Kusanyiko jijini Indianapolis, Indiana, 1925
1925—Miaka Mia Moja Iliyopita
GAZETI la The Watch Tower la Januari 1, 1925 lilisema hivi: “Wakiwa na tarajio kubwa, Wakristo wameutazamia kwa hamu mwaka huu.” Hata hivyo, makala hiyo iliendelea kusema hivi: “Wakristo hawapaswi kuhangaika kupita kiasi kuhusu mambo yatakayotokea mwaka huu hivi kwamba washindwe kufanya kwa shangwe kazi ambayo Bwana amewatuma wafanye.” Wanafunzi wa Biblia walitarajia jambo gani mwaka wa 1925? Na waliendeleaje kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana licha ya kuvunjika moyo?
MATARAJIO YALIYOAHIRISHWA
Mwaka wa 1925, Wanafunzi wa Biblia wengi walitarajia kurudishwa kwa Paradiso duniani. Kwa nini? Ndugu Albert Schroeder, ambaye baadaye alikuja kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alieleza hivi: “Ilifikiriwa kwamba wafuasi watiwa-mafuta wa Kristo waliobaki, wangeenda mbinguni na kuwa sehemu ya Ufalme na kwamba wanaume waaminifu wa zamani kama vile, Abrahamu, Daudi na wengine, wangefufuliwa na kuwa wakuu ili watawale katika serikali duniani kama sehemu ya ufalme wa Mungu.” Kadiri mwaka ulivyozidi kusonga na matumaini yao kutotimia, inaeleweka kwamba baadhi yao walivunjika moyo.—Met. 13:12.
Licha ya kuvunjika moyo, Wanafunzi wa Biblia wengi waliendelea kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya kuhubiri na kutambua hata zaidi jukumu lao la kuwa Mashahidi wa Yehova. Kwa mfano, fikiria kazi waliyofanya ili kutangaza kweli katika maeneo ya mbali.
VITUO VYA REDIO VYAONGEZEKA
Kwa sababu ya mafanikio ya kituo cha redio cha WBBR mwaka wa 1924, Wanafunzi wa Biblia walijenga kituo kingine chenye uwezo mkubwa, wakati huu karibu na jiji la Chicago, Illinois. Jina la kituo hicho kipya lilikuwa WORD. Ralph Leffler, mtaalamu wa mambo ya redio aliyeshiriki katika ujenzi wa kituo hicho, anakumbuka hivi: “Nyakati za usiku wakati wa majira ya baridi, kituo cha WORD kilisikika hadi sehemu za mbali zaidi.” Kwa mfano, familia moja ambayo iliishi umbali wa zaidi ya kilomita 5,000 katika jiji la Pilot Station, Alaska, walisikiliza matangazo ya kwanza ya kituo hicho cha redio. Baada ya kusikiliza, familia hiyo iliandika barua kwa wafanyakazi wa kituo hicho ili kuwashukuru kwa kutayarisha programu hiyo ya kiroho yenye kutia moyo.
Kushoto: Minara ya kurusha mawimbi ya kituo cha WORD jijini Batavia, Illinois
Kulia: Ralph Leffler akifanya kazi katika kituo cha redio
Gazeti la The Watch Tower la Desemba 1, 1925 lilisema hivi kuhusu uwezo mkubwa wa kutangaza wa kituo hicho: “WORD ni mojawapo ya vituo vyenye uwezo mkubwa sana nchini Marekani kinachotumia wati 5,000. Matangazo ya kituo hicho yamefika vizuri katika eneo la pwani ya mashariki na magharibi ya Marekani, Kuba na eneo la mbali zaidi kaskazini mwa Alaska. Wengi ambao hawakuwahi kusikia kweli, wamependezwa nayo kwa kusikiliza kituo hicho.”
George Naish
Wakati huohuo, Wanafunzi wa Biblia walijitahidi pia kutumia zaidi redio ili kuhubiri habari njema nchini Kanada. Mwaka wa 1924, kituo cha redio cha CHUC kilijengwa huko Saskatoon, Saskatchewan. Kilikuwa mojawapo ya vituo vya kwanza vya redio vya dini nchini Kanada. Kufikia mwaka wa 1925, kituo hicho kidogo kilihitaji kuhamishwa. Hivyo, shirika la Watch Tower Society lilianza kumiliki kituo hicho na kuhamisha studio zake katika jengo la Regent Building, jumba la sinema la zamani huko Saskatoon, walilonunua na kulirekebisha kwa ajili ya kusudi hilo.
