Maswali kutoka kwa Wasomaji
● Je! Mathayo 26:74 inamaanisha kwamba mtume Petro alipopatwa na mikazo alitumia maneno machafu?
Hapana. Mstari huu unaeleza namna Petro alivyotenda baada ya Yesu kukamatwa, wakati aliposhtakiwa kuwa mmoja wa wafuasi Wake. Tunasoma hivi kuhusu kano la tatu la Petro: “Ndipo [Petro] akaanza kulaani na kuapa akisema, Simjui mtu huyu [Yesu].”—Mathayo 26:74.
Katika lugha fulani-fulani maneno “kulaani” na “kuapa” yanaweza kuwa na maana ya kutumia usemi mchafu. Lakini wakati Petro ‘alipolaani’ na “kuapa” hakuwa akitumia usemi najisi au mchafu kama watu wengi wanavyofanya wakiwa wamekasirika.
Katika Biblia, katika Kiebrania cha kwanza kabisa na na hata Kigiriki cha kwanza kabisa, ‘laana’ ilikuwa kutakia mtu au kitu mambo maovu. Haikuwa usemi mchafu na hata nyakati nyingine ilikuwa haisemwi kwa hasira. (Mwanzo 3:14, 15; 4:11, 12) Ili kuthibitisha ukweli wa maneno fulani, mtu angeweza kutamka laana (maneno ya uthabiti). Kwa kufanya hivyo alikuwa akisema, ‘Ikiwa ninalosema si kweli, na nilaaniwe; uovu na unipate mimi.’ Vivyo hivyo, mtu angeweza ‘kuapia’ jambo fulani, kwa njia hiyo akila kiapo kwamba lilikuwa kweli na kwamba mabaya yampate kama halikuwa kweli.
Kwa hiyo Petro hakuwa akitumia maneno machafu bali alikuwa akijaribu kwa woga kuwasadikisha walio karibu naye kwamba makano yake yalikuwa ya kweli. Ni wazi kwamba huo ulikuwa uongo aliolazimika kuutolea toba. (Luka 22:61, 62) Hata hivyo, Biblia inaonyesha wazi kwamba Wakristo wanapaswa kuepuka maneno machafu, ikituambia hivi: “Neno lo lote lililo ovu lisitoke vinywani mwenu.”—Waefeso 4:29.