Mwenendo Mzuri—Ushuhuda Wenye Nguvu
KUMPENDA sana Yehova Mungu na wanadamu wenzao kunawaongoza Wakristo wa kweli wajiendeshe wenyewe katika njia yenye kusifika. Mwenendo wao mzuri ‘unayapamba mafundisho ya Mungu.’ (Tito 2:10) Unafanya mafundisho hayo yawe yenye kuwavutia watu wenye mioyo minyofu. Kwa kweli, wengi ambao sasa wanashirikiana na mashahidi wa Yehova wa Kikristo kwanza walivutwa kwenye ujumbe wa Biblia kwa kutazama ushuhuda wenye nguvu ukitolewa kwa mwenendo wenye kusifika.
● Alipokuwa akifanya kazi Forodhani katika Atlanta, Georgia, mwanamke alikutana na mmoja wa mashahidi wa Yehova. Kwa habari ya Shahidi huyu, anaandika hivi: “Kulikuwako jambo fulani lililokuwa tofauti sana juu ya mwanamke huyu. Adabu na mwenendo wake vilikuwa tofauti karibu na wanawake wote wafanya kazi. Tukafanya urafiki na, wakati wa maongezi fulani, akaniambia kwamba alikuwa mmoja wa mashahidi wa Yehova.
“Ijapokuwa kwanza hili lilionekana jambo geni kwangu, nilitaka nisikie zaidi juu yake. Wakati alipojibu maulizo yangu mengi, nikafahamu kwamba hakika hii ilikuwa kweli.”
Leo hii mwanamke huyu ni shahidi wa Yehova, aliyejiweka wakf na kubatizwa vile vile.
● Msimamizi wa mkahawa mkubwa katika United States alipendezwa sana wakati Shahidi alipoanza kufanya kazi huko. Wapishi na waendeshaji wa magari 25 na kati ya wanawake 50 na 75 walikuwa wakifanya kazi katika mkahawa. Lakini Shahidi ndiye aliyekuwa tofauti na wengine wote. Muda si muda akajulikana kama mmoja wa wafanya kazi bora. Yeye hakutukana wala kuvuta tumbako, kushiriki katika mazungumzo yasiyofaa wala kuhudhuria karamu zo zote wakiisha kumaliza kazi hata kidogo. Vile vile yeye alivitumia vile vipindi vya kupumzika kwa faida nzuri apate kufikiria mambo ya Biblia.
Yote haya yalimpendeza sana msimamizi. Alijaribu amsaidie kwa kutoa kwake nafasi ya kupumzika wakati wa sikukuu za kidini. Lakini Shahidi huyu alikuwa akizikataa nafasi hizi, sikuzote akieleza kwa Maandiko sababu gani asingezishiriki.
Mwisho yule msimamizi alianza kuuliza maulizo zaidi. Akiona kupendezwa kwake, Shahidi alimwelekeza kwa mmoja wa Mashahidi wanaume, na funzo la nyumbani la Biblia lilianzishwa pamoja na yeye.
Halafu, msimamizi huyu akamwoa Shahidi ambaye mwenendo wake ulikuwa umemvuta, akaacha kazi yake ya msimamizi na, kama shahidi wa Yehova aliyebatizwa, akaingia huduma ya “upainia.” Sasa kwa muda wa miaka kumi na mitatu amekuwa akitumikia kama mwangalizi asafiriye.
● Akisimulia mambo ambayo yeye mwenyewe aliona, Shahidi kutoka California anasema hivi: “Watu wanapofikiri juu ya mashahidi wa Yehova wanafikiria utendaji wao wa mlango kwa mlango. Lakini sivyo ilivyokuwa na mimi. Mimi nilifikiwa na Shahidi shuleni. Hatukuwa katika darasa moja au urafiki wo wote. Lakini nilimtazama toka mbali. Nikaweza kujua kwamba alikuwa tofauti na jambo hili lilinipendeza mimi.
“Siku moja Shahidi huyu akanifikia mimi na dada yangu pacha akauliza kama tungependa kujifunza Biblia pamoja naye. Mimi nikakubali kwa vyepesi, lakini dada yangu hakuona maana. Wakati wa mafunzo yetu, nilipomjua sana Shahidi huyu, niliweza kuona kwamba maoni yake yote juu ya maisha yalikuwa tofauti. Alikuwa bila wasiwasi bali mwenye furaha na uradhi. Alikuwa mwenye maisha safi yenye adili na alikuwa hashughuliki na shughuli za baada ya shule.
“Kulipopita muda kidogo dada yangu pacha akaacha kujifunza lakini mimi nikaendelea. Dada yangu aliendelea kunivunja moyo na akaniwekea vikwazo. Ndugu yangu vile vile alinivunja moyo, zaidi alipoona nilivyoanza kuacha namna nilivyokuwa nikivaa. Hata baba yangu alijaribu kunizuia nisijishughulishe.
“Wakati ulipoendelea nikaanza kuona tofauti zaidi kati ya mashahidi wa Yehova na ulimwengu. Kwa mfano, penye kusanyiko langu la kwanza kuhudhuria kweli nilianza kuona tofauti kati ya urefu wa kadiri wa marinda na mavazi ya Mashahidi na urefu wa mavazi yangu, yaliyokuwa kama ya ulimwengu. Kwa kweli, niliona haya sana kwa sababu ya hili hata siku nzima ya mwisho wa kusanyiko nikavaa eproni ili nifiche rinda langu fupi.”
Leo kijana huyu wa kike, pamoja na yule Shahidi ambaye alikutana naye shuleni, anashiriki katika huduma ya wakati wote kama painia. Anashukuru sana kwa vile alimwona mtu fulani shuleni aliye tofauti, mtu fulani aliyeonyesha Ukristo katika kila njia.
Kwa wazi mwenendo mzuri wa Kikristo unatoa ushuhuda wenye nguvu na unasaidia sana kutoa tangazo la hadhara la kweli ya Biblia. Je! hili si jambo la kutosha kuwatia Wakristo wa kweli moyo zaidi waache kumpenda kwao Mungu na jirani kuwaongoze waendeleze mwenendo mzuri katika nyakati zote?