Je! Wewe Unaishi kwa Ajili ya Kile Uwezacho Kupata Katika Maisha Sasa?
“Ikiwa wafu hawatafufuliwa, ‘na tule na kunywa, kwa maana kesho tutakufa.’ Msipotezwe. Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri.”—1 Kor. 15:32, 33, NW.
1. Viumbe vya kibinadamu vinaonyeshaje vinaona ubora wa kuwa na uhai, lakini ni tukio gani linalowapata walio hai wote?
UHAI! Lo! namna ulivyo mali yenye thamani sana! Akili na mwili wa kibinadamu vimefanywa kwa ajabu. Hapana mtu mwenye akili nzuri anayetaka aukomeshe uhai, bali anataka aendelee kuishi, hata yangawa magumu yenye kuongezeka na mikazo ya ulimwengu leo. Kuna tamaa hiyo yenye nguvu ya kushikilia zawadi hii ya uhai yenye thamani sana, kuendelea kujifunza juu na kujifurahisha mambo yaliyo karibu yetu. Jitihada zenye azimio zinafanywa ili kuizuia mauti na kuwa na afya na furaha ya kutosha. Lakini, kwa kuendelea na pasipo huruma mauti inamfikia kwa siri kila mwanadamu katika muda wake mfupi wa maisha wa karibu miaka 70. Kaburi nalo linameza wenye haki na vile vile waovu, wenye kuishi maisha ya kujinyima mambo ya anasa na vile vile wenye kuishi maisha ya upotevu.—Zab. 89:48.
2. Wengi wamekuwa na maoni gani, na haya yanaonyeshwaje kwa namna wanavyoenenda wenyewe?
2 Kwa sababu ya misiba ya maisha na kukaribia sana kwa mauti, huenda kutokana na maoni ya kimwili, kuwaza kwa kibinadamu mtu akaona kuwa jambo linaloelekea kuwa si la kweli: Kuishi maisha mema yenye adili kungeonekana kuwa kusiko na maana, kusikothawabisha. Kwa watu wengi, maisha yatakayofuata kufa ni hadithi tu ya uongo. Ikiwa uzima ndio uu huu tu, basi sababu gani usipate yote uwezayo kupata ndani yake wakati ungali waishi? Ikiwa akili bora inasema, ‘Jizuie mwenyewe na ujiepushe na vitu vyenye kudhuru, ingawa ni vyenye kupendeza sana,’ kuwaza kwa kibinadamu kunapingana na hilo kwamba ni bora kujifurahisha hivi na kufurahi sana kuliko kuishi maisha ya kujinyima na yenye vizuizi, kwa sababu utakufa, utaoza na kusahauliwa tu na vizazi vya wakati ujao kama kila mtu mwingineo. Kuna ubora gani katika kujinyima? Oh, ndiyo, ikiwa unajizoeza ambayo kwa adili ni mema, huenda zikawako faida fulani za afya na huenda magumu fulani yakaepukwa. Vile vile, kuna kumbu-kumbu ya kwamba muda wa maisha ambao umekwisha kupunguzwa huenda ukapunguzwa hata zaidi na matendo mabaya yanayofanywa; lakini heri kujifurahisha haya kwa kadiri uwezavyo, ndivyo wengi wanavyowaza, kuliko kuishi miaka michache zaidi ya unyonge na yenye taabu wakati wa uzee.
3. (a) Ni maulizo gani yanayojitokeza yenyewe kwa sababu ya kupingana kati ya filosofia ya ulimwengu huu na Biblia? (b) Paulo ananyoshaje mambo juu ya kuishi kwa ajili ya anasa za kichoyo tu?
3 Kwa sababu ya yote haya, Biblia inasema hivi: “Mtu mwaminifu atakuwa na baraka tele.” (Mit. 28:20) Je! hii ni kweli? Kwa kutoa kanuni za juu za adili ili kuongoza mwenendo wa mwanadamu, je! Biblia inasema yanayoweza kutendeka? Ikiwa mtu anajitahidi kuzifuata hizi, je! kweli itamfaidi? Tena, ikitukia mauti, je! mtu anaweza kwa uhakika kutumainia maisha bora nyumaye kwa sababu ya matendo yake ya uaminifu? Ikiwa mwanadamu angekuwa zao tu la maendeleo yenye mageuzi, pasipo kuwa chini ya daraka la mtu juu ya ambavyo angejiendesha mwenyewe isipokuwa jamii ya watu ambayo yeye ni sehemu yake, basi kanuni na ahadi za Biblia zingelaumiwa sana. Hili ndilo jambo ambalo mtume Paulo anasema katika kuwaandikia Wakristo katika Korintho: “Ikiwa wafu hawatafufuliwa, ‘na tule na kunywa, kwa maana kesho tutakufa,” Upesi Paulo anaendelea kusema juu ya wazo hili la kichoyo sana kwa kuonya hivi: “Msipotezwe. Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri. Amkeni mkiwa makini katika njia ya haki na msijizoeze dhambi, kwa maana wengine hawana maarifa ya Mungu. Mimi ninasema ili niwatahayarishe.”—1 Kor. 15:32-34, NW.
4. (a) Ilikuwa filosofia gani ya Waepikureo? (b) Ibrahimu na watu wengine wenye imani walionyeshaje kwamba hawakuwa na maoni haya juu ya maisha na wakati ujao?
4 Wakati alipokuwa katika Ugiriki, Paulo alikutana na filosofia hii ya Waepikureo, waliosadiki kwamba imempasa mtu aishi katika njia hiyo ili ajipatie raha zaidi katika maisha, lakini afanye hivyo kwa kadiri ndogo ili aepuke taabu inayoletwa na kufuata mno anasa. Hawakufikiria sana wakati ujao isipokuwa kuendelea kujifurahisha anasa mpaka kufa. Lakini hivyo sivyo watu waaminifu kama Ibrahimu walivyoona juu yake. Juu ya hawa, Paulo aliandika hivi: “Hawa wote wakafa katika imani, wasijazipokea zile ahadi, bali wakaziona tokea mbali na kuzishangilia, na kukiri kwamba walikuwa wageni, na wasafiri juu ya nchi.” Wao hawakuipoteza imani na kujitia katika mazoea maovu yaliyokuwa karibu nao. Katika kumbukumbu la Mungu wako hai sana na karibuni Mungu atawafufua kwenye uzima ulio kweli kweli katika dunia ya paradiso chini ya utawala wake wa Ufalme.—Ebr. 11:13; Mt. 22:31, 32; Yohana 6:39, 40.
5. Biblia inatofautishaje matokeo ya kuishi ili kutosheleza mwili na kuishi kwa kiroho?
5 Ni vyepesi kujidanganya wenyewe kutenda kosa au kukosa uwezo wa kujiadibishia wenyewe ili tupate faida zenye kuendelea za mwendo mzuri wa tendo ikiwa tumesitawisha tamaa moyoni. Ni mazoea ya watu wote kujaribu kutoa sababu za kuonyesha mwendo huo kuwa wenye akili. Tena Paulo anashauri kwa maneno haya, “Msidanganyike,” kisha anaongeza hivi: “Mungu hadhihakiwi; kwa kuwa cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna. Maana yeye apandaye kwa mwili wake, katika mwili wake atavuna uharibifu; bali yeye apandaye kwa [roho, katika roho] atavuna uzima wa milele.” (Gal. 6:7, 8) Wale ambao wameshirikiana na mashahidi wa Yehova na ambao wamefuatisha maisha zao na yale ambayo Biblia inafundisha wanaweza kushuhudia kwamba wamebarikiwa sana hata sasa. Kwa sababu wao hawaishi maisha ya kujiachilia, wanaepuka matokeo ya kuogofya ya mwendo huo, matokeo ambayo mara nyingi yanatia mauti ya mapema. Zaidi ya hili, wamewekewa akiba ya uzima wa milele ikiwa wanaendelea na mwendo huu kwa uaminifu.—Rum. 6:23.
6. Kwa sababu gani imekuwa haraka hata zaidi leo kuwa macho na kuangalia mwenendo wetu?
6 Tunapolinganisha Maandiko na mambo yanayotukia karibu na sisi, hakuwezi kukawako shaka kwamba sisi tumeendelea sana kuwa katika wakati na mwisho wa taratibu hii isiyomwogopa Mungu. Wakristo wanaweza kuthibitisha kwamba Biblia inasema sawasawa wakati inapotuambia ya kwamba ingekuwa vigumu hata zaidi katika wakati huu kuendelea katika njia nyembamba inayoongoza kwenye uzima. Vishawishi vya kisasa vya ulimwengu ni vyenye nguvu na Ibilisi hajapoteza ujanja wake katika kuwadanganya na kuwaongoa wasiojihadhari. Sikuzote kuna hatari ya kurudia katika violezo vya kale vya kufikiri na mwenendo au kuziacha tamaa mpya zisizopendeza kwa Yehova zisitawi. Moyo ni mdanganyifu, mwili ni dhaifu, kujiadibisha si kwepesi. Katika unabii wake juu ya mwisho wa taratibu hii, Yesu alionya hivi: “Basi, jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajia ghafula, kama mtego unasavyo; kwa kuwa ndivyo itakavyowajilia watu wote wakaao juu ya uso wa dunia nzima.”—Luka 21:34, 35.
7. Kufikiri na maoni ya ulimwengu huu yanawezaje kuanza kwa werevu kumvuta Mkristo? Imetupasa sikuzote tujikumbushe wenyewe juu ya nini?
7 Ili tuhakikishe kwamba hatudanganywi au kunaswa kana kwamba katika mtego, inatupasa tujiulize wenyewe maulizo yenye kuchunguza ili tuyajaribu makusudi yetu ya ndani-ndani, tamaa zetu za kisiri, mapenzi yetu yaliyositirika. Tunaishi kwa ajili ya nini? Ni jambo moja kusema tunaishi kwa kutumainia uzima katika taratibu mpya ya Mungu, lakini ni jambo jingine kuishi hasa kupatana na matakwa ya Mungu kila siku. Wakristo hawawezi kuiacha filosofia yenye werevu ya Waepikureo ya ulimwengu huu iwadanganye na, mbele ya wao kujua, waanze kuishi kwa ajili ya anasa za leo, wasije wakafa kesho. Au, wakiwa na mashaka juu ya kuamua kuishi katika Taratibu Mpya, huenda wakaanza kuona uzuri wa anasa za ulimwengu huu, wasitake kuzikosa kabisa. Inatupasa tujiulize wenyewe sikuzote hivi: Tunaishi kwa ajili ya nini? Kwa ajili ya anasa za ulimwengu huu au kwa ajili ya “uzima ulio kweli kweli” katika taratibu mpya ya Mungu?—1 Tim. 6:17-19.
JE! WEWE WAISHI KWA AJILI YA ANASA ZA KUNYWA?
8, 9. (a) Kwa sababu gani wengi wanafanya anasa hata wakalewa? (b) Ni matokeo gani mabaya yametokana na ulevi?
8 Mamilioni ya Waepikureo wa kisasa wamezidi mno kunywa hata wanalewa. Wameonja matokeo ya kupita kadiri katika matumizi ya vileo, na hivi ndivyo wanavyotaka bila kujali gharama au hasara za afya, kazi na jamaa. Haya na vizuizi vinaondok’a, kuleta hali ya kutosumbuliwa. Mambo ya ukali yanageuka kuwa mambo yenye furaha sana. Masumbuo yanaondoka. Choko-choko inaondolewa kabisa; kuwa na daraka kunaachiliwa mbali. Kwa kweli, mtu anaona raha sana na kusahau masumbuo ya maisha. Lakini, je! haya ndiyo maisha kweli? Ukifikiria hali ya kuzimia ambayo ndani yake mtu amekuwamo, mwenendo na usemi wa aibu ambao huenda amekuwa na hatia yake, maumivu makubwa mno ya mwili wakati wa kulevuka na hasara ambayo amefanya juu ya ujamaa wake na wengine, jibu la busara lingepaswa liwe lenye nguvu sana, Hapana’—Mit. 20:1; 23:20-35.
9 Ni jambo la busara kwamba Mungu angeona inafaa kukataza ulevi. Wakati wa ulevi akili hazifanyi kazi sawasawa na mara nyingi mtu anafanya mambo yenye aibu. Kuna mengi mno ambayo yeye anajiona anaweza kuyafanya, kumbe ukweli wenyewe ni kwamba akili na uamuzi wake vimeharibika sana. Makumi ya maelfu wanakufa kila mwaka kwa sababu mlevi alidhani alikuwa na akili ya kutosha kuendesha gari lake afike kwake au akajitia katika matata kwa sababu ya jambo dogo sana. Mamilioni wanakufa kwa ugonjwa wa ini, kuweweseka na magonjwa mengine yanayokamatana na ulevi. Katika nchi nyingi, ugonjwa unaotokana na vileo unapangwa kama mwuaji Namba 3, kufuata ugonjwa wa moyo na ugonjwa wa donda baya.
10. (a) Ingawa huenda mtu asilewe, kuna hatari gani katika kuvitumia mno vileo? (b) Imempasa mtu afikirie nini wakati hajawakaribisha wageni wake kwa vileo?
10 Lakini, ijapokuwa huenda mtu asiwe akilewa, huenda kwa kweli akawa akinywa kwa anasa sana, na hii ndiyo hatari kubwa kwa Wakristo. Si watumiaji wote wa vileo ambao ni walevi. Ugonjwa wa vileo ni tamaa ya kutaka sana vileo. Jaribu zuri ni kujiuliza mwenyewe hivi, Je! mimi ninaishi kwa ajili ya anasa hii na kila siku kutamani sana hali ya kujiona mwenye raha sana ninayopata kutokana na unywaji wa vileo? Ijapokuwa kunywa ni shauri la kipekee ikiwa mtu halewi, inaelekea kwamba kileo kitakuwa ni kitu ambacho mtu anategemea sana, kitu cha lazima ambacho hawezi kuishi bila hicho. Tena, kuna kuelekea kwa kuwakwaza wengine kwa matumizi yasiyo ya busara ya vileo. Wakati rafiki wanapokutembelea jioni, je! wewe unasisitiza kwamba washiriki vileo pamoja na wewe, wajapokuwa hawataki kufanya hivyo? Huu waweza kuwa ukaribishaji mbaya na huenda ikawa ni kutaka kuwashawishi wengine wajiunge nawe katika udhaifu. Kusiwe watu wa kulazimishwa au kushawishwa kunywa ikiwa hawataki kufanya hivyo. (Rum. 14:17-21) Si lazima kukutana huku kwa starehe kuwe kusikopendeza ikiwa vinywaji vya namna hii havitolewi. Kwa hakika ikiwa mtu anakunywa kwa kadiri tu, ikiwa mtu anachagua kunywa, naye haishi kwa kusudi la kupata raha isiyofaa kutokana na vileo, atakuwa na baraka nyingi.
JE! WEWE WAISHI KWA AJILI YA ANASA ZA MASHIRIKA YA KILIMWENGU?
11. Ni tamaa gani kwa habari ya ushirika ambayo Yehova alitia katika mwanadamu, na imetupasa tukumbuke nini katika kuitosheleza tamaa hii?
11 Wakati Yehova alipomwumba mwanadamu, Yeye alitia ndani yake tamaa yenye nguvu ya kushirikiana. Akiwa peke yake kwa muda wo wote mrefu, kwa asili mwanadamu anatamani awe pamoja na viumbe vyenzake vya kibinadamu, vya kusema navyo, vya kula navyo, vya kucheza navyo, vya kufanya kazi pamoja navyo, ndiyo, awe mbele ya wengine ambao, kama yeye mwenyewe wanahitaji ushirika. Kifungo cha upweke ni adhabu isiyo na huruma. Walakini, inawapasa Wakristo wawe wateuzi katika kuchagua washiriki wao. Haikuwa kwa bahati tu kwamba Paulo akatia maneno, “Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri,” alipokuwa akipinga filosofia ya Waepikureo yenye kuenea ya wakati huo: “Na tule na kunywa, kwa maana kesho tutakufa.” Mkristo angechukua kufikiri huko wapi isipokuwa katika kushirikiana na wale ambao wangekuamini na kukuzoea? Inawapasa Wakristo wajue kwamba kuna namna mbili zilizo mbalimbali za uvutano leo—Aina ya Kimungu, ya kitheokrasi, ya Kikristo, na ile ambayo ni ya kilimwengu, ya kidunia na isiyo ya Kikristo.
12. Jambo gani linalokubaliwa juu ya kushirikiana na ulimwengu, lakini ni lazima mpaka uwekwe wapi katika kushirikiana na watu wa kilimwengu?
12 Bila shaka, Wakristo wanazungukwa na watu wenye fikira za kilimwengu na hali ya ulimwengu huu. Katika kusali kwa Yehova kwa ajili ya wafuasi wake, Yesu alisema: “Siombi kwamba uwatoe katika ulimwengu; bali uwalinde na yule mwovu. Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.” (Yohana 17:15, 16) Ingempasa mtu aishi kama mkaa peke yake, ajitenge kabisa na jamii ya kibinadamu, ikiwa angeepuka asishirikiane kabisa na walimwengu. (1 Kor. 5:9-13) Walakini, zaidi ya ushirika ambao ni wa lazima kabisa katika kazi zetu za kimwili, shuleni, wakati mtu anapokuwa katika huduma ya shambani, au katika nyakati nyingine, haifai iweko tamaa yo yote ya kujihatirisha wenyewe na fikira zenye kuharibu na mara nyingi mwenendo mbaya wa walimwengu.—Kum. 7:3, 4.
13. (a) Huenda ndugu akatoa sababu namna gani ikiwa ana kazi inayotaka kushughulika na watu wa kilimwengu? (b) Huenda dada akatoa sababu gani ikiwa mwanamume asiyeamini anaonyesha kupendezwa naye? (c) Kwa sababu gani shauri la Biblia kuoa “katika Bwana tu” ni lenye kufaa?
13 Kwenye akili hili ni shauri lenye kufaa na jema, lakini hatari inatokea wakati hali zinapojitokeza zenyewe ambapo mashirika ya kilimwengu yanapoonekana kuwa yenye kutamanika kwa moyo. Kwa mfano, huenda ndugu akawa na kazi ya kimwili na anaona ni lazima ashirikiane sana na walimwengu, awakaribishe, na vivyo hivyo. Huenda akatoa sababu za kuonyesha kwamba ushirika huo ni wa lazima ili aendeshe kazi yake inayotumiwa kumpatia yeye na jamaa yake riziki. Fikiria, tena, hali ya dada aliyemo katika kundi ambaye huenda anataka kuolewa. Huenda wasiweko ndugu wengi katika rafiki zake za Kikristo wenye umri wa kuoa. Yeye anafahamu sana kwamba anazidi kuzeeka. Huenda mwanamume ambaye amejuana naye kwa miezi fulani kazini pake akaonyesha kupendezwa naye. Ikiwa dada huyu anapendezwa na mwanamume huyo, mara hiyo akili na moyo vinaanza kutoa sababu za kuonyesha kufaa kwa kupendezwa naye. Huenda akawa ni mwanamume mwenye urafiki, mzuri sana. Hanywi pombe wala kuvuta sigara. Yeye hachukii dini. Huenda hata ukasikia ikisemwa kwamba yeye ana hali ya urafiki mzuri kuliko na wengine kati ya ndugu za Kikristo anaowajua. Au kutaja mfano mmoja wakati dada mwingine alipoolewa na mtu asiyeamini na mwisho mwanamume huyo akasaidiwa akawa Mkristo. Labda lilo hilo laweza kufanywa wakati huu. Walakini, taabu ambazo zimewapata wengi zinakubaliana na Biblia hapa katika kuonyesha kwamba kuelekea kwa jambo hili kuwa hivyo ni kudogo sana. Pahali pake, kuna uwezekano wenye nguvu wa kwamba yule asiyeamini atamgeuza Mkristo na kutoka katika njia ya uzima. Kutii kwa mtu amri ya Biblia kuoa “katika Bwana tu” kutataka kujiweza na uvumilivu, lakini sikuzote tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anajua kilicho chema kwa watu wake. Yeye anataka si kuwalinda na maumivu mengi yanayofuatana na mwendo usio wa hekima tu, bali vile vile anataka watu wake wawe wenye furaha.—1 Kor. 7:39, 40.
14. Ni vishawishi gani vinavyowapata vijana hasa?
14 Vijana wanalo shawishi kubwa la kushirikiana na vijana wa kilimwengu wenye umri kama wao wenyewe. Mara nyingi wanasongwa ili washiriki katika vikundi vya michezo, vyama vya michezo na magenge. Kuna tamaa ya kutaka kukubaliwa na mara nyingi, ili akubaliwe, inampasa mtu aonyeshe kwamba atakuwa akifanya mambo yasiyo ya haya na hata yasiyo ya maandiko. Ni vyepesi kufuata mitindo ya kilimwengu katika kujipamba na mavazi, au kushawishwa kuchukua gazeti lenye kuvuta macho sana na lenye kuvuta tamaa za kimwili. Vile vile kuna kishawishi cha televisheni au sinema zinazoonyesha jeuri, kukazia mambo ya ukatili au kutukuza mambo ya kiume na ya kike. Vile vile, wako watungaji wa vitabu juu ya filosofia, walaumu, na wengineo, ambao sisi hatutaki tushirikiane nao. Ikiwa tunavisoma vitabu hivi, inakuwa kama kuketi mbele yao na kuwaacha wazijaze akili zetu mawazo yao juu ya uzima.—1 Kor. 3:18-20; 1 Tim. 6:20, 21.
15. Ni shauri gani zuri linalotolewa katika Maandiko juu ya ushirika, na kulitii hili ni faida na ulinzi namna gani kwa Wakristo?
15 Wakristo waaminifu wanaisadiki Biblia wakati inaposema: “Basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu.” (Yak. 4:4) Wanaona busara nzuri katika amri hii: “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa; kwa maana pana urafiki gani kati ya haki na uasi? Tena pana shirika gani kati ya nuru na giza? Tena pana ulinganifu gani kati ya Kristo na Beliari [Shetani]? Au yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini? Kwa hiyo, tokeni kati yao, mkatengwe nao, asema [Yehova], msiguse kitu kilicho kichafu, nami nitawakaribisha.” (2 Kor. 6:14, 15, 17) Wakitii shauri hili, hawajiachi wenyewe washawishwe katika kushirikiana sana na wasioamini nao wanapunguziwa masikitiko mengi. Wanapendezwa na ushirika wa ndugu zao za Kikristo na kufanya nao urafiki wenye kuendelea, wenye kutumainika. Hapa ushirika unajenga kuliko kubomoa. Unamsaidia mtu aendelee na mradi wake wa “uzima ulio kweli kweli” katika taratibu mpya ya Mungu.—Ebr. 11:24, 25.
JE! WEWE UNAISHI KWA AJILI YA NAFASI ZA KUCHEZEA AU KUFANYA UASHERATI?
16. (a) Maana yake nini ‘kuchezea uasherati’? (b) Kwa sababu gani matembezi ya kirafiki ya mvulana pamoja na msichana si mchezo wa vivi hivi?
16 ‘Kuchezea’ maana yake ni kujifurahisha, kama kwa kitu cha kuchezea; kupisha wakati katika mchezo. Kuchezea uasherati ni kuufanyia mchezo pasipo kufanya uasherati au uzinzi wenyewe. Viungo vya uzazi si vitu vya kuchezea, bali vinatolewa na Yehova kwa kusudi la uzazi, vitumiwe na watu waliooana pamoja na wenzi wao. Biblia inalaumu mwenendo mpotovu, na ni wazi kwamba kuchezea uasherati ni mwenendo mpotovu, ambao matokeo yake yanaweza kuwa kutengwa na ushirika. (Gal. 5:19; Marko 7:21-23) Ikiwa mtu anadhani ya kuwa mwenendo huo mchafu unakubalika mradi anaepuka kufanya ngono, anajipumbaza tu mwenyewe. Matembezi ya kirafiki ya mvulana pamoja na msichana si mchezo wa vivi hivi bali yamepaswa yawe na kusudi la ndoa. Ikiwa mtu hana kusudi la kuoa au kuolewa au ni mchanga mno kuchukua madaraka ya ndoa, basi yampasa ayachunguze makusudi yake juu ya sababu gani anataka kufanya urafiki na mtu mwingine. Yeye anaelekea wapi, au, tukisema katika njia nyingine, yeye anaanza kuishi kwa ajili ya nini?
17. Ni mambo gani, yanayopaswa kuepukwa na Wakristo, yanasaidia kuchezea uasherati?
17 Mara nyingi kuchezea uasherati kunaanza na ushirika mbaya. Mazoea haya yameenea sana kati ya walimwengu. Ni vyepesi kushawishwa wakati uko katikati yao. Maongezi yao, sinema, vitabu, magazeti na vitabu vinavyoonyesha mambo ya umalaya, upuzi, mavazi yenye kubana au yenye kuonyesha uchi, vyote hivi vinasaidia kufanyiza na kusitawisha tamaa mbaya katika moyo. Kusuhubiana na mwenzi wa fulani huenda kukaonekana kuwa si kubaya, lakini mara nyingi huku kunaongoza kwenye matokeo mazito.—Efe. 5:3-5.
18. Ni maulizo gani yanayotolewa kwa kila mmoja afikirie katika kuyapima makusudi yake katika ushirika wa wanaume na wanawake?
18 Haya ni maulizo kwa kila mmoja kuyafikiria katika kuyapima makusudi yake, lakini yasiyotaka Sosaiti kutoa amri juu yake: Ijapo ninyi bado kuoana, je! mnashikana mikono kwa sababu mnaona raha kwa kufanya hivyo? Je! unacheza dansi pamoja kwa sababu unapata furaha kwa sababu mwili wako unagusana na mwili wa mwingine? Je! unaaga kwa kubusu kwa sababu unaona inachochea, ingawa hujaoa au kuolewa? Barua zinazopokewa na Sosaiti zinaonyesha kwamba mara nyingi uasherati ulianza katika njia hizo.
19. Kwa sababu gani mtu hawezi kumlaumu Mungu kwa kumwumba mwanamume na mwanamke wakiwa na viungo vya uzazi wakati hivi vinapotumiwa ili kufanya dhambi juu yake Yeye?
19 Biblia inasema waziwazi sana katika kusema hivi: “Ni heri mwanamume asimguse mwanamke.” (1 Kor. 7:1) Hatuwezi tukalaumu viungo vya uzazi ambavyo Mungu ametia ndani ya mwanamume na mwanamke ikiwa vinatumiwa kwa kufanya dhambi. Vimefanywa ili viendelee katika hali ya kutulia mpaka misukumo inapopokewa kutoka akilini na moyoni kuviamsha. Ikiwa mwanamume na mwanamke wanachagua kuoana na wakiisha kuoana, inafaa kabisa wafurahie kuwa pamoja, wakigusana katika matendo ya mahaba. Jambo hili linawaletea wote wawili raha, na wakichagua, huenda mahaba hayo yakawaongoza katika kufanya ngono wenyewe. Walakini, mwanamume au mwanamke asiyeoa au kuolewa hawezi kutazamiwa kuanza mchezo huu wenye kuongoza kwa mambo mengine pasipo kutokea mambo mazito. Uwezo wa kuitikia umo mwilini. Umetulia mpaka uamshwe. Kuliko kufurahisha, ule mchezo wa kugusa unaweza kuwasha tamaa kwa vyepesi kutaka kukaribiana zaidi: kubusu, kushikana viungo vya uzazi na kuendelea sana mpaka kufanya uasherati au uzinzi. Huenda yote haya yasitokee kwa pindi moja, lakini tamaa inaweza kuongezeka sana wakati mtu anapofikiria raha anayopokea na kutazamia pindi nyingine apate kuipokea, hata kutunga na kufanya mpango wa udanganyifu ili kutokeza pindi hiyo.
20. Mtu anawezaje ‘kuvituliza’ viungo vya mwili wake kwa habari ya matendo mabaya?
20 Kwa hekima, Biblia inawashauri Wakristo hivi: “Kwa hiyo, vitulizeni viungo vyenu vya mwili vilivyopo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, nyege, tamaa yenye kudhuru, na kutamani, ambayo ndiyo ibada ya sanamu. Kwa sababu ya mambo hayo hasira kuu ya Mungu inakuja.” (Kol. 3:5, 6, NW) Daktari anakupiga sindano ya kuzuia usisikie maumivu ili atulize mishipa wakati anapokuwa karibu kuanza kupasua sehemu fulani ya mwili. Sisi tunaweza kuvituliza viungo vyetu vya mwili kwa habari ya tamaa mbaya na maelekeo mabaya kwa kuondoa nguvu ya tamaa mbaya katika moyo na akili, na kwa kusitawisha tamaa nzuri, ambazo kubwa ya hizo imepaswa iwe kufanya mapenzi ya Mungu.—1 The. 4:3-7; 1 Pet. 4:2-5.
21. Imewapasa Wakristo waazimie kufanya nini wakati wa maoni na mazoea ya ulimwengu huu?
21 Waache Waepikureo wa kisasa waseme kwamba mwendo wa Kikristo haufai, ikiwa wanataka, lakini kwetu sisi si jambo lisilofaa wakati matumizi ya kanuni za Biblia katika maisha zetu yanapofanyiza furaha nyumbani, kutuepusha na matokeo yenye hatari ya kaswende na kisonono na ugonjwa unaoletwa na vileo, kutukaribisha karibu sana na wale wanaotoa ushirika wenye kujenga na kutusaidia tuwe na dhamiri safi na hali yenye kukubalika mbele za Mungu. Sisi tunashukuru zawadi ya uzima na tunataka tuufurahie milele katika amani na furaha. Sisi hatutaki tuitupe kwa ajili ya dakika chache za muda za raha ya kimwili. Sisi tunatumaini kabisa kwamba Mungu atatupa uzima wa milele katika taratibu yake mpya kama thawabu kwa uaminifu wetu. Kuwapenda wenzetu kunatuongoza tuwaambie wengine juu ya tumaini hili la ajabu wakati tunapoendelea kujitahidi sana tuishi kwa kuitumainia taratibu mpya ya Mungu.
[Picha katika ukurasa wa 343]
Wengi wanaishi kwa ajili ya anasa ya kunywa. Wewe waishi kwa ajili ya nini?
[Picha katika ukurasa wa 344]
Kukaribisha walimwengu kwa sababu za kazi kunaleta hatari ya werevu. Mashirika hayo huenda yaonekane yenye kutamanika kwa moyo
[Picha katika ukurasa wa 347]
Huenda matembezi ya urafiki ya wavulana na wasichana yakaonekana kuwa si mabaya, lakini yanaweza kuongoza kwenye uasherati