Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w73 12/15 kur. 575-576
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
w73 12/15 kur. 575-576

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

● Kulingana na Kumbukumbu la Torati 6:8, 9, Waisraeli waliamriwa ‘waifunge sheria ya Mungu kama dalili juu ya mkono wao’ na waiache itumike kama ‘utepe katikati ya macho yao.’ Je! hii ifahamike kama ilivyo?​—U.S.A.

Waelezaji wengi wa Kiyahudi wameitumia amri hii kama ilivyo. Hili vile vile ni mojawapo la mafungu ya Biblia yanayotumiwa ili kutegemeza mazoea ya kuvaa hirizi (vikasha ambavyo ndani yake mna vifungu kutoka katika Maandiko Matakatifu). Walakini, uchunguzi wa maneno yanayotangulia na yanayofuata na maandiko mengine unaonyesha waziwazi matumizi ya mfano.

Kuanzia na Kumbukumbu la Torati 6:6 na kuendelea mpaka mstari wa 9, tunasoma hivi: “Na maneno haya [mimi Yehova] ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako; nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii, na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo. Yafunge yawe dalili juu ya mkono wako, nayo yatakuwa kama utepe katikati ya macho yako. Tena yaandike juu ya miimo ya nyumba yako, na juu ya malango yako.”

Na ifahamike kwamba kifungu hiki hakisemi kwamba amri hizo zilipaswa ziandikwe mahali fulani kisha zivaliwe katikati ya macho au juu ya mkono au zibandikwe kwenye miimo na malango. Amri zenyewe zilipaswa ‘zifungwe kama dalili juu ya mkono’ na zilipaswa zitumike kama ‘utepe katikati ya macho.’ Kwa wazi, basi, maana inayotumiwa hapa inafanana sana na ile inayosemwa katika Mithali 7:2, 3: “Uzishike amri zangu ukaishi, na sheria yangu kama mboni ya jicho lako. Zifunge katika vidole vyako; ziandike juu ya kibao cha moyo wako.” Kwa wazi si kama ilivyo. Isingewezekana kuandika amri juu ya moyo, na kuzifungia kwenye vidole amri zilizoandikwa kungemzuia mtu asitimize kazi. Kusudi linalofaa lisingetumikiwa.

Vile vile, kwa habari ya Sikukuu ya Kupitwa, ukumbusho wa kukombolewa kwao katika Misri, Yehova aliwaamuru Waisraeli hivi: “Nayo itakuwa ishara kwako katika mkono wako, na kwa ukumbusho kati ya macho yako, ili kwamba sheria ya [Yehova] ipate kuwa kinywani mwako; kwani [Yehova] alikutoa utoke Misri kwa mkono wenye uwezo.” (Kut. 13:9) Tena, ni wazi kwamba ukumbusho wenyewe usingeweza kufungwa juu ya mikono wala kutumika kama ukumbusho ule ule katikati ya macho yao. Lakini Waisraeli wangeweza kukumbuka kila mara lile ambalo Mungu alikuwa amewafanyia, kana kwamba liliandikwa katikati ya macho yao au kana kwamba ni ishara juu ya mikono yao.

Vivyo hivyo wangeweza kuziweka sikuzote amri za Yehova mbele yao bila kujali kwamba walikuwapo nyumbani au karibu na malango ya mji, ambapo kwa kawaida watu walikusanyika na wazee wa mji walishughulika na kesi. Haikuwapasa Waisraeli waitunze sheria ya Mungu katika mioyo yao na kuifundisha kwa watoto wao tu. Vile vile iliwapasa waonyeshe kwa tendo (kama linavyoonyeshwa kwa mikono) kwamba waliifuata. Kana kwamba sheria ya Mungu iliandikwa katikati ya macho yao ili wote waione, iliwapasa wajionyeshe wenyewe waziwazi kama wenye kuitegemeza. Hii ndiyo ingekuwa njia yenye matokeo zaidi sana ya kuendeleza uaminifu kuliko kuvaa vifungu vya maneno kutoka katika sheria ya Mungu au kuandika vifungu hivyo juu ya miimo yao au malango.

Hata mnafiki angeweza kuvaa vikasha vyenye maandiko. Kwa kweli, Yesu Kristo aliwalaumu Mafarisayo kwa ‘kupanua hirizi zao ambazo walivaa kama vitu vya kuwalinda.’ (Mt. 23:5) Kwa kupanua vikasha hivi, kwa wazi walitaka wawafanye wengine wadhani kwamba walikuwa na bidii ya kushika Torati. Lakini hawakujali kusudi lake la kweli. Kwa sababu hiyo, ishara zao za nje hazikumaanisha kitu.

Bila shaka sisi leo imetupasa tutake kujionyesha wenyewe kuwa watumishi watiifu wa Yehova kutoka kwa moyo. Hii ina maana kwamba mioyo yetu imepaswa ituongoze tuitikie uongozi wa Neno la Mungu lililoandikwa kwa utii wenye kushukuru. Akili zetu zimepaswa ziwe juu ya mambo yaliyo mazito, ya haki, yenye kupendeka, yenye staha, safi na yenye sifa njema. (Flp. 4:8) Katika lo lote tunalofanya, imetupasa ‘tulifanye kwa nafsi yote kama kwa Yehova, na si kwa wanadamu.’ (Kol. 3:23, NW) Ndiyo, kila tendo letu limepaswa lionyeshe kwamba amri za Mungu ziko mbele yetu sikuzote.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki