Washiriki Wapya Wawili wa Baraza Linaloongoza
OKTOBA 5, 2024, tangazo la pekee lilitolewa katika mkutano wa kila mwaka. Ndugu Jody Jedele na Ndugu Jacob Rumph waliwekwa rasmi kuwa washiriki wa Baraza Linaloongoza. Ndugu hao wawili wamemtumikia Yehova kwa uaminifu kwa miaka mingi.
Jody Jedele na Damaris, mke wake
Ndugu Jedele alizaliwa Missouri, Marekani na alilelewa katika kweli. Familia yao iliishi karibu na eneo lisilohubiriwa kwa ukawaida. Hivyo, alikutana na ndugu wengi kutoka katika malezi mbalimbali waliotembelea eneo hilo ili kuhubiri habari njema. Upendo na umoja wao ulimchochea sana. Alibatizwa Oktoba 15, 1983, katika miaka yake ya mapema ya utineja. Alifurahia huduma, na baada ya kumaliza shule ya sekondari, alianza upainia wa kawaida Septemba 1989.
Alipokuwa kijana, wazazi wa Ndugu Jedele walikuwa na zoea la kumpeleka yeye na dada yake kutembelea Betheli. Matembezi hayo yaliwachochea watoto hao kuweka lengo la kutumikia Betheli—lengo ambalo wote wawili walifikia. Ndugu Jedele aliwasili katika Betheli ya Wallkill Septemba 1990. Alianza kufanya kazi katika Idara ya Usafi na baadaye katika Huduma za Matibabu.
Wakati huohuo, kulikuwa na ongezeko katika makutaniko ya Kihispania yaliyokuwa karibu na Betheli na kulikuwa na uhitaji wa akina ndugu. Hivyo, Ndugu Jedele alijiunga katika kutaniko mojawapo na kuanza kujifunza Kihispania. Muda mfupi baadaye, alikutana na Damaris, dada painia katika mzunguko wao. Mwishowe, walifunga ndoa, na wakaendelea na utumishi wa Betheli.
Mwaka wa 2005, waliondoka Betheli ili kuwatunza wazazi wao waaminifu. Wakati huo, walitumikia wakiwa mapainia wa kawaida. Ndugu Jedele alifundisha katika Shule ya Utumishi wa Painia, na alitumikia katika Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali katika eneo lao na katika Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa.
Mwaka wa 2013, Ndugu na Dada Jedele walialikwa tena Betheli kwa ajili ya mradi wa ujenzi wa Warwick. Tangu wakati huo, wametumikia pia katika Betheli ya Patterson na Wallkill. Ndugu Jedele amefanya kazi katika Idara ya Usanifu-Majengo na Ujenzi na Huduma za Habari za Hospitali. Machi 2023, aliwekwa rasmi kuwa msaidizi katika Halmashauri ya Utumishi. Anapokumbuka migawo aliyofurahia, anasema hivi: “Unapopata migawo mipya, nyakati fulani unaweza kuhisi umelemewa. Lakini wakati huo ndipo unapopaswa kukumbuka kumtegemea Yehova kwa sababu yeye ndiye husababisha kuwa.”
Jacob Rumph na Inga, mke wake
Ndugu Rumph alizaliwa California, Marekani. Alipokuwa mtoto, mama yake alikuwa mhubiri asiyetenda, lakini alijitahidi kumfundisha kweli za Biblia. Pia, kila mwaka alimtembelea nyanya (bibi) yake, aliyekuwa Shahidi mwaminifu. Alimsaidia aanze kupendezwa na kweli, na alipokuwa na umri wa miaka 13, aliomba kufundishwa Biblia. Alibatizwa Septemba 27, 1992, alipokuwa tineja. Jambo la kufurahisha ni kwamba mama yake alianza tena kuwa mhubiri anayetenda. Pia, watu wake wote wa karibu wa familia wakaanza kufanya maendeleo na kubatizwa.
Alipokuwa kijana, Ndugu Rumph aliona furaha ambayo mapainia walikuwa nayo. Hivyo, alianza kufanya upainia Septemba 1995, baada ya kumaliza shule ya sekondari. Mwaka wa 2000, alihamia Ekuado ili kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa. Huko alikutana na Inga, dada painia kutoka Kanada, na mwishowe walifunga ndoa. Baada ya kufunga ndoa, waliishi katika mji mmoja nchini Ekuado uliokuwa na kikundi kidogo cha wahubiri. Leo, kuna kutaniko imara katika mji huo.
Baada ya muda, Ndugu na Dada Rumph waliwekwa rasmi kuwa mapainia wa pekee na baadaye walitumikia katika kazi ya kuzungukia makutaniko. Mwaka wa 2011, walialikwa katika darasa la 132 la Shule ya Gileadi. Baada ya kuhitimu, walitumika katika maeneo mbalimbali duniani na walifurahia aina mbalimbali za utumishi, kama vile utumishi wa Betheli, umishonari, na kuzungukia makutaniko. Ndugu Rumph pia alikuwa na pendeleo la kufundisha katika Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme.
Kwa sababu ya janga la COVID-19, Ndugu na Dada Rumph walirudi Marekani. Walialikwa Betheli ya Wallkill na Ndugu Rumph alizoezwa katika Idara ya Utumishi. Mwishowe walirudi katika ofisi ya tawi ya Ekuado, ambapo Ndugu Rumph alitumikia katika Halmashauri ya Tawi. Mwaka wa 2023, walihamishiwa Warwick. Januari 2024, Ndugu Rumph aliwekwa rasmi kutumikia akiwa msaidizi katika Halmashauri ya Utumishi. Anapokumbuka utumishi mbalimbali aliofanya, anasema hivi: “Jambo linalofanya mgawo uwe wa pekee si eneo, bali ni watu unaotumikia pamoja nao.”
Tunathamini bidii ya ndugu hao, na tunaendelea “kuwaheshimu sana watu wa namna hiyo.”—Flp. 2:29.