Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w73 3/1 kur. 113-118
  • Msaada Kutoka Juu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Msaada Kutoka Juu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SALA NI YA LAZIMA ILI KUEPUKA MAJARIBU
  • MSAADA WAKATI WA MAJARIBU
  • MLANGO WA KUTOKA KATIKA MAJARIBU
  • SALA HAIZUIWI NA HALI YA UPWEKE
  • Kushinda Udhaifu wa Kibinadamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Jinsi ya Kupinga Vishawishi
    Amkeni!—2014
  • “Ili Msiingie Katika Jaribu”
    Endeleeni Kukesha!
  • 1 Wakorintho 10:13—“Mungu Ni Mwaminifu”
    Mistari ya Biblia Yafafanuliwa
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
w73 3/1 kur. 113-118

Msaada Kutoka Juu

“Kesheni, mwombe, msije mkaingia majaribuni”​—Mt. 26:41.

1, 2. (a) Mtume Petro alipoandika maneno haya, “Mkeshe katika sala,” labda alikuwa akifikiria tukio gani? (b) Ni shauri gani ambalo Yesu aliwapa mitume watatu waliokuwa wameshindwa ‘kuendelea kukesha’?

“LAKINI mwisho wa mambo yote umekaribia; basi, iweni na akili, mkeshe katika sala.” Wakati mtume Petro alipoandika maneno hayo ya kuwashauri Wakristo, labda alikuwa akifikiria ule usiku ambao yeye, Yakobo na Yohana walikuwa wameshauriwa na Yesu kusali. Walikuwa katika Bustani ya Gethsemane. Wakati wa kusalitiwa kwa Yesu kulikaribia. Yesu aliwaambia hawa watatu: “Nafsi yangu inasikitika sana, hata mauti. Kaeni hapa na kuendelea kukesha pamoja na mimi.”​—1 Pet. 4:7; Mt. 26:38, NW.

2 Ndipo Yesu alipoendelea mbele kidogo, akaanguka kifudifudi akamwomba Baba yake wa mbinguni hivi: “Baba yangu, ikiwezekana, kikombe hiki kiniepuke; walakini si kama nitakavyo mimi, bali kama utakavyo wewe.” Aliporudi kwa wanafunzi watatu, Yesu aliwakuta wamelala usingizi. Akamwambia Petro hivi: “Je! hamkuweza kukesha pamoja nami hata saa moja? Kesheni, mwombe, msije mkaingia majaribuni.”​—Mt. 26:39-41.

3. Bila kujali shauri la Yesu, mitume waliitikiaje, ikisababisha maelezo gani kutoka kwa Yesu?

3 Tena, kwa mara ya pili, Yesu akaenda kusali, akimwomba Mungu kwamba mapenzi Yake yatimizwe. Halafu akarudi na tena akawakuta wanafunzi watatu wamelala usingizi, “maana macho yao yamekuwa mazito.” Kwa mara ya tatu Yesu akawaacha akasali. Aliporudi kwa mitume, alisema: “[Wakati kama huu ndio ninyi mnalala na kupumzika!] tazama, saa imekaribia, na Mwana wa Adamu anatiwa katika mikono ya wenye dhambi. Ondokeni, twende zetuni! Tazama, yule anayenisaliti amekaribia.” Alipokuwa angali akisema maneno hayo, Yuda Iskariote alikaribia akiwa na kundi la watu wenye silaha ili Yesu apate kukamatwa.​—Mt. 26:42-47.

SALA NI YA LAZIMA ILI KUEPUKA MAJARIBU

4. (a) Ni onyo gani la waziwazi ambalo mitume walikuwa wamepokea mbele ya kuingia katika hali zenye majaribu? (b) Petro aliitikiaje onyo hili?

4 Wanafunzi wa Yesu waliingia majaribuni​—ijapokuwa maonyo kutoka kwa Bwana wao! Mitume watatu walikuwa kazini na walidhaniwa kuendelea kukesha, lakini walijilaza wakapata usingizi, wakati Yesu mara tatu alipokuwa akishughulika na kusali. Kweli, labda ulikuwa umepita wakati wa manane na kwa kweli wanafunzi walikuwa wakisinzia, lakini Yesu akijua sana kwamba roho ilikuwa na nia bali mwili ni dhaifu, akawa amewaambia wakeshe na kusali! (Mt. 26:41) Walikuwa wameonywa mbele ya kuingia katika hali zenye majaribu, Yesu akisema: “Ninyi nyote mtachukizwa kwa ajili yangu usiku huu; kwa kuwa imeandikwa, Nitampiga mchungaji, na kondoo wa kundi watatawanyika.” (Mt. 26:31) Katika njia hii walikuwa wameonywa kwa unabii wa Zekaria 13:7 uliokuwa karibu kutimizwa. Walakini, Petro alijibu onyo la Yesu, akisema hivi: “Wajapochukizwa wote kwa ajili yako, mimi sitachukizwa kamwe.” Lakini Petro aliambiwa kwamba angefanya hata vibaya zaidi​—angemkana Bwana Yesu mara tatu!​—Mt. 26:31-35.

5. Mitume walipopatwa na jaribu, walifanya nini, lakini ingaliwapasa wafanye nini?

5 Yesu alikuwa amewawekea wanafunzi wake mfano katika jambo hili la kukesha na kuwa macho kwa kusali. Lakini mitume walishindwa kufahamu namna maneno ya Yesu yangetimizwa. Basi walifanya nini? Kuliko kusali wao hawakujali! Ingaliwapasa kusali, waombe msaada kutoka juu. Lakini hapa walikuwa hawafanyi hivyo. Hawakuwa wakikesha; walikuwa hawasali sikuzote, na hivyo iliwapasa waingie majaribuni.

6. (a) Ni “kujaribiwa” gani ambako ni tayari kuja juu ya “ulimwengu wote,” kama Yesu alivyotabiri katika Ufunuo 3:10? (b) Kwa kuwa jaribu halijamalizika bado, kuna onyo gani kwa Wakristo katika hili?

6 Haya yaliyowapata wanafunzi watatu yanatukumbusha maneno ya Yesu yaliyosemwa kwa “malaika” wa kundi la Filadelfia, yaliyoandikwa katika Ufunuo 3:10: “Kwa kuwa umelishika neno la subira yangu, mimi nami nitakulinda, utoke katika saa ya kujaribiwa iliyo tayari kuujilia ulimwengu wote, kuwajaribu wakaao juu ya nchi.” Tangu kuja kwa “wakati wa mwisho” uliotabiriwa, mikazo kutokana na vyanzo vya kibinadamu na kutokana na vyanzo visivyoonekana vya kishetani imekuwa ya kuogofya sana, katika pande za mambo ya kimwili, zisizo na imani, zenye utukuzo wa mataifa. Jaribu limekuwa la kuamua kama mtu yuko upande wa taratibu hii mbovu ya mambo au tuko upande wa ufalme wa Mungu. Jaribu kubwa leo ni kutaka mtu ashindwe na mikazo hii ya kilimwengu na mavutano na kuwa upande wa taratibu hii ya mambo. Jaribu hili la ulimwenguni pote katika kipindi cha wakati mfupi kwa kulinganisha, kama “saa,” hakijamalizika bado. Hivyo Wakristo wa kisasa wanaonywa kwamba wako katika siku yenye jaribu. Wao, vile vile, kama Wakristo wa karne ya kwanza, yawapasa wawe macho na kuomba ili waepuke kuingia katika majaribu.

7, 8. (a) Kwa sababu gani Mungu anaruhusu majaribu yawajie Wakristo, na ni njia gani ambayo Mungu anatayarisha ili tupate msaada kutoka juu? (b) Zaidi kuingia majaribuni ni shauri la nini, na hivyo sala inasaidiaje?

7 Kwa kuwa Wakristo leo wanapatwa na majaribu mengi, ni lazima wajue namna ya kutoka katika hayo. Unawezaje kutoka katika majaribu? Ukumbuke kwamba Yehova Mungu hamjaribu ye yote kwa mabaya, bali yeye anaruhusu majaribu yawajie watumishi wake waaminifu ili kujaribu ukamilifu wao kwake na uaminifu wao kwa ufalme wake. Lakini kumbuka, wakati wa kujaribiwa tunayo njia ya sala, iliyo wazi wakati wote na inayopatikana wakati wote. Tunaweza kupata msaada kutoka juu wakati wo wote.

8 Kama Biblia inavyoonyesha, kuingia majaribuni zaidi ni shauri la tamaa. (Yak. 1:13-15) Basi angalia usije ukasitawisha tamaa mbaya, kwa maana ukifanya hivyo, ndipo kishawishi kinapokuvutia katika dhambi! Inatupasa tukeshe kwa kusali, kwa maana sala inatusaidia sisi kuepuka tamaa ya kichoyo. Sala hiyo yenye unyofu wa moyo inakimbiza tamaa yo yote ya kichoyo; inatuokoa na kamba za kushawishi na nguvu yao yote ya kichoyo yenye kuvuta. Ni lazima tusali ili tukeshe, na sala, vile vile, itaisafisha mioyo yetu. Ndiyo, Mungu atatusaidia ikiwa tunamwomba atusaidie. Tunahitaji msaada huo kutoka juu kwa sababu majaribu lazima yatokee kwetu. Na wakati yanapotokea, kumbuka onyo la kimungu: Uwe macho na kusali!

MSAADA WAKATI WA MAJARIBU

9. Mtume Paulo anaandikaje juu ya jaribu katika 1 Wakorintho 10:13, na inakamatana na uaminifu wa Mungu namna gani?

9 Ni jambo la lazima kwa Wakristo kufahamu kwamba Mungu wao mwaminifu hawaruhusu wajaribiwe zaidi kuliko wawezavyo kuvumilia. Kama mtume Paulo anavyoandika katika 1 Wakorintho 10:13: “Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.” Hii ina maana kwamba Yehova Mungu ni mwaminifu katika muda wote wa utendaji wa jaribu, mpaka yeye anayepatwa nalo ajue namna ya kulishinda kwa msaada utokao kwa Yehova, na analiepuka jaribu.

10, 11. (a) Kama inavyoonyeshwa na yaliyowapata Waisraeli, hasa mtume anasema juu ya majaribu gani? (b) Sababu gani majaribu hayo yatakuja juu ya Wakristo vile vile, na Mungu anaturuhusu tuonyeshe nini?

10 Sasa, imetupasa tukumbuke kwamba mtume Paulo hapa katika 1 Wakorintho 10:13 anasema zaidi juu ya majaribu, si juu ya mateso. Yeye alikuwa akisema juu ya majaribu yaliyo “kawaida ya wanadamu.” Mwanzoni mwa mstari huu wa kumi na tatu alisema: “Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu.” Kawaida ya wanadamu gani? Zaidi kawaida ya wanadamu wa Israeli wa kale waliokuwa katika agano na Yehova. Kwa maana katika mistari inayotangulia ya sura hii mtume alizungumza juu ya majaribu yaliyokuja juu ya Wayahudi wa asili, na namna maelfu yao walivyoanguka kwa majaribu. Anatokeza habari ya mambo yaliyowapata na kuanguka kwao kama onyo ili Wakristo wapate kuwa waangalifu wasije wakaangukia katika hali zile zile. Waisraeli hao walishirikiana na wapagani, na maelfu ya Waisraeli waliangukia katika uasherati, kama mtume Paulo alivyosema: “Wala tusifanye uasherati, kama wengine wao walivyofanya, wakaanguka siku moja watu ishirini na tatu elfu.” (1 Kor. 10:8) Vile vile waligeukia kwenye ibada ya sanamu, kuteta na kunung’unika. Yehova aliruhusu majaribu haya yaje juu yao ili aone yaliyokuwa katika mioyo yao, kwamba walimpenda Yehova Mungu wao ama sivyo.​—Kum. 8:1-3.

11 Basi majaribu hayo yote yanawajia Wakristo leo ambao vile vile wako katika agano na Yehova, kwa kuwa wao ndio waliofananishwa na watu hao wa kale, Waisraeli wa asili na “kundi kubwa la watu waliochangamana.” (Kut. 12:37, 38; Hes. 11:4-6) Kwa kuturuhusu tujaribiwe, Yehova anaweza kujua sisi ni watu wa namna gani moyoni. Ndipo, Mungu anapofanya mlango wa kutokea katika jaribu lakini anatuacha tuonyeshe namna tulivyo kweli, yaliyo katika mioyo yetu, kwamba tunachukia mabaya na tunapenda mema.

MLANGO WA KUTOKA KATIKA MAJARIBU

12. Je! Mungu anafanya mlango wa kutokea kwa kuondoa tu jaribu, na tukio juu ya Musa linaonyeshaje jibu lako?

12 Katika Neno lake Yehova anaahidi kwamba “pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea.” Namna gani? Kwa kuondoa jaribu tu? Hapana, Mungu haondoi jaribu, kama vile wakati mtu anapojaribiwa kufanya uasherati au kunung’unika. Inafaa tukumbuke kwamba wakati Haruni na Miriamu walipomnung’unikia ndugu yao Musa, kwamba yeye alikuwa na cheo kikubwa mno na kwamba wao hawakuwa na cheo cha kutosha, Mungu hakuwaondolea wanung’unikaji hawa jaribu kwa kumwondoa Musa katika cheo, sivyo? Ndivyo, alimwacha Musa aendelee kuwa katika cheo, kwa maana yeye alikuwa mtu ambaye Yehova alichagua na alikuwa mtu anayefaa kwa kazi hiyo. Haruni na Miriamu ndio waliopaswa watii. Namna gani? Iliwapasa wapate maoni ya kitheokrasi juu ya mambo. Iliwapasa wafahamu kwamba Yehova Mungu ni Mfalme na kwamba inawapasa watii mipango yake. (Hes. 12:1-16) Hivyo hatuwezi kutazamia kwamba wakati majaribu yanapokuja tunaweza kutoka mara moja katika jaribu na kuepuka wakati halijamalizika. Sivyo, lazima jaribu liendelee mpaka limalizike; ndipo Mungu atakapojua kama sisi tuna ukamilifu na uaminifu kwake.

13, 14. (a) Ikiwa hatuwezi kuepuka kujaribiwa, basi, Mungu anafanya mlango wa kutokea namna gani? (b) Ni mambo gani yaliyowapata Waisraeli wa kale yanayoonyesha kwamba Yehova hawaachi watu wake wajaribiwe wasivyoweza kuvumilia? (c) Yaliyompata Yusufu yanaonyeshaje lazima ya kutangulia kujitayarisha?

13 Basi, ikiwa hatuwezi kuepuka kupatwa na majaribu, mlango wa kutokea uko wapi? Mungu anatupa mlango wa kutokea kwa kutupa sisi kanuni zake za kitheokrasi, ambazo, tukizifuata, zitatusaidia tuepuke kufanya mabaya. Tena, Mungu anajua majaribu ambayo tunaweza kuvumilia. Kwa hiyo yeye haruhusu majaribu yasiyowezekana kwetu kuyavumilia yaje juu yetu. Kwa mfano, wakati Waisraeli walipotoka Misri, habari ya Biblia inasema hivi: “Mungu hakuwaongoza kwa njia ya nchi ya Wafilisti, ijapokuwa ilikuwa ni ya karibu; maana Mungu alisema, Wasije wakaghairi watu hawa hapo watakapokutana na vita, na kurudi Misri.” (Kut. 13:17) Hivyo Mungu hakuwaruhusu waende njia ya moja kwa moja kuelekea Nchi ya Ahadi kupitia “Njia ya Gaza.” Waisraeli hawakuwa na vifaa vya vita au kujitayarisha kupigana na majeshi ya Wafilisti yaliyozoezwa sana kupigana vita. Hivyo kwa fadhili Yehova alichagua njia ya Bahari ya Shamu kwa ajili ya watu wake. Ndivyo Israeli asivyotiwa katika kupigana na Wafilisti wakati huo, kwa maana Mungu alijua wasingeweza kuvumilia jaribu hilo.

14 Tunaweza kuwa wenye kushukuru kwa vile Yehova hatutii katika majaribu ambayo hatuwezi kuvumilia; tena tunaweza kuwa wenye kushukuru sana kwa vile anatangulia kututayarisha sisi ili tuweze kuvumilia majaribu na kuyashinda kwa ukamilifu. Kwa kusudi hili Mungu anatangulia kutujenga kwa kiroho. Lakini ole wetu ikiwa hatufaidiki na matayarisho haya ya mbele yanayotolewa na Mungu! Fikiria jaribu lililomjia Yusufu wakati alipojaribiwa na mke wa Potifa afanye uasherati. (Mwa. 39:7-12) Je! tunaweza kuwa kama Yusufu? Yeye alikuwa ametangulia kujipasha habari juu ya sheria za Mungu kwa habari ya mambo hayo.

15. (a) Tutapata matokeo gani ikiwa tunatangulia kujitayarisha kwa majaribu? (b) ‘Kuikimbia ibada ya sanamu’ kutatusaidia namna gani kushinda majaribu?

15 Ndiyo, Yehova Mungu anatuonyesha mlango wa kutokea zaidi kwa kutangulia kutueleza namna ya mwenendo ambao anatazamia kwetu. (Gal. 5:19-23) Ndipo tunaweza kushinda majaribu yote mwanzo mpaka mwisho, tukishika ukamilifu, kuonyesha uaminifu chini ya jaribu. Lakini inatupasa tutii shauri la mtume Paulo. Akiisha kusema juu ya namna Mungu atakavyotusaidia katika shauri hili la jaribu anaongeza kusema: “Kwa ajili ya hayo, wapenzi wangu, ikimbieni ibada ya sanamu.” (1 Kor. 10:14) Ibada ya sanamu si kuabudu sanamu, mifano na vinginevyo tu. Mtume Paulo alionya kwamba ‘kutamani ni ibada ya sanamu.’ Ni kwa sababu kutamani kunamfanya mtu ajifanye mwenyewe kuwa sanamu, na tamaa za kichoyo zinakuwa ndilo jambo kubwa sana katika maisha ya mtu. Lakini ikiwa ‘tunakimbia’ namna zote za ibada ya sanamu, tunakuwa tumejitayarisha kwa kufaa kukutana na wakati ujao na majaribu ambayo huenda yakatokea.​—Kol. 3:5; 1 Kor. 6:18.

16, 17. (a) Mtu anapopatwa na jaribu, sababu gani kutegemea nguvu zake si jambo la hekima? (b) Ni moyo gani ambao inatupasa tuepuke, kama inavyoonyeshwa na mfano wa Israeli wa kale walipokuwa penye mpaka wa Nchi ya Ahadi? (c) Ni mwendo gani wa tendo utakaotuwezesha sisi tujiunge katika kusema maneno ya mtume katika 2 Timotheo 4:17,18?

16 Wakati wo wote Yehova anaporuhusu jaribu lije juu yetu, na tufanye jambo fulani ili tusimame imara! Kwa jambo moja tunaweza kuendelea katika sala na kutafuta msaada kutoka juu! Katika njia hii hatutaitegemea nguvu yetu wenyewe. Kama mtume Paulo anavyosema: “Kwa hiyo anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.” (1 Kor. 10:12) Bila kujali muda ambao Mkristo amekuwa akimtumikia Mungu, bado yampasa kushindana na ubinadamu, mwili wake wenye dhambi. Ikiwa wanadamu zamani wamejaribiwa na hali fulani katika nyakati zenye hatari na wakaanguka, basi sisi vile vile kama wanadamu tunaweza kuanguka. Sisi tungali tumo katika taratibu hii mbovu ya mambo na majaribu yake yote ya kutaka kufuata njia mbaya. Mwisho u karibu, lakini inatupasa tuwe waangalifu tusifikiri hatuwezi kuanguka. Hapana, ni jambo la hekima tusifikiri tuna nguvu sana ndani yetu wenyewe kwamba hatuwezi kuanguka. Israeli alikuwa karibu sana na Nchi ya Ahadi, na hata hivyo, ingawa kuwa kwao karibu sana, kulikuwako majaribu mazito, na watu 24,000 walianguka penye mpaka wenyewe wa nchi. Vivyo leo haitupasi hata kidogo tuone kwamba ni hatari ndogo kuangukia katika jaribu. Mngojee Yehova Mungu, na jaribu litapita. Yehova Mungu atakuwa mwaminifu kwa Neno lake naye atatuokoa katika jaribu.

17 Kwa hiyo mtumaini Mungu wakati unapopatwa na majaribu. Katika sala omba, ukisema: “Baba yetu uliye mbinguni . . . usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu.” Ndipo tutakapoweza kusema pamoja na mtume Paulo hivi: “Bwana alisimama pamoja nami akanitia nguvu. . . . Bwana ataniokoa na kila neno baya, na kunihifadhi.”​—Mt. 6:9-13; 2 Tim. 4:17, 18.

18, 19. (a) Ni jaribu la namna gani ambalo limekuja juu ya maelfu ya watu wa Yehova katika nyakati za karibuni, na wameshindaje jaribu hilo? (b) Akipatwa na jaribu la “kutiwa damu mishipani ama kifo,” Shahidi kutoka Surinam alionaje mlango wa kutoka katika jaribu hili?

18 Kuna maelfu ya Mashahidi ambao katika nyakati za karibuni walipatwa na majaribu ya kupokea kutiwa damu mishipani. Wachache wameanguka katika jaribu hili kwa kukazwa na madaktari na wengine, lakini watu wa Yehova kwa jumla wamepinga jaribu hili, wakishikamana na Neno lake, linalosema waziwazi hivi: ‘Jiepushe na damu.’ (Matendo 15:20, 29) Na wamefanya hivi kwa kuzifuata sana kanuni za Biblia na kwa njia ya sala. Mfikirie Shahidi kutoka Surinam ambaye kwa ghafula akawa mgonjwa sana alipokuwa katika meli. Aliondolewa katika meli katika Haiti, ili apate matabibu huko. Daktari alieleza kwamba kwa sababu ya vidonda vya tumboni vyenye kutoka damu ilikuwa ama “kutiwa damu mishipani ama kifo.”

19 Shahidi huyu alionaje jaribu hili kubwa? Aliandika hivi: “Mimi nilikuwa huko zaidi ya maili elfu moja kutoka kwa jamaa yangu. Labda wao hata hawakujua kwamba nilikuwa katika hali hii yenye hatari. Hapakuwa na ye yote kati ya ndugu zangu za Kikristo ambaye ningeweza kusema naye. Maneno ‘kutiwa damu mishipani ama kifo’ yaliingia katika akili zangu. Kwa wazi wale watu wa hospitali walidhani nitakufa bila shaka. Nilimwomba Yehova. Hata ijapokuwa mara nyingine nilijiona upweke, niliweza kuzungumza na Yeye sikuzote. Lo! namna lilivyo jambo la ajabu kuweza kumtwika Yehova mashaka yako yote, kwa kuamini kabisa kwamba yeye anawaangalia watumishi wake. Ikiwa ingekuwa lazima nife, basi nilijua kwamba ningefufuliwa. Tumaini la ufufuo lilinitia mimi nguvu katika uamuzi wangu nisikubali damu.” Mwisho Shahidi huyu aliokolewa katika jaribu hili, na alipona bila kutiwa damu mishipani. Kwa kuzifuata sana kanuni za Biblia na kwa kukesha kwa kusali alishinda jaribu.

SALA HAIZUIWI NA HALI YA UPWEKE

20-22. Eleza sababu gani sala ni msaada wa ajabu kutoka juu.

20 Tunapohitaji msaada wa kimungu upesi, sala ndiyo njia inayopatikana sana kwa msaada wa mara hiyo na wa moja kwa moja. Kwa kuwa Yehova Mungu halali usingizi, hakuna kukawia. “Anayekulinda wewe hawezi kusinzia kabisa.” (Zab. 121:3, NW) Kuna msaada wa mara hiyo kutoka juu kwa wale wanaomwendea Mungu katika sala. Si kama kuandika barua kisha kungojea jibu kwa siku fulani. Na kuna mengi sana ya kuombea, si kwa ajili yetu wenyewe tu bali kwa ajili ya ndugu zetu za Kikristo vile vile.

21 Kuzungumza kwa njia ya sala si mara hiyo bila kuchukua dakika nyingi tu; kunaweza kupitishwa katika kila namna ya kizuizi cha upweke. (Yona 2:1-10) Mmisionari aliyefungwa katika Uchina kwa miaka mitano katika hali ya upweke alimkumbuka nabii Danieli wakati aliposema: “Nilisali mara tatu kila siku mbele ya wote ambao wangepita karibu na chumba changu cha gereza.” Matokeo? Akasema: “Lo! namna sala ilivyoniletea nguvu ya kiroho na faraja! Na kwa njia hii wote wakanijua kama mhudumu wa Kikristo.” Lo! msaada wa ajabu kutoka juu kwa kujibu sala!​—Dan. 6:10.

22 Tena, Mkristo anaweza kuomba roho takatifu yenye kufariji, inayopenya kila namna ya kizuizi, kuta za vifungo na vizuizi. Hakuna kitu kiwezacho kuzuia roho ya Mungu wakati tunapoimba na tunapostahili kuipokea.

23-25. (a) Ni kuogofya gani ambako hakukumwogofya kijana wa Kikristo katika Guadeloupe, na kwa sababu gani? (b) Kwa sababu ya kushika kwake ukamilifu, matokeo yalikuwa nini?

23 Si zamani sana mmoja wa mashahidi wa Yehova katika Guadeloupe aliogofishwa kwa hali ya upweke. Kijana huyu alishikamana na kutokuwamo. (Yohana 15:19) Aliwekwa katika jela na akatunzwa peke yake katika chumba cha gereza. Ndipo alipokazwa. Maogofyo yalikuwa hivi: “Usipogeuza akili zako, utawekwa kifungoni kwa miaka isiyopungua miwili. Isitoshe, utakuwa peke yako katika chumba cha gereza kwa muda wote huo, basi ufikiri vizuri​—peke yako kwa miaka miwili!” Sasa, ni jibu gani ambalo walirudishiwa na kijana huyu wa Kikristo?

24 Alijibu hivi: “Basi, hivyo ndivyo ninyi mnavyofikiri. Lakini mimi sitakuwa peke yangu hata kidogo, kama ninyi mnavyosema! Yehova Mungu atakuwa pamoja na mimi na atanitia mimi nguvu kwa roho yake.”

25 Wakuu walishangazwa na jibu hilo. Tena, mwenendo wake mzuri uliwastaajabisha. Miezi ikapita, na ukaja wakati wa kusanyiko la Mashahidi. Lo! ilikuwa ajabu kumwona kijana yule akihudhuria kipindi cha kufungua kusanyiko! Alikuwa amefunguliwa siku iliyotangulia. Na alitoa maono yake penye kusanyiko. Mkuu wa jela alikuwa apo hapo, bila kujulikana kwa kijana. Wakati uliofuata hapo mkuu huyu alimwambia mhudumu-msimamizi wa kijana huyu hivi: “Kwa sababu ya mwenendo wake mzuri wa Kikristo na uamuzi wake usiovunjika, je! unajua ambavyo mke wangu aliniambia? Alisema, ‘Ninyi msifikiri kwamba mmefanya hivyo kwa mapenzi yenu wenyewe. Sivyo, bali ni Mungu wake, Yehova, ambaye amefanya hivyo kwa ajili yake ili ahudhurie kusanyiko lake. Mungu wake, Yehova, ni mwenye nguvu zaidi kuliko mungu wetu!’ “

26. Kwa sababu gani imetupasa tukumbuke shauri jema katika 1 Petro 4:7, na hivyo hatari inapotokea imetupasa tufanye nini?

26 Mkikutana na hali ya upweke, mateso, majaribu na mikazo, ninyi mashahidi waaminifu wa Yehova mwaweza kushinda, kwa utukufu kwa sifa Yake. Msaada wenu unatoka juu. Lakini kumbukeni shauri jema la mtume Petro: “Mkeshe katika sala.” (1 Pet. 4:7) Kwa taabu Petro alijifunza maana ya hili usiku ule Bwana Yesu alipomwambia kuendelea kukesha na “mwombe, msije mkaingia majaribuni.” (Mt. 26:41) Hatari inapotokea, uwe mwangalifu usije ukaacha bila kufanya lo lote juu yake, bali omba juu yake. Ndipo utakapopata msaada kutoka juu na kushinda majaribu, na kutoa asante kwa Yehova. Yeye atakufanyia mlango wa kutokea, kwa maana “Mungu ni mwaminifu.”

​—Kutoka The Watchtower, Sept. 1, 1972.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki