Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w73 1/15 kur. 44-47
  • Je! Mwenendo Unaowapasa Wanaume na Wanawake Una Maana

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Mwenendo Unaowapasa Wanaume na Wanawake Una Maana
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JE! KWA KWELI “ADILI MPYA” NI MPYA?
  • JE! ADILI NI ISHARA YA UNYONGE?
  • SABABU GANI MWENENDO UNAOWAPASA WANAUME NA WANAWAKE UNA MAANA
  • KUFANYA UCHAGUZI WENYE HEKIMA NA MATOKEO MEMA YA MILELE
  • Je! Ni Busara Kutofanya Ngono Kabla ya Kufunga Ndoa?
    Kupata Faida Zote za Ujana Wako
  • Maoni Yako Juu ya Ngono—Yanafanyiza Tofauti Gani?
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Ngono—Ni Shauri Gani Hasa Lihalofaa?
    Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Vijana, Je! Mwenendo Safi Unaosemwa na Biblia Ndiyo Njia Bora?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
w73 1/15 kur. 44-47

Je! Mwenendo Unaowapasa Wanaume na Wanawake Una Maana

Mambo ya hakika ambayo vijana wanataka kujua

WATU wengi leo wanaona kwamba kuwa na unyumba bila kuoana ni kwa maana. Vijana wanaonekana zaidi kati ya watu hawa.

Wale wanaokataa jambo hili kabisa kwa sababu ya kushikilia kanuni za adili mara kwa mara wanaonewa huruma au hata kudharauliwa kama wenye mitindo ya kale, wayonge, wajinga au wasiojua desturi za kiasili. Je! ndivyo walivyo? Je! mambo ya hakika yanaonyesha nini?

JE! KWA KWELI “ADILI MPYA” NI MPYA?

Kwa kweli, hakuna cho chote kilicho kipya au cha “kisasa” juu ya ufisadi. Umekuwapo kwa muda mrefu, mrefu sana. Watu wa Sodoma na Gomora waliuzoea karibu miaka elfu mbili mbele ya kuzaliwa kwa Yesu. Ukisoma historia ya Milki ya Kirumi ya kale utaona kwamba ilijulikana sana kwa sababu ya ufisadi wa namna zote zinazoendeshwa leo. Kwa kweli, kuanguka kwake zaidi kulisababishwa na ufisadi.

Basi sababu gani tufikiri kwamba kinachoitwa “Adili Mpya” leo kina jambo fulani jipya? Ni kitu kile kile cha kale, namna zake tofauti zikiwa ni kwamba kimeenea sana kuliko kuwa katika sehemu moja tu, na kwamba kimejulikana sana katika nchi zinazojifanya kuwa ni za Kikristo.

Huenda ukawa umesoma makala juu ya habari inayosema kwamba wimbi lililoko sasa la “uhuru” wa umalaya linatokana na usitawi wa kisasa wa dawa za kuzuia uzazi, zinazodhaniwa kuwafanya watu huru na woga wa mimba zisizo halali. Au kwamba maendeleo ya udaktari kwa kuondoa magonjwa ya viungo vya uzazi yameendeleza “uhuru” wa umalaya. Je! sisi ni wapumbavu tunapokataa kufuata maelezo haya? Tena, mambo ya hakika ni yapi?

Mambo ya hakika ni kwamba mimba zisizotakiwa ni nyingi zaidi sasa kuliko wakati mwingine wo wote. Hesabu ya watoto wa haramu inaongezeka kwa kasi, na hii ni wazi katika zinazoitwa nchi “zenye maendeleo” ambapo dawa za kuzuia uzazi zinatumiwa kwa wingi. Katika United States, kwa mfano, karibu mmoja kati ya watoto 12 wanaozaliwa ni wa haramu; katika Sweden ni karibu mmoja kati ya kila watoto saba.

Ongeza na hesabu kubwa ajabu ya kuharibu mimba kunakofanywa, karibu milioni moja kila mwaka katika United States peke yake. Kwa hiyo ni vyepesi kuona kwamba dawa za kuzuia uzazi hazitoi uhuru uliohakikishwa kabisa wa kutopata mimba. Ni upumbavu kufikiri vingine.

Tena, madaktari katika nchi nyingi wanapendezwa kuona magonjwa ya viungo vya uzazi yakienea kwa mweneo mkubwa, vijana wengi wasiofika miaka ishirini wakipatwa. Katika United States kaswende sasa ni wa pili wa kifua kikuu kati ya magonjwa ya kuambukizana yanayosababisha vifo vingi. Na mara kwa mara wale wanaoambukizwa wanajua wakiwa wamechelewa mno kuzuia uharibifu mkubwa wa miili yao. Sababu gani ujihatirishe kwa uharibifu wa maisha yako yote, labda hata upofu au kutoweza kuzaa kama matokeo ya ufisadi?

JE! ADILI NI ISHARA YA UNYONGE?

Je! ni ishara ya unyonge mtu anapokataa kuingilia ngono mbele ya ndoa? Basi, ungesema ni kipi kinachochukua jitihada zaidi, kushindwa na nyege au kuzizuia?

Kwa kweli, mtu ye yote mnyonge anaweza kushindwa na nyege. Lakini inataka “mwanamume” kweli kweli (au “mwanamke” kweli kweli) kushinda kichocheo hicho mpaka kumpata mwenzi wa ndoa. Inataka nguvu hata zaidi leo wakati ambao maelekeo ya dunia yote yanaelekea upande mwingine; inataka kuuondosha mkondo, kushindana na mvuto.

Kitabu cha Biblia cha Mithali kinatoa habari kwa kutoa mfano juu ya jambo hili. Kinasimulia namna kijana kati ya “wajinga,” kwa kukosa nia njema ya moyo, anavyotanga na kufika pahali ambapo anakaribiwa na kahaba. Chini ya mkazo wa ubembelezi wa werevu wa mwanamke huyu, anashindwa na ‘anafuatana naye mara hiyo, kama vile ng’ombe aendavyo machinjoni; au mpumbavu kuadhibiwa katika pingu.’ (Mit. 7:6-23) Hakuwa na nguvu za adili kumwezesha kupinga.

Tofauti na hilo, Wimbo wa Sulemani unatueleza juu ya mwanamwali (kijana wa kike) wa kuvutia wa Shunem aliyeshinda vishawishi vyote vilivyotolewa na mfalme tajiri, akichagua kubaki mwaminifu kwa mchungaji kijana aliyetazamia kuolewa naye. Ndiyo, kuliko kuwa “mlango” ambao ungeweza kufunguliwa mara moja kwa wepesi, aliwahakikishia kaka zake kwamba yeye alikuwa imara kama “ukuta” katika uamuzi wake wa kuendelea kuwa bikira kwa ajili ya mwanamume aliyekuwa akimngoja.​—Wim. 8:8-10.

SABABU GANI MWENENDO UNAOWAPASA WANAUME NA WANAWAKE UNA MAANA

Sababu kubwa ya mwenendo unaowapasa wanaume na wanawake kuwa na maana ni kwamba hiyo ndiyo njia iliyowekwa na Yeye ambaye anajua mengi zaidi juu ya furaha ya kibinadamu, Yeye ambaye, kwa kweli, aliwezesha kuwe na ngono: Yehova Mungu. Kama Mpaji wetu wa uzima yuna haki ya kutuambia la kufanya, kuweka sheria za mwenendo juu ya matumizi ya viungo vyetu vya uzazi pamoja na nguvu zake za kupisha uhai.

Kupitia kwa mtume Paulo, Mungu anatuambia: “Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu.” (Ebr. 13:4) Uasherati hautii ndani tu ngono ya kufanywa ovyo ovyo na mtu ye yote tu​—unatia ndani vile vile na ngono kati ya watu waliochumbiana ambao bado hawajaoana.

Neno la Mungu linapinga waziwazi uasherati na mwenendo wo wote mwingine wa upotovu. Linasema kwamba watu wanaozoea mambo kama hayo hawana sehemu katika ufalme wa Mungu. (Gal. 5:19-21; Efe. 5:5) Uhakika huu wa sheria ya Mungu kwa kweli ni kwa faida yetu. Vichocheo vya nyege vinaweza kuwa vyenye nguvu sana, na nyakati zinafika katika maisha ya watu wengi ambapo inakuwa vyepesi kushindwa na mkazo wa jaribu. Kama sheria ya Mungu ingekuwa isiyoeleweka vizuri na dhaifu bila shaka haingetusaidia sana nyakati hizo. Lakini kwa kuwa i wazi sana na ni yenye nguvu inatusaidia kuwa macho, inategemeza uhodari wetu wa kufuata yaliyo mema, na, la maana zaidi, inatusaidia kujifunza kuchukia mwendo mbaya. Je! wewe unachukia mwendo wa ufisadi? Sababu gani inakupasa ufanye hivyo?

Ikiwa nyakati nyingine mwendo huo unaelekea kukuvuta, jiulize mwenyewe: ‘Je! mimi ningetaka wale wengine katika jamaa yangu wauingilie, wazazi wangu au ndugu na dada zangu? Je! mimi ningetaka wawe na watoto wa haramu? Je! hii ingeongeza upendo wangu na heshima kwao?’ Kama sivyo, je! haifai kuuchukia mwendo huo?

Namna gani juu ya watoto wanaozaliwa katika mwendo huo wa ufisadi? Kama ungekuwa na mtoto wa namna hiyo​—je! ungemtunza? Mama yako na baba yako? Je! wewe mwenyewe? Ungemtunzaje? Na je! mtoto mwenyewe angeonaje anapokua na kufahamu namna alivyozaliwa? Au kama ungekataa kuchukua daraka lako na kumpeana mtoto alelewe na mtu mwingine, je! watu wengine wangekuonaje? Je! ungejisikiaje wewe mwenyewe? Unaweza kuficha juu ya kuzaliwa kwake, halafu kumpeleka mtoto akatunzwe na mtu mwingine na kwa njia hiyo ujaribu kuepuka aibu na daraka. Lakini huwezi kujitoroka mwenyewe, sivyo?

Kwa kweli, je! ni faida gani imewahi kupatikana kutokana na mwendo wa ufisadi? Sababu gani mambo mengi yasiyopendeza yanakamatana nao, kutia ndani na magonjwa ya viungo vya uzazi yanayosababisha kulemaa, kuharibu mimba, mapigano yanayoletwa na wivu na hata mauaji? Sababu gani katika nchi ambapo mna “uhuru” mkubwa wa umalaya, kama katika Denmark na Sweden, hesabu ya talaka ni mojawapo ya zilizo juu zaidi katika ulimwengu? Je! talaka inaonyesha fanaka au kushindwa? Je! ni ishara ya furaha ya kweli au ya kukosa furaha na uradhi?

Mwenendo unaowapasa wanaume na wanawake una maana vile vile kwa sababu wanaoshikamana nao wana maelekeo ya kufanikiwa zaidi katika ndoa. Hii ni kwa sababu wameichukua ndoa kwa kuiheshimu sana, wakiheshimu mpango wa Mungu na kuwaheshimu wenzi wao wa wakati ujao na haki yao wote wawili ya kumpata mwenzi msafi katika ndoa.​—Linganisha 2 Wakorintho 11:2; Waefeso 5:26, 27.

Kwa kweli, kadiri unavyojitunza kuepuka mwenendo mpotovu au kuepuka kufanya lo lote unalotaka wakati wa kuchumbia, ndivyo na kufanikiwa kwako katika ndoa kutakavyoelekea. Ndipo wewe na mwenzi wako hamtakuwa mkinung’unikiana kwa sababu ya mashaka juu ya kama ulimwoa au kuolewa na mwenzako kwa ajili ya upendo au kutosheleza nyege tu ndiyo ilikuwa nia. Ndoa, hata hivyo, si mwungano tu wa miili miwili​—ni mwungano wa watu wawili. Na kila mmoja imempasa amheshimu na kumpenda mtu yule mwingine ikiwa ndoa italeta furaha ya milele.

KUFANYA UCHAGUZI WENYE HEKIMA NA MATOKEO MEMA YA MILELE

Upendo ambao msingi wake ni kutosheleza nyege si upendo wa kuendelea milele. Ni upendo wa kichoyo. Upendo wa namna hiyo unaonyeshwa kwa habari ya mmojawapo wa wana wa Daudi aliyeitwa Amnoni. Alimpenda dada yake mzazi mmoja ambaye alikuwa mrembo aliyeitwa Tamari. Halafu kwa hila akamlazimisha kulala naye. Nyuma ya hapo, kukatokea nini? Habari inatuambia: “Kisha Amnoni akamchukia machukio makuu sana; kwa kuwa ‘machukio aliyomchukia yakawa makuu kuliko yale mapenzi aliyokuwa amempenda kwanza.” Akamfukuza nje. (2 Sam. 13:1-19) Haya basi, ikiwa wewe u kijana wa kike, je! kwa upumbavu utafikiri kwamba kwa sababu kijana mwanamume fulani ana upendo wenye shauku kwako na anataka ulale naye hii inaonyesha anakupenda kwa moyo? Huenda nyumaye akawa sawasawa na Amnoni.

Mke wa afisa wa Kimisri Potifa alionyesha kupendezwa kwa namna ile ile na Yusufu. Alipoyashinda majaribu yake yote ya kumkosesha, ndipo alipoonyesha wazi-wazi nia yake. Kwa ukali alimwambia mume wake uongo juu ya Yusufu, akimfanya afungwe bila sababu.​—Mwa. 39:7-20.

Ndiyo, kinachoitwa “uhuru” wa umalaya kinageuza kinachopaswa kuwa kizuri na kisafi kuwa ovyo na cha kuchukiza.

Kwa hiyo, unataka kipi​—nyakati fulani fupi za raha ya ngono pamoja na hatari zote na magumu yanayotiwa ndani, au uradhi wa kuwa na dhamiri safi mbele za Mungu na watu wote, pamoja na kujiheshimu, kila siku?

Ikiwa unataka kujiepusha na ufisadi, basi jiepushe na mambo yanayouelekea; mazungumzo ambayo kila mara ni juu ya wanawake au wanaume, kusoma vitabu au picha ambazo lengo lake ni moja tu​—kuchochea nyege. Pahali pa mambo hayo fanya akili yako, macho yako na ulimi wako vijazwe na mambo mema, ukijaribu kufikia miradi inayofaa inayoleta faida za milele na isiyoacha aibu au maumivu ya moyo.

Zaidi ya yote, imarisha ujuzi wako na shukrani kwa Muumba wako na kwa haki na hekima ya njia zake na makusudi. Mwelekee katika sala na ukaze moyo wako katika mambo anayoahidi kwa wale wanaomtumikia. Unaweza kushikamana na mwenendo unaowapasa wanaume na wanawake ikiwa kweli unataka, kwa kuwa Yehova Mungu na Mwanawe watakupa nguvu unazotaka ili kufanya hivyo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki