JUNI 1-7, 2026
WIMBO 111 Sababu za Kuwa na Shangwe
Unaweza Kuwa na Furaha Unapochukiwa
“Wenye furaha ni ninyi watu wanapowachukia.”—LUKA 6:22.
JAMBO KUU
Kwa nini tunaweza kuwa na furaha tunapochukiwa kwa sababu ya kumtumikia Yehova.
1. Ni maneno gani yenye kushangaza ambayo Yesu alisema kuhusu kuchukiwa?
KATIKA Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alisema: “Wenye furaha ni ninyi watu wanapowachukia.” (Luka 6:22) Ni lazima maneno hayo yaliwashangaza wasikilizaji wake. Kwa kweli, hakuna anayefurahia kuchukiwa. Kwa nini Yesu alisema maneno hayo? Hilo ni swali zuri la kufikiria kwa sababu wafuasi wa Yesu leo wanachukiwa na watu wengi. Tutazungumzia kwa nini tunachukiwa na kwa nini tunaweza kuwa na furaha tunapochukiwa.
KWA NINI TUNACHUKIWA?
2-3. Ni sababu gani moja inayofanya Wakristo wa kweli wateswe, na inawezaje kubadili maoni yetu kuhusu wale wanaotupinga? (Yohana 16:2, 3)
2 Tunachukiwa kwa sababu tunamwabudu Yehova. Yesu alisema hivi kuhusu wale ambao wangewatesa na hata kuwaua baadhi ya wafuasi wake: “Hawamjui Baba wala mimi.” (Soma Yohana 16:2, 3.) Ni nani hasa anayepaswa kulaumiwa inapohusu chuki ambayo watu wa Mungu wanaoonyeshwa? Ni Shetani. Yeye ni “mungu wa mfumo huu wa mambo.” (2 Kor. 4:3, 4) Anawapofusha watu ili wasijue ukweli kumhusu Yehova na anawashawishi wawapinge wale wanaomjua na kumpenda Mungu. (Yoh. 8:42-44) Kujua hilo kunawezaje kubadili maoni yetu kuwaelekea? Jambo moja ni kwamba kutambua kuwa wamedanganywa kunaweza kutusaidia kuepuka kuwachukia.
3 Fikiria mfano wa Pavel,a anayeishi katika nchi ambayo kazi yetu imepigwa marufuku. Kwa kuwa aliendelea kumwabudu Yehova kwa uaminifu, alikamatwa, akapigwa kikatili, na kuwekwa katika kifungo cha peke yake kwa miezi mingi. Pavel anasema hivi: “Nimeona wazi kwamba mateso yanatokana na upinzani wa roho waovu kuelekea ibada safi. Inaonekana kwamba watu wengi wanaofanya kazi katika magereza hawatuchukii. Ni kwamba tu wanafanya kazi yao.” Ndugu nchini Kroatia, aliyevumilia mateso makali kutoka kwa wazazi wake wasioamini, alisema hivi: “Nimetambua kwamba adui yangu hasa ni Shetani, na si wazazi wangu.”—Efe. 6:12.
4. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Yesu na mwanafunzi Stefano? (Tazama pia picha.)
4 Hatuwachukii wapinzani wetu. Kwa kweli, tunaweza hata kusali kwa ajili yao. (Mt. 5:44) Kuhusiana na hilo, tunaweza kujifunza kutoka kwa Yesu na mwanafunzi Stefano. Alipokuwa ametundikwa na wanajeshi Waroma katika mti wa mateso, Yesu alisali hivi: “Baba, wasamehe.” (Luka 23:34) Yesu alikuwa akimwomba Yehova awasamehe wanajeshi hao waliopewa kazi ya kumuua. Huenda pia alikuwa akifikiria wale waliokuwa katika umati ambao walichochewa na maadui wake wa kidini wapaze sauti zao wakitaka auawe. Yesu alitambua kwamba watu hao hawakujua hasa ni nini walichokuwa wakifanya. Vivyo hivyo, mwanafunzi Stefano alimwomba Mungu awasamehe wale waliotaka kumuua. (Mdo. 7:58-60) Je, Yehova alijibu sala ya Yesu na ya Stefano? Ndiyo. Wengi ambao walihusika katika kumhukumu Yesu na kumuua, baadaye walitubu, wakaonyesha imani katika Yesu, na kubatizwa. (Mdo. 2:36-41) Na angalau mtu mmoja aliyeidhinisha kuuawa kwa Stefano—Sauli wa Tarso—alikuja kuwa Mkristo na alijutia sana matendo mabaya aliyofanya kwa sababu ya kutojua.—1 Tim. 1:13.
Kama tu Yesu na mwanafunzi Stefano walivyosali kwa ajili ya wale waliowatesa, sisi pia tunaweza kusali kwa ajili ya wale wanaotutesa (Tazama fungu la 4)
5. Umejifunza nini kutokana na kisa cha César?
5 Leo pia, Yehova anaendelea kujibu sala zinazotolewa kwa ajili wale wanaotupinga. Fikiria kisa cha César, anayeishi nchini Venezuela. Baba yake aliipinga vikali kweli. César anasema hivi: “Mama yangu alikuwa mke na mama mzuri. Ingawa sikuzote alitanguliza Ufalme maishani, kamwe hakumpuuza baba yangu. Alitufundisha mimi na ndugu na dada zangu wa kimwili kumheshimu baba yetu. Pia, alitufundisha kumtii isipokuwa iwe ametuomba tufanye jambo ambalo ni kinyume na mapenzi ya Mungu.” Kadiri miaka ilivyopita, mtazamo wa baba yake ulianza kubadilika. César anasema hivi: “Siku moja, baada ya kusali kutoka moyoni, nilimuuliza baba yangu ikiwa angependa kujifunza Biblia pamoja nami. Ni vigumu kwangu kueleza hisia nilizokuwa nazo aliposema ndiyo.” Baada ya muda, baba ya César alibatizwa. Si wapinzani wote wanaofikia hatua ya kubatizwa, lakini baadhi hubadili mtazamo wao kutuelekea baada ya kujionea jinsi tunavyozungumza kwa heshima na mwenendo wetu mzuri. Tunafurahi sana wanapofanya hivyo! Tunasubiri kwa hamu kuona jinsi Yehova, “Mwamuzi wa dunia yote” mwenye rehema, atakavyowavuta watu kama hao kwake.—Mwa. 18:25.
6. Kulingana na Marko 13:13, ni sababu gani nyingine inayofanya tuchukiwe?
6 Tunachukiwa kwa sababu tunamheshimu Yesu. Yesu alisema kwamba Wakristo wa kweli wangechukiwa na watu wote “kwa sababu ya jina [lake].” (Soma Marko 13:13.) “Jina” la Yesu linawakilisha nini? Linawakilisha sifa na mamlaka yake akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Tunachukiwa na watu ambao wameweka tumaini lao katika viongozi wa hapa duniani, na si kwa yule ambaye Yehova amemchagua kutawala ulimwengu wote, Yesu Kristo. Yesu amekuwa akitawala akiwa Mfalme wa Ufalme tangu mwaka wa 1914. Hivi karibuni, ataondoa serikali zote zinazopinga mamlaka yake.
7-8. Kwa nini baadhi ya watu wa Yehova wanadhihakiwa? (Yohana 15:18-20) (Tazama pia picha.)
7 Tunachukiwa kwa sababu tunaukataa ulimwengu wa Shetani. Yesu alieleza kwamba wafuasi wake wangechukiwa kwa sababu wao “si sehemu ya ulimwengu.” (Soma Yohana 15:18-20.) Kama Wakristo wa mapema, tunakataa mitazamo, mwenendo, na njia ya kuzungumza ya ulimwengu huu usiomwogopa Mungu. Kwa sababu hiyo, ndugu na dada wengi wamedhihakiwa kazini au shuleni. (1 Pet. 4:3, 4) Hata hivyo, tunafurahi kwamba, mwishowe baadhi ya wale wanaotupinga wamebadili maoni yao kutuelekea na wanatuheshimu kwa sababu ya msimamo wetu.
8 Fikiria kisa cha Ignacio, aliye Amerika ya Kati. Mwalimu mmoja wa kiume katika shule aliyosoma alimdhihaki kwa miaka mingi kwa sababu ya viwango vyake vya juu vya maadili. Hata hivyo, kabla ya Ignacio kuhitimu shule, mwalimu huyo alimuuliza aliwezaje kuishi kulingana na kanuni za Biblia licha ya kudhihakiwa sana. Ignacio alimweleza kwamba anaona sheria za Mungu kuwa ulinzi. Kisha akamwalika mwalimu huyo katika mkutano wa kutaniko. Ignacio alishangaa mwalimu huyo alipohudhuria! Mwalimu huyo alivutiwa sana na upendo aliojionea kutanikoni hivi kwamba akaendelea kuhudhuria mikutano. Baadaye, kwa sababu ya kujifunza Biblia, mwalimu huyo alikabili upinzani pia. Lakini aliendelea kufanya maendeleo ya kiroho na mwishowe akabatizwa.
Haidhuru umri tulio nao, tunaweza kutetea imani yetu kwa ujasiri na mafanikio (Tazama fungu la 8)b
9-10. (a) Ni sababu gani nyingine inayowafanya Wakristo wawe tofauti na ulimwengu wa Shetani? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa mtume Paulo?
9 Pia, tuko tofauti na ulimwengu wa Shetani kwa sababu hatuungi mkono upande wowote inapohusu masuala ya siasa na vita. (Yoh. 18:36) Kupatana na shauri kwenye andiko la Waroma 13:1, tunajitahidi kuwa raia wanaotii sheria za nchi. Hata hivyo, tukiwa Wakristo, hatuungi mkono upande wowote katika migogoro ya kisiasa, hivyo hatugombei vyeo vya kisiasa au kuwapigia kura wagombea wa vyeo vya kisiasa. Kwa nini? Kwa sababu sisi ni washikamanifu kwa Yehova na Ufalme wake chini ya utawala wa Kristo. Mashahidi wengi wa Yehova wamefungwa kwa sababu ya imani yao ya Kikristo. Hata hivyo, ndugu na dada waliofungwa gerezani wanaendelea kuhubiri. Kwa njia hiyo, wanamwiga mtume Paulo ambaye kwa miaka mingi alikuwa katika kifungo cha nyumbani na pia gerezani. (Mdo. 24:27; 28:16, 30) Aliendelea kuwahubiria wote waliomsikiliza, kutia ndani walinzi wa gereza, maofisa wa mahakama, magavana, wafalme, na huenda hata maofisa wa Maliki Mroma Nero.—Mdo. 9:15.
10 Vivyo hivyo, ndugu zetu waliofungwa gerezani wanawahubiria watu wote watakaowasikiliza, kutia ndani mahakimu, maofisa wa serikali, na walinzi. Ndugu mmoja aliyefungwa gerezani kwa zaidi ya miaka sita kwa sababu ya kutounga mkono upande wowote katika masuala ya kisiasa alisema kwamba aliona muda wote aliokaa gerezani kama mgawo aliopewa na Yehova wa kutafuta watu walio kama kondoo, na si kama adhabu. Tunafurahi sana Yehova anapotutumia kuwahubiria habari njema watu kama hao! (Kol. 4:3) Acheni tuchunguze sababu nyingine tulizo nazo za kuwa na furaha hata wakati watu wanatuchukia kwa sababu ya kumtumikia Yehova.
KWA NINI TUNAWEZA KUWA NA FURAHA TUNAPOCHUKIWA?
11. Kupatwa na mateso kunawezaje kuimarisha imani yako? Toa mfano.
11 Tunajua kwamba chuki ya ulimwengu inatimiza unabii wa Biblia. Katika unabii wa kwanza kwenye Biblia, Yehova alitabiri kwamba Shetani na uzao wake wa mfano—wale wanaomfuata—wangewachukia wale wanaompenda na kumtumikia Yehova. (Mwa. 3:15) Yesu alionyesha ukweli wa maneno hayo ya kinabii, kwa kueleza mara nyingi kwamba wale wanaomtumikia Yehova watateswa, kama ilivyorekodiwa na waandikaji wa vitabu vyote vinne vya Injili. (Mt. 10:22; Marko 13:9-12; Luka 6:22, 23; Yoh. 15:20) Na waandikaji wengine Wakristo wa Biblia walifanya hivyo pia. (2 Tim. 3:12; Yak. 1:2; 1 Pet. 4:12-14; Yuda 3, 17-19) Hivyo tunapoteswa, hatushtuki. Badala yake, tunafurahi kwamba unabii wa Biblia unatimizwa. Hilo linatuhakikishia kwamba tunamtumikia Mungu wa kweli. Dada anayeishi katika nchi ambayo kazi yetu imepigwa marufuku anasema hivi: “Nilipojiweka wakfu kwa Yehova, nilijua kwamba ningekabili mateso sasa au baadaye. Hivyo, majaribu hayakuniogopesha, wala kunishtua.” Mume wake alikuwa mmoja kati ya wapinzani wake wengi. Alimtendea kwa njia isiyofaa na alichoma Biblia yake na machapisho yanayotegemea Biblia. Lakini badala ya kurudi nyuma kwa woga, imani ya dada yetu iliendelea kuimarika. (Ebr. 10:39) Anasema hivi: “Mateso yalitabiriwa mapema, hivyo nilijua kwamba ni lazima yatukie. Kupatwa na mateso kulinithibitishia kwamba hii ni dini ya kweli.”
12. Ni nini kilichomsaidia ndugu mmoja kukabiliana na mateso?
12 Ingawa tunatarajia kuteswa, huenda bado ikawa vigumu kwetu kuvumilia. Ndugu mmoja aliandika hivi kuhusu wakati alipokuwa gerezani: “Nyakati fulani, nilihisi nimeshuka moyo au mwenye wasiwasi, na ningelia tu.” Ni nini kilichomsaidia ndugu huyo kukabiliana na hali hiyo? Alisema hivi: “Sikuzote nilisali. Nilianza siku kwa kusali kila asubuhi. Wakati wa mchana nilisali wakati hali yoyote ngumu ilipojitokeza. Na nilipokasirika kwa sababu ya ukosefu wa haki, nilijifungia bafuni na kusali.” Ndugu yetu alitafakari pia kuhusu mifano ya kale na ya siku zetu ya watu walioonyesha utimilifu. Hilo lilimsaidia kuvumilia mateso na kupata amani ambayo Yesu aliwaahidi wafuasi wake.—Yoh. 14:27; 16:33.
13. Ni nini kinachoweza kutusaidia kushinda chuki?
13 Upendo tulio nao una nguvu za kushinda chuki. Yesu alimpenda Baba yake kwa moyo wake wote, hadi siku alipokata pumzi. Yesu aliwapenda pia rafiki zake. (Yoh. 13:1; 15:13) Tunapositawisha upendo kama huo kwa Yehova na kwa ndugu na dada zetu, sisi pia tutaweza kushinda chuki. Jinsi gani? Ili kupata jibu, fikiria mfano wa mtume Paulo.
14. Ni nini kilichomsaidia Paulo kusimama imara hata alipokabili kifo?
14 Muda mfupi kabla ya kuuawa, Paulo alimwandikia Timotheo, rafiki yake mpendwa hivi: “Mungu hakutupatia roho ya woga, bali roho ya nguvu na ya upendo.” (2 Tim. 1:7) Paulo alimaanisha nini? Paulo alikuwa akisema kwamba upendo wenye nguvu kumwelekea Yehova unaweza kumchochea Mkristo kuwa tayari kuvumilia majaribu makali sana. (2 Tim. 1:8) Hapana shaka kwamba upendo ambao Paulo alikuwa nao kumwelekea Yehova ulimsaidia kukabili kifo kwa ujasiri bila kuiacha ibada ya kweli.—Mdo. 20:22-24.
15. Ndugu na dada zetu wameonyeshaje upendo usio na ubinafsi kuelekea ndugu na dada zao katika siku zetu? (Tazama pia picha.)
15 Kwa kweli, tunawapenda waabudu wenzetu ambao wanabaki imara wanapokabili mateso. Leo, baadhi ya ndugu na dada wako tayari kuhatarisha uhai wao kwa ajili ya ndugu na dada zao, kama Akila na Prisila walivyofanya walipohatarisha uhai wao kwa ajili ya Paulo. (Rom. 16:3, 4) Kwa mfano, nchini Urusi, ndugu na dada wengi wameenda kwenye mahakama ili kuwatia moyo wale ambao wamekamatwa. Dada mmoja aliyekamatwa alipoona kikundi kikubwa cha ndugu na dada zake wa kiroho mahakamani, alipata faraja na kulemewa na hisia hivi kwamba hakuweza kuzungumza kwa muda fulani. Upendo usio na ubinafsi wa waabudu wenzake ulimwimarisha alipohitaji hasa kuimarishwa. Kwa kweli, tunafurahi sana kwamba tuna upendo wenye nguvu za kushinda chuki!
Hata katika maeneo ambayo kazi yetu imepigwa marufuku au kuzuiwa, ndugu na dada zetu wamewaonyesha Wakristo wenzao upendo usio na ubinafsi (Tazama fungu la 15)c
16. Kwa nini mtume Petro alisema kwamba wale wanatendewa kwa njia isiyofaa kwa sababu ya kumtumikia Mungu wana sababu ya kuwa na furaha? (1 Petro 4:14)
16 Tunajua kwamba tunapovumilia licha ya kuchukiwa tunapata kibali cha Mungu. (Soma 1 Petro 4:14.) Mtume Petro alisema kwamba wale wanaovumilia kutendewa kwa njia isiyofaa kwa sababu ya kumtumikia Mungu wana sababu ya kuwa na furaha. Kwa nini? Kwa sababu kutendewa huko kwa njia isiyofaa ni uthibitisho kwamba roho ya Mungu “inatulia juu [yetu].” Petro alijua jinsi mtu anavyohisi anapokuwa na kibali cha Mungu na kuvumilia mateso. Muda mfupi baada ya siku ya Pentekoste 33 W.K., polisi wa Kiyahudi wa hekaluni walitumwa kumkamata Petro na mitume wengine kwa sababu ya kuhubiri. Lakini kwa ujasiri Petro alitetea imani yake. (Mdo. 5:24-29) Hata baada ya kupigwa viboko, yeye na mitume wenzake hawakuacha kuhubiri. Badala yake, walishangilia kwa sababu “walikuwa wamestahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina [la Yesu].” Sisi pia tunaweza kushangilia tunapovumilia majaribu.—Mdo. 5:40-42.
17. Yesu aliwaambia nini wanafunzi wake usiku kabla ya kifo chake?
17 Katika usiku kabla ya kifo chake, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Yeyote anayenipenda atapendwa na Baba yangu, nami nitampenda.” (Yoh. 14:21) Tunasubiri kwa hamu wakati ambapo tutapendwa—na si kuchukiwa—kwa sababu ya kumtumikia Yehova! (2 The. 1:6-8) Tunaposubiri wakati huo, acheni tupate faraja na nguvu kutokana na sababu nyingi tulizo nazo za kuwa na furaha tunapochukiwa.
WIMBO 149 Wimbo wa Ushindi
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.
b MAELEZO YA PICHA: Igizo linamwonyesha Ignacio akimhubiria mwalimu wake.
c MAELEZO YA PICHA: Igizo linaloonyesha akina ndugu na dada wakimuunga mkono mwabudu mwenzao anayeenda kufungwa kwa sababu ya imani yake.