Kwa sababu ya kituo hicho, watu wengi walioishi katika maeneo yaliyo na watu wachache ya Saskatchewan walisikia habari njema kwa mara ya kwanza. Kwa mfano, katika mji mmoja ulio mbali, mwanamke aliyeitwa Bi. Graham aliomba chapisho linalotegemea Biblia baada ya kusikiliza kituo hicho cha redio. Ndugu George Naish anakumbuka hivi: “Ni kana kwamba kilio chake ‘Tufundisheni!’ kilisikika kwa sauti na waziwazi hivi kwamba tulimtumia mabuku yote ya Studies in the Scriptures.” Baada ya muda mfupi, Bi. Graham alikuwa akitangaza ujumbe wa Ufalme katika eneo la mbali zaidi.
KUREKEBISHA UELEWAJI WA MAFUNDISHO YETU
Toleo la The Watch Tower la Machi 1, 1925, lilikuwa na makala muhimu yenye kichwa, “Kuzaliwa kwa Taifa.” Kwa nini makala hiyo ilikuwa muhimu sana? Kwa muda fulani, Wanafunzi wa Biblia walijua kwamba Shetani alikuwa na tengenezo lililofanyizwa na roho waovu wasioonekana waliokuwa mbinguni na duniani lilifanyizwa na mifumo ya kidini, kibiashara, na kisiasa. Hata hivyo, kupitia makala hiyo, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” aliwasaidia akina ndugu kuelewa kwamba Yehova pia ana tengenezo lake ambalo ni tofauti kabisa na tengenezo la Shetani na linalolipinga. (Mt. 24:45) Kwa kuongezea, mtumwa alieleza kwamba Ufalme wa Mungu ulikuwa umezaliwa mwaka wa 1914 na kwamba mwaka huo, kwa sababu ya matokeo ya ‘vita vilivyotokea mbinguni,’ Shetani na roho wake waovu walitupwa kutoka mbinguni na kudhibitiwa duniani.—Ufu. 12:7-9.
Baadhi ya watu waliona ikiwa vigumu kukubali uelewaji huo mpya. Hivyo, makala hiyo ilisema hivi: “Ikiwa kuna wasomaji wa gazeti la The Watch Tower ambao hawakubaliani na jambo lililoandikwa, inapendekezwa kwamba wamsubiri Bwana kwa utulivu na umakini, sikuzote wakidumisha moyo safi.”
Hata hivyo, Tom Eyre, aliyekuwa kolpota (ambao sasa wanajulikana kama painia) kutoka Uingereza, alieleza jinsi Wanafunzi wa Biblia wengi walivyohisi kuhusu makala hiyo, alisema hivi: “Akina ndugu walisisimuka waliposikia ufafanuzi wa Ufunuo 12. Tulipotambua kwamba Ufalme ulikuwa umeanzishwa mbinguni, tulikuwa na hamu kubwa sana ya kushiriki habari hizo njema na wengine. Bila shaka, hilo lilituchochea kuongeza utendaji wetu na kutusaidia kuona jinsi ambavyo Yehova angetimiza mambo makubwa zaidi wakati ujao.”
KUTOA USHAHIDI KUMHUSU YEHOVA
Leo, Mashahidi wa Yehova wanajua vizuri maneno ya Isaya 43:10: “‘Ninyi ni mashahidi wangu,’ asema Yehova, ‘Naam, mtumishi wangu ambaye nimemchagua.’” Hata hivyo, kabla ya 1925, andiko hilo halikuwa limezungumziwa sana katika machapisho yetu. Hilo lingebadilika. Katika mwaka wa 1925, gazeti la The Watch Tower lilizungumzia andiko la Isaya 43:10 na 12 katika matoleo 11 ya gazeti hilo!
Mwishoni mwa mwezi wa Agosti 1925, Wanafunzi wa Biblia walihudhuria kusanyiko jijini Indianapolis, Indiana. Kwenye ujumbe wa kuwakaribisha uliokuwa kwenye programu ya kusanyiko, Joseph F. Rutherford alisema hivi: “Tumekuja katika kusanyiko hili . . . kuimarishwa na Bwana ili tuweze kurudi shambani tukiwa na nguvu mpya za kuwa mashahidi wake.” Katika kusanyiko hilo la siku nane, wahudhuriaji walitiwa moyo kutumia kila fursa kutoa ushahidi kumhusu Yehova.
Siku ya Jumamosi, Agosti 29, Ndugu Rutherford alitoa hotuba yenye kichwa, “Mwito wa Kuanza Kutenda Tena.” Katika hotuba yake, alikazia umuhimu wa kutoa ushahidi aliposema hivi: “Yehova anawaambia watu wake . . . : ‘Ninyi ni mashahidi wangu . . . nami ni Mungu.’ Kisha anawapatia amri hii iliyo wazi, kwa maneno haya mazito: ‘Inueni ishara kwa ajili ya watu.’ Hakuna mtu mwingine duniani anayeweza kuinua ishara kwa ajili ya watu isipokuwa [watu wake], wale walio na roho ya Bwana, na ambao ni mashahidi wake.”—Isa. 43:12; 62:10.
Trakti Ujumbe wa Tumaini
Baada ya hotuba ya Ndugu Rutherford, kwa pamoja wahudhuriaji walikubali azimio lenye kichwa, “Ujumbe wa Tumaini,” lilionyesha kwamba Ufalme wa Mungu ndio tumaini la kweli la kupokea “baraka za amani, ufanisi, afya nzuri, uhai, uhuru, na furaha ya kudumu.” Baadaye, azimio hilo lilitafsiriwa katika lugha kadhaa na kuchapishwa kwenye trakti. Nakala milioni 40 hivi zilisambazwa.
Wanafunzi wa Biblia hawakuitwa Mashahidi wa Yehova hadi baada ya miaka kadhaa kupita. Hata hivyo, waliendelea kutambua hata zaidi jukumu lao la kuwa mashahidi wake.
KUWARUDIA WALE WALIOPENDEZWA
Kadiri idadi ya Wanafunzi wa Biblia ilivyozidi kuongezeka duniani, ndivyo ambavyo walitiwa moyo zaidi kuwarudia wale ambao awali walipendezwa na habari njema. Baada ya kampeni ya kusambaza trakti Ujumbe wa Tumaini, chapisho la Bulletina lilitoa mwongozo huu: “Fanyeni mipango ili kuwarudia nyumbani wale ambao mmewaachia trakti ya Ujumbe wa Tumaini.”
Toleo la Januari 1925 la chapisho la Bulletin lilitia ndani ripoti ifuatayo kutoka kwa Mwanafunzi wa Biblia jijini Plano, Texas: “Tunashangaa kwamba tunaporudi katika maeneo tuliyohubiri mara kadhaa, mara nyingi tunapata matokeo mazuri zaidi kuliko kwenye maeneo mapya. Mji mdogo katika eneo letu umehubiriwa mara tano hivi katika kipindi cha miaka kumi. . . . Hivi karibuni, Dada Hendrix na mama yangu walihubiri katika eneo hilo na kuwaachia watu vitabu vingi zaidi kuliko wakati mwingine wowote.”
Kolpota kutoka nchini Panama aliandika hivi: “Watu wengi walionifukuza nilipowahubiria nyumbani kwao walibadili mtazamo wao nilipowatembelea kwa mara ya pili au ya tatu. Utendaji wangu mwingi mwaka huu ulihusisha kuwarudia wale niliowatembelea zamani; na nimepata matokeo mazuri sana kutoka kwa baadhi yao.”
WATAZAMIA WAKATI UJAO KWA HAMU
Katika barua yake ya kila mwaka kwa makolpota wote, Ndugu Rutherford alitoa muhtasari huu wa utendaji wa mwaka mzima na kuzungumzia kazi iliyo mbele yao. Alisema hivi: “Katika mwaka huu, tumepata pendeleo la kuwafariji wanaohuzunika. Kazi hiyo imetuletea shangwe moyoni . . . Mwaka ujao utatusaidia kupata fursa za kutoa ushahidi kumhusu Mungu na ufalme wake na kuwaonyesha wengine ni nani walio waabudu wake wa kweli. . . . Acheni sisi sote tuendelee kuinua sauti zetu na kumwimbia sifa Mungu na Mfalme wetu.”
Mwishoni mwa mwaka wa 1925, akina ndugu walikuwa wakifanya mipango ili kupanua Betheli ya Brooklyn. Mwaka wa 1926, wangeanza mradi mkubwa zaidi wa ujenzi kuwahi kufanywa na tengenezo.
Ujenzi katika Adams Street, Brooklyn, New York, 1926
a Sasa linaitwa Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo.