Mtumaini Mungu, Si Ufahamu Wako Mwenyewe
WATU wanaomtolea Yehova Mungu ibada ya pekee wanafahamu kwamba maamuzi yote ya mwisho ya wanadamu yako mikononi mwake. Mfalme Daudi, katika shauri lake la kumwaga mwanawe na mrithi wake Sulemani, alisema: “[Yehova] hutafuta-tafuta mioyo yote, na kuyatambua mawazo yote ya fikira.”—1 Nya. 28:9; 1 Sam. 16:7.
Kwa sababu hizo haitupasi tuwe na mashaka juu ya hukumu ambayo watu fulani au vikundi fulani vitapata. Lakini, Yehova anatupa uongozi ili tufuate mwendo utakaoleta hukumu njema kwetu na vile vile tuwasaidie wengine kuwa na hali ifaayo mbele za macho ya Mungu.
Kwa sababu ya kukamatana na maoni ya moyoni yenye huruma sana yaliyomo kuwapasa watoto wachanga, na kwa sababu ya kanuni ya Mungu ya ustahili wa jamaa, iliyozungumzwa katika makala zilizotangulia, maulizo fulani juu ya habari hii yanatokea ambayo yanastahili kuzungumzwa.
WATOTO WA KULELEWA
Wengine wameuliza, ‘Namna gani juu ya watoto wachanga ambao ni wa kulelewa? Je! wao hawamo katika umoja wa jamaa ambayo wamelelewa, na hali yao na Mungu haiamuliwi na hali ya wazazi wanaowalea?’ Inaelekea kuwa hivyo. Ikiwa wazazi wanaowalea ni Wakristo wa kweli, watamfundisha mtoto wa namna hiyo kweli ya Neno la Mungu. Ikiwa mtoto mwenyewe ni mtii kwa wazazi wake wanaomlea na kwa sheria za Mungu anazoweza kufahamu, basi, alilosema mtume Paulo katika 1 Wakorintho 7:14 bila shaka lingeweza kutumika katika hali hii.
Kwa upande mwingine, mtoto mwenyewe anaweza kulelewa na wazazi wasio Wakristo. Inaelekea kwamba angeonwa kama mshiriki wa hukumu ya wazazi wanaomlea mbele za Mungu. Kweli, ikiwa mtoto ni mwenye umri wa kutosha kufahamu wema na ubaya na anafanya hivyo, akionyesha upendo wa kweli kwa haki, akitafuta kwa bidii kujua na kufuata kweli hata ingawa wazazi wake wanaomlea hawafanyi hivyo, basi huenda akapata kibali cha Mungu.—Eze. 18:14-18; 33:18, 19.
Katika hali ambazo mume na mke wamemchukua mtoto wamlee kihalali na kwa hiyo wamejitwalia madaraka juu yake, wana sehemu kubwa katika kuamua hali ya mtoto katika njia nzuri au mbaya. Lakini watu au waume na wake wanaomweka mtoto tu nyumbani awe wa udugu, au watu wanaolipwa kwa sababu ya kumtunza mtoto, hawawezi kumtazamia mtoto huyo aje chini ya kibali cha Mungu kwa sababu tu wao ni watunzaji wake. Si wao walio na madaraka juu ya mtoto, na kanuni ya ustahili wa jamaa haingetumika hapa. Lakini, ikiwa, wakati ambao mtoto yu mikononi mwao, wanamfundisha katika Neno la Mungu kwa kadiri wawezayo, hii, kwa kweli, itakuwa kwa hali njema yake akitii na kufuata mambo mema anayojifunza.
Walio watumishi wa Mungu wanapaswa kufanya yote wawezayo kuwafundisha wengine kweli, lakini wale wasio na madaraka kamili ya mtoto haiwapasi wadhani kwamba wanaweza kujiingiza katika haki za wazazi. Ikiwa mtu fulani ana jamaa wasioamini, ni madaraka ya wazazi katika jamaa kama hizo zisizoamini kuwazoeza watoto, na Mungu anawaruhusu kufanya hivyo kama watakavyo. Kwa kweli, kama nafasi imetolewa ya kuwaambia watoto kama hao kweli, jambo hili linaweza kufanywa. Lakini kupita kadiri, kwa mfano, kujaribu kuwatafutia usimamizi wa kihalali watoto hao, kungekuwa ni kuingilia mambo ya wengine. (1 Pet. 4:15) Mungu hafanyi hivyo; sababu gani sisi tufanye hivyo? Acha yote mikononi mwa Mungu, anayewatunza wenye mioyo mizuri.
HATARI YA KUMWOA ASIYEAMINI
Inapaswa iangaliwe kwamba, hata ingawa Mungu anaubariki umoja wa jamaa ambapo mmoja tu ndiye mwamini, ni jambo lisilo la hekima sana kwa Mkristo kumwoa mtu asiyeamini. Kwa sababu, ingawa Mungu anaona kukamatana kwa ndoa kama kitu kitakatifu, hii haina maana ya kwamba magumu yenye kuhuzunisha sana hayawezi kutokea. Ni vigumu zaidi kuwafundisha watoto njia ya Mungu katika nyumba iliyogawanyika kwa njia ya kidini. Asiyeamini huenda akajaribu kutangua mafundisho ambayo watoto wanapokea, au hata huenda akajaribu kuyazuia mafunzo yenyewe. Hii inaweza kuwa na matokeo yenye kudhuru kwa watoto. Huenda wakakosa kujitiisha kwa mambo waliyofunzwa na mzazi anayeamini, na, kama ndivyo, watoto hawa watashiriki katika hukumu ya Mungu juu ya mzazi asiyeamini.
Hali ngumu sana huenda ikatokea ikiwa yule asiyeamini anaamua kutengana na anayeamini kwa sababu ya kutoelewana kwa njia ya kidini. Ikiwa asiyeamini anasisitiza kutengana, anayeamini anaweza kumruhusu (mumewe au mkewe) aondoke. Mtume Paulo anataja kwamba “ndugu mume au ndugu mke hafungiki. Lakini Mungu ametuita katika amani.” (1 Kor. 7:15) Lakini namna gani ikiwa wana watoto? Huenda asiyeamini akajaribu kuwachukua watoto. Huenda hata akapewa ruhusa ya kuwaangalia na korti. Basi nafasi ndogo aliyo nayo anayeamini ya kuwaona na kusema nao juu ya njia ya Mungu huenda isitoshe kuwageuza watoto wenyewe katika njia inayofaa. Hata ikiwa asiyeamini anaondoka, akimwachia anayeamini watoto, namna ulivyo ugumu unaoletwa kwa anayeamini! Inamwongezea mwenzi wa Kikristo mizigo zaidi, kuwa ni lazima awatunze watoto, wakati ule ule akitunza hali yao ya kiroho kwa njia inayofaa.
Ndiyo, watu wasiooa haiwapasi kutotii shauri la mtume kwa ajili ya hali njema yao wenyewe ya kiroho na ile ya watoto ambao huenda wakazaliwa katika umoja na mtu asiyeamini. Mtume anafuata shauri la Biblia kwa Waisraeli, kutofanya mapatano ya ndoa na wasioamini, anapowashauri wajane waoe “katika Bwana tu.”—1 Kor. 7:39; Kum. 7:3, 4.
Kwa upande mwingine, kwa wale ambao tayari wamemwoa au wakaolewa na mtu asiyeamini, ama wamo katika hali nyingine zinazofunga ambazo zingeleta magumu fulani kwa habari ya utumishi kwa Mungu, mtume anasema: “Kila mtu na akae mbele za Mungu katika hali iyo hiyo aliyoitwa nayo.” (1 Kor. 7:24) Ikiwa mtu amekwisha kuoa tayari anapopata ujuzi wa kweli, na mwenzi wake hawi mwamini, hata hivyo, Mungu anahesabu kukamatana huko kama kitu kitakatifu. Lakini mtu asiyeoa akija kuoa mtu asiyeamini haweki ushirika wake na Mungu kwanza. Anahatirisha kwa uzito hali yake ya kiroho na kuongeza mkazo zaidi juu ya ukamilifu wake.
WATUMAINIFU KATIKA HAKI YA MUNGU
Kuna maulizo yanayotokea kwa habari ya kanuni ya ustahili wa jamaa. Biblia haiyajibu yote. Inaacha hukumu ya kila mtu mmoja mmoja kwa Yehova na Mwanawe, ambaye amemweka auhukumu ulimwengu kwa haki.—Matendo 17:31; 2 Tim. 4:1.
Je! inatupasa tuwe na wasiwasi na kufikiri-fikiri juu ya ni nani atakayeokoka “dhiki kuu,” au ni nani atakayefufuliwa? Tukiishi kulingana na amri za Mungu sasa na kutangaza habari njema kwa uwezo wote tulio nao, tutakuwa tukifanya mapenzi ya Mungu.
Na kwa habari ya hukumu za Yehova, tukija kumjua Mungu tutamtumainia, na tutakuwa kama Ibrahimu, ambaye, akijua haki na rehema ya Mungu, alivitumia kama msingi wa maombi kwa ajili ya watu walioishi katika miji mibaya ya Sodoma na Gomora, akisema: “Huenda wakawapo wenye haki hamsini katika mji, utaharibu, wala hutauacha mji kwa ajili ya hao hamsini wenye haki waliomo? Hasha, usifanye hivyo, ukamwue mwenye haki pamoja na mwovu, mwenye haki awe kama mwovu. Hasha; Mhukumu ulimwengu wote asitende haki?” Rehema ya Yehova isiyo na kifani ilionyeshwa kwa kusikiza maombi ya Ibrahimu kufikia habari ya kwamba kama watu kumi tu wenye haki wangepatikana katika jimbo hilo, Mungu angeiacha miji kabisa.—Mwa. 18:22-33.
Kwa hiyo, pahali pa kusumbuka kupita kadiri, ni bora kumngoja Yehova, wakati ule ule kuendelea kufanya mapenzi yake kwa imani iliyoonyeshwa na mtunga Zaburi, aliyesema: “Najua ya kuwa hukumu zako ni za haki, Ee [Yehova].”—Zab. 119:75.