendo wao haukuwa mchache. Upesi kijana wa kike akarudi kwenye hema yake kuwaambia wa jamaa yake jambo lililotukia.
Nusu saa nyumaye, akifuatana na ndugu zake, dada zake na marafiki, kijana wa kike akarudi tena kwenye hema ya Shahidi, akimkaribisha yeye na mkewe wakae nao jioni moja. Nyuma ya hapo, kwa muda wa majuma mawili, Shahidi, mara nyingi, alizungumza na watu hawa juu ya Biblia. Halafu wakaacha kuonana, kwa maana walihamia kambi nyingine mbali kidogo. Lakini, walikwisha peana anwani na, kwa hiyo, mwishowe Shahidi akafahamu matokeo ya tendo lake la fadhili.
Katika kambi ile ya mbali ile jamaa ya Kiislamu ilikuwa na majirani mashahidi wa Yehova na kwa hiyo waliwezeshwa kujifunza hata zaidi juu ya Maandiko Matakatifu. Kulingana na habari ya juzijuzi, wana wawili na binti mmoja tayari wanashiriki katika utumishi wa mlango kwa mlango wa mashahidi wa Yehova. Wazazi wanakaribia kufanya vile vile.
Nguvu za kuonyesha fadhili kwa wale wanaopinga kweli zinaonyeshwa na lililotukia kwa Shahidi katika Honduras. Hapo nyuma msimamizi wa kijeshi alijaribu kumshurutisha kuingia katika jeshi, hata kutisha kumwua. Mwishowe huyu msimamizi akapoteza cheo chake na kwa hiyo ikamlazimu atafute kazi. Aliajiriwa kama msaidizi katika mojawapo ya kazi za uchimbaji wa madini katika nchi hiyo. Ikatukia ya kwamba Shahidi ambaye alikuwa ametendea mabaya alikuwa katika kazi ile ile ya kimwili. Bila kujua yaliyokuwa yametendeka, bwana mwenye kusimamia kazi akamwagiza mtu huyu afanye kazi chini ya uongozi wa Shahidi yule.
Msimamizi huyu wa zamani wa kijeshi akaogopa sana, akifikiri kwamba Shahidi angelipiza kisasi. Lakini Shahidi alimtendea mkosaji wake wa kwanza kwa fadhili, akigawana chakula chake cha mchana naye. Hii ilimvuta sana yule mtu. Hakuweza kuamini ya kwamba alikuwa akitendewa kwa fadhili na mtu ambaye maisha yake alikuwa ametisha. Polepole jambo hili likamfanya apendezwe na Biblia.
Kwamba fadhili inaweza kufanya mageuzi kama hayo katika watu inashuhudia nguvu zake. Inapaswa vile vile kuwa kichocheo cha kusikiza shauri la Biblia la kuonyesha fadhili.