Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 10/1 kur. 435-439
  • Taratibu ya Kale ya Wanadamu Itakapoondokea Taratibu Mpya ya Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Taratibu ya Kale ya Wanadamu Itakapoondokea Taratibu Mpya ya Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • PIGANO LA “PEMBE KUMI” NA “MNYAMA” JUU YA MWANA-KONDOO
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 10/1 kur. 435-439

Taratibu ya Kale ya Wanadamu Itakapoondokea Taratibu Mpya ya Mungu

1, 2. (a) Babeli Mkuu itaharibiwa kwa njia gani? (b) Ufunuo 17:17 wasema nini juu ya zile “pembe kumi” na “mnyama” mwekundu sana?

“KAHABA MKUU,” Babeli Mkuu, atakapoharibiwa katika “dhiki kubwa” inayokaribia sana, sehemu ya muda mrefu ya taratibu ya kale ya wanadamu itaondoka. Milki hiyo ya Kibabeli ya ulimwengu ya dini ya uongo itaharibiwa na vipenzi vyake vya zamani. Yaani, uharibifu wake utakuja kupitia kwa “pembe kumi” za mfano zilizo juu ya “vichwa saba” vya yule “mnyama” mwekundu sana, yaani, tengenezo la mataifa yote la amani na usalama wa ulimwengu. Tengenezo hilo la baada ya vita liliundwa katika mwaka wa 1919 W.K. likaanza kutenda kwanza kwa jina la Ushirika wa Mataifa.

2 Kwa habari ya zile “pembe kumi” zinazomfanya “mnyama” awe mwenye sura ya kuogofya sana, Ufunuo 17:17 wasema hivi. “Maana Mungu ametia mioyoni mwao kufanya shauri lake, na kufanya shauri moja, na kumpa yule mnyama ufalme wao hata maneno ya Mungu yatimizwe.”

3. (a) Ni nini kinachofananishwa na “pembe kumi”? (b) Kwa habari ya uhusiano ambao ungekuwa kati ya serikali za kisiasa, Ufunuo 17:17 wasema nini?

3 Kwa kuwa na mkutano wa amani wa mwaka wa 1919 serikali mpya za kisiasa ziliundwa. Kwa njia hiyo kukawa na “pembe” za mfano nyingi zaidi baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza kuliko ilivyokuwa mara kabla yake. Wakati huo ulizo likawa la haraka, yaani, Ni uhusiano gani ambao ungekuwa kati ya serikali zote za kisiasa za ulimwengu? (Zote zilifananishwa na “pembe kumi,” kwa vile hesabu hiyo kumi hutumiwa katika Biblia kumaanisha wote, hesabu kamili.) Kwa habari ya ulizo hili, “Mungu ametia mioyoni mwao kufanya shauri lake.” Hilo lingeweza kuwaje?

4. Mungu alikuwa amekwisha kueleza “shauri lake” namna gani juu ya jambo ambalo Mataifa wangefanya, na shauri hilo lilikuwa nini?

4 Kwa mfano, Zaburi ya Pili ilieleza wazo lake juu ya hili, kwamba wafalme wa Mataifa wa dunia na wakuu wa serikali wangekutana pamoja wapingane na Yeye na mfalme wake aliyewekwa. (Linganisha Matendo 4:24-30.) Katika Danieli 2:44 alikwisha kutabiri tayari uharibifu wao wote kama wapinzani wasiogeuka wa enzi kuu yake ya ulimwengu wote. Sasa shauri lake lilikuwa kwamba yale Mataifa, yanayofananishwa na “pembe kumi,” yamepaswa yafuate bila shaka mwendo fulani wa tendo ambao ungempa yeye sababu nzuri mbele ya kuumba kote ya kuharibu mataifa hayo. Shauri lake lilikuwa kwamba imewapasa watende pamoja kama kikundi kilichoungana cha mataifa, ili apate kuwaharibu wote pamoja kwa wakati mmoja. Hili ndilo jambo hasa walilolifanya. Kwa njia hiyo twaweza kuona namna Mungu, kwa mwendo wake mwenyewe wa tendo, alivyotia mioyoni mwa zile “pembe kumi” za mfano wafanye shauri lake.

5. Kama ilivyotabiriwa, ni kazi gani ambayo inazipasa zile “pembe kumi” zifanye kama vyombo vya Yehova?

5 Zile “pembe kumi” za mfano, mataifa ambayo ni wanachama wa tengenezo la amani na usalama wa ulimwengu, zina kazi ya kufanya kama vyombo vya Yehova Mungu. Ni kazi gani hiyo? Ni kuiharibu milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, inayofananishwa na Babeli Mkuu. Malaika wa Mungu anamwambia mtume Yohana hivi: “Na zile pembe kumi ulizoziona, na huyo mnyama, hao watamchukia yule kahaba, nao watamfanya kuwa mkiwa na uchi, watamla nyama yake, watamteketeza kabisa kwa moto.”​—Ufu. 17:16.

6. Hilo litamaanisha nini kwa njia inayowezekana?

6 Hili lamaanisha kwamba miungano yo yote ya Dini na Serikali, Kanisa na Serikali, ambayo imekuwako mpaka wakati huo, itavunjwa. Makanisa yo yote ya taifa au yanayoruhusiwa na kuungwa mkono na Serikali yaliyoko mpaka wakati huo hayataungwa mkono tena na Serikali (yatatengwa na Serikali). Msamaha wa kutolipa kodi ambao serikali imetoa kwa matengenezo ya kidini utaachwa. Hata vyama vya Jumuiya ya Wakristo vya kuchapa na kueneza Biblia vitazuiwa. Kazi ya misheni ya makanisa ya Jumuiya ya Wakristo itakoma. Makasisi wa majeshi na wa makundi wataachishwa kazi. Kuadhimishwa kwa Easter na Krismas na Yom Kippur (Siku ya Upatanisho) na Sikukuu ya Kupitwa (Pasaka) kutaachwa. Utajiri mkubwa wa matengenezo ya kidini, mali zo zote zitakazosalia watekaji nyara watakapokwisha kuteka kwa nguvu wanachotaka, zitanyang’anywa na serikali za kisiasa katika taabu yao mbaya ya uchumi. Ye yote, mwanamume au mwanamke, atakayevaa vazi la pekee la kidini lenye kumtambulisha kama mshiriki wa tengenezo la kidini la Jumuiya ya Wakristo, kutamfanya ashambuliwe au akamatwe kama adui au anayetaka kuiharibu Serikali. Ijapo huenda kwa wengi ikaonekana kushangaza, Jumuiya ya Wakristo itatoweka​—milele!

PIGANO LA “PEMBE KUMI” NA “MNYAMA” JUU YA MWANA-KONDOO

7. (a) Baada ya kuharibiwa kwa Babeli Mkuu, ni mpambano gani utakaotukia? (b) Ni nini ambacho hasa mashahidi wa Kikristo wa Yehova watakuwa wakipambanisha wakati huo?

7 Ndipo​—mpambano kati ya wale watakaosalia duniani wakati huo. Yule mnyama mwekundu sana mwenye vichwa saba, pembe kumi na wakaaji wa dunia ambao bado ‘wanamstaajabia’ mnyama yule watakuwa kwenye ule upande mmoja wa shindano. Mashahidi wa Kikristo wa Yehova watakaosalia watakuwa kwenye ule upande mwingine. Kwa kuwa yule mnyama mwekundu sana ni “sanamu” tu ya yule mnyama mwenye vichwa saba, pembe kumi aliyepanda kutoka baharini na anayesujudiwa na watu wanaodhani hakuna mtu “awezaye kufanya vita naye,” hii yamaanisha kwamba wale mashahidi wa Kikristo wa Yehova watakuwa wakimpambanisha kweli kweli “mnyama” huyu wa mfano ambaye sanamu yake ilifanywa. Mnyama huyu atokaye baharini alifananisha taratibu ya kisiasa ya ulimwenguni pote ya utawala wa kibinadamu, taratibu iliyopewa “nguvu zake na kiti chake cha enzi na uwezo mwingi” na Shetani Ibilisi. (Ufu. 13:1-8) Taratibu hii ya kisiasa ya duniani pote ina mataifa 144 wanaoiwakilisha katika Umoja wa Mataifa wa kisasa, lile tengenezo la mataifa yote ambalo sasa ndiyo “sanamu” ya mnyama aliyepanda kutoka katika “bahari” ya wanadamu. Hiki ndicho itawapasa mashahidi wa Yehova wapambanishe wakati huo!

8. “Mnyama” mwenye pembe mbili “anenaye kama joka” ni nini, kama ilivyotabiriwa katika Ufunuo 13:11-13? (b) Umoja wa Mataifa unatajwa kama “sanamu” ya “mnyama” gani, na nani aliyeshauri kufanywa kwa “sanamu” hii ya kisiasa?

8 Miongoni mwa vikundi hivyo vya mataifa vilivyo na wanachama katika “sanamu” hiyo ya mnyama ni ile iliyokuwa zamani Milki ya Uingereza (British Empire) (ambayo, tangu mwaka wa 1931 W.K., imejiunda upya kama British Commonwealth of Nations, yaani, Jumuiya ya Madola ya Uingereza), na United States ya Amerika ya Kaskazini. Vikundi hivi viwili visemavyo Kiingereza vimetenda pamoja katika taabu za ulimwengu, hata vikaungana pamoja kuwa mamlaka ya ulimwengu ya mwungano wa sehemu mbili, mamlaka ya ulimwengu ya Waingereza na Waamerika, Mamlaka ya Ulimwengu ya Saba ya unabii wa Biblia. Kwa kawaida Mamlaka ya Ulimwengu ya Saba hii imefanya kazi pamoja na yule mnyama wa mfano na imetenda kama mnenaji au nabii wa taratibu ya kinyama ya kisiasa ya ulimwenguni pote. Kwa sababu hii inafananishwa katika Ufunuo 13:11-13 kama mnyama mwenye kunena kama joka anayepanda juu kutoka katika “nchi” aliye na pembe mbili kama zile za mwana-kondoo. Kwa kufaa sana mamlaka hii ya ulimwengu yenye pembe mbili au mwungano wa sehemu mbili ina uanachama katika Umoja wa Mataifa wa leo, maana ni hii Mamlaka ya Ulimwengu ya Waingereza na Waamerika iliyoshauri na kuanzisha kufanywa kwa “sanamu” ya kisiasa ya yule “mnyama” aliyepanda kutoka katika “bahari.”​—Ufu. 13:14, 15.

9. (a) Kulingana na mambo ya hakika ya historia, kuundwa kwa Ushirika wa Mataifa na Umoja wa Mataifa kulitokeaje? (b) Kwa uhakika, Umoja wa Mataifa ni wonyesho wa nini upande wa wanasiasa wa kilimwengu?

9 Wakati Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilipokuwa ikivuma, aliyekuwa wakati huo Waziri Mkuu Lloyd George alifikiria kuundwa kwa Ushirika wa Mataifa baada ya vita ili utende kama kizuizi cha vita nyingine ya ulimwengu. Aliyekuwa rais wa Amerika wakati wa vita, T. W. Wilson, alishughulika sana ili asimamishe Ushirika huo. Vilevile, katika miezi ya kumalizia ya vita ya ulimwengu ya pili, United States kama mshiriki mwingine wa yule “mnyama” mwenye pembe mbili ilisaidia kuundwa kwa mwandani wa Ushirika wa Mataifa uliokuwa umekufa wakati huo. Katika Oktoba wa mwaka wa 1945 tengenezo hili lililofanywa upya la amani na usalama wa ulimwengu likatokea kama Umoja wa Mataifa. Kwa kweli, ilikuwa ni “sanamu” ile ile ya kale ya “mnyama” wa kisiasa, lakini ikiwa na jina jipya. Ilishauriwa na kuanzishwa na wanasiasa wa ulimwengu kwa kupinga ufalme wa Kimasihi wa Mungu ambao mashahidi wa Kikristo wa Yehova walikuwa wameanza kuutangaza na kuupendekeza tangu kumalizika kwa Majira ya Mataifa katika mwaka wa 1914.

10. (a) Basi, kulingana na maana halisi ya Ufunuo, sura ya 17, ni nini ambacho mashahidi wa Kikristo wa Yehova watapaswa wapambanishe baada ya kuharibiwa kwa Babeli Mkuu? (b) Ni serikali gani ambayo Mashahidi hawa wanawakilisha?

10 Kwa msaada wa hayo yaliyotangulia, wakati Ufunuo, sura ya kumi na saba, inaposema juu ya “mnyama” mwekundu sana, mwenye vichwa saba, pembe kumi, imetupasa tufikirie nguvu yenyewe inayoongoza “sanamu” hii ya mfano, yaani, taratibu ya ulimwenguni pote ya kisiasa ya serikali inayofananishwa na yule mnyama aliyepanda kutoka baharini. Yule mnyama mwenye pembe mbili aliyepanda kutoka katika nchi, yaani, Mamlaka Mbili za Mwungano za Ulimwengu za Waingereza na Waamerika, ndiyo sehemu kuu yenye kuongoza ya taratibu kubwa zaidi ya kisiasa inayofananishwa na mnyama wa baharini. Kwa hiyo, mataifa yaliyo wanachama wa ile “sanamu” ya mfano watakapokwisha kuharibu Babeli Mkuu wa kidini, ni taratibu ya ulimwenguni pote isiyo ya kidini ya serikali ya kisiasa ambayo mashahidi wa Kikristo wa Yehova itawapasa wapambanishe. Watakuwa wangali wakisimama imara kwa ajili ya ufalme wa Kimasihi wa Mungu kama utawala peke yake wa ulimwengu wa wanadamu ulio na haki. Ni serikali hii ya kimbinguni wanayowakilisha. Kwa kweli, mabaki waliotiwa mafuta ya Waisraeli wa kiroho ndio “mabalozi” wa serikali ya Kimasihi.​—2 Kor. 5:20; Efe. 6:20, NW.

11. (a) “Aina ya dini” itakayobaki baada ya kuharibiwa kwa Babeli Mkuu itakuwa ipi? (b) Dini hii inahusuje maoni ya mtu juu ya kujitia katika mambo ya kisiasa ya ulimwengu, na kwa sababu gani?

11 Sehemu ya kwanza ya “dhiki kubwa” iliyotabiriwa na Yesu Kristo itaishia na uharibifu wa Babeli Mkuu wa kidini. (Mt. 24:21, 22; tazama pia Danieli 12:1.) Sasa hali yenye hatari itakuwa imefikiwa duniani! Mashahidi wa Kikristo wa Yehova wasaliao watakuwa ndio waabudu peke yao wa Mungu mmoja aliye hai na wa kweli, Muumba mbingu na dunia. Namna yao ya ibada ndiyo “dini” ambayo sasa serikali za kisiasa zenye mageuzi zimekuwa haziwezi kuifutilia mbali; na itakuwa hivyo kwa sababu hii ndiyo “aina ya dini isiyo na madoa au kasoro machoni pa Mungu Baba yetu.” (Yak. 1:27, The New English Bible) Mataifa yasiyomwabudu Mungu hayataridhika mpaka waone “aina ya dini” hii inafutiliwa mbali itoke katika dunia. Ni hii “aina ya dini” ndiyo imefanya mashahidi wa Kikristo wa Yehova wasaliao wasichangamane na mpango mpya wa kisiasa, wasiwe “sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19; 17:14, 16, NW) Wakati wote wao wako upande wa enzi kuu ya ulimwengu wote ya Mungu, Yehova Aliye Juu Zaidi.

12. (a) Ni ulizo gani litakalolazimisha kujibiwa wakati huo? (b) Mataifa yataonyeshaje kwamba wameungana katika upinzani wao juu ya ufalme wa Kimasihi wa Mungu?

12 Ulizo lenye kusumbua sana, Nani atakayeitawala dunia pasipo ushindani? sasa limefikia kiasi cha kutokeza matata. Mataifa yasiyo ya kidini yamekaza moyo sana kwamba ufalme wa Kimasihi wa Mungu hautachukua utawala wa dunia yote, ambayo wanadai kuwa eneo lao. Kwa umoja, kana kwamba kwa njia ya tengenezo la Umoja wa Mataifa, wataonyesha upinzani wao wa kushinda au kushindwa juu ya ufalme wa Kimasihi wa Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu, ulio mikononi mwa Mwana-Kondoo wake, Yesu Kristo. Mwisho wa “nyakati za Mataifa” katika mwaka wa 1914 hauna maana kwao. Watakataa kuondoka, watakataa kuzikabidhi enzi zao za kitaifa kwa Mfalme wa Kimasihi wa Mungu aliyewekwa, Mwana-Kondoo. Hawatakubali kamwe pasipo vita, na mataifa yenye silaha nyingi za atomiki yanajiona kuwa na uwezo mwingi na tayari kwa mpambano huo. Haya, sasa, kwenye mpambano wa kushinda au kushindwa!

13. Eleza masimulizi ya mambo haya kama yanavyopatikana katika Ufunuo 17:12-14.

13 Ufunuo 17:12-14 wasema juu ya vita hii ya vita vyote vya vizazi vyote: “Zile pembe kumi ulizoziona ni wafalme kumi [mamlaka zote za kisiasa za kidunia] ambao [katika siku za Yohana] hawajapokea ufalme [kwa kuwa wanachama wa Ushirika wa Mataifa​—Umoja wa Mataifa] bado, lakini wapokea mamlaka kama wafalme muda wa saa moja pamoja na yule mnyama. Hawa wana shauri moja, nao wampa yule mnyama [tengenezo la ulimwengu la amani na usalama] nguvu zao na mamlaka yao. Hawa watafanya vita na Mwana-Kondoo, na Mwana-Kondoo atawashinda, kwa maana Yeye ni Bwana wa Mabwana, na Mfalme wa Wafalme; na hao walio naye ndio walioitwa, na wateule, na waaminifu.”

14. Je! watawala wa kisiasa wataweza kumwona Mwana-Kondoo Yesu Kristo ili wapigane naye hasa, na mtume Paulo anaonyeshaje hili?

14 Mtume Paulo asimulia juu ya Mwana-Kondoo huyu wa Mungu ambaye wakati mmoja alitolewa dhabihu sasa akiwa katika hali yake tukufu, alipokuwa akimwandikia mmisionari mwenzake Timotheo na kusema: “Nakuagiza mbele za Mungu anayevihifadhi hai vitu vyote, na mbele za Kristo Yesu, aliyeyaungama maungamo mazuri yale mbele ya Pontio Pilato [liwali wa Kirumi wa Uyahudi], kwamba uilinde amri hii pasipo mawaa, pasipo lawama, hata kufunuliwa kwake Bwana wetu Yesu Kristo; ambako yeye kwa majira yake atakudhihirisha, yeye aliyehimidiwa, Mwenye uweza peke yake, Mfalme wa wafalme, Bwana wa mabwana; ambaye yeye peke yake [kati ya mabwana na wafalme hao wote] hapatikani na mauti, amekaa katika nuru isiyoweza kukaribiwa; wala hakuna mwanadamu aliyemwona [katika hali yake tukufu ya kutopatikana na mauti], wala awezaye kumwona.” (1 Tim. 6:13-16) Kwa hiyo, zile “pembe kumi” za mfano za yule “mnyama,” Umoja wa Mataifa, hazitaweza kumwona Mwana-Kondoo Yesu Kristo ili kupigana naye moja kwa moja juu ya suala la utawala wa ulimwengu.

15. Basi, wale “wafalme kumi” wataelekeza shambulio lao juu ya nani?

15 Walakini, lile pigano ambalo “wafalme kumi” watapigana litaelekezwa juu ya wale walio wajumbe waonekanao wa kidunia wa Mwana-Kondoo wa kifalme, Yesu Kristo. Hawa watakuwa mashahidi wa Kikristo wa Yehova, kutia na mabaki waliotiwa mafuta wa Waisraeli wa kiroho na ule “mkutano mkubwa” wa watangazaji walio wakf wa “habari njema ya ufalme.” (Mt. 24:14) Ijapokuwa uchafu wa ulimwengu na taabu ya mataifa, hawa watakuwa bado wanajifurahisha paradiso ya kiroho yenye kibali ya Mungu, ulinzi na ibada safi pamoja na matunda yote ya roho Yake katika maisha zao.

16. Mataifa wanaposhambulia wanafunzi waaminifu wa Yesu, wanafanya vita juu ya nani hasa?

16 Mwana-Kondoo Yesu Kristo alisema maneno katika unabii wake juu ya “mwisho wa taratibu ya mambo” ili watiwe moyo, na maneno hayo yalikuwa kwamba lo lote alilotendewa “mmojawapo wa hao ndugu zangu” za kiroho lilikuwa kana kwamba alitendewa Mfalme mwenyewe. (Mt. 24:3, NW; 25:40) Sasa, kanuni hiyo ingali yatumika wakati tumo hasa katika kipindi hicho cha “mwisho wa taratibu ya mambo.” Basi, katika kufanya vita juu ya wanafunzi waaminifu wa Yesu Kristo kwa kusudi la kuwaangamiza, mataifa yanafanya vita na Mwana-Kondoo aliyetukuzwa wa Mungu. Hivyo mashahidi wa Kikristo wa Yehova watafahamu kwamba vita hiyo si juu yao hasa, bali yafanywa juu ya Mungu na Mwana-Kondoo wake.

​—Kutoka Kitabu Man’s Salvation Out of World Distress at Hand!, sura ya 14.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki