Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w73 10/1 kur. 455-456
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
w73 10/1 kur. 455-456

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

● Timotheo wa Pili 3:6, 7 inasema: “Katika hao wamo wale wajiingizao katika nyumba za watu, na kuchukua mateka wanawake wajinga wenye mizigo ya dhambi, waliochukuliwa na tamaa za namna nyingi; wakijifunza sikuzote, ila wasiweze kabisa kuufikia ujuzi wa kweli.” Wanaume na wanawake wanaotajwa katika fungu hili ni akina nani?​—U.S.A.

Mstari unaotangulia (2 Tim. 3:5) unafunua wazi kwamba wanaume hawa wachafu wanatoka kati ya watu “wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake.” Wao ni kama wale wanaoelezwa na mtume Paulo kama “mitume wa uongo, watendao kazi kwa hila, wanaojigeuza wawe mfano wa mitume wa Kristo” na ‘watumishi wa Shetani wanaojigeuza kila mara wawe watumishi wa haki.’ (2 Kor. 11:13-15) Katika karne ya kwanza C.E. waalimu hawa wa uongo walitisha hali ya Wakristo ya kundi la Korintho, wakimfanya mtume Paulo aandike upesi: “Nachelea; kama yule nyoka alivyomdanganya Hawa kwa hila yake, asije akawaharibu fikira zenu, mkauacha unyofu na usafi kwa Kristo. Maana yeye ajaye akihubiri Yesu mwingine ambaye sisi hatukumhubiri, au mkipokea roho nyingine msiyoipokea, au injili nyingine msiyoikubali, mnatenda vema kuvumiliana naye!”​—2 Kor. 11:3, 4.

Si kwamba tu wanaume hao walitaka kuchafua Wakristo kwa njia ya mafundisho ya uongo, lakini vile vile walijaribu kuwatia wengine katika mwenendo wa ufisadi. Kama mwanafunzi Yuda alivyoona: “Kuna watu waliojiingiza kwa siri, watu walioandikiwa tangu zamani hukumu hii, makafiri, wabadilio neema ya Mungu wetu kuwa ufisadi, nao humkana yeye aliye peke yake Mola, na Bwana wetu Yesu Kristo.”​—Yuda 4.

Timotheo wa Pili 3:6 inaonyesha kwamba wanaume hawa waasi wa imani ya kweli wanakaza fikira zao kuelekea “wanawake dhaifu.” (NW) Hii haielekezi kwa wanawake wote kwa jumla kama ‘vyombo visivyo na nguvu’ walio tofauti na wanaume, kama vile katika 1 Petro 3:7. Kuliko hivyo, inaelekeza kwa wanawake ambao ni dhaifu kwa kiroho au kwa adili, kama maneno yanayozunguka yanavyoonyesha. Waasi wa imani ya kweli hawaendeshi maoni yao mabaya waziwazi kwa uhodari, bali ‘wanajiingiza katika nyumba za watu kwa ujanja,’ Wanajipendekeza kwa hao “wanawake dhaifu” (NW) na, kupitia kwao, wanajaribu kuwavuta wale wengine wa nyumba hiyo. Kwa kutokuwa na msingi mwema katika mafundisho ya Kikristo, hao “wanawake dhaifu” mara moja wanapatwa na waalimu wa uongo ambao labda kwa njia ya mapendezi na usemi wa kujipendekeza wanajifanya waonekane kama watumishi wa haki.

Hawa “wanawake dhaifu” wanaelezwa vile vile kama “wenye mizigo ya dhambi” na kama “waliochukuliwa na tamaa za namna nyingi.” Hii kwa wazi inamaanisha kwamba nia na tamaa zenye dhambi vinawalemea. Kwa kweli hawachukii kilicho kibaya wala hawapendi haki kwa kweli. Nia zao zenye dhambi zinafanya watekwe vyepesi na waalimu wa uongo, bila shaka hata wengine wa wanawake hawa wakijiachilia waingizwe katika mazungumzo ya kufanya ufisadi ati kwa sababu Mungu anaufahamu udhaifu wa kibinadamu na ni mwenye rehema nyingi na mwenye kusamehe.

Inaonekana wazi sababu “wanawake dhaifu” kama hao wangekuwa “wakijifunza sikuzote, ila wasiweze kabisa kuufikia ujuzi wa kweli.” Kwa kutokuwa na nia inayotakiwa ili kupata ufahamu na kuthamini kabisa kweli ya Kikristo, hawaendelezi hali yao ya kiroho. Wanaweza kuendelea kujifunza mambo, lakini hawaelewi maana ya mafundisho yote ya Kikristo ili wajipatanishe nayo. Kwa kujiruhusu kuvutwa na waalimu wa uongo, hali yao inazidi tu kuwa mbaya.

Bila shaka, kuna wanawake wengi wema, na hata wanaume, ambao wanajifunza kweli ya Biblia na kushikamana nayo. Lakini, zaidi katika Kristendomu, wanawake kwa kawaida wanakuwa na wakati wa kujifurahisha na kwa jumla hawamo katika ulimwengu wa shughuli kama wanaume walivyo, na kwa kawaida wanakazia fikira kwenye mambo ya kidini. Wanawake wanaelekea kuwaheshimu wanaume wenye vyeo vya juu na ambao ni wenye maneno ya kuvuta. Kwa hiyo wanaweza kupatwa na wanaume kama hao kama mtume anavyoeleza. Wanaweza kuvutwa vyepesi na wanaume wenye choyo au wafisadi ambao wanajifanya kuwa wenye hekima na ujuzi mwingi. Wanaume hawa wanajipa udhuru kwa mwendo wao wa ufisadi kwa kusema kwamba Mungu anajua sisi sote tu wasiokamilika na kwamba Mungu anasamehe, lakini kwa ubaya wanajaribu kumsingizia Mungu ili watimize makusudi yao.

Hawa alikuwa mfano wa mtu ambaye, hata ingawa yeye alijua amri ya Mungu, hakuja kumjua Mungu kwa kumshukuru, kumpenda na kwa kuwa mwaminifu kwake. Akawa mwanamke dhaifu akiongozwa na tamaa yake. Shetani Ibilisi alimtumia kama chombo cha kumsuta Mungu na kumvuta Adamu kwenye dhambi.​—Mwa. 3:1-5.

Kwa kuwa wanaume wafisadi wanaweza vile vile kupenya katika kundi la watu wa Mungu katika hizi “siku za mwisho,” maneno ya Paulo yanatilia mkazo lazima ya Wakristo wa kweli kuwa macho ili kuelewa mafundisho ya uongo na kuwaza kubaya. (2 Tim. 3:1) Mtu anayetaka kuwa katika hali ya kukubalika kila mara mbele za Yehova Mungu anapaswa kutia bidii awezavyo ili ‘kuendelea kutembea kwa umoja na Kristo Yesu, akiwa mwenye shina na mwenye kujengwa katika yeye na kufanywa imara katika imani.’ (Kol. 2:6, 7) Hii inataka funzo la mafundisho yote ya Kikristo kama yalivyo katika Maandiko Matakatifu na matumizi ya mambo yaliyojifunzwa. Ndipo, wakati watu wanapotoa mawazo yanayotofautiana na Neno la Mungu, mtu hatadanganywa na kutegwa na nia zenye dhambi.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki