Mashahidi wa Yehova Huwatendeaje Watu Ambao Wameacha Kuwa Mashahidi?
Tunajitahidi kuwatendea watu wote kwa upendo, fadhili, na heshima. Ikiwa Shahidi wa Yehova amepunguza bidii yake au ameacha kushirikiana na Mashahidi wenzake katika ibada, tunajitahidi kuwasiliana naye na kumhakikishia kwamba tunampenda, na pia tunajaribu kumsaidia arudie ibada yake.—Luka 15:4-7.
Katika visa fulani, matendo ya mtu yanaweza kufanya aondolewe kutanikoni. (1 Wakorintho 5:13) Lakini kabla mtu huyo hajafikia hatua ya kuondolewa kutanikoni, tunajitahidi kumsaidia ili asifikie hatua hiyo. Tunafanya hivyo kwa sababu tunawapenda sana waabudu wenzetu. Na hata ikiwa mtu huyo ataondolewa kutanikoni, bado tutamtendea kwa upendo na heshima, kama Biblia inavyotutia moyo tufanye.—Marko 12:31; 1 Petro 2:17.
Ni nini kinachosababisha mtu aondolewe kutanikoni?
Biblia inasema waziwazi kwamba Mkristo akitenda dhambi nzito bila kutubu, anapaswa kuondolewa kutanikoni.a (1 Wakorintho 5:11-13) Biblia inaonyesha ni dhambi gani ambazo zinaweza kumfanya mtu aondolewe kutanikoni. Kwa mfano, inataja mambo kama vile uzinzi, ulevi, kuua, kuwatendea watu wa familia kwa ukatili, na wizi.—1 Wakorintho 6:9, 10; Wagalatia 5:19-21; 1 Timotheo 1:9, 10.
Hata hivyo, mtu aliyetenda dhambi nzito haondolewi kutanikoni moja kwa moja. Kwanza kabisa, wazeeb wa kutaniko hujaribu kumsaidia abadili mwenendo wake. (Waroma 2:4) Wanamtendea kwa upole na fadhili. (Wagalatia 6:1) Wazee wanapomtendea mtenda dhambi kwa njia hiyo, wanaweza kumgusa moyo, na kumsaidia kutambua kwamba amefanya makosa na hivyo kuchochewa kutubu. (2 Timotheo 2:24-26) Ikiwa mtu huyo amesaidiwa mara kwa mara, lakini bado anaendelea kuvunja sheria za maadili za Biblia bila kutubu, ni lazima aondolewe kutanikoni. Wazee watalitangazia kutaniko kwamba mtu huyo si Shahidi wa Yehova tena.
Wazee hujitahidi kumsaidia mtenda dhambi abadili mwenendo wake kwa kumtendea kwa upole na fadhili
Kuna faida gani ya kumwondoa kutanikoni mtu ambaye ameazimia kuendelea kutenda dhambi? Kwanza, kwa kufanya hivyo, kutaniko linaunga mkono viwango vya Mungu vya usafi wa kiadili, na pia linajilinda kutokana na uvutano mbaya wa mtu huyo. (1 Wakorintho 5:6; 15:33; 1 Petro 1:16) Isitoshe, mtu huyo aliyetenda dhambi anaweza kuchochewa kuacha kutenda dhambi na kufanya mabadiliko yanayohitajika.—Waebrania 12:11.
Mashahidi wa Yehova huwatendeaje wale ambao wameondolewa kutanikoni?
Biblia inawaambia Wakristo ‘waache kushirikiana’ na mtu ambaye ameondolewa kutanikoni, na ‘hata wasile chakula pamoja na mtu wa namna hiyo.’ (1 Wakorintho 5:11) Kwa hiyo, hatushirikiani na mtu ambaye ameondolewa kutanikoni. Hata hivyo, hatumpuuzi. Tunamtendea kwa heshima. Anaweza kuhudhuria mikutano yetu ya kidini, na Mashahidi wa Yehova wanaweza kumsalimu.c Pia, anaweza kuwaomba wazee wamsaidie ili arudi kutanikoni.
Wale walioondolewa kutanikoni wanakaribishwa kuhudhuria mikutano yetu
Hali inakuwaje mtu anapoondolewa kutanikoni lakini mume, mke, au watoto wake bado ni Mashahidi wa Yehova? Ingawa hamwabudu Yehova pamoja na familia yake tena, uhusiano wao wa kifamilia bado unaendelea. Kwa kuwa wanaishi katika nyumba moja, uhusiano wake pamoja na mume, mke, na watoto unaendelea, na wanaendelea kutendeana kwa upendo.
Mtu aliyeondolewa kutanikoni anaweza kuwaomba wazee wamtembelee, na wanapomtembelea watampa ushauri wa Biblia kwa upendo, na kumtia moyo kwa fadhili atubu na kumrudia Mungu. (Zekaria 1:3) Akiacha mwenendo usiofaa na kuonyesha kwa matendo yake kwamba anataka kuishi kulingana na viwango vya Biblia, atakaribishwa tena kutanikoni. Kutaniko ‘litamsamehe kwa fadhili na kumfariji,’ kama Wakristo wa Korintho walivyofanya mtenda dhambi mmoja alipoacha kutenda dhambi.—2 Wakorintho 2:6-8.
Wale waliokuwa wameondolewa kutanikoni na ambao wamerudi wanahisije sasa?
Ona maelezo ya baadhi ya Mashahidi wa Yehova waliokuwa wameondolewa kutanikoni lakini baadaye wakaamua kumrudia Mungu.
“Nilipoamua kurudi kutanikoni, nilifikiri kwamba wazee wataniuliza mambo yote niliyokuwa nikifanya kwa miaka yote hiyo niliyokuwa nimeondolewa kutanikoni. Lakini walichoniambia ni, ‘Tunataka ukazie fikira mambo utakayofanya kuanzia sasa.’ Baada ya kusikia hilo, nilipata utulivu mwingi.”—Maria, Marekani.
“Ndugu na dada kutanikoni walifurahi sana niliporudi. Nilihisi ninathaminiwa. Walinisaidia nihisi kwamba wamenisamehe na kwamba Yehova amenisamehe pia, na hilo lilinisaidia kusonga mbele. Sikuzote wazee walikuwa tayari kunisaidia kurudia hali nzuri ya kiroho. Walinifariji na kunisaidia kutambua kwamba bado Yehova ananipenda na ananithamini.”—Malcom, Sierra Leone.
“Yehova anawapenda sana watu wake na anataka tengenezo lake liwe safi. Hilo linanifurahisha sana. Huenda watu wengine wakafikiri kwamba huo ni ukatili, lakini hilo ni tendo la upendo na linahitajika. Ninafurahi kwamba Baba yetu wa mbinguni ni Mungu mwenye upendo na anayesamehe.”—Sandi, Marekani.
a Awali, tulikuwa tukiwarejelea watenda dhambi wasiotubu kuwa wametengwa na ushirika. Lakini sasa tunasema wameondolewa kutanikoni, kwa sababu hayo ndiyo maneno yanayotumiwa na Biblia.
b Wazee ni wanaume Wakristo walio wakomavu wanaofundisha kwa kutumia Maandiko na kuwachunga watu wa Yehova kwa kuwasaidia na kuwatia moyo. Hawalipwi kwa kazi wanayofanya.—1 Petro 5:1-3.
c Katika visa fulani visivyo vya kawaida, mtu anaweza kuondoka kutanikoni na kisha kuanza kujaribu kuliharibu kutaniko kwa kuwavunja moyo ndugu na dada kutanikoni au kwa kuwachochea wafanye mambo mabaya. Katika kisa kama hicho, tunatii amri ya Biblia ya ‘kutomsalimu’ mtu kama huyo.—2 Yohana 9-11.