Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ Je! kuna mambo ambayo inatupasa tuepuke kusema tunapopelekea Yehova sala?
Ndiyo, kunayo. Inatupasa tuepuke kusema katika sala zetu mambo yanayosikika kuwa ya kumfanya Yehova mtani wetu na kuwapa wengine (katika sala zinazosemwa mbele ya watu wote) kiwazo cha kwamba hatuonyeshi heshima. Kusema maneno kama “Habari za mchana, Yehova” na “Mpe Yesu salamu zetu” hayafai, wala maelezo yenye kuchekesha au hata kufanya mizaha katika sala zetu. Kwa sababu gani?
Sababu moja ni kwamba, wakati maneno hayo yanaposemwa katika sala inayotolewa mbele ya watu wote, yataelekea kuwashtua au kuwaudhi wanaosikiliza. (Warumi 14:21) Lakini kuna sababu ya ndani zaidi inayofanya maneno kama hayo yapase kuepukwa, hata katika sala zetu za faragha. Hayo ni maneno tunayotumia katika maongezi yetu na watu tunaolingana nao katika cheo. Yanapotumiwa katika sala, yanadokeza kwamba mtu hamwogopi Mungu wala hamheshimu, na yanatokeza maoni ya kwamba anayesali kwa njia hiyo amesahau kwamba yeye ni duni kabisa akilinganishwa na Yehova,—Mwanzo 18:27; linganisha Luka 18:9-14.
Ni kweli kwamba Wakristo wanatiwa moyo wasitawishe uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Sisi tunampenda na ndiye Baba yetu wa kimbingu. (Mathayo 6:9; 22:37) Kwa kweli, huenda wanadamu fulani wakaitwa rafiki zake. (Yakobo 2:23) Tena, tunakaribishwa tuseme na Yehova kwa uhuru wa kusema na kumweleza mawazo na matatizo yetu ya ndani kabisa.—Zaburi 55:1, 2; Wafilipi 4:6; Waebrania 4:16; 1 Yohana 3:21,22.
Hata hivyo, Yehova anadai kwamba wale wanaomfikia yeye wawe na mwelekeo unaofaa. Alisema: “Mtu huyu ndiye nitakayemwangalia, mtu aliye mnyonge, mwenye roho iliyopondeka, atetemekaye asikiapo neno langu.” (Isaya 66:2) Bidii ya moyoni inatakwa pia. “Nirudieni mimi kwa mioyo yenu yote,” ndivyo Yehova alivyowaambia watu wake. (Yoeli 2:12, 13) Mbele zake sisi hatuna dai lo lote la kwamba tuna ustahili, hatuna sababu ya kujitanguliza, hatuna haki ya kudai mambo.
Biblia inatoa shauri hili la ziada kwa wale wanaompelekea Yehova sala: “Kwa hiyo watu humwogopa; yeye hawaangalii walio na hekima moyoni.” “Atawafanyia wamchao matakwa yao, naye atakisikia kilio chao na kuwaokoa.” (Ayubu 37:24; Zaburi 145:19; ona pia Zaburi 39:5, 12.) Kwa hiyo, ingawa Yehova anakuwa tayari sikuzote kusikiliza sala zetu, njia tunayotumia kusema naye inapasa ionyeshe kwamba sisi tunajisikia kuwa hatufai, na pia kwamba tuna heshima kubwa kwake. Njia nyingine yo yote ya kumfikia ingedokeza kwamba tuna umbelembele, ukosefu wa unyenyekevu, au ukosefu wa kuchukua mambo kwa uzito.
Nyakati nyingine watoto wanatumia katika sala zao maneno ya kuzoeleana sana na mtu yanayofanya hata wazazi wao wachekelee. Maneno hayo ni wonyesho wenye kuvutia wa unyofu wa kitoto na yanaonyesha jinsi wanavyomwona Yehova kuwa mtu halisi. Hata hivyo, watu wazima, wakiwa na utambuzi wao mkubwa zaidi juu ya mambo yanayohusika, wanapaswa waepuke kuchezea mambo yasiyo ya kufanyiwa mchezo. Inawapasa wamfikie Yehova kwa bidii, kwa woga wenye heshima, kwa unyenyekevu, pamoja na staha na uzito.—1 Wakorintho 13:11.