Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Je! ni kuonyesha kutoaminiana kwa Mkristo kuandika maafikiano juu ya biashara fulani pamoja na Mkristo mwingine?—U.S.A.
Hapana, kwa maana kuandika mambo ya biashara kunaweza kuwa fadhili na ulinzi kwa wote wanaopaswa. Kunaweza kuzuia kutopatana kwingi nyumaye.
Maafikiano yaliyoandikwa yanaweza kuzuia kukosea kwa kutokusudia kwa sababu ya kutoelewana katika mapatano yaliyosemwa kwa maneno. Kwa habari ya watu wengine, inakuwa lazima Mkristo aliye wakf atunze habari za mambo mengi kila siku. Halafu, tena, magumu yanatokea yanayotaka fikira zake. Kwa wazi hawezi kukumbuka kila kitu. Kama angalitegemea akili yake kabisa, ajapokuwa ana moyo mwema sana, yawezekana atasahau mapatano mengine au kuwa na mashaka juu ya kama aliyatimiza. Mapatano yaliyosemwa kwa maneno hayaruhusu sana nafasi ya kuhakikisha mambo. Na, yakiwa yasiyofahamika vizuri, wale wanaoyafanya mapatano ya maneno huenda wawe na maoni mbalimbali kwa uaminifu juu ya yanayotakiwa.
Maafikiano yaliyoandikwa vile vile yanaweza kuwa msaada katika kulitii onyo la Biblia: “Msiwiwe na mtu cho chote, isipokuwa kupendana.” (Rum. 13:8) Kwa wazi, kama mtu angesahau mapatano fulani kwa kutokusudia, asingejua anapaswa kuyatimiza. Nako kushindwa kwake kwa kutokusudia kungeleta maoni machungu, zaidi ikiwa yule mtu mwingine angeanza kufikiri kwamba nduguye wa Kikristo ni mchoyo na asiyetegemeka.
Jambo jingine linalofanya maafikiano yaliyoandikwa yawe bora ni mashaka ya maisha ya kibinadamu. Ni kama vile mwandikaji mwenye hekima wa Mhubiri alivyosema: “Wakati na bahati huwapata wote.” (Mtu. 9:11) Ni hekima kweli kweli kuwa na mapatano yaliyoandikwa kusudi kwamba, ikiwa lazima, mtu aweze kuhakikisha kwamba anastahili malipo au utumishi kuliko kupata hasara kubwa kwa sababu hawako mashahidi walio hai kuhakikisha dai lake.
Maandiko yanakubali kuandika maafikiano waziwazi. Kwa mfano, nabii wa Yehova Yeremia, kwa uongozi wa kimungu, alinunua shamba kutoka kwa mwana wa mjomba wake. Fedha ya ununuzi ilipimwa mbele ya mashahidi. Fedha ilipolipwa, mikataba miwili, yawezekana inayofanana, iliandikwa kwa kulingana na sheria za halali zilizokuwako. Mkataba mmoja uliachwa wazi, yawezekana kusudi kwamba uweze kutazamwa kwa wepesi na watu wenye kupendezwa. Ule mkataba mwingine ulitiwa sahihi na mashahidi nao ukatiwa muhuri. Kwa hiyo, kama ukweli wa mkataba usiotiwa muhuri ungetiliwa shaka, mkataba uliotiwa muhuri ungefunuliwa na kulinganishwa na usiotiwa muhuri. Shughuli yote ilikuwa ya waziwazi, ikitukia “mbele ya Wayahudi wote walioketi katika uwanda wa walinzi.” Nyuma ya hapo mikataba yote miwili ilitiwa ndani ya chombo ipate kutunzwa salama. (Yer. 32:6-14) Hivyo, miaka mingi nyumaye, ungalipatikana uhakika wa kwamba kila kitu kilikuwa kimeshughulikiwa sawasawa.
Kwa hiyo, kuliko kuonyesha kutoaminiana, kufanya mapatano yaliyoandikwa kwaweza kuwa onyesho la tamaa yenye unyofu ya kutimiza mapatano ya mtu.