Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w25 Septemba kur. 26-30
  • Yehova Alitusaidia ‘Kusitawi Mahali Tulipopandwa’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Alitusaidia ‘Kusitawi Mahali Tulipopandwa’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Habari Zinazolingana
  • Baraka za Yehova Zilipita Matarajio Yangu Yote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
  • Yehova ‘Amevinyoosha Vijia Vyangu’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
  • Yehova Ni Ngome na Nguvu Yangu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Kukabiliana na Mabadiliko Unapopata Mgawo Mpya
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
w25 Septemba kur. 26-30
Mats na Ann-Catrin wakiwa wamesimama kando ya gari lao kwenye eneo la mashambani.

SIMULIZI LA MAISHA

Yehova Alitusaidia ‘Kusitawi Mahali Tulipopandwa’

LIMESIMULIWA NA MATS NA ANN-CATRIN KASSHOLM

HUENDA maneno “sitawi mahali ulipopandwa” yakaonekana kuwa ushauri wenye kushangaza. Lakini wenzi wa ndoa kutoka Sweden, Mats na Ann-Catrin, “walipandwa” mara nyingi. Jinsi gani, na ushauri huo uliwasaidiaje?

Ndugu na dada Kassholm walihudhuria Shule ya Gileadi mwaka wa 1979 na kwa miaka mingi “wamepandwa,” au wamepewa migawo ya kutumikia nchini Iran, Mauritius, Myanmar, Tanzania, Uganda, na Zaire. Walipokuwa katika Shule ya Gileadi walimsikia mwalimu wao, Jack Redford, akitoa ushauri uliowasaidia walipokuwa “wakipandwa,” “waking’olewa,” na “kupandwa upya” mara nyingi. Acheni watusimulie.

Mats, tafadhali anza kwa kutueleza jinsi ulivyopata kweli.

Mats: Alipokuwa akiishi nchini Poland wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, baba yangu alijionea unafiki mwingi katika Kanisa Katoliki. Hata hivyo, mara nyingi alikuwa akisema, “Ni lazima kuna dini ya kweli mahali fulani!” Baada ya muda, niliweza kujithibitishia kwamba kulikuwa na dini ya kweli. Nilinunua vitabu vingi ambavyo havikuwa vipya. Kitabu kimoja kilikuwa cha rangi ya bluu chenye kichwa, Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. Kichwa hicho kilinivutia sana, na nikakisoma kitabu hicho chote usiku uleule baada ya kukipata. Ilipofika asubuhi, nilijua kwamba nimeipata kweli!

Kuanzia Aprili 1972 na kuendelea, nilisoma machapisho mengi ya Mashahidi wa Yehova na kupata majibu ya maswali yangu ya Biblia. Nilihisi kama yule mfanyabiashara katika mfano wa Yesu ambaye baada ya kupata lulu moja yenye thamani kubwa, aliuza vitu vyote alivyokuwa navyo ili kuinunua. ‘Niliuza’ mipango yangu ya kufuatilia elimu ya chuo kikuu na kuwa daktari—ili kununua “lulu” ya kweli niliyopata. (Mt. 13:​45, 46) Nikabatizwa Desemba 10, 1972.

Katika mwaka mmoja, wazazi wangu na ndugu yangu mdogo pia wakakubali kweli na kubatizwa. Nilianza utumishi wa wakati wote Julai 1973. Kati ya mapainia wenye bidii waliokuwa kutanikoni kwetu, kulikuwa na dada mrembo na wa kiroho anayeitwa Ann-Catrin. Tulipendana na kufunga ndoa mwaka wa 1975, na kwa miaka minne tuliishi katika mji maridadi wa Strömsund, nchini Sweden, ambako watu wengi walitaka kujifunza Biblia.

Ann-Catrin: Baba yangu alijifunza kweli alipokuwa akimalizia masomo yake ya chuo kikuu jijini Stockholm. Ingawa nilikuwa na umri wa miezi mitatu tu wakati huo, bado alinipeleka kwenye mikutano na katika kazi ya kuhubiri. Mama hakupenda jambo hilo na alijaribu kuthibitisha kwamba mafundisho ya Mashahidi hayakuwa ya kweli. Lakini alishindwa, hivyo baada ya muda yeye pia alibatizwa. Nilibatizwa nilipokuwa na umri wa miaka 13, na nilipokuwa na umri wa miaka 16, nilianza upainia. Baada ya kutumikia katika mji wa Umeå, kulikokuwa na uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme, nikapewa mgawo wa upainia wa pekee.

Baada ya Mats na mimi kufunga ndoa, tulipata shangwe ya kuwasaidia watu kadhaa kujifunza kweli. Miongoni mwao alikuwa Maivor, msichana tineja aliyeacha lengo lake la kuwa mwanamichezo mashuhuri na kuja kuwa mwandamani wa dada yangu mdogo wakiwa mapainia. Walihudhuria Shule ya Gileadi mwaka wa 1984, na wanatumikia wakiwa wamishonari nchini Ekuado.

Katika migawo yenu mingi ya umishonari, mlifuata jinsi gani ushauri wa “kusitawi mahali mlipopandwa”?

Mats: “Tulipandwa upya” mara nyingi katika migawo mipya. Lakini tulijitahidi ‘kutia mizizi” kwa kumwiga Yesu, hasa sifa yake ya unyenyekevu. (Kol. 2:​6, 7) Kwa mfano, badala ya kutazamia ndugu na dada wenyeji wafanye mambo kwa njia ambayo sisi tumezoea, tulijitahidi kuelewa kwa nini walifanya mambo kwa njia tofauti. Tulitaka kuelewa utamaduni na njia yao ya kufikiri. Kadiri tulivyozidi kumwiga Yesu, ndivyo tulivyohisi kwamba ‘tumepandwa kando ya vijito vya maji,’ ili kusitawi popote tulipopewa mgawo.—Zab. 1:​2, 3.

Mats na Ann-Catrin wakiwa wamebeba mizigo na chakula.

Safari za kutembelea makutaniko zilikuwa sehemu ya kawaida ya maisha yetu

Ann-Catrin: Ili mti ukue baada ya kupandwa upya, unahitaji pia mwangaza wa jua. Sikuzote Yehova alithibitika kuwa “jua” letu. (Zab. 84:11) Alitupatia ndugu na dada wa kiroho wenye upendo. Kwa mfano, katika kutaniko letu dogo jijini Tehran, Iran, tulijionea ukaribishaji wageni uliokuwa wa kawaida nyakati za Biblia. Tulitamani sana kubaki nchini Iran, lakini Julai 1980, Mashahidi wa Yehova walipigwa marufuku rasmi na tukapewa saa 48 ili kuondoka nchini humo. Tukapewa mgawo nchini Zaire (sasa inajulikana kuwa Kongo) katika bara la Afrika.

Nyumba iliyo kwenye kijiji nchini Zaire.

Pindi za furaha kwenye mgawo wetu nchini Zaire, 1982

Nilipojua kwamba tumepewa mgawo barani Afrika, nililia. Mambo ambayo nilikuwa nimesikia kuhusu nyoka na magonjwa barani Afrika yaliniogopesha. Lakini marafiki wetu wawili wa karibu waliotumikia huko kwa miaka mingi walituambia hivi: “Bado hamjafika huko! Nendeni mkajaribu, na mtaona—mtaipenda Afrika.” Na ilikuwa hivyo! Ndugu na dada wana upendo na ni wachangamfu. Kwa kweli, tulipolazimika kuondoka Zaire miaka sita baadaye kwa sababu ya marufuku, nilitabasamu kwa sababu nilitambua kwamba sasa nilikuwa nikisali kwa Yehova hivi: “Tafadhali, turuhusu tubaki Afrika.”

Mmejionea baraka gani katika utumishi wenu kwa Yehova?

Ann-Catrin akiwa ameketi mwenye kiti cha kukunja kando ya gari lao aina ya Volkswagen Kombi.

“Chumba chetu cha kulala” nchini Tanzania, 1988

Mats: Baraka moja tuliyopata ni kuwa na urafiki wa karibu pamoja na wamishonari kutoka katika nchi na utamaduni mbalimbali. Pia, katika baadhi ya migawo, tulipata shangwe ya pekee inayotokana na kuongoza mafunzo mengi ya Biblia—nyakati nyingine kila mmoja wetu alikuwa na mafunzo ya Biblia 20 hivi! Sitasahau kamwe upendo na ukaribishaji wageni wa ndugu na dada barani Afrika. Tulipotembelea makutaniko nchini Tanzania, ndugu na dada wengi walituonyesha ukaribishaji wageni ‘uliopita uwezo wao’ tulipoegesha kando ya nyumba zao gari letu aina ya Volkswagen Kombi, lililokuwa “chumba chetu cha kulala.” (2 Kor. 8:3) Jambo lililokuwa la pekee sana kwetu ni wakati tuliouita kipindi cha hadithi. Wakati huo, mwishoni mwa kila siku, mimi na Ann-Catrin tuliketi na kuzungumzia matukio ya siku hiyo na kumshukuru Yehova kwa kuwa pamoja nasi.

Ann-Catrin: Kwa upande wangu, nimepata shangwe kubwa kwa kufahamiana na ndugu na dada kutoka ulimwenguni kote. Tulijifunza lugha mpya—kutia ndani Kifarsi, Kifaransa, Kiganda, na Kiswahili—huku tukifurahia utamaduni wa aina mbalimbali. Tuliwasaidia wanafunzi wapya, tukapata marafiki wa kweli, na tulifanya nao kazi “bega kwa bega” katika utumishi wa Yehova.—Sef. 3:9.

Tulijionea pia uumbaji mbalimbali wa Yehova wenye kuvutia. Kila mara tulipokubali mgawo mpya katika utumishi wetu kwa Yehova, tulihisi ni kana kwamba tuko safarini pamoja na Yehova akiwa Mwongozaji wetu. Ametufundisha mambo ambayo hatungeweza kamwe kujifunza tukiwa wenyewe.

Mkusanyo wa picha: 1. Mats na Ann-Catrin wakimhubiria mama pamoja na watoto wake. 2. Ann-Catrin akimhubiria mwanamume Mmaasai.

Kuhubiri katika maeneo tofauti nchini Tanzania

Mlikabili changamoto gani, na mlizishughulikiaje?

Mats: Tuliugua magonjwa kadhaa, kutia ndani malaria. Na Ann-Catrin alifanyiwa upasuaji wa dharura mara kadhaa. Pia, tulikuwa na wasiwasi kuhusu wazazi wetu waliokuwa wanazeeka; hivyo, tunawashukuru sana ndugu na dada zetu wa kimwili waliowatunza tulipokuwa katika migawo yetu. Walitimiza jukumu hilo kwa uaminifu, subira, shangwe, na upendo. (1 Tim. 5:4) Hata hivyo, pindi fulani tulijihisi vibaya kwa sababu tulitamani kufanya mengi zaidi ya kuwategemeza tu tukiwa mbali.

Ann-Catrin: Mwaka wa 1983, tulipokuwa tukitumikia nchini Zaire, nilipata ugonjwa wa kipindupindu. Daktari alimwambia Mats, “Mtoe nchini humu leo!” Siku iliyofuata, tulipanda ndege ya mizigo—ndege pekee iliyopatikana—ambayo ilikuwa inaelekea Sweden.

Mats: Tulilia kwa uchungu kwa sababu tulihisi kwamba hatungeweza kuendelea na mgawo wetu wa umishonari. Hata hivyo, Ann-Catrin alipona, ingawa daktari alikuwa amesema kwamba hangepona. Na mwaka mmoja baadaye, tuliweza kurudi Zaire, wakati huu tulipewa mgawo katika kutaniko dogo la Kiswahili jijini Lubumbashi.

Ann-Catrin: Tulipokuwa jijini Lubumbashi, nilipata mimba lakini ikaharibika. Ingawa hatukuwa tumepanga kuwa na familia, ilikuwa vigumu sana kwangu kukabiliana na kifo cha mtoto wetu. Hata hivyo, wakati huo wa huzuni tulipata zawadi tusiyotarajia kutoka kwa Yehova. Tulianzisha mafunzo mengi ya Biblia kuliko wakati mwingine wowote. Chini ya mwaka mmoja, idadi ya wahubiri kutanikoni iliongezeka kutoka wahubiri 35 hadi 70, na hudhurio la mikutano liliongezeka kutoka watu 40 hadi 220. Tulikuwa na mengi ya kufanya katika huduma na baraka za Yehova zilinipatia faraja nyingi sana. Hata hivyo, bado tunamkumbuka na kumzungumzia mtoto wetu mpendwa mara nyingi. Tunasubiri kwa hamu kuona jinsi Yehova atakavyoponya maumivu yetu yote ya kihisia wakati ujao.

Mats: Pindi moja, Ann-Catrin alipata ugonjwa wa kuchoka kupita kiasi. Nami niligunduliwa kuwa nina ugonjwa wa kansa ya utumbo mpana iliyokuwa imefika hatua ya nne. Lakini sasa ninaendelea vizuri, na Ann-Catrin anafanya yote awezayo katika utumishi wake kwa Yehova.

Tumetambua kwamba si sisi tu tunaokabiliana na majaribu. Baada ya mauaji ya kimbari ya mwaka wa 1994, tuliwatembelea ndugu na dada wengi kutoka Rwanda waliokuwa katika kambi za wakimbizi. Tulipojionea imani, uvumilivu, na ukaribishaji wao wageni, tulijifunza jinsi Yehova alivyo na nguvu za kuwategemeza watu wake haidhuru jaribu wanalopitia.—Zab. 55:22.

Ann-Catrin: Tulipata changamoto nyingine tulipohudhuria programu ya kuweka wakfu ofisi ya tawi nchini Uganda mwaka wa 2007. Baada ya programu, tulisafiri pamoja na kikundi cha wamishonari na Wanabetheli 25 tukielekea Nairobi, Kenya. Kabla ya kufika kwenye mpaka wa Kenya, ghafla lori liliyumba na kuhamia upande wetu wa barabara na likagongana uso kwa uso na basi letu. Dereva na ndugu na dada zetu watano walikufa papo hapo; dada yetu mmoja alikufa baadaye hospitalini. Tunatamani sana kuwaona tena rafiki zetu!—Ayu. 14:​13-15.

Hatimaye nilipona majeraha yangu. Lakini mimi na Mats tulikuwa miongoni mwa abiria kadhaa waliopatwa na ugonjwa wa kuwa na wasiwasi kupita kiasi kwa sababu ya tukio lenye kutisha (PTSD). Katika kisa changu, wasiwasi huo ulifanya niamke usiku nikiwa na dalili kama za mtu anayepata mshtuko wa moyo. Jambo hilo liliniogopesha sana. Lakini sala tulizotoa kwa Yehova za kutoka moyoni, pamoja na faraja tuliyopata kutoka katika baadhi ya maandiko tuliyoyapenda, yalitusaidia kukabiliana na hali hizo. Pia, tuliwaona wataalamu wa afya, jambo ambalo lilitusaidia. Sasa tumepata nafuu, na tunamwomba Yehova atusaidie tuwafariji watu wengine wanaokabiliana na ugonjwa huo.

Ulipoeleza kuhusu jinsi ambavyo mmeweza kukabiliana na hali ngumu, ulisema kwamba Yehova “aliwabeba kama mayai mabichi.” Ulimaanisha nini?

Mats: Msemo wa Kiswahili, “Tumebebwa kama mayai mabichi” unamaanisha kwamba kama tu vile mtu anavyobeba kwa uangalifu mayai mabichi ili yasivunjike, Yehova ametutegemeza kwa wororo katika kila mgawo tuliopewa. Sikuzote tumepata kile tulichohitaji, na hata zaidi ya tulichohitaji. Njia moja ambayo tulihisi upendo na utegemezo kutoka kwa Yehova ni kupitia hisia mwenzi ambazo tulionyeshwa na Baraza Linaloongoza.

Ann-Catrin: Ningependa kueleza mfano wa jinsi Yehova alivyotutegemeza kwa wororo. Siku moja, nilipigiwa simu na kujulishwa kwamba baba yangu aliyekuwa nchini Sweden, alikuwa amepelekwa katika chumba cha wagonjwa mahututi. Mats alikuwa ametoka tu kupona ugonjwa wa malaria. Hatukuwa na uwezo wa kununua tiketi za ndege kwenda nyumbani, hivyo tuliamua kwamba tunahitaji kuuza gari letu. Kisha, tukapigiwa simu mara mbili; simu moja ilitoka kwa wenzi wa ndoa waliopata taarifa kuhusu hali yetu na walitaka kutulipia tiketi moja. Simu nyingine ilitoka kwa dada mwenye umri mkubwa aliyekuwa ametunza pesa kwenye kisanduku ambacho aliandika, “Kwa ajili ya mtu mwenye uhitaji.” Baada ya dakika chache, Yehova alikuwa ametusaidia kupata tiketi tulizohitaji!—Ebr. 13:6.

Unapotafakari kuhusu miaka zaidi ya 50 mliyotumikia katika utumishi wa wakati wote, umejifunza mambo gani?

Mats na Ann-Catrin wakiwa wamesimama pamoja kwa shangwe.

Katika mgawo wetu mpya nchini Myanmar

Ann-Catrin: Nimejifunza kwamba nguvu zetu zinatokana na “kuwa watulivu na kuwa na tumaini.” Tunapomtumaini Yehova, kwa njia fulani anafanya vita vyetu viwe vita vyake. (Isa. 30:15; 2 Nya. 20:​15, 17) Kwa kumtumikia Yehova kwa uwezo wetu wote katika kila mgawo, tumepata baraka nyingi zaidi kuliko ambazo tungepata kwa kufanya jambo lingine lolote.

Mats: Jambo kuu nililojifunza ni kumtegemea Yehova katika kila hali na kuona jinsi atakavyotenda kwa niaba yangu. (Zab. 37:5) Hajashindwa kamwe kunisaidia kama alivyoahidi. Bado tunaona ukweli wa jambo hilo kwenye mgawo wetu wa sasa katika Betheli nchini Myanmar.

Tunatumaini kwamba vijana wengi wanaotaka kupanua huduma yao watajionea upendo mshikamanifu uleule ambao Yehova ametuonyesha. Tuna uhakika kwamba watajionea hilo ikiwa watamruhusu Yehova awasaidie kusitawi kikamili, popote watakapopandwa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